Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Monday, September 17, 2012

Msondo Ngoma bado wanatamba

Wapiga gitaa wa bendi ya Msondo Ngoma Abdul Ridhiwani, kushoto, na Zahoro Bangwe, kulia,
wakiburudisha mashabiki wao hivi karibuni wakati bendi hiyo ilipotumbuiza kwenye ukumbi wa Max Bar, Ilala Bungoni, Dar es Salaam.

Msondo Ngoma ni moja ya bendi kongwe za muziki wa dansi za Tanzania. Zamani ilikuwa inaitwa NUTA Jazz.

Picha na habari zimetolewa na Rajabu Mhamila.

Sunday, September 16, 2012

Mada yangu ya leo: polisi na waandamanaji

Kuna mambo mawili muhimu yanajitokeza baada ya kuuwawa kwa mwandishi wa habari wa Channel Ten wa Iringa, Daudi Mwangosi, tarehe 2 Septemba 2012. Kwanza, Jeshi la Polisi, ambalo mmoja wa askari wake ameshafikishwa mahakamani kwa tuhuma za kuhusika na mauaji hayo, linahitaji kutoa mafunzo maalum ya namna polisi waliyopo kwenye eneo la maandamano wanavyopaswa kusimamia suala la amani katika maandamano.

Siyo kila tukio la mkusanyiko wa watu linahatarisha mali au maisha ya raia, kwa hiyo ni dhahiri pia kuwa siyo lazima kila mara kutumia nguvu zisizokuwa za lazima dhidi ya raia. Polisi wanafunzi wanapaswa kupewa elimu inayojenga taswira kuwa anaepinga serikali iliyoko madarakani siyo lazima pia awe ni adui wa Taifa au anaetishia usalama wa Taifa.

Picha inayojitokeza baada ya baadhi ya matukio ambapo polisi wameua raia ni kama vile kazi kuu ya polisi ni kuhakikisha kuwa upinzani halali wa kisiasa unaminywa kiasi cha kutosha na kuondoa kabisa uwezekano wa serikali iliyopo madarakani kuondolewa madarakani kwa njia za kidemokrasia.

Polisi wapate mafunzo kuwaelimisha kuwa kazi yao siyo kulinda maslahi ya kisiasa ya serikali iliyopo madarakani, na wafunzwe kukubali uwezekano kuwa chama chochote kilichopo upande wa upinzani kinaweza hatimaye kushinda uchaguzi na kuongoza serikali.

Jambo la pili na ambalo ni muhimu sana ni kuwa sasa waandishi wa habari wapate mafunzo ya namna ya kukusanya habari kwenye maeneo yenye usalama mdogo ili kupunguza tishio kwa usalama na maisha yao. Polisi anafanya kazi kwa amri, na kuna mazingira mengi ya kisheria yanayomruhusu polisi kutumia silaha kwa jinsi ambavyo anaona ni sawa kutokana na mazingira yanayomkabili. Polisi anayefukuzwa na kundi la waandamanaji ambao anaamini wanakusudia kumuua hatasita kutumia silaha yake dhidi ya kundi hilo. Huu ni mfano tu; haya sidhani kama ni mazingira yaliyotokea kwenye tukio lilisobabisha kifo cha Daudi Mwangosi.

Jambo la msingi ni kuwa, hata pale ambapo tunajua tunayo haki, si busara hata kidogo kubishana na mtu ambaye ameshika silaha na anaamini kuwa anatekeleza amri halali aliyopewa na mkubwa wake. Na hili haliwezi kubadilika mpaka itolewe elimu ambayo itambadilisha polisi Mtanzania ili atumie mbinu tofauti kukabiliana na waandamanaji.

Friday, September 14, 2012

Biashara ya vyuma chakavu na ufisidi (ni ufisidi, siyo ufisadi)

Miaka kadhaa iliyopita, mafundi toka Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) walijenga mnara mdogo wa kumbukumbu kijijini Butiama, sehemu ambapo ilianguka ndege ya kivita aina ya Mig, mara baada ya kuanza vita vya Kagera mwaka 1978.

Ujenzi huo uliambatana na njia ya kupita kwa miguu iliyojengewa mabomba ya chuma kuanzia barabara kuu mpaka sehemu ilipoanguka ndege, umbali wa kama mita 100 hivi.


Manara wa kumbukumbu ilipoanguka ndege ya JWTZ, eneo la Mwitongo, Butiama. Vyuma vyote vilivyo pembeni vimenyofolewa na wachuuzi wa vyuma chakavu.
Haikupita muda mrefu, wachuuzi wa biashara ya vyuma chakavu walikata mabomba yote na kuyapeleka kwa wanunuzi wa vyuma chakavu. Mnunuzi mmoja mkku wa vyuma chakavu yuko Mwanza.

Ni hawa hawa unaweza kuwasikia wakipigia makelele kuwepo kwa ufisidi (ni ufisidi, siyo ufisadi) nchini, wakinyoosha vidole kwa baadhi ya viongozi wetu, wakati hata wao wanayoyafanya hayapishani sana na yale wanayoyakemea.

Thursday, September 13, 2012

Mada yangu ya leo: kufahamu Kiingereza siyo kuwa msomi

Mada yangu leo si ndefu sana, lakini naamini ni muhimu.

Nianze na tukio moja la zamani. Niliwahi kufahamiana na raia mmoja wa Uingereza ambaye aliishi na kufanya kazi Dar es Salaam kwenye miaka ya tisini, akiwa mwajiriwa wa kampuni moja ya ulinzi. Huyu alikuwa mtu mmoja mcheshi, na mchangamfu kwa wengi aliyefahamiana nao ingawa kwa aliyewaongoza kazini alikuwa mkali sana.

Kuna Mtanzania mwenzangu ambaye naye alikuwa akifahamiana naye na alimheshimu sana, siyo tu kama binadamu mwenzake lakini naamini kwa wadhifa wake muhimu wa kuongoza kampuni yenye wafanyakazi wengi wenye jukumu la kulinda mali na makazi ya wateja wa hiyo kampuni.

Miaka kadhaa ilipita na yule Mtanzania mwenzangu siku moja aliniambia: "Unafahamu? Kumbe yule jamaa amesoma mpaka darasa la nne tu!"

Mtanzania mwenzangu, ambaye alikuwa na shahada ya chuo kikuu, hakuamini kuwa mtu aliyemdhania ni msomi mwenzake kumbe alikuwa amesoma mapaka darasa le nne tu, pamoja na kupewa jukumu la kuongoza kampuni moja mashuhuri ya Tanzania.

Tatizo nililoliona mimi lilikuwa la lugha. Kwa kipimo cha Mtanzania mwenzangu yule Mwingereza alikuwa anazungumza Kiingereza safi kabisa kuliko ambacho yeye alikuwa anamudu kuongea na kwa mantiki aliyofikia ingekuwa ni dhahiri kuwa yule jamaa alikuwa ni msomi. Kwa sababu tu anaongea Kiingereza kizuri kuliko cha kwake.

Nilimuuliza: "Sasa utamdharau kwa sababu ya ya elimu yake, wakati wote huo ukimwona ni mtu wa maana sana?"

Haya yalitokea zaidi ya miaka 20 iliyopita lakini tatizo la kumpa mtu uzito mkubwa zaidi kwa sababu anaongea Kiingereza vizuri bado lipo mpaka leo.

Jeneral Ulimwengu achangia majadiliano ya katiba mpya

Kwa idhini ya Jenerali Ulimwengu, natoa sehemu ya mada ailiyotoa kwenye kongamano la kujadili katiba mpya lililofanyika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, tarehe 15 Januari 2012.

************************************************
Ninavyoangalia jamii ya Tanzania ilivyo sasa hivi, pamoja na mambo yote mema tuliyonayo, tumejaliwa watu wenye kuheshimiana, wenye kupendana,  kwa kiwango kikubwa. Tunaanza kuchukiana chukiana, lakini kwa sababu ya mipangilio mibaya na kujitawala vibaya. Lakini kimsingi, watu wetu ni watu wema. Watawala wao ndiyo waovu.
 
Matokeo yake ni kuwa tumejenga jamii ya watu katika kiwango ambacho kinatisha cha watu wa aina zifuatazo:-
-          Watu wasioaminika
-          Matapeli
-          Wababaishaji
-          Na wapuuzi
Sisi, pamoja na watawala wetu.
 
Watu warushaji katika mahusiano ya kibiashara kiasi kwamba hatuaminiki katika nchi jirani. Mara mafuta yamechakachuliwa; mara ukiuza pamba wameweka mawe. Ali mradi, tumekuwa sisi ni waNigeria wa eneo hili la Afrika.
 
Watu tunaoonea wanyonge. Kuwaibia masikini. Kuwapora wahanga wa ajali, na kuwaua albino kwa imani za kijinga. Washirikina tunaoamini ujinga wakati uthibitisho wa teknolojia tunao mikononi. Kwamba tunaweza ku-Google, search engine ya Google, kutafuta mchawi mahiri yuko wapi.
 
Ujuha wa kiasi hicho. Na wengine sasa wanakwenda bungeni. Watu na jamii fasta fasta. Wenye tamaa ya kupata utajiri wa haraka bila kufanya kazi. Tumekubali wito wa:
-          Kuwa mjanja!
-          Chizika!
-          Pandisha mzuka!
-          Full kujirusha!

 Ambayo yote yametujaza upuuzi wa kibambucha.

Jamii isiyopenda kujifunza. Tumevifanya vitabu ni kama wakwe zetu, tunaogopa kuvifunua wakati tunaona jinsi majirani zetu, kwa mfano, Kenya, vijana wanavyohangaika kujisomea. Ukienda Nairobi, nenda Saritz Centre, uende bookshop ile angalia jinsi wanavyosoma halafu mnaogopa Wakenya watachukuwa nafasi zetu; Wakenya watachukuwa ardhi yetu.

Bora waje Wakenya kuliko kuwa na wajinga wakaharibu nchi hii. 

Watu wakutoa majibu mepesi mepesi kwa maswali mazito. Kwa sababu hatupendi kusumbua akili zetu. Wapiga kura wanaouza kura zao kwa bakuli la kunde, na kisha kulalamika wasipopata uongozi wa kuwafanyia kazi. Watu wasiojua misingi ya haki. Wanaochoma moto mwizi wa kuku, lakini mwizi wanamchagua kumpeleka bungeni.

Kumi, kwa ufupi, watu na jamii iliyopotea.

Jamii hii haiwezi kuandika katiba. Mpaka i-address masuala haya. Mimi naamini kabisa tukienda kuandika katiba sasa hivi, nakubaliana na Issa [Prof. Issa Shivji], kwamba kama hiyo Tume ya Rais itakuwa na watu wanawakilisha makundi mbalimbali, itaanza kuzungumza na hali yenyewe tuliyo nayo ndiyo hii, yaani fanya unavyotaka, hutapata chochote cha maana kwa sababu humu ndani kutakuwa na wezi, wazandiki, matapeli, wababaishaji, wala rushwa. Kila mtu anajaribu kuweka nafasi yake mbele. Na maslahi yake mbele.

Sasa tufanye nini? Yuko Mzee Ibrahim Kaduma hapa. Natumai kuwa kitabu chake kilichozinduliwa juzi kitakuwa hapa. Ili kupambana na haya niliyoyasema, ambayo ni magonjwa makubwa, ni majanga makubwa, na ndiyo yanatawala, hebu turudi kwenye misingi.

Moja: Binadamu wote ni ndugu zangu na Afrika ni moja.
Nitatumikia nchi yangu na watu wake wote.
Nitajitolea nafsi yangu kuondoa umasikini, ujinga, maradhi, na dhuluma.
Ongeza na rushwa.
Nne: Rushwa ni adui wa haki sitapokea wala kutoa rushwa.
Cheo ni dhamana, sitatumia cheo changu wala cheo cha mtu mwingine kwa faida yangu.
Hebu niambie ni watu gani ndani ya Serikali wanaweza kusimama hadharani wakasema maneno haya?
(Hadhira: hawapo!)
Sasa tuwafanye wayaseme haya. Katika uandikaji...katika mchakato mzima wa kujadili katiba mpya, tufike mahala tuwalazimishe watu waliomo katika utawala, wasimame mbele yetu waseme hivi: Cheo ni dhamana. Sitatumia cheo changu wala cha mtu mwingine kwa manufaa yangu. Waseme! Halafu tuwapime.
Nitajielimisha kwa kadri ya uwezo wangu na kutumia elimu yangu kwa faida ya Nchi.
Nyie wasomi hapa chuoni mnasema hiyo? Au? Nasikia wanafunzi wengi sana mnasoma accountancy. Accountancy ni somo zuri lakini sasa sijui mnataka kwenda kufanya kazi wapi?
Nitashirikiana na wenzangu wote kujenga nchi yetu.
Nitasema kweli daima. Fitna kwangu mwiko.
Nitakuwa raia mwema wa Tanzania, Afrika, na Dunia nzima.

Tuyatafakari hayo. Tuwe na muafaka wa kitaifa. Tuwe na maridhiano, tuwe na makubaliano. Tuwe na national charter,  kutokana na hilo sasa ndiyo twende na michakato mingine aliyosema Shivji [Prof. Issa Shivji] ya kujenga misingi ya maelewano nchini na kuandika katiba mpya itakayotuongoza kwa miaka hamsini au mia ijayo. Nawashukuruni sana.