Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Showing posts with label sanaa na wasanii. Show all posts
Showing posts with label sanaa na wasanii. Show all posts

Wednesday, November 20, 2013

John Kitime aelezea historia yake

Zamani, kwenye miaka ya tisini, niliwahi kumiliki gazeti lliloitwa Sanaa na Michezo ambalo lilichapisha makala kuhusu maisha ya mwanamuziki John Kitime, ambaye sasa hivi yuko na Kilimanjaro Band, Wananjenje.

Wakati huo aliwasilisha maelezo yake ambayo yalitumika kuandika makala fupi iliyochapishwa kwenye gazeti hilo.

Huyu hapa tena, John Kitime, akielezea maisha yake ndani ya muziki.
"Nilianza kwanza kupiga gitaa mwaka 1968 nikiwa kwenye mwaka wangu wa kwanza wa shule ya sekondari. Tangu napata kumbukukumbu tulikuwa na gitaa nyumbani wakati wote. Baba yangu alipiga gitaa tangu alivyokuwa mdogo. Yeye ni mtaalamu wa nyimbo za asili na ana mamia ya tunzi ambazo kwa bahati mbaya hazijarekodiwa.

Mwaka 1968 nilianza masomo yangu ya sekondari na baba yangu aliniruhusu kupiga gitaa. Alikuwa ni mtu aliyesisitiza masomo kwanza.

Mwaka 1975 niliunda bendi ndogo kwetu Iringa na baadhi ya wanachama wa bendi hiyo waliendelea kimuziki na kupata umashuhuri mkubwa. Wawili kati yao, Ally Makunguru na Nicholas Mlapone, wako nje ya nchi. Makunguru yuko Mombasa, Kenya na Mlapone yuko Ujerumani.Kundi hili hili ndiyo lilikuwa chimbuko  ya bendi kubwa, Tancut Almasi Orchestra.

Mwaka 1980 niliondoka Iringa na kuelekea Dar es Salaam na nilianza kufanya kazi kama msomaji wa prufu wa gazeti la Daily News. Wakati wa ziada nilikuwa mwanamuziki wa bendi ya Osheka, bendi ambayo ilivunjika mwaka 1981. Lakini ilikuwa bendi ambayo ilikuwa na wanamuziki wazuri sana kama Martin Ubwe ambaye sasa hivi ni kiongozi wa bendi ya Mionzi ambayo iko Mbeya, na Sammy Mhina ambayo ni mpiga ngoma wa Heart Strings Band.

Mwaka 1983 nilipata fursa ya kuigiza kwenye sehemu ndogo ya filamu inayoitwa Wimbo wa Mianzi iliyotolewa kwa ushirikiano kati ya Kampuni ya Filamu Tanzania na One World Production (OUP), kampuni ya Uholanzi. Nilipewa pia mkataba wa kutunga nyimbo kwa ajili ya filamu hiyo.

Ilikuwa wakati natafuta wanamuziki wa kurekodi muziki wa filamu hiyo ndipo nilikutana na Tchimanga Assosa, mwanamuziki mashuhuri wa Congo ambaye aliwahi kupiga muziki na bendi ya Lipua Lipua na Orchestra Kamale, ambaye alikuwa anakusudia kuunda bendi na tukaunda bendi iliyoitwa Orchestra Mambo Bado. Nillikuwa na bendi hiyo kwa miaka miwili.

Baada ya hapo nikajiunga na Orchestra Makassy iliyomilikiwa na Mzee Makassy. Bendi hii wakati huo ilikuwa na mwanamuziki Fan Fan Mosesengo (aliyekuwa na Marehemu Lwambo Luanzo Makiadi} na pia Remmy Ongala, ambaye sasa amejijengea jina kubwa akiwa na Orchestra Super Matimila. Sasa hivi Fan Fan yuko London (Uingereza) akiongoza bendi yake mwenyewe, Somo Somo. Pia mwanamuziki mwingine aliyeunda Orchestra Makassy alikuwa Kinguti ambaye sasa yuko na Bicco Stars.

Baada ya hapo nikaunda bendi yangu mwenyewe, TX Seleleka. Nilipata vyombo kutoka kwa rafiki yangu Mholanzi Kick Van den Hevel ambaye baadaye tena alichukua vyombo hivyo hivyo na kuanzisha bendi ya Tatunane. TX Seleleka ilipiga muziki hoteli ya New Africa kama bendi ya hoteli kwa mwaka mmoja halafu ikavunjika baada ya Kick kuchukua vyombo vyake.

Mwaka 1986 nilirudi Iringa nikawa mwanamuziki mwanzilishi wa Tancut Almasi Orchestra bendi ambayo ilikuwa inaundwa na wanamuziki miongoni wa waliyo bora kuliko wote nchini: Kasaloo Kyanga na Kyanga Songa, mapacha wa Ki-Congo waimbaji; wapiga gitaa wawili Shaban Yohana, ambaye sasa hivi ni kiongozi wa Vijana Orchestra, na Kawelee Mutimwana, kiongozi msaidizi wa MK Group; Mafumu Bilali, mpiga saksafoni mahiri ambaye sasa yuko Japani na Zanzibar Sound;kinanda wakati huo kilipigwa na Abdul Salvador, kiongozi wa Washirika Stars, na wanamuziki wengine wengi ambao wameendelea kuwa na sifa kila walipoenda.

Mwaka 1990 nyimbo zangu mbili nilizotunga nikiwa na Tancut, Lungulye na Afrika Nakulilia, zilishinda mashindano ya Top Ten Show zikichukua nafasi ya kwanza na na pili. Nilishinda zawadi ya redio kaseti ya National ambayo nasikitika nililazimika kuiuza ili kupata pesa za kurekodi hii kaseti yangu ya sasa.

Nyimbo nane kwenye hizi ninazorekodi sasa ni uzoefu wangu kutoka kwenye hii miaka yote, bila kusahau ushawishi wa baba yangu. Hii nyimbo Ifipwepo ni utunzi wa baba yangu, nikiwa nimeupangilia kwenye muziki.

Ningekuwa na nafasi nzuri ningeweza kurekodi vizuri zaidi, na kutoa aina nyingi zaidi za muziki. Nakiri kuwa kaseti hii nimeirekodi kwa madhumuni ya kuiza kwa hadhira ya Watanzania ili niweze kurudisha pesa na kununua redio kaseti nyingine."
Taarifa nyingine zinazohusiana na hii:

Saturday, November 24, 2012

Jimmy ChangChuu, msanii toka Bagamoyo atembelea Butiama

Jimmy ChangChuu, ni msanii anayeishi na kufanya kazi Bagamoyo. Baadhi ya kazi anazofanya ni pamoja na kuchonga vinyago, kufinyanga, kuandaa michoro ya grafiti (michoro ya ukutani) na ni mwanamitindo.

Aidha hushiriki kwenye matangazo ya televisheni na anafahamisha kuwa ameshiriki kwenye kipindi televisheni cha cha Dume Challenge. Hivi karibuni alitembelea Butiama na yafuatayo ni maoni yake kuhusu Butiama.
***************************************************

"Naishi hizi sehemu mbili, Dar es Salaam na Bagamoyo, kwa sababu Bagamoyo ni sehemu yangu ambayo napata msukumo, ni sehemu iliyotulia. Mizunguko ya Dar es Salaam kidogo inakuwa inanishinda lakini ninapohitajika Dar es Salaam nakuwepo na familia.

Hii ni mara yangu ya kwanza kufika Butiama. Mara ya kwanza nilipokuja tu ile mandhari ilinifanya nijisikie kama niko na amani, nilipata amani kwenye moyo. Mazingira yametulia, yaani hakuna kitu ambacho kinaweza kikajiingiza wakati unafikiria kufanya kitu fulani au wakati uanataka kufanya kitu. Kwa hiyo ni sehemu ambayo imetulia ambayo inaweza kukupa msukumo.

Ni ngumu sana kupata msukumo kwenye sehemu ambapo kuna vitu vinapita ambavyo vinakuvuruga lakini hapa unaona hali asili ya mazingira, unaona ndege, yaani vitu ambavyo vinakufanya unaona kuwa kuna Muumba ambaye ametengeneza hivi vitu. Ni vitu ambavyo vinavutia kweli.

Kitu ambacho kinaweza kufanya niwaambie watu waje Butiama ni mazingira na hali ya utulivu halafu nikiangalia chimbuko la kabila la Wazanaki kuna vitu ambavyo nilikuwa nikiviangalia ambavyo vina nguvu kubwa ambavyo ukiviangalia kwa juu juu huwezi kuviona, lakini kuna vitu ambavyo vipo ambavyo vimemfanya Mwalimu Nyerere akawa ana nguvu kwenye maamuzi yake, vitu ambavyo vinaendana na tamaduni yetu ya Kitanzania na ambavyo Mwalimu aliviweka kwenye siasa yake na kwenye mila na hakutoka nje ya mila yake kusikiliza mila za kigeni. Alisimama yeye pale aliposimama kutoka kwenye chimbuko la tamaduni yake.

Kwa hiyo unakuta sasa hata katika utawala wake hakutoka nje sana kwa sababu hata nikiangalia nilivyokwenda makumbusho [Makumbusho ya Mwalimu J.K. Nyerere] kule kuna vitu ambavyo nimesoma na Nyerere mwenyewe alikuwa anakwambia elimu ya wakoloni ilikuwa inawaandaa wao kuwatumikia wakoloni siyo kuwaandaa kuweza kujiendeleza wao wenyewe.

Kitu kizuri kama watu wanataka kuwa kwenye siasa na kuwa viongozi wazuri wanapaswa kujifunza kutoka kwa Nyerere na aliyoyafanya. Tangu akiwa shuleni alianza kuwa kiongozi na alichaguliwa na watu. Watu waliona Mwalimu alikuwa na kitu fulani wakamchagua. Siyo kwamba yeye alipendekeza 'mimi nataka kuwa kwenye nafasi hii.' Watu walimuona kuwa ana kitu ambacho anaweza kuchangia kwa wengine na pia alikuwa na uwezo wa kushawishi wengine."

Saturday, November 10, 2012

Konyagi watoa ala za muziki kwa Msondo Ngoma

Kampuni inayotengeneza kinywaji Konyagi imetoa zawadi ya ala za muziki kwa bendi kongwe ya muziki wa dansi nchini, Msondo Ngoma.
Msondo Ngoma jukwaani.
Akikabidhi hizo ala, Mkurugenzi Mkuu wa Tanzania Distilleries Limited ambao ndiyo watangenezaji wa Konyagi, alisema vifaa hivyo vimetolewa kwa ajili ya kuenzi utamaduni wa Mtanzania na kuiwezesha Msondo Ngoma kuwa imara katika kutoa burudani kwa Watanzania.

Alisema, "Msondo ni bendi kongwe tangu kuanzishwa kwake mwaka 1964. Imesimama imara katika kutoa burudani ya uhakika kwa Watanzania na kutumia nyimbo zake katika kuelimisha, na kufunza jamii ya Watanzania walio wengi."

Alisema kwa kuwapatia vyombo hivyo, Msondo Ngoma itakuwa moto wa kuotea mbali katika kutoa burudani ya uhakika, hali itakofanya bendi nyingine kuwa wasindikizaji katika tasnia ya muziki wa dansi nchini.

Mkurugenzi wa bendi hiyo, Maalim Gurumo, alisema kwa sasa wana deni kubwa kwa Watanzania na kampuni ya Konyagi katika kutoa burudani ya uhakika baada ya kupatiwa vifaa hivyo.
Mkurugenzi wa Tanzania Distilleries Limited David Mgwasa, wa pili kutoka kulia, akikabidhi ala kwa wanamuziki wa Msondo Ngoma.
"Tunaamini baada ya leo kupata vifaa hivi tutatoa burudani ya uhakika sanjari na kukijenga vyema kikosi chetu kwa lengo la kukiimarisha," alisema Gurumo.

Kiongozi wa bendi, Saidi Mabela, alitoa shukurani kwa kampuni ya Konyagi kwa kuwapatia vyombo na aliahidi kuendelea kutoa burudani safi kwa Watanzania na Afrka kwa ujumla.
Habari kamili ziko hapa.

Thursday, October 25, 2012

Msanii Kingkapita ametoa nyimbo mpya

Msanii wa Hip Hop, Kingkapita, ametoa kibao kipya chenye jina: Shikamoo pesa.



Taarifa aliyoisambaza mwenyewe inaeleza:
"Nilimshirikisha Tash, mzee wa chapia mulemule kutoka Arachuga. Nyimbo imerekodiwa katika studio za Rocanna Basemennt chini ya producer Jimmy Jizze na master kumaliziwa Home Town Record chini ya master Traveller."

Sikiliza kibao hicho hapa: http://www.hulkshare.com/7u4tpclsbwu8

Monday, September 17, 2012

Msondo Ngoma bado wanatamba

Wapiga gitaa wa bendi ya Msondo Ngoma Abdul Ridhiwani, kushoto, na Zahoro Bangwe, kulia,
wakiburudisha mashabiki wao hivi karibuni wakati bendi hiyo ilipotumbuiza kwenye ukumbi wa Max Bar, Ilala Bungoni, Dar es Salaam.

Msondo Ngoma ni moja ya bendi kongwe za muziki wa dansi za Tanzania. Zamani ilikuwa inaitwa NUTA Jazz.

Picha na habari zimetolewa na Rajabu Mhamila.

Saturday, May 19, 2012

Dimpoz kuzindua 'single' yake mpya Bilicanas Dar Jumapili 20 Mei 2012

Taarifa toka Mroki Mroki zinasema kuwa msanii Omy Dimpoz atazindua 'single' yake mpya leo kwenye Klabu ya Bilicanasa ya Jijini Dar es Salaam. Picha na habari kwa hisani ya Mroki Mroki wa Digital Company & FK Blog.
BAADA ya kutamba na wimbo wake wa Nai Nai, msanii anaekuja juu kwa kasi na mshindi wa Tuzo mbili za Kili Music Award 2012, Omy Dimpoz, anataraji kuzindua 'single' yake mpya ya Baadae katika ukumbi wa Club Bilicanas jijini Dar es Salaam.

Akizungumza na mtandao huu wa Kijamii, meneja wa msanii huyo, Mbaruku Issa ‘Mubenga’ alisema kuwa maandalizi yote yamekamilika na show itakuwa ya uhakika na ya kuvutia.

Mubenga amesema Ommy Dimpoz anataraji kuzindua wimbo huo alioufanyiwa kazi na mwandaaji wa muziki Man Water huku akkimba pamoja na mwanadada Angel.

Aidha Mubenga amesema Dimpoz atasindikizwa na wakali wa Bongo Fleva, Diamond, Ben Pol pamoja na msanii Alawi Jr pamoja na Ma DJ wakali wa Bongo kutoka kundi la Super Deejayz.

Tayari Dimpoz ameshaanza kuwasikilizisha wimbo huo baadhi ya mashabiki wake wa mikoa ya Mwanza na Moshi wakati wa Ziara ya Wakali wa Kili Music Awartd 2012 inayoendelea ambapo leo atakuwa Mbeya chini ya udhamini wa bia ya Kilimanjaro.

“Wimbo ni mkali na mashabiki wanaukubali vilivyo na tunaomba mashabiki wa Bongo Fleva make tayari kwa singo hiyo mpya itakayoanza sasa kuchezwa katika vituo vya redio na kumbi za burudani nchini kote baada ya uzinduzi huo,” alisema Mubenga.

Mubenga amewataka wakazi wa Jiji la Dar es Salaam ambao ni mashabiki na wapenzi wa muziki wa kizazi kipya kujitokeza kwa wingi kumuunga mkono Dimpoz katika uzinduzi huo wa aina yake katika Klabu ya Bilicanas katikati ya jiji la Dar es Salaam Jumapili.

Saturday, March 31, 2012

Gumzo za Nyamisisi

Muda si mrefu uliopita nilikuwa Nyamisisi kwenye barabara kuu inayounganisha Manispaa ya Musoma na jiji la Mwanza.

Wakati nikisubiri basi la kuelekea Mwanza nilisikia mazungumzo ya baadhi ya wakazi wa eneo lile.

Kwanza mmoja wao alianza kuwaarifu wenzake kuhusu mtu ambaye wanamfahamu ambaye alikuwa amehamia Urusi na ambaye kwa mujibu wa mtoa taarifa huyo mtu alikuwa anapata kipato kikubwa huko Urusi.

Nilitafakari sababu ya kumhamisha mtu kutoka Nyamisisi hadi Urusi na sikuipata. Hata hivyo nilivyoendelea kusikiliza yale mazungumzo nikagundua sikuwa nimeelewa vizuri. Aliyekuwa akizungumziwa alikuwa Malouda, mcheza kandanda maarufu ambaye anacheza soka ya kulipwa nchini Urusi.

Mazungumzo yalihamia kuhusu malipo makubwa ya wacheza mpira na wanamuziki. Mchangiaji mmoja alisisitiza kuwa wanamuziki wanalipwa pesa nyingi zaidi kuliko wacheza mpira na katika kusisitiza hoja yake alisimulia yaliyomkuta David Beckham.

Alieleza Beckham, akiwa Marekani, aliingia kwenye duka la nguo kwa madhumuni ya kununua nguo na akamwambia mwenye duka afunge duka kwa sababu sehemu ile haikuwa salama, na yeye alikusudia kununua nguo zenye thamani iliyo sawa na shilingi milioni 50.

Mwenye duka akamuuliza Beckham: "Wewe ni nani mpaka nifunge duka?"
Beckham: "Mimi ni David Beckham."
Mwenye duka: "Unafanya shughuli gani?"
David Beckham: "Ni mchezaji wa mpira."

Kwa mujibu wa mtoa taarifa wa Nyamisisi, yule mmiliki wa duka alimwambia Beckham: "toka hapa!" na akamfukuza dukani kwake.

Mtoa maelezo aliendelea kuwahadithia wenzake kuwa wasanii maarufu ulimwenguni ni matajiri zaidi kuliko wachaeza mpira wa miguu ingawa kuna baadhi ya waliyomsikiliza walipinga hiyo hoja.

Baada ya muda basi la Mwanza likafika na kuninyima fursa ya kuendelea kusikiliza gumzo za Nyamisisi.
posted from Bloggeroid

Wednesday, March 9, 2011

Msanii Hardman ateuliwa katika Tuzo za Muziki za Kilimanjaro

Kwa mujibu wa taarifa iliyopokelewa toka kampuni ya Maisha Music, msanii wake, Hardman, ameteuliwa kushindania Tuzo ya Muziki ya Kilimanjaro Kilimanjaro,
Bango la Hardman la uzinduzi wa album yake, Imebaki Stori, uliyofanyika Desemba 2010
Taarifa hiyo pia inatoa wito na maelekezo kwa mashabiki wa Hardman kumpigia kura ili aweze kushinda.
Taarifa kamili hii hapa: 
Toleo hili la barua taarifa limejikita zaidi juu ya uteuzi wa Hardmad ni msanii wa reggae na dancehall ambaye kwa sasa anasimamiwa na kampuni ya Maisha Music. Katika tuzo za mwaka huu amefanikiwa kuteuliwa katika vipengele viwili navyo ni; kipengele cha wimbo bora wa reggae ambapo ameingiza ameingiza nyimbo mbili, na kipengele kingine ni kile cha wimbo bora wa kushirikishwa, na ni kutokana na kushirikishwa kwake katika wimbo wa Mwana FA na AY “Dakika Moja”.  

Haya ni mafanikio makubwa kwetu pamoja na Hardmad, na tunaamini kuwa hii imetokana na kujituma kwake kwa bidii pamoja na ushirikiano baina yetu. Sisi tunamtakia kila la heri katika tukio hili muhimu kwa maisha yake kama msanii. Maisha Music inapenda pia kuwatakia mafanikio marafiki zetu wengine ambao wamo katika kinyangányiro hiki mwaka huu, baadhi yao ni Jhikoman, Warriors From The East, Ras Rwanda, Lamar, Fid Q, Ray C na Chidi Beenz.

Washindi wa tuzo za Kilimanjaro wanapatikana kwa kupiga kura. Hii inamaanisha kwamba wimbo utakaopata kura nyingi kutoka kwa mashabiki na wapenzi ndiyo utakoshinda. Tafadhali mpigieni Hardmad kura zenu kwa wingi ili aweze kufanikiwa kuibuka kidedea kwani tunaamini anastahili na unaweza kuthibitisha kwa kusikiliza kazi zake kupitia katika linki zilizowekwa hapo chini.

Unaweza kumpigia kura kwa njia mbili tofauti ambazo ni; kwa kubonyeza katika linki iliyoonyeshwa hapo chini na pili ni kwa kutuma ujumbe mfupi wa simu. Iwapo utaweza basi unayo ruhusa ya kutumia njia zote mbili. Angalizo: Kwa kuwa Hardmad ana nyimbo mbili katika kipengele kimoja tunapendda kuwashauri wadau wetu kuupigia kura wimbo wa Ujio Mpya ambao amemshirikisha Enika. Vinginevyo kunaweza kuwa na uwezekano wa kura kugawanyika katika nyimbo mbili.

Katika wimbo wa Ujio mpya tumeshangaa kuona kuwa limeongezwa jina geni la msanii ambaye hatumfahamu (BNV). Tunadhani kuna makosa
yamefanyika na tunajaribu kuwasiliana na wahusika ili kuona namna ya kuliondoa.

Namna ya kupiga kura:

KWA MTANDAO (rahisi sana): 

Gonga kwenye linki hii: http://www.kilitime.co.tz/awards/2009/nominees_2007.php (Na ni kwa mwaka 2011), na ikifunguka gonga kwenye nyimbo unazotaka kuzipigia kura, andika anuani yako ya barua pepe na bonyeza “VOTE”. Kumbuka kubonyeza katika linki ya kuhakiki na utatumiwa barua pepe ya kutoka KTMA (Kilimanjaro Tanzanian Music Awards), vinginevyo kura yako haitasajiliwa! Unaweza kupiga kura moja tu kwa anuani moja ya barua

SIMU:

"Wimbo bora wa Reggae":

Andika K179 katika ujumbe mfupi na tuma kwa namba 15747 ili kuupigia kura wimbo wa "Ujio Mpya - Hardmad Feat. Enika" 
Andika K186 katika ujumbe mfupi na tuma kwa namba 15747 ili kuupigia kura wimbo wa "What you feel inside - Hardmad"

(Unaweza kupiga kura moja tu katika kila kipengele kwa kila namba ya simu).

"Wimbo bora wa kushirikishwa:

Andika W137 kwa ujumbe mfupi na kisha tuma kwa namba 15747 ili kuupigia kura wimbo wa "Dakika Moja - Mwana FA & AY feat. Hardmad" 

Tunakushukuru sana kwa ushirikiano wako na msaada ambao tunaamini utaweza kumfikisha Hardmad katika kilele cha mafanikio anayostahili. Tuna matarajio ya mengi mazuri katika harakati za kimuziki kwetu pamoja na wasanii tunaoshirikiana nao. Kwa ufafanuzi zaidi unaweza kusikiliza na kuangalia baadhi ya nyimbo katika Myspace au Youtube au kwenye kurasa za Hardmad katika mitandao ya Facebook na Myspace. Albamu mpya ya Hardmad “Imebaki Story” kwa sasa inapatikana pia kwa njia ya mtandao, na unaweza kuipata kwa kubonyeza hapa kwa Itunes pamoja na maduka mengine ya kwenye mtandaoni. 

Hivi sasa Maisha Music ipo katika maandalizi ya maonyesho kadhaa ya utambulisho wa albamu ya Hardmad katika miji mbalimbali hapa Tanzania pamoja na Kenya mwezi wa Aprili. Taarifa sahihi pamoja na tarehe zitatangazwa muda si mrefu.

Tafadhali tusaidie kusambaza taarifa hii kwa wapendwa, marafiki pamoja na wadau wengiine wa muziki!

Kila la heri na asante sana kutoka
Timu ya MAISHA MUSIC

Saturday, December 4, 2010

Hardmad amerudi tea ulingoni

Baadaya ya kimya kirefu na kujifua kisawasawa, Hardmad amerudi tena kwa kishindo. Na safari hii amekuja na albamu inayokwenda kwa jina Imebaki Story ambayo ina jumla ya nyimbo 11.

zilizorekodiwa katika studio za 41 Records, Tatoo Records, na Maisha Studios za Dar es Salaam, na Click Studio ya Copenhagen, Denmark.

Usanifu umefanywa katika Studio za C4 nchini Denmark. Kwa kipindi cha mwezi mmoja Hardman alikuwa amejichimbia kambini kwa ajili ya mazoezi kwa kushirikiana na Kaka Zao Band atakayokuwa akifanya nayo maonyesho.

Picha na habari kutoka kwa Kwame Mchauru wa Maisha Music.

Sunday, September 12, 2010

Jagwa Music waendeleza rirandi nchini Denmark

Jagwa Music ni kikundi ambacho kinapiga muziki wa Mchiriku, au Mnanda, kama vijana wengi wanavyopenda kuuita. Wasanii hawa sasa hivi wako katika ziara ya maonyesho mawili nchini Denmark.

Jana usiku walianza makamuzi ya kasi kubwa. Leo hii, kuanzia saa mbili usiku watakuwa katika mji wa Roskilde kwa ajli ya makamuzi mengine.

Ziara hii, itayakayohitimishwa tarehe 13 Septemba, ni kwa ajli ya kujitangaza kwa ajili ya maandalizi ya ziara nyingine ndefu hapo mapema mwaka 2011.


Waratibu wa safari hii ni kampuni ya Jahazi Music, na kwa maandalizi yote nchini Tanzania wanashirikiana na kampuni ya Maisha Music.


Mwenyeji wa ziara hii nchini Denmark ni kampuni ya GlobalCPH. Kikundi hiki kinamilikiwa na George Sultani Jolijo, na kusimamiwa na kampuni ya Maisha Music Tanzania Limited.