Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Showing posts with label michezo. Show all posts
Showing posts with label michezo. Show all posts

Saturday, September 2, 2017

Hivi Mwalimu Nyerere alikuwa Yanga au Simba?

Hivi Mwalimu Nyerere alikuwa Yanga au Simba? Hili ni swali ambalo nimewahi kuulizwa sehemu ambayo sikutarajia kabisa kuulizwa.

Mwaka 2012, nikiwa kwenye moja ya misafara yangu ya kukwea Mlima Kilimanjaro nikiongozana na walimu na wanafunzi wa Shule ya Sekondari ya Wasichana ya Loreto ya Mwanza, nilipokea simu wakati tukitembea kati ya kambi ya Horombo na kambi ya Kibo.

Aliyenipigia simu alijitambulisha akisema mimi hununua vocha za simu kwenye kibanda chake mjini Musoma.

Alinisimulia kuwa alikuwa anabishana na wenzake, baadhi yao wakisema Mwalimu Nyerere alikuwa mwanachama wa Yanga, wengine wakipinga na kusema siyo kweli. Akaniomba mimi nimalize ubishi wao.

Kwanza, ingawa nilikuwa kwenye njia ya Marangu kuelekea kwenye kilele cha Mlima Kilimanjaro, njia ambayo inasemekana kuwa ni moja ya njia rahisi za kufika kileleni, ukweaji Mlima Kilimanjaro wakati wote unampa mtu changamoto za kila aina.

Mawasiliano ya simu za kiganja huwa ni ya kubahatisha kutegemea na sehemu ulipo na kutegemea na hali ya hewa. Mlimani kwenyewe pumzi inavutika kwa kutumia nguvu na jitihada ya ziada. Aidha, kwa sababu ya baridi chaji ya betri ya simu haikai kwa muda mrefu.

Kwa sababu hizo, unapopigiwa simu, unategemea itahusiana na suala la dharura au linalohusiana na kazi au suala lingine la aina hiyo.

Lakini nilielewa kuwa, kwa aliyenipigia simu, kufahamu kama Mwalimu Nyerere alikuwa mwanachama wa Yanga au la ilikuwa muhimu kwake kwa wakati ule.

Nilimwambia kuwa hata mimi husikia kuwa Mwalimu Nyerere alikuwa mwanachama wa Yanga, na wakati fulani wazee wa Yanga walitembelea Butiama nikawauliza swali hilo lakini kwa wakati ule aliponiuliza sikukumbuka walinijibu nini.

Ninachokumbuka ni kusikia mtu akisema kuwa kadi namba 1 ya Dar es Salaam Young Africans huwa haijulikani kapewa nani, na ndiyo hiyo watu wanasema ilikuwa kadi ya Mwalimu Nyerere.

Mwalimu Nyerere mwenyewe aliposimulia kuhusu kuhudhuria mechi za soka alisema ilikuwa muhimu kuwa asikae mtu mbele yake, kwa sababu kila wakati mchezaji alipokaribia kufunga goli naye alikuwa akirusha mguu mbele kupiga mpira hewa.

Bofya kwenye picha hapo chini kusoma taarifa juu ya mechi chache za mpira ambazo Mwalimu Nyerere alihudhuria:
Mwaka 1972, Rais Jaffar El Nimeiry wa Sudan akisalimiana na wachezaji wa Taifa Stars kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, kwenye mechi ya soka dhidi ya timu ya taifa ya Sudan.
Taarifa nyingine kama hii:
http://muhunda.blogspot.com/2013/07/simba-sports-club-wakaribishwa-butiama.html

Friday, December 12, 2014

Mabondia na unga (sehemu ya tatu ya awamu tatu)

Promota wa ndondi za kulipwa, Ibrahim Kamwe, anaeleza kwa nini baadhi ya mabondia wanajiingiza kwenye biashara ya madawa ya kulevya.
Ibrahim Kamwe
Ukiangalia umbumbumbu na maskini tulionao mabondia, hapo wajanja wenye pesa zao, wafanyabiashara, na baadhi ya viongozi wanatumia udhaifu tulionao mabondia kutuhadaa kwa kutupatia safari za nje za kimichezo au matembezi ya kwenda kufanya mazoezi ughaibuni na hatimaye kutubebesha mihadarati (madawa ya kulevya) bila kujua kwa kutuwekea katika mizigo tunayosafiri nayo. Wakati mwingine kuna baadhi ya wafanya biashara hao wenye pesa zao hukuweka wazi wakati unaenda pigana umbebee mzigo wake na atakulipa pesa nyingi. Hapo ndipo tunapobanwa ukiangalia nyumbani tunalalia telemka tukaze, tunashindia tembele mlo mmoja, msosi wa kengele tena kwa masimango, mfukoni huna kitu na wala huna kazi itakayokupatia pesa ya kula kwa wakati huo. Hapo sijaingiza mambo ya kodi, na demu wangu namlinda vipi.

Hii njaa na umaskini tulio nao mabondia ndiyo inawapa nguvu vigogo kututumia kwa kutubebesha madawa ya kulevya kusafirisha nje wakijua wazi hatuwezi kataa kutokana na dhiki tuliyo nayo. Tutakubali tu kwani hakuna apendae kulala njaa, kulala pachafu, au kuvaa midabwada.

“Siwezi acha dili la pesa kama hili wakati jina langu kubwa kila kona linatajwa mitaani na vyombo vya habari lakini mimi binafsi nauli ya daladala sina. Siku ya tatu leo nakula mlo mmoja kwa siku, watoto hawapo katika hali nzuri, mazoezi yenyewe sifanyi kwa raha nafikiria nitapata wapi mshiko. Leo unaniletea ishu ya pesa niikatae si nitakuwa kichaa?”


“Wadau wenzangu wa ngumi ,wapambe wao, na walio karibu na sisi mabondia wana nguo za bei kubwa wanapendeza, wana magari. Ukiangalia mimi bondia ndiye mtendaji wao mkuu nipo ovyo sina kitu mfukoni wala tumboni, madeni kibao yaani majanga matupu.”

Ushauri wangu kwa serikali au taasisi zinazohusika na wanaolichukia jambo hili kiukweli - maana wengine hujifanya kulichukia mdomoni pembeni ndiyo watendaji wakuu wa kuwatumia wanamichezo au wasanii kwa faida zao - mabondia au wanamichezo tuboreshewe maeneo yetu ya michezo ikiwemo katika vilabu vyetu na maeneo ya mazoezi, na vifaa viongezwe. Ikiwezekana kodi ya vifaa vya michezo ipunguzwe ili viwe vingi nchini mabondia wasibabaike na vya kuazima au kuangalia katika TV vifaa vya wenzetu.


Serikali iwajali mabondia, isaidie kudhamini semina za walimu wa ngumi ili wawaongoze vyema vijana wao. Magym ya makusudi yajengwe na maeneo ya wazi wasigawane wenye pesa na viongozi kwa faida zao. Wajenge sehemu za michezo ya ndani, na kama pia itatumika njia ya kutoa madarasa matupu katika mashule yetu kwa ajili ya kutuachia sehemu ya mazoezi ya jioni itasaidia sana kukuza mchezo na walimu wenye taaluma kufundisha vizuri kuliko mabondia kufundishana vichochoroni na kutokuwa na nidhamu ya mchezo wala maisha.

Sunday, December 7, 2014

Mabondia na unga (sehemu ya pili ya awamu tatu)

Promota wa ndondi za kulipwa, Ibrahim Kamwe, anaeleza kwa nini baadhi ya mabondia wanajiingiza kwenye biashara ya madawa ya kulevya.
Siku za hivi karibuni kuna vimaendeleo kidogo kwa baadhi ya mabondia; tunafanya mazoezi katika vilabu vya pombe kwa kuwalipa kodi ya mazoezi wenye baa. Naweza kusema Tanzania hakuna sehemu rasmi za kufanyia mazoezi ya ndani zilizotengwa na serikali kwa ajili ya raia wake wapenda michezo na kama zipo ni chache na ziko katika makambi ya jeshi kwa masharti magumu kwa raia wa kawaida. 

Siku za nyuma wakazi wa mjini kama vile Kisutu, Gerezani na Kariakoo walikuwa wanafanya mazoezi pale Arnatoglou. Siku hizi huwezi kusikia kuna mwanamichezo katokea Gerezani au Kariakoo. Iliyobaki kwao ni kuuza na kutumia madawa ya kulevya na kukimbizana na wafanyabiashara wa maeneo hayo. Naweza kuilaumu serikali kwa kutoendeleza michezo bali ilishiriki kuuwa kabisa michezo maeneo hayo na mengineyo zaidi.

Kwa sisi tulioanza kukua kimichezo pambano la ngumi likiandaliwa huwa tunalipwa kuanzia shilingi 5,000/- mpaka 20,000/- kwa mapambano haya madogomadogo na iwapo kutakuwa na pambano kubwa na kupata bahati ya kucheza unaweza kulipwa shilingi 40,000/- mpaka 100,000/-. Mapambano makubwa yanaweza kuwa moja, mawili, au matatu kwa mwaka; hayazidi hapo. Haya mapambano madogo tunaweza pata mawili mpaka sita kwa mwaka.

Msiwaone mabondia wakicheza mkadhani wana kipato kikubwa. La hasha! Ni wale tu wachache waliobahatika kupata wadhamini au waratibu wenye uwezo wa kipesa ndiyo kidogo hutoka.

Kwa sisi wengine ukiangalia elimu ya kusoma hatuna, kazi hakuna, na mchezo wa ngumi tunaupenda na pengine tuna vipaji na kufanya vizuri katika mapambano yetu. Hivyo mchezo ndiyo huwa kama ajira yetu kwa sababu tunapata chochote kidogo kupitia mchezo huo kuliko kuiba au kukimbizana na mapolisi katika kamari na kuishia jela.

Kwetu sisi mabondia huona ni jambo la kifahari na hufurahi mno pale tu tunapopata pambano la nje ya nchi na hufurahia kupanda ndege na vile vimisosimisosi tunavyopata tukiwa mahotelini ugenini. Tukihadithiana mambo ya safari uswahilini kwetu tunahisi tunakosa mambo mengi ya raha.

Hapo ndipo mawakala wa ngumi hutupata na mabondia huwa wanadiriki kukubali kwenda kucheza popote tukijua tutapanda ndege, tunakula raha bila kujali  na wala kuhoji tuendako tutalipwa kiasi gani cha pambano nitakalocheza wala kujua usalama wangu.


(itaendelea na sehemu ya tatu)

Tuesday, November 25, 2014

Mabondia na unga (sehemu ya kwanza ya awamu tatu)

Promota wa ndondi za kulipwa, Ibrahim Kamwe, anaeleza kwa nini baadhi ya mabondia wanajiingiza kwenye biashara ya madawa ya kulevya.
Ibrahim Kamwe
Asili ya mabondia wengi  duniani wanatoka katika familia duni. Kwa mfano hapa kwetu ni nadra kumkuta bondia ametoka Upanga, Oysterbay, au Masaki ushuwani, nikiwa na maana  mabondia wengi wanatoka uswahilini. Ni watu wa hali duni. Wengi wetu hatujakalia madawati ya shule na wengine tuliojitahidi tumefika darasa la tano au sita. Kama wazazi walikomaa ndiyo tunamaliza la saba.

Baadhi yetu tukiwa na umri wa kuanzia miaka sita nyumbani huwa tunaanza kupewa uzowefu wa kuuza visheti, maandazi, vitumbua, karanga n.k. na vikibaki nyumbani hauli chakula mpaka viishe. Shuleni mwalimu mkali, darasani hafundishi mpaka usome tuisheni ndiyo unapata kufundishwa kidogo, na ukishindwa maswali yake unapata viboko vya ghadhabu. Hapo ndipo tunapoamua kuachana na shule na kutinga mitaani. Michezo yetu ni katika madampo na vichochoroni na tukifikia umri wa kuanzia miaka 12 na kuendelea tunajua jinsi ya kutafuta pesa kwa kuuza njiwa, kucheza kamari, malani, kuiba kuku na bata, na kwa wale walio watukutu zaidi kuuza na kuvuta bangi ni sehemu ya maisha ya kawaida tu huku mitaani kwetu.

Mara nyingi mlo kwetu ni mmoja tu kiubishoo au kuwa wageni ndiyo tunakula milo miwili. Katika maisha yetu muda mwingi tupo huru na michezo kuliko kusoma, hasa kolokolo, ngoma, mpira, na ngumi. Mpira tunacheza mabarabarani, vichochoroni, na kwenye madampo, wakati ngumi tunajifundisha katika makamali, vichochoroni, au uwani kwa kina masta. Begi au tairi linafungwa juu ya mti, tizi linaendelea bila vifanyio vya mazoezi vilivyo rasmi. Mwendo mdundo tunasonga na tunashinda au kufanya vizuri katika mashindano yetu tunayoshiriki na hali yetu duni hii hii ya kimaisha, na majina yetu kutangazwa sana katika vyombo vya habari na kupata umaarufu mkubwa nchini, nchi jirani na hata nchi za Ulaya.

Lakini ukibahatika kututembelea na kuangalia tunapoishi na familia zetu na umaarufu tuliyonao, utakuta maisha yetu mabovu na yanasikitisha.

(itaendelea na sehemu ya pili)

sehemu ya pili ya makala hii

Sunday, July 14, 2013

Mzee Mwinyi alisema kila enzi na kitabu chake?

Alisemaje Mzee Ali Hassan Mwinyi, rais mstaafu wa Tanzania? Kila enzi na kitabu chake?

Sikumbuki vizuri lakini enzi za uongozi wake alitamka maneno yanayofanana na hayo akimaanisha kila rika linafikiwa na matukio au mitazamo ambayo, kwa muda, inachukua umuhimu fulani katika jamii. Halafu baada ya muda yanakuja mengine na yale ya mwanzo yanapoteza umuhimu.
Hili basi la abiria (kwenye picha) lina rangi za timu ya soka ya Uingereza, Manchester United. Na upande wa mbele limeandikwa "Manchester United". Bila shaka mmiliki ni shabiki wa timu hiyo mashuhuri. Linafanya safari zake kati ya Musoma na Bunda.

Nyuma ya basi kuna picha ya mchezaji ambaye sifahamu ni nani na wala simfananishi na mchezaji yeyote mashuhuri ambaye ninamfahamu. Bila shaka wenye enzi zao wanamtambua.

Mimi ingewekwa picha ya Mbaraka Mwinshehe ningemtambua.

Wednesday, February 13, 2013

Francis Cheka kutetea ubingwa wa Afrika dhidi ya Thomas Mashali Mei Mosi


Taarifa kwa vyombo vya habari toka Shirikisho la Ngumi la Kimataifa Afrika (IBF/Africa) linaarifu kuidhinishwa kwa pambano la utetezi la ubingwa wa IBF Africa unaoashikiliwa na Mtanzania Francis Cheka. Habari kamili hizi hapa:
********************************************
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
FEBRUARY 13, 2013
   Francis Cheka (kushoto) akiwa na Adam Tanaka (katikatia) na Thomas Mashali (kulia)
Shirikisho la Ngumi la Kimataifa Afrika (IBF/Africa) limetoa kibali kwa bondia Francis Cheka ambaye ni bingwa wa Afrika katika uzito wa Super Middle kutetea ubingwa wake dhidi ya bondia Thomas Mashali wa Tanzania. 

Mabondia hao wawili leo tarehe 13 February walikutana katika hoteli ya Ndekha, iliyoko Magomeni Kondoa na kutia sahihi mkataba wa kupigana pambano hilo ambalo limepangwa kufanyika siku ya Mei Mosi katika ukumbi wa PTA jijini Dar es Salaam.

Thomas Mashali ambaye ndiye bingwa wa Afrika ya Mashariki na Kati (ECAPBF) katika uzito wa Middle ana kiwango kizuri cha kushindana na Francis Cheka katika pambalo hilo.

Hii itakuwa mara ya pili kwa bondia Francis Cheka kutetea mkanda alioushinda tarehe 29 April 2012 dhidi ya bondia machachari Mada Maugo wa Tanzania. Cheka aliutetea vyema mkanda wa ubingwa wa IBF/Afrika dhidi ya bondia Chiotcha Chimwemwe ambaye ni Afisa katika jeshi la Malawi siku ya Boxing Day (26 Decewmber 2012) katika jiji la Arusha.

Kama Francis Cheka atashinda tena pambano hili, atapewa nafasi ya kupigana kugombea mkanda wa IBF wa mabara (IBF I/C) .

Pambano hili linaandaliwa na kampuni ya Mumask Investment and Gebby Pressure ya jijini Dar es Salaam chini ya uratibu wa Adam Tanaka.

Imetumwa na:

UONGOZI
Shirikisho la Ngumi la Kimataifa Africa (IBF/Africa)
Dar-Es-Salaam, Tanzania 

Taarifa nyingine inayohusiana na hii
http://muhunda.blogspot.com/2012/05/ngowi-kusamamia-pambano-la-ubingwa-wa.html

Friday, February 8, 2013

Mtanzania apata nafasi ya kugombea ubingwa wa Dunia IBF



TAARIFA KWA UMMA
FEBRUARY 6, 2013
DAR-ES-SALAAM, TANZANIA

Bingwa wa IBF katika bara la Afrika uzito wa unyoya (Featherweight) Ramadhani Shauri amepewa nafasi ya kugombea ubingwa wa dunia wa IBF kwa vijana walio chini ya miaka 25 katika uzito wa Lightweight. Shauri ambaye alishinda taji la ubingwa wa IBF katika bara la Afrika mwaka jana baada ya kumpiga bondia Sunday Kizito wa Uganda ana rekodi ya mapambano 17.


IBF imeamua kumpatia Shauri nafasi ya kugombea ubingwa huo wa dunia kwa vijana baada ya kuangalia mkanda wa video wa pambano lake la ubingwa wa Afrika na kuridhika kuwa anaweza kushindania ubingwa huo wa vijana,

Mabondia wengi wa Marekani ambao walikuja kuwa mabingwa wa dunia na kuweza kupata pesa nyingi walianza kuwa mabingwa wa dunia kwa vijana na hivyo kuweza kupanda chati kwenye viwango vya IBF. Mbondia hao ni kama Bernard Hopkins, Floyd Mayweather na Oscar De la Hoya.
Ramadhani shauri akiwa na mkanda wa ubingwa wa IBF Afrika.
Kama Shauri atashinda na kuwa bingwa wa dunia upande wa vijana atakuwa kwenye macho ya mapromota wakubwa duniani kama kina Dong King, Bob Arum na wengine wengi. Nafasi kama hii inaipa nchi ya Tanzania nafasi nzuri sana ya kujitangaza kibiashara na utalii kwani dunia inaiona kuwa kati ya nchi zinazotoa mabingwa wa dunia.

Kama Shauri atashinda taji hili atakuwa Mtanzania wa kwanza tangu historia ya ngumi nchini kuweza kushinda taji la shirikisho kubwa kati ya manne duniani ambayo ni IBF, WBA, WBO na WBA.

Shirikisho la Ngumi la Kimatafia Afrika (IBF/Africa) ambalo lina makao yake makuu ya kuhudumia bara la Afrika, Ghuba ya Uajemi na Mashariki ya Kati ndilo lililomtafutia Shauri nafasi aliyopata.

IBF/Africa inawahamasisha Watanzania walio na mapenzi mema na nchi yao pamoja na makampuni mbalimbali binafsi ya umma yajitokeze kwa wingi kumpatia Shauri ufadhili wa kuweza kuligombea taji hili.
Mungu mbariki bondia Ramadhani Shauri, Mungu ibariki Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Amen.

Imetolewa na:
UTAWALA
Shiriklisho la Ngumi la Kimataifa Afrika (IBF/Africa)
Dar-Es-Salaam, Tanzania

Sunday, January 27, 2013

Kwenye soka huwa nashangilia wanyonge siku zote


Makala hii niliandika zaidi ya miaka mitatu iliyopita kwenye blogu yangu ya lugha ya Kiingereza. Nairudia hapa kwa wale ambao hawakupata fursa kuisoma wakati huo, tarehe 30 Juni 2009. Nimekosa kuangalia mapambano ya Kombe la Mataifa ya Afrika yanayoendelea sasa hivi nchini afrika Kusini lakini ningekuwa nafuatilia mashindano hayo ningekuwa nawapigia debe wanyonge, timu ambayo hakuna shabiki anatarajia itashinda.
*********************************************
Mimi siku zote hushangilia wanyonge, hususani kwenye michezo. Kwa hiyo nilifurahishwa Jumapili iliyopita nilipowasha televisheni na kushuhudia hali isiyo ya kawaida ambapo timu ya taifa ya Marekani ikiwa inaongoza kwa goli moja bila majibu na, kabla ya kipenga cha nusu ya kwanza kusikika, ikiongoza kwa magoli mawili dhidi ya miamba ya soka Brazil kwenye pambano la fainali za mabara la FIFA nchini Afrika ya Kusini.

Katika ulimwengu wa soka Brazil inatisha, ni taifa kubwa wakati Marekani ni bwana wadogo. Katika lugha ya vita na silaha Brazil ni mzinga wa upana wa milimita 130 wakati Marekani ni kama bastola ndogo isiyojaza hata mfuko wa shati. Kwa hiyo si ajabu kumsikia kocha wa Marekani Bob Bradely akisema baada ya timu yake kushindwa: "Ni matarajio yangu kuwa watu katika sehemu mbalimbali duniani wataona kuwa tunayo timu na wachezaji wazuri. Ni hatua kubwa kwetu."
Timu ya Taifa ya Brazil iliyoshinda Kombe la Dunia mwaka 1970 nchini Mexico.
Timu nilizozishabikia kwenye mashindano zilikuwa mlolongo wa timu zilizoorodheshwa na FIFA kwa ubora lakini orodha ile ikiwa imewekwa kichwa chini miguu juu, yaani zile za mwisho ndiyo nilipendelea zaidi zishinde.

Katika kipindi cha pili Brazil walisawazisha mabao yote mawili na kuongeza bao la tatu la ushindi ambalo lilikuwa uthibitisho kuwa Brazil itabaki inatawala ulimwengu wa soka, angalau kwa sasa.

Habari njema kwa timu nyingine ambazo zitapambana na Brazil kwenye Kombe la Dunia la FIFA mwakani nchini Afrika ya Kusini ni kuwa bingwa wa FIFA wa mabara - ambapo mabingwa wa mabara wanapambana dhidi yao - hajawahi kutwaa ubingwa wa dunia mwaka unaofuata.

Taarifa zinazohusiana na hii:
http://muhunda.blogspot.com/2010/07/mada-yangu-ya-leo-ni-nani-ataibuka.html
http://muhunda.blogspot.com/2010/06/hii-kali.html

Monday, January 7, 2013

Miraji Mrisho Kikwete ateuliwa Makamu wa Rais wa IBF/Afrika Maendeleo ya Vijana

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
JANUARY 6, 2012

Shirikisho la Ngumi la Kimataifa Afrika (IBF/Africa) limemteua Bw. Miraji Mrisho Kikwete kuwa Makamu wa Rais anayeshughulikia maendeleo ya vijana katika bara la Afrika, Ghuba ya Uajemi na Mashariki ya Kati. Uteuzi wa Miraji unaanza January mwaka mpya 2013.

Katika kumteua Miraji,  Rais wa IBF katika bara la Afrika, Ghuba ya Uajemi na Mashariki ya Kati Bw.  Onesmo Ngowi alisema kuwa Miraji ana uwezo wa kuwahamasisha na kuwaunganisha vijana katika shughuli za maendeleo.

Aliendelea kusema kuwa Miraji atakuwa anawahamasisha vijana, kuwaunganisha, kuwajengea uwezo wa kimaendeleo yatakayoratibiwa na IBF.

Aidha, Rais huyo alisema kuwa Miraji atakuwa anabuni njia mbalimbali za kuwaunganisha vijana wa Afrika, Ghuba ya Uajemi na Mashariki ya Kati ili waweze kufaidika na miradi ya IBF ambayo inalenga kwenye elimu, kujenga vipaji pamoja na kuwaunganisha kwenye biashara ya utalii wa michezo.

Katika mkutano wake wa mwaka uliofanyika katika jiji la Honolulu, jimbo la Hawaii, nchini Marekani hivi karibuni IBF iliupokea mradi wa “Utalii wa Michezo” uliobuniwa na kuwakilishwa na Rais wa IBF katika bara la Afrika, Ghuba ya Uajemi na Mashariki ya Kati Mtazania Onesmo Ngowi.

Lengo kuu la mradi huo ni kulifanya bara la Afrika, hususan Tanzania, kuwa kitovu kikuu cha “Utalii Michezo” hivyo kujenga uchumi imara. Nchi za Tanzania na Ghana ziliteuliwa kuwa nchi za mfano kwenye mradi huo.

Katika mradi huo, IBF itatumia mtandao ilionao katika nchi zaidi ya 203 duniani kuhamasisha wanachama wake na famlia zao, wapenzi pamoja na marafiki zao kuja Afrika/Tanzania kutalii pamoja na kuwekeza katika miradi mbalimbali.

Uteuzi wa Miraji utasaidia kuwaunganisha vijana ili waweze kuchangia na kufaidika na biashara ya utalii kwenye mradi huo na umefanywa wakati muafaka.

Miraji ambaye ni mjasiriamali amejipambanua katika maendeleo ya jamii na ana mchango mkubwa sana katika kuendeleza vijana nchini Tanzania.

Rais Ngowi alimwelezea Miraji kama tegemeo ambalo vijana wanalihitaji kwani wanahitaji uhamasishaji wa hali ya juu na Miraji ana uwezo wa kufanya kazi hiyo kwa ufanisi mkubwa kwani alishawahi kuifanya kwa kipindi kirefu.

Miraji Mrisho Kikwete ni msomi wa Chuo Kikuu cha nchini Oman ambako amesomea elimu ya utawala wa biashara ambayo ndiyo lengo kuu la uteuzi wake. Ana haiba ya kupendwa na vijana pamoja na uwezo wa kujichanganya nao.

Imetolewa na:


Makao makuu
IBF Afrika, Ghuba ya Uajemi na Mashariki ya Kati
Dar-Es-Salaam, Tanzania

Thursday, December 20, 2012

Bondia Fadhili Majia kupambana kwenye mchujo wa kuwania ubingwa wa mkanda wa Jumuiya ya Madola


Taarifa kutoka kwa Onesmo Ngowi, Mkurugenzi wa Bodi ya Baraza la Ngumi la Jumuiya ya Madola (CBC), inaarifu kuwa bondia Fadhili Majia amepewa nafasi ya kupambana na bondia wa Ghana Isaac Quaye katika mpambano utakaoamua bondia atakayepata fursa ya kugombea mkanda wa Jumuiya ya Madola kwenye uzito wa Flyweight.

Taarifa kamili hii hapa:

Bodi ya Wakurugenzi ya Baraza la Ngumi la Jumuiya ya Madola (CBC) imepiga kura kumruhusu bondia wa Tanzania Fadhili Majia apambane na bondia Isaac Quaye wa Ghana katika mchujo (Elimination) wa kutafuta mpinzani atakayekutana na bingwa wa mkanda wa Jumuiya ya Madola katika uzito wa Flyweight Kevin Satchell wa Uingereza. Mpambano wa Fadhili Majia na Isaac Quaye utafanyika jijini Accra, Ghana tarehe 22, Februari 2013.

Rais wa Kamisheni ya Ngumi za Kulipwa Tanzania (TPBC) Onesmo Ngowi ni mmoja wa wakurugenzi wa bodi ya Baraza la Ngumi la Jumuiya ya Madola na alikuwa wa kwanza kumpigia bondia Fadhili Majia kura ili acheze na Quaye.

Hii itakuwa mara ya kwanza kwa bondia Fadhili Majia kugombea mkanda wa Jumuiya ya Madola ambayo inaziunganisha nchi zote zilizokuwa zinatawaliwa na himaya ya Uingereza.

Wakati huo huo Bodi ya Wakurugenzi ya Baraza la Ngumi la Jumuiya ya Madola imepitisha azimio la kuruhusu ubingwa wa baraza hilo katika bara la Afrika. Ubingwa huo utakuwa unajulikana kama “CBC Africa Zone” na tayari wapo mabondia kadhaa wa nchi za Afrika ya Magharibi ambao wameshandaa mapambano mwakani.

Napenda kuwahamasisha mapromota wa Kitanzania kuchangamkia fursa hizi adimu na kuandaa mapambano ya ubingwa wa "CBC Africa Zone" kwa manufaa ya mabondia wetu.

TPBC imejiandaa kuwatafutia mabondia wa Kitanzania mapambano mengi ya nje ili waweze kujijenga kimchezo na pia kuweza kupata kipato kizuri.

Imetumwa na mimi:

Onesmo Ngowi
Rais, Kamisheni ya Ngumi za Kulipwa Nchini (TPBC)
Mkurugenzi wa Bodi ya Baraza la Ngumi la Jumuiya ya Madola (CBC)

Bondia Fadhili Majia kupambana kwenye mchujo wa kuwania ubingwa wa mkanda wa Jumuiya ya Madola


Taarifa kutoka kwa Onesmo Ngowi, Mkurugenzi wa Bodi ya Baraza la Ngumi la Jumuiya ya Madola (CBC), inaarifu kuwa bondia Fadhili Majia amepewa nafasi ya kupambana na bondia wa Ghana Isaac Quaye katika mpambano utakaoamua bondia atakayepata fursa ya kugombea mkanda wa Jumuiya ya Madola kwenye uzito wa Flyweight.

Taarifa kamili hii hapa:

Bodi ya Wakurugenzi ya Baraza la Ngumi la Jumuiya ya Madola (CBC) imepiga kura kumruhusu bondia wa Tanzania Fadhili Majia apambane na bondia Isaac Quaye wa Ghana katika mchujo (Elimination) wa kutafuta mpinzani atakayekutana na bingwa wa mkanda wa Jumuiya ya Madola katika uzito wa Flyweight Kevin Satchell wa Uingereza. Mpambano wa Fadhili Majia na Isaac Quaye utafanyika jijini Accra, Ghana tarehe 22, Februari 2013.

Rais wa Kamisheni ya Ngumi za Kulipwa Tanzania (TPBC) Onesmo Ngowi ni mmoja wa wakurugenzi wa bodi ya Baraza la Ngumi la Jumuiya ya Madola na alikuwa wa kwanza kumpigia bondia Fadhili Majia kura ili acheze na Quaye.

Hii itakuwa mara ya kwanza kwa bondia Fadhili Majia kugombea mkanda wa Jumuiya ya Madola ambayo inaziunganisha nchi zote zilizokuwa zinatawaliwa na himaya ya Uingereza.

Wakati huo huo Bodi ya Wakurugenzi ya Baraza la Ngumi la Jumuiya ya Madola imepitisha azimio la kuruhusu ubingwa wa baraza hilo katika bara la Afrika. Ubingwa huo utakuwa unajulikana kama “CBC Africa Zone” na tayari wapo mabondia kadhaa wa nchi za Afrika ya Magharibi ambao wameshandaa mapambano mwakani.

Napenda kuwahamasisha mapromota wa Kitanzania kuchangamkia fursa hizi adimu na kuandaa mapambano ya ubingwa wa "CBC Africa Zone" kwa manufaa ya mabondia wetu.

TPBC imejiandaa kuwatafutia mabondia wa Kitanzania mapambano mengi ya nje ili waweze kujijenga kimchezo na pia kuweza kupata kipato kizuri.

Imetumwa na mimi:

Onesmo Ngowi
Rais, Kamisheni ya Ngumi za Kulipwa Nchini (TPBC)
Mkurugenzi wa Bodi ya Baraza la Ngumi la Jumuiya ya Madola (CBC)

Friday, December 14, 2012

Francis Cheka avuliwa ubingwa wa mabara wa IBF

Kwa mujibu wa taarifa ya Rais wa  International Boxing Federation (IBF), bondia Francis Cheka ambaye alitwaa unbingwa wa mabara wa IBF wa uzito wa middleweight tarehe 28 Aprili 2012 baada ya kumshinda bondia Mada Maugo, amevuliwa ubingwa huo baada ya kushiriki kwenye pambano ambalo halikupata idhini ya IBF.

Pambano lililomvua ubingwa Cheka ni aliloshiriki dhidi ya Karama Nyilawila tarehe 29 Septemba 2012.
Francis Cheka alipotwaa ubingwa wa mabara wa IBF, tarehe 28 Aprili 2012.
Taarifa fupi ya Lindsay Tucker, ambaye ni mwenyekiti wa ubingwa wa IBF/USBA imeeleza kuwa kutokana na kanuni 5.H iwapo bingwa anashiriki katika pambano ambalo halijaidhinishwa na IBF katika uzito wake, basi ubingwa wake utatangazwa kuwa wazi pasipo kuzingatia iwapo bingwa huyo ameshinda au ameshindwa hilo pambano.

Sunday, September 23, 2012

Pambano la ndondi Oktoba 14 kumuenzi Mwalimu Nyerere

Mabingwa wa uzito wa kati (kilo 72.5) wa Uganda na Tanzania wanaotambuliwa na Tanzania Professional Boxing Organization (TPBO) watapambana tarehe 14 Oktoba mwaka huu Friends Corner Bar, Manzese, Dar es Salaam katika pambano lilioandaliwa kumuenzi Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, aliyefariki zaidi ya miaka 12 iliyopita.

Pambano hilo litawapambanisha bingwa wa Tanzania Thomas Mashali, juu, na bingwa wa Uganda, Med Sebyala, chini.


Mchezo huo utakuwa wa kuwania ubingwa wa Afrika Mashariki.

Bondia Sebyala ameshawahi kupambana na kushindwa kwa pointi na bondia Francis Cheka, bingwa wa mabara wa Afrika anayetambuliwa na International Boxing Federation (IBF). Aidha, ameshawahi kupambana na Rashidi Matumla na ingawa mapambano yote alishindwa kwa pointi, alitoa upinzani mkali kwa mabondia hao Watanzania.

Bondia Mashali anayo sifa ya kutoa vichapo vikali kwa wapinzani wake na kuwapumzisha kwa knock-out za mapema.

Taarifa kutoka TPBO zinaeleza kuwa kwa kumuenzi Mwalimu Nyerere na kuthamini juhudi zake za kuendeleza michezo TPBO itaandaa mapambano ya ngumi kwenye kila maadhimisho ya kifo chake tarehe 14 Oktoba.

Friday, July 20, 2012

Mtanzania Ramadhani Shauri kupambana na Mganda Sande Kizito kuwania ubingwa wa mabara wa IBF Afrika

Mtanzania Ramadhani Shauri atapanda ulingoni siku ya Idd pili kupambana na bondia Sande Kizito kutoka Uganda kugombea mkanda wa IBF katika bara la Africa katika uzito wa unyoja (Featherweight).

Shauri anayefanya mazoezi yake Ubungo, Dar es Salaam, maeneo ya Mabibo na anafundishwa na kocha Mzazi anayetamba kuwa na mabondia wenye nidhamu na vipaji vya hali ya juu.

Ramadhani Shauri ni bondia chipukizi mwenye umri wa miaka 19 na historia yake ya ngumi inafurahisha kila anayeisoma na kuisikia. Ana haiba nzuri inayovutia na anafananishwa na bondia Sugar Ray Leonard wa Marekani kutokana na haiba yake na upiganaji wake.
Ramadhani Shauri, katikati, akiwa ameshika mkanda atakaoupigania dhidi ya bondia Sande Kizito. Kulia ni promota wa pambano, Lucas Rutainurwa na kushoto ni mwandishi wa blogu hii na ambaye pia ni Makamu wa Rais wa Kamisheni ya Ngumi za Kulipwa Tanzania (TPBC), Madaraka Nyerere.
Sugar Ray Leonard alitamba katika miaka ya 70 na 80. Shauri ni Mfalme anayekuja na hivi sasa anatishia maisha ya mabondia wengi katika bara la Afrika.

Ramadhani Shauri ana nidhamu ya hali ya juu na maisha yake katika ngumi yanafurahisha kwa jinsi anavyoishi kwa nidhamu na kufanya mazoezi ya kujijenga katika ngumi. Katika maisha yake anajiepusha sana na matatizo ambayo vijana wengi wametumbukia kama vile uvutaji wa bangi, ngono zembe na mambo mengine yasiyo na malengo katika maisha.

Huyu ndiye kweli Mfalme anayekuja katika ngumi za kulipwa na nchi yetu imepata bahati kubwa sana kuwa na kipaji cha bondia kama huyu.

Mpambano wa Shauri umepewa jina la “The Rumble in the City of Heaven’s Peace” (Vurumai katika Jiji la Amani).

Thursday, June 14, 2012

Francis Cheka kupambana na Joseph Kaseba siku ya Saba Saba

Bingwa wa IBF wa Afrika wa uzito wa Super Middleweight, Francis Cheka, ataingia ulingoni tarehe 7 Julai 2012 kupambana na Joseph Kaseba katika pambano linaloandaliwa na Global na kuratibiwa na Kaike
Francis Cheka, kushoto, na Joseph Kaseba, kulia.
Siraju.

Cheka alitwaa ubingwa wa mabara wa IBF afrika alipomshinda Mada Maugo katika pambano liliofanyika ukumbi wa PTA Dar es Salaam tarehe 28 Aprili 2012.

Pambano hilo litakuwa pambano la kwanza kufanyika katika uwanja mpya wa Taifa wa Dar es Salaam. Baadhi ya mapambano yatakayosindikiza pambano hilo ni pamoja na Adiphoce Mchumia dhidi ya Ramadhani Kido, Amos Mwamakula dhidi ya Rashini Ali, Mkongo Kanda Kabongo dhidi ya  Said Mbelwa, na bondia chipukizi Ibrahimu Class toka kambi ya masumbwi Ilala inayonolewa na kocha Habibi Kinyogoli atapambana na Sadiki Momba.

Picha na habari kwa hisani ya superdboxingcoach.

Sunday, June 3, 2012

Onesmo Ngowi ateuliwa kuandaa mkutano wa mwaka wa IBF 2012

Shirikisho la Ngumi la Kimataifa na Chama cha Ngumi cha Marekani (IBF/USBA) limemteua Rais wa Shirikisho hilo katika bara la Afrika, Mashariki ya Kati na Ghuba ya Uajemi,  Mtanzania Onesmo Ngowi kuwa Mwenyekiti wa Kamati ya kuandaa mkutano wa 30 wa Shirikisho hilo mwakani. Mkutano wa 30 wa IBF/USBA unatarajiwa kufanyika katika jiji la Berlin nchini Ujerumani kuanzia tarehe 24 hadi 30 Juni mwaka 2013.
Ngowi alichaguliwa na wajumbe wa mkutano mkuu wa shirikisho la IBF/USBA uliomalizika Hilton Hawaiian Village Resort, jijini Honolulu, Hawaii, Marekani tarehe 2 Juni. Uteuzi wa Ngowi unafuatia juhudi zake alizozifanya kuendeleza shirikisho hilo katika bara la Afrika tangu ateuliwe na Rais wa zamani wa IBF/USBA Robert Lee Sr. mwaka 1999 jijini New Jersey, Marekani. Onesmo Ngowi anakuwa mtu wa kwanza kutoka bara la Afrika kushika nyadhifa kubwa katika taasisi ya ngumi duniani na hii inaisaidia sana Tanzania na bara zima la Afrika kijitangaza vyema katika nyanja mbalimbali kama vile utalii na bishara.

Katika Kamati hiyo ya maandalizi kuna wajumbe sita nao ni ; Louis Priluker  wa Marekani, Roberto Rea wa Italia, Lahcen Oumghar wa Uholanzi na Roberto Ramirez wa  Mexico. Kamati hiyo itafanya shughuli zake katika kipindi cha mwaka mmoja na itakutana mara nne kwa mwaka. Sekretarieti ya Kamati ya Ngowi itakuwa katika jiji la New Jersey nchini Marekani kuliko na makao makuu ya shirikisho hilo duniani.

Mkutano huo wa Honolulu uliazimia kufanya mkutano wa IBF kwaka 2014 katika bara la Asia na mwaka 2015 IBF itafanya mkutano wake katika bara la Afrika mahali ambapo patateuliwa.

Ngowi  anawahimiza Watanzania ambao wako katika uandaaji wa mikutano kuchangamkia nafasi hii ambayo itawaleta watalii zaidi ya 1,000 nchini toka nchi zaidi ya 200 duniani. Hii ni nafasi ya nadra sana katika biashara na watanzania ni muhimu wakachangamka kama wenzao wengine katika nchi zinazokuwa wenyeji wa mikutano kama hii.

Saturday, June 2, 2012

Wadau wa IBF wakiwa Honolulu

Rais wa shirikisho la ngumi la IBF Daryl Peoples, katikati, akiwa amesimama na Rais wa IBF Afrika, Mashariki ya Kati na Ghuba ya Uajemi, Onsemo Ngowi, kulia, pamoja na promota maarufu wa ngumi za kulipwa toka Thailand, Jimmy Chaichotchuang, walipotembelea Pearl Harbour katika kisiwa cha Honolulu.

Wanahudhuria kikao cha mwaka cha IBF ambacho kinafanyika huko Honolulu na kitamalizika leo.

Sunday, May 13, 2012

Timu ya waTanzania DMV yatoka sare na Ethiopia B

Timu ya waTanzania DMV imetoka sare, bila kufungana, na timu ya Ethiopia B katika mchezo uliochezwa jana huko Burtonsville, Maryland, nchini Marekani katika ligi ya Diaspora World Cup.
Kikosi kamili cha timu ya waTanzania DMV wakiwa na mdhamini mpya wa timu hiyo, mbunifu wa mitindo ya Kwetu, Missy Temeke, akiwa na na shabiki Didi Vava, katika uwanja wa Greencastle, uliopo Burtonsville, Maryland.
Mchezaji wa timu ya Ethiopia akipambana vikali na Yousouf Godson Liuzinho, kipindi cha kwanza, katika ligi ya 2011 Diaspora World Cup kwenye kiwanja cha Greencastle, kilichopo Burtonsville, Maryland.
Wachezaji wa wa timu ya Ethiopia wakiwania freekick katika dakika ya 62 ya mchezo huo.
Didi Vava, kushoto, akiwa na Sharif Qullatein, Dogo Hudhaifa Shatry, na mmiliki wa blog ya swahilivilla Abou Shatry, wakiwa katika jukwaa la wapenzi wa timu ya waTanzania DMV.
Mdhamini wa timu ya waTanzania DMV ambaye ni mwanamitindo na mbunifu wa mitindo ya Kwetu Fashion Design, Missy Temeke, akiwa na Bendera ya Taifa.

Picha na habari kutoka kwa mwana blog Abou Shatry wa http://swahilivilla.blogspot.com/

Saturday, May 12, 2012

Timu ya Tanzania DMV kuchuana na Ethiopia (B) leo

Katika mchezo wa ligi ya 2011 Diaspora World Cup unaoendelea katika viwanja vya Hyattsville na Germantown, jijini Maryland nchini Marekani, timu ya Tanzania DMV itachuana vikali na timu ya Ethiopia leo hii Jumamosi May 12, 2012 saa 6:00 mchana katika kiwanja cha Greencastle, kilichopo Burtonsville, Maryland.
Kundi (B) Timu ya wa Ethiopia katika mchezo wa awali walifungwa mabao 3-0 na timu ya Malawi ndani ya uwanja cha Greencastle, Burtonsville, Maryland. Leo Ethiopia watajiandaa vikali ili kutaka kurudisha nguvu zao kwa mchezo waliopoteza dhidi ya timu hiyo ya Malawi, ambayo leo itapambana na Armenia saa 7:00 mchana. Katika mechi ya awali Armenia waliwabamiza Nigeria bao 4-1.

Tanzania DMV katika mchezo wa kwanza siku ya Jumapili 29 April 2012 walifanikiwa kuwabamiza Ghana mabao 3-2 ndani ya uwanja wa SoccerPlex Stadium uliyopo Ager Road Hyattsville Maryland.

Kama kawaida yao timu ya Tanzania DMV inawaomba Watanzania wote ushirikiano wenu ili kuipa changamoto timu ya Watanzania DMV. Mnaombwa pia kufika mapema saa 5:00 kuzowea mazingira kabla ya mchezo huo kuanza.

Sehemu ya mchezo utakaochezwa leo hii ni Fairland Field 3928 Greencastle Rd. Burtonsville, Maryland 20866 Habari na http://swahilivilla.blogspot.com/

Habari na picha kutoka http://swahilivilla.blogspot.com/ na Abou Shatry.

Wednesday, May 9, 2012

Bondia Selemani Kidunda afuzu kushiriki michezo ya Olimpiki ya London

Pichani, mwenyekiti wa chama cha ngumi za ridhaa Tanzania, Michael Changarawe, kushoto, akimpongeza bondia Selemani Kidunda kwa kufuzu kushiriki michezo ya Olimpiki ya London Uingereza akiiwakilisha Tanzania.

Michezo ya Olimpiki itachezwa jijini London kuanzia tarehe 27 Julai hadi 12 Agosti, 2012.

Picha na habari kwa hisani ya superboxingcoach.