Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Showing posts with label Mada yangu ya leo. Show all posts
Showing posts with label Mada yangu ya leo. Show all posts

Friday, March 23, 2018

Ukitaka kula usiende jikoni

Nina desturi ya kununua mahindi ya kuchoma yanayouzwa mitaani. Nilichoshuhudia miezi kadhaa iliyopita kimenipunguzia hamu ya kula tena mahindi hayo.

Nilisogelea mchoma mahindi na kuchagua mhindi uliyokuwa tayari juu ya jiko la mkaa. Baadaye kidogo, mmoja wa mahindi aliyokuwa akichoma ulianguka chini na kuseleleka mbali na alipokaa.

Alimtuma mwanae kuuokota chini na akaurudisha jikoni kuendelea kuuchoma baada ya kuufuta mchanga. Haukuwa ule mhindi niliyouchagua mimi ila nilitambua kuwa muda si mrefu atafika mteja kama mimi na kulishwa mhindi huo na, bila shaka, kuambukizwa minyoo.

Lakini haikuwa hatari ya kupata minyoo tu. Mchoma mahindi alikuwa na kikohozi. Na kila alipokohoa aliziba mdomo akitumia mkono wake wa kulia, ikiwa ni tabia ile ambayo baadhi wamefundishwa ili kuwakinga wengine kuathirika na athari za maambukizo yanayoweza kusambazwa na anayekohoa.

Tatizo ni kuwa ni mkono huo huo aliutumia kugeuzia mahindi aliyokuwa anachomea wateja, pamoja na langu. Mkono ulikuwa unatoka mdomoni na kushika mhindi.

Aliponiambia mhindi wangu umeiva, badala ya kuanza kula pale pale kama ilivyokuwa desturi yangu, nikamuomba aufunge vizuri nikaondoka nao lakini sikuula na ndiyo ikawa mwisho wa kununua mahindi ya njiani.

Labda kwa sababu nimeanza kulima mahindi nitakuwa nachoma mahindi ninayovuna shambani kwangu.

Nimewahi kusikia msemo kuwa ukitaka kula chakula cha mgahawa usiingie jikoni. Utakayoyaona huko yatakatisha njaa yako.

Saturday, July 30, 2016

Mada yangu ya leo: mwizi ni mwizi tu

Sikumbuki niliisoma wapi habari hii, lakini kuna kichwa cha habari cha toleo la gazeti la hivi karibuni liliarifu kuwa yule mtuhumiwa wa kuiba milioni 7 kwa dakika "mwenye asili ya Kiarabu" amefikishwa mahakamani.

Kwanza, nitamke wazi kuwa hili suala liko mahakamani na mimi simhukumu mtuhumiwa. Namtetea kwa kubaguliwa. Akikutwa na hatia, nitazungumzia hilo.

Mwizi ni mwizi tu, hata kama ni kabila yako. Uandishi wa aina hii wa kubainisha kuwa mtuhumiwa ana asili ya Uarabu ni hatua ya wazi ya kubagua mtu kwa rangi yake ya ngozi. Maana inayojitokeza ya makala hii ni kuwa kama angekuwa Mbantu akutwe na hatia ya kuiba milioni 7 kwa dakika, tatizo lingekuwa dogo zaidi. Labda milioni 7 ingekuwa 2 tu kwa sababu tu mwizi alikuwa ana rangi tofauti ya ngozi.

Thursday, September 10, 2015

Mada yangu ya leo: Hii siyo siasa

Tuawasikia baadhi ya viongozi waandamizi wa Chama cha Mapinduzi (CCM) wakimtaka mgombea urais wa UKAWA akubali wakutane kwenye mdahalo ili waeleze maovu yake. Yeye anasema kama wana ushahidi kuhusu maovu yake waende mahakamani. Hii siyo siasa.

Nionavyo mimi, siasa ingekuwa hivi:

1. Kama una tuhuma dhidi ya mgombea urais husubiri awe rais kwanza. Unasema yale unayoyafahamu. Akisha kuwa rais halafu utafanya nini? Utaomba mdahalo?

2. Mpiga kura ana haki ya kufahamu taarifa zote muhimu juu ya wagombea kabla hajafikia uamuzi wa kumchagua yule ambaye anaona anafaa. Kuamua kuwa taarifa hizo ni kama mali adimu haina tofauti na kujifanya mtaalamu wa bishara (au taaluma nyingine) ambaye ametumia muda mwingi kupata elimu na uzoefu kwenye taaluma yake halafu anaamua, kwa haki kabisa, kuwa taarifa hizo hazitoki mpaka kwa masharti yanayomnufaisha yeye, au kwa pesa au kwa njia nyingine atakayoamua. Ni wajibu wa kiongozi yoyote makini kumpa mpiga kura taarifa sahihi, hasa wakati wa uchaguzi.

3. Mpaka sasa, tumemsikia mtuhumiwa akisema kuwa hana tuhuma yoyote na, kwa mantiki hiyo, anaposema nendeni mahakamani ni sawa kabisa. Wale wenye taarifa hizo wakaziibue mahakamani. Watuhumiwa wachache sana hukubali kosa nje ya mahakama.

Kwa hayo machache, sisemi kuwa tuhuma ni za uongo.

Ninachoona ni kundi moja ambalo limekosa ujasiri wa kutamka wanalotaka kutamka na badala yake kuwafanya wapiga kura kubaki wanabishana wenyewe kwa wenyewe na ujinga wao* (kama ujinga huo upo kweli) bila kuwapa taarifa ambazo zinaweza kuwasaidia kufanya chaguo sahihi.

Kama huo ujasiri unakosekana, basi ni bora kunyamaza tu. Kuwafanya wapiga kura kuwa wajinga mara ya pili ni hatari kisiasa.

Huo ndiyo ujumbe wango leo hii.

*Wale ambao mtakimbilia kwenye Tume ya Mawasiliano kunilalamikia kuhusu kutumia neno "ujinga" ni kwamba siyo tusi, ni hali ya kutofahamu tu.

Saturday, July 26, 2014

Mada yangu ya leo: siyo kila aliye chumbani amelala usingizi

Siyo kweli kuwa kila aliye chumbani amelala usingizi. Nitafafanua.

Ninapokuwa kijijini Butiama sehemu kubwa ya kazi yangu inahusu kutangaza kijiji hiki kama kivutio cha utalii wa kihistoria na kiutamaduni. Nafanya kazi hiyo kwa taarifa ninazoweka mtandaoni na kwa mawasiliano ya moja kwa moja (kwa simu na barua pepe) na wale wanaopanga safari za kutembelea Butiama.Vitendea kazi vyangu ni kompyuta ambayo ninayo chumbani kwangu, na simu. Chumba changu ni ofisi yangu. Mimi nikisema naenda ofisini inanichukua chini ya dakika moja kufika kazini, kwa sababu ni safari ya kutoka kitandani kwangu mpaka kwenye meza yenye kompyuta.

Nafahamu wataalamu wanasema zipo athari za kuweka ofisi nyumbani lakini hiyo siyo mada yangu ya leo. Ninachosisitiza sasa ni kuwa mabadiliko ya teknolojia yamerahisisha kuhama na ofisi sehemu yoyote tunayotaka. Kompyuta na simu zimepunguza ulazima wa aina fulani za wafanyakazi kuwepo ndani ya jengo mahususi ili kutekeleza majukumu yao.
Ofisini kwangu.
Kwa bahati mbaya mabadiliko haya ya teknolojia hayako wazi kwa kila mtu. Kwa wengi kazi halisi ni inayofanyika katika sehemu mahususi, mathalani shambani, kiwandani, au ofisini, na kwa kijijini inaonekana kuwa ni kazi iwapo tu inamtoa mtu jasho.

Ukijifungia chumbani (kwangu ni ofisini) kuanzia asubuhi mpaka jioni unadhaniwa kuwa umelala usingizi. Kuna siku nilisikia mgeni anaambiwa kuwa nimelala na nikalazimika kutoka ndani kumkaribisha chumbani aliyetamka maneno hayo na kumuonyesha kuwa chumbani kwangu ni ofisini kwangu.

Kama nilvyosema siyo kila aliyekuwa chumbani amelala usingizi.

Friday, November 1, 2013

Mtwara sawa lakini Loliondo hapana?

Nimekuwa na msimamo unaofanana kidogo na sera ya serikali juu ya rasilimali za Tanzania; kwamba ni mali ya Watanzania wote, na siyo ya wale walio karibu na hiyo rasilimali. Sikubaliani na hoja kuwa wale wananchi walio karibu na rasilimali ndiyo wapewe upendeleo zaidi juu ya kufaidika na rasilimali hiyo.

Sababu yangu ya msingi ni kuwa kufanya upendeleo wa aina hiyo kutajenga ubaguzi dhidi ya Watanzania wengine. Watanzania wengine wataonekana kuwa "wanaingilia" rasilimali inayopaswa kutumika na wale wazawa wa eneo husika tu. Na ndiyo maana napata shida kuunga mkono hoja ya baadhi ya Watanzania, kama wale wananchi wa Mtwara, wanaodai rasilimali ya gesi ni yao kwanza.

Lakini hatuwezi kusema hatuelewi kwanini kuna madai kama yao. Unaweza kujenga hoja nzuri kuzungumzia kwanini wananchi wa Mtwara wanaamua kuwa gesi ya Mtwara ni yao. Ni ubovu wa sera za muda mrefu za serikali zilizopuuza umuhimu wa kuhakikisha kuwa Watanzania wanafaidika na rasilimali yao. Haya ni matokeo ya muendelezo ule wa sera zinaotoa vipengele vya upendeleo kwa wawekezaji na ulipaji wa mrahaba pekee. Mwekezaji aliweza kumiliki asilimia 100 ya mradi wa rasilimali muhimu na kuilipa serikali au kodi kidogo au kusamehewa kabisa na kiwango cha mrahaba ambacho, kimsingi, kilikuwa kidogo sana.

Wananchi waliofundishwa miaka nenda rudi kuwa yatosha kutoa misamaha ya kodi kwa wawekezaji na malipo ya mrahaba wa chini ya asilimia tano hawakuelewa hilo somo na hawataweza kulielewa hata kwa karne nzima. Matokeo yake ni kupoteza imani kabisa kwa serikali na maamuzi yoyote inayoyafanya kwenye eneo la uwekezaji. Tunachoshuhudia sasa ni wananchi "kuchukua chao mapema"; kwamba rasilimali ambazo ziko jirani nao ni lazima ziwape faida wao. Watanzania wengine wahangaike na mali zilizopo maeneo yao. 

Huu ni mwanzao wa kuparaganyika kwa nchi. Wale wasio na rasilimali watakula wapi? Watapata ajira wapi? CHADEMA wamejaribu kuelezea namna utaratibu wa kila mtu na chake (majimbo) na kidogo kilichopo kipelekwe kwenye serikali kuu lakini kwangu mimi sera hii ina walakini kuwa itaanza kupandikiza hisia kuwa Mlima Kilimanjaro una wenyewe. Hali kadhalika Serengeti, Selous, na mbuga nyingine ambazo zinaliingizia Taifa mabilioni ya shilingi kila mwaka. Vivyo hivyo kwa gesi na mafuta yanayosubiriwa kwa hamu.

Badala ya kuitaka serikali iwajibike zaidi katika kuwanufaisha wananchi wake, tunaanza kugawana kile kidogo kilicho jirani yetu. Ni sawasawa na wenyeji kugombania makombo baada ya chakula kutengewa wageni.

Kutegemea kuwa jambo litatokea (ubaguzi wa watu kutokana na maeneo yao ya asili) hakuthibitishi kuwa jambo hilo kweli litatokea. Lakini binadamu wote tunaishi kwa kufanya maamuzi kuhusu yaliyokwisha tokea zamani, ya sasa, na matarajio yetu ya yale yanayoweza kutokea. Ndiyo msingi wa mipango yote thabiti, kwa hiyo siyo rahisi kujenga hoja kupuuza hoja za aina hii.

Sasa basi tugeukie Loliondo. Wakati siungi mkono madai ya wananchi wa Mtwara naunga mkono madai ya wale wa Loliondo ambao wanapinga kusudio la serikali la kutenga kilomita za mraba 1,500 kwa wawekezaji kwa shughuli za utalii, pamoja na serikali kutaka watu hao wahame kupisha shughuli za uwekezaji. Wamasai wapatao 30,000 na ng'ombe zao wahamishwe ili kupisha shughuli za utalii.

Bado nina msimamo kuwa Tanzania ni ya wote lakini kwa wakazi wa tarafa ya Loliondo, ambao wengi wao ni wafugaji na wanaoishi maisha yanayotegemea sana ardhi wanayokalia kwa ustawi wao na wa mifugo yao, kugawa hayo maeneo kwa matumizi ya wawekezaji ni kuwanyima Watanzania hawa chanzo cha msingi kinachobeba mfumo wao wa maisha.

Hii ni sawa na kuhatarisha uhai wao. Hasara atayopata mkazi wa Loliondo atakayehamishwa haiwezi kamwe kufidiwa na kiasi chcochote cha pesa, hata kama pesa hizo zisingieishia serikalini na zikagawiwa kwa wakazi hao.

Mkazi wa Mtwara ana haki kuhoji serikali ionyeshe faida kwake (na kwa Watanzania wengine) ya sera ya muda mrefu ya uwekezaji, lakini hata kama madai ya kuweka Mtwara viwanda muhimu vya sekta ya gesi haitatimizwa, maisha ya mwana-Mtwara hayatabadilika kwa kiasi kikubwa kulinganishwa na athari na matatizo makubwa ambayo atayapata mkazi wa Loliondo ambaye maisha yake yataathrikia kutokana na kuhamishwa kwenye ardhi ambayo anaitegemea kila siku kwa maisha yake na kwa mifugo yake.

Katika mazingira haya, madai ya wananchi hawa wa Loliondo ni sahihi kabisa, kwa maoni yangu. Ya Mtwara bado yanahitaji kujengewa hoja zaidi.

Taarifa nyingine zinazohusiana na hii:
http://muhunda.blogspot.com/2010/09/john-mnyika-wa-chadema-anajibu-hoja.html
http://muhunda.blogspot.com/2010/10/amani-millanga-bado-anahoji-sera-ya.html

Tuesday, April 30, 2013

Bara la Afrika lapewa sauti kwenye tamasha la filamu la nchini Ubelgiji, Afrika Filmfestival

Mwishoni mwa mwezi Machi mwaka huu nilihudhuria tamasha la filamu nchini Ubelgiji linalojulikana kama Afrika Filmfestival.

Ni tamasha linalofanyika kila mwaka na huhusisha kuonyeshwa filamu nyingi kuhusu bara la Afrika zinazoonyeshwa ndani ya kumbi mbalimbali zilizopo kwenye miji kadhaa ya nchini Ubelgiji.
Bango la Afrika Filmfestival la mwaka huu. Picha: Lilian Nabora. Picha zaidi za Afrkia Filmfestival zinapatikana hapa:  https://www.facebook.com/media/set/?set=a.440201782735019.1073741834.199073470181186&type=1
Madhumuni ya tamasha hilo ni kutoa fursa kwa Waafrika wenyewe kuizungumzia Afrika kwa njia ya filamu za kubuni na zisizo za kubuni. Ni dhahiri kuwa watengeneza filamu wasio Waafrika hawalioni bara la Afrika kwa mtazamo ule ule ambao mzaliwa wa bara hili anaweza kuwa nao. Na aghalabu, mtazamo wa wasiyo Waafrika kuhusu bara la Afrika huwa mara nyingi unatoa taswira ya bara lenye matatizo mengi pasipo mafanikio, jambo ambalo siyo kweli.

Kwenye tamasha la mwaka huu baadhi ya filamu kutoka Tanzania zilizoonyeshwa ni pamoja na The Teacher's Country, filamu isiyo ya kubuni na ambayo nimeshiriki kama mmojawapo wa Watanzania wanne wanaotoa maoni yao kuhusu miaka 50 ya uhuru wa Tanganyika.

Bara la Afrika linapata fursa ya kujisemea nchini Ubelgiji kila mwaka kupitia Afrika Filmfestival.

Wednesday, April 24, 2013

Mada yangu ya leo: Ukiritimba wa Tanzania ni kikwazo kwa maendeleo

Mojawapo wa vikwazo vikubwa kwa utendaji kazi Tanzania ni ukiritimba. Ni janga la Taifa, nadiriki kusema. Nimeshuhudia katika siku chache zilizopita tatizo hili kwenye taasisi kadhaa, ikiwa ni pamoja na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA).

Nilimsindikiza mwekezaji mmoja kwenye ofisi ya kanda ya Kituo cha Uwekezaji Tanzania kuwasilisha maombi ya kusamehewa malipo ya kodi ya nyongeza ya thamani kwa mujibu wa sheria ya uwekezaji. Taratibu zinataka muombaji afuate hatua hizi:

1.       Achukue ankara kwa muuzaji wa bidhaa ambazo zinaombewa msamaha
2.       Ajaze fomu maalumu ya maombi ya kusamehewa kodi ya nyongeza ya thamani
3.       Awasilishe katika ofisi ya Mamlaya ya Mapato Tanzania fomu (kwenye mkoa ambako mradi unaendelezwa) ili idhini ya kusamehewa kodi itolewe; na
4.       Arudi kwa muuzaji na kulipia bidhaa bila kodi na kuchukuwa hivyo vifaa

Tatizo liko katika ngazi nyingi. Kwanza, taratibu zote za kuomba misamaha ya kodi au zinafanyika Dar es Salaam au kwenye makao makuu ya Kituo cha Uwekezaji na Mamlaka ya Mapato Tanzania, au kwenye ofisi za kanda za kituo cha uwekezaji. Ofisi hizi za kanda siyo nyingi kwa hiyo, kwa mwekezaji ambaye hayuko Dar es salaam au jirani na ofisi za kanda,  inamlazimu aingie gharama kubwa ya kusafiri mara kwa mara kati ya eneo la mradi kwenda kwenye maeneo hayo ambapo maamuzi ya kusamehewa kodi yanachukuliwa.

Si hivyo tu, lakini kwa mwekezaji ambaye hayuko Dar es salaam au jirani na mji mkubwa hulazimika mara kwa mara kupata mahitaji ya vifaa vya ujenzi kutoka sehemu mbali mbali za Tanzania. Mathalani, kwa mwekezaji aliyeko Butiama, anahitaji kusafiri mara kwa mara kwenda nje ya mkoa wa Mara kununua vifaa mbalimbali, ikiwa ni pamoja na Mwanza na Dar es Salaam.

Tatizo la ukiritimba, ambalo wapanga taratibu wa Dar es Salaam (na watunga sheria wa Dodoma) huwa hawalioni, ni hili na linaonekana vizuri kwa mfano halisi wa namna ambavyo mwekezaji wa Butiama anapaswa kupata msamaha wake wa VAT:

1.       Anasafiri kwenda Mwanza au Dar es Salaam kupata ankara ya vifaa ambavyo anataka kununua. Nasisitiza kuwa analazimika kusafiri kwa kuwa tunafahamu kuwa, tofauti na nchi zilizoendelea, kwetu ni muhimu kuona vifaa kabla ya kuvinunua.
2.       Anajaza fomu ya kuomba msamaha wa kodi na kuiwasilisha kwenye ofisi ya Mamlaka ya Mapato Tanzania ya Mkoa wa Mara, na kupewa idhini. Ofisi ya mkoa pia ina jukumu la kukagua mradi na kuhakikisha kuwa unaendelezwa.
3.       Anarudi Dar es Salaam au Mwanza kulipia vifaa bila malipo ya kodi, na kuchukuwa vifaa.

Jambo ambalo nimejifunza ni kuwa hali ya kutoaminiana kati ya ofisi za Mamlaka ya Mapato Tanzania katika ngazi mbalimbali (makao makuu na mikoani) ndiyo inayosababisha hizi taratibu za ajabu za kufanya muombaji alazimike kwenda Dar es Salaam au Mwanza mara mbili ili kukamlisha mzunguko wa manunuzi na kupata msamaha wa kodi.

Nilimuuliza Meneja wa Mkoa wa TRA Mwanza: “Hivi usingeweza kumpigia simu meneja mwenzako Musoma na kupata uthibitisho kuwa mradi huu ni halali na unaendelezwa Butiama?”

Alinijubu kuwa, kwanza, sheria na kanuni haziruhusu. Mwekezaji anatakiwa apate barua ya Mkuu wa Wilaya alipo (kutihibitisha uwepo wa mradi katika wilaya yake) ambayo inapaswa kuwasilishwa kwenye ofisi za Mamlaka ya Mapato ya Mkoa, na jalada la mwekezaji kufunguliwa likiwa na orodha ya vifaa vilivyoruhusiwa msamaha wa kodi. Halafu, kila mwekezaji anapofanya manunuzi ofisi ya TRA Mkoa itapunguza vile vilivyonunuliwa. Aidha, ofisi hiyo tu ndiyo yenye mamlaka ya kufanya ukaguzi wa mradi kuhakiki vifaa visitumike tofauti na ilivyoombwa na mwekezaji.

Meneja huyo wa Mwanza alinitolea mifano kadhaa ya wawekezaji wasiyo waaminifu ambao walipewa misamaha ya kodi lakini hawakuwa na miradi yoyote ya uwekezaji waliyoendeleza, na badala yake wakatumia vifaa vilivyosamehewa kodi kwa matumizi mengine. Alimalizia kwa kusema: “Unajua watu wamekuwa wadanganyigu sana siku hizi kwa hiyo lazima kuchukuwa tahadhari.”

Nilimuuliza iwapo taratibu zote zimekamilishwa, kwanini ofisi yoyote ya TRA katika mkoa wowote wa Tanzania isiweze kuwasiliana na ofisi ya TRA iliyopo kwenye mkoa wenye mradi ili kutihibitisha  uwepo wa mradi ili kumpunguzia mwekezaji ambaye ni mwaminifu safari ya nenda rudi ili kukamilisha mzunguko. Bado hakuona kuwa ni tatizo ambalo mamlaka inapaswa kusumbuliwa nalo na kwake yeye tatizo la msingi lilikuwa kudhibiti wasiyo waaminifu bila kujali athari kwa wale waliyo waaminifu.

Kwa maoni yangu tatizo la kudhibiti uhalifu linagubikwa pia na uvivu wa kufikiri mbinu za kudhibiti wahalifu. Kwa hiyo linapoonekana tatizo, uamuzi unakuwa kudhibiti utendaji badala ya kurahisisha utendaji. Sasa hivi Tanzania ina Mkongo wa Taifa ambao ungeweza kutumika vizuri kufanya mawasiliano kati ya ofisi za TRA za mikoa ili taarifa muhimu za wawekezaji ziweze kupatikana kwenye ofisi yoyote ya TRA nchini.

Si hivyo tu, kompyuta zimejaa kwenye maofisi ya Tanzania. Zinatumia kwa ajili ya nini? Nimeshuhudia kwenye maofisi kadhaa hutumika kisikilizia nyimbo za kwenye CD na kuangalia televisheni. Nina hakika pia hutumika kwa ajili ya Facebook, Twitter, na shughuli nyingine za mtandao ambazo kamwe haziwezi kumpunguzi bugdha mwekezaji anayejaribu kuomba msamaha wa kodi ya nyongeza ya thamani.

Nilimwambia yule meneja wa Mwanza kuwa iwapo polisi wa Tanzania wangekuwa wanafanya kazi kama TRA, basi hali ya uhalifu ingekuwa mbaya kuliko ambavyo ilivyo sasa. Kwa sababu Mtanzania angetenda uhalifu Butiama akahamia Kibondo akiwa na uhakika kuwa polisi wa Kigoma wakimwona watasema kuwa siyo kazi yao kumkamata kwa sababu kosa limefanyika kwenye Mkoa wa Mara. Kwangu mimi  TRA ni chombo cha kitaifa na huduma yao haiwezi kuishia ndani ya mipaka ya mikoa. Ama sivyo tuambiwe sasa kuwa Chama cha Mapinduzi kinaanza kutekeleza sera za CHADEMA kwa kupitia njia za panya.

Nilijaribu kueleza kwa meneja wa Kituo cha Uwekezaji Tanzania kwenye ofisi yao ya kanda iliyopo Mwanza adha hii ya ukiritimba, na hasa kufanyika Dar es Salaam kwa maamuzi ya masuala mbali mbali. Kwa maoni yake (na baadhi ya sheria zinaelekeza hivyo) kuna maamuzi mengi ambayo yanaweza kuidhinishwa na maafisa mahususi tu ambao wako Dar es Salaam.

Nilimkumbusha kuwa kuna maelfu wa maafisa hapa nchini wanaotekeleza majukumu kwa niaba ya rais kwa hiyo labda umefika wakati kupitia upya sheria na kuangalia uwezekano wa kukaimishwa kwa baadhi ya maamuzi yanayokwamisha utendaji.

Kuacha Mamlaka ya Mapato, ipo mifano mingine mingi kwenye taasisi nyingine ambayo nayo inaathiri utendaji katika sehemu mbalimbali za nchi. Mfano mmojawapo ni huduma za kampuni za simu. Ni mara kadhaa nimepiga simu kwenye kitengo cha huduma kwa wateja katika mojawapo ya kampuni za simu kulalamikia huduma fulani nikaambiwa: “njoo ofisini.” Hawa waliyoniambia “njoo ofisini” hawakuwa na ofisi Musoma, kwa hiyo “njoo ofisi” kwangu inamaanisha “njoo/nenda Mwanza”, safari ya kilomita 190.

Tatizo la vitengo vya huduma kwa wateja kwenye kampuni hizi za simu ni kuwa wanapaswa kuwa na watu wenye uwezo wa kutoa maelekezo kutatua tatizo kwa njia ya simu, lakini labda kwa kutokuwa na watu ambao wamepewa mafunzo ya kutosha, wanaposhindwa kumaliza tatizo lako wanasema: “njoo ofisini.”

Tanzania ina watu wengi kuliko wanaoishi Dar es Salaam. Hili likizingatiwa, matatizo mengi ya ukiritimba yatapungua.

Taarifa nyingine zinazofanana na hii:

Thursday, March 21, 2013

Mada yangu ya leo: Viongozi wakae maofisini na kupunguza uzinduzi

Kwa maoni yangu, viongozi wetu hawana muda wa kutosha kukaa kwenye ofisi zao na kufanya kazi ambayo walipa kodi wanatarajia zisimamiwe na viongozi wao. Sababu kubwa inayosababisha tatizo hili ni viongozi wetu kukubali mialiko ya uzinduzi wa kila jambo ambalo Watanzania wanaweza kubuni.

Na hapa sizungumzii viongozi wakuu tu wa nchi, nazungumzia viongozi wa ngazi zote kwa sababu nchini Tanzania imekuwa desturi sasa kwa kila jambo kuwa na uzinduzi rasmi, kuanzia kanda mpya ya kwaya mpaka kinywaji kipya.

Lakini ni dhahiri kuwa mifano inayopatikana kwa urahisi inawahusu viongozi wakuu wa nchi kwa kuwa habari zao zinaandikwa zaidi kuliko zile za viongozi wa ngazi za chini.

Angalia mifano ifuatayo ya Rais, Makamu wa Rais, na Waziri Mkuu, na utapata picha ya ukubwa wa tatizo hili:

Rais Jakaya Kikwete
Makamu wa Rais Dk. Mohamed Bilal
Waziri Mkuu Mizengo Pinda

Ni dhahiri kuwa kwa kila kiongozi kuna sehemu au shughuli fulani ambayo anapaswa kuhudhuria kwa sababu ya umuhimu wa shughuli yenyewe na nafasi yake katika uongozi, lakini ni dhahiri kuwa kuna shughuli nyingine nyingi ambazo hazina umuhimu kwa viongozi wetu kuhudhuria.

Kuna umuhimu kwa sheria kutumika kutamka shughuli rasmi ambazo viongozi wa ngazi ya Taifa wanapaswa kuhudhuria ili kupunguza mlolongo wa shughuli ambazo tunaoona zinazinduliwa na viongozi hawa. Hili likifanyika, litapunguza gharama kwa serikali na pia kuwapa muda mkubwa zaidi viongozi wetu kubaki kwenye sehemu zao za kazi na kusimamia vyema shughuli za serikali.

Kama nilivyosema awali, hapa nimetoa mifano ya viongozi wa kitaifa kwa sababu ndiyo mifano iliyo rahisi kuitoa. Lakini hili ni tatizo lililopo katika ngazi zote, kuanzia mawaziri mpaka watendaji wa vijiji.

Watanzania nao wabadilishe fikra kuwa haiwezekani kuchapa kazi bila kufanya uzinduzi.

Tuesday, February 5, 2013

Mada yangu ya leo: Tulipie gazeti na kupanga kurasa?

Mara kwa mara hununua gazeti na ninapoanza kusoma nakuta kuwa kurasa za ndani hazijapangwa kwa mtiririko wa kawaida, namba za mwisho zikiwa zimetangulia. Mathalani, unaweza kusoma kurasa ya tano na ukiendelea unakuta inafuata kurasa ya 19.

Hii inatokana na mpangilio mbaya wa karatasi zilizomo ndani zenye kurasa nne kila moja. Ni rahisi kurekebisha huu mkanganyiko kwa kupanga vyema tu hizo kurasa na kuendelea kusoma gazeti kwa mtiririko uliyokusudiwa na wahariri.

Kwa hiyo mara kwa mara hujikuta najaribu kurekebisha huo mpangilio uliokusudiwa na naamini wasomaji wengine wengi hufanya hivyo. Hii ni kazi ambayo inapaswa kufanywa na wachapishaji lakini ni dhahiri kuwa hawaifanyi, au kwa kuona haina umuhimu, au yawezekana kuwa mashine ambazo zinapaswa kufanya kazi hii ya kupanga kurasa hazifanyi kazi vizuri.

Kwa sababu yoyote iliyopo ni suala ambalo halipaswi kuendelea. Mteja alipie gazeti, halafu apange kurasa za gazeti? Hii ni bidhaa ambayo haijakamilika. Haina tofauti na kwenda kwa kinyozi halafu akukabidhi mashine ya kunyolea nywele na kukwambia ukate nywele zako mwenyewe halafu ukimaliza akudai hela.

Thursday, November 1, 2012

Mada ya yangu ya leo: aliyeikashifu Kurani aadhibiwe

Kwa hali ya kawaida, mtoto aliyedhalilisha kitabu kitukufu cha dini ya Kiislamu angeweza kuadhibiwa kwa kuchapwa bakora na mzazi wake au kupewa adhabu nyingine nzito ambayo watoto wote wanaokosea hupewa.

Lakini tukio liliotokea siyo la kawaida, kama ambavyo tumeshuhudia madhara yaliyofuata na vurugu zilizotokana na kitendo kile. Makanisa yalivamiwa na mali nyingi kuporwa na kuharibiwa. Uporaji wa mali haufanani hata kidogo na Uislamu kwa hiyo ni dhahiri kuwa katika kundi la watuhumiwa wa matukio haya ambalo linasemekana kuwa ni la waumini wa dini ya Kiislamu walishiriki pia watu ambao hawakusukumwa na hasira ya kudhalilishwa kwa Kurani na dini ya Kiislamu bali ni watu waliyoona fursa ya kuharibu na kupora mali.

Tanzania inayo sheria inayosimamia watuhumiwa ambao wako chini ya umri wa miaka 18. Ni dhahiri hakuna ubishi kuwa huyo mtoto alifanya kosa hilo. Jambo moja ambalo linaweza kuepusha manung'uniko ya dhati ya waumini wa dini ya Kiislamu kulalamikia kile kitendo ni kufikisha suala la yule mtoto mahakamani bila uchelewesho. Kufanya hivyo kutaondoa kabisa kisingizio cha wale ambao wanatafuta fursa ya kufanya fujo kwa kisingizio cha kutetea hadhi na heshima ya dini ya Kiislamu.

Nina hakika yule mtoto tayari anajutia kitendo chake, lakini suala la kutafuta suluhu baina ya waumini wa dini mbalimbali, na suala la kulinda amani nchini linahitaji hatua za kisheria zichukuliwe haraka dhidi yake.

Wednesday, October 31, 2012

Mada yangu ya leo: Jinsi elimu duni inavyohatarisha amani

Nimewahi kuuliza waandishi wa habari wawili, mmoja toka Kenya na mwingine Mtanzania, swali moja: raia wanaamini yuko kiongozi ambaye si mwizi? Mkenya alisema Wakenya wote wanaamini kuwa viongozi wao siyo waaminifu. Mtanzania naye alisema Watanzania wengi zaidi nao wanaamini kuwa viongozi wetu siyo waaminifu.

Madhumuni ya msingi ya kutoa elimu ni kumwezesha mwanafunzi kusoma, kuhesabu, na kuandika. Madhumuni mengine ya muhimu ni kumwezesha mwanafunzi kuwa mdadisi, mchambuzi, mwenye uwezo wa kufikiri, na hata mwenye uwezo ya kupinga kwa hoja yale ambayo anafundishwa. Pengine hili la pili lingeweza kuwa muhimu kuliko lile la kwanza kama isingekuwa haiwezekani kupata uwezo huu wa pili bila kuwa na uwezo wa kusoma, kuhesabu, na kuandika.

Hali duni ya elimu iliyopo sasa inatoa nafasi ndogo sana kwa wanafunzi kuvuka ngazi ya kwanza na kuingia ngazi ya pili. Tunao wanafunzi wa sekondari wasiokuwa na uwezo wa kusoma na kuandika. Tunao wahitimu wa elimu ya juu ambao hawana uwezo wa kuridhisha kulinganisha na wenzao waliosoma miaka ya sitini na ya sabini.
Maisha ya baadaye ya hawa watoto yatakosa amani iwapo mfumo wa elimu hautaboreshwa.
Leo hii wanaopta elimu nzuri ni asilimia ndogo sana ya mamilioni ya Watanzania ambao wanapata elimu hafifu. Kwa sababu hii kila mwaka ongeko la Watanzania wenye uwezo wa kuchambua, kutafakari, kudadisi, na kupinga kwa hoja masuala mbabali mbali wanazidi kupunguka na tena kwa kasi kubwa.

Siasa ya vyama vingi imefanikiwa kifuchua maovu mengi ya siasa za chama kimoja, lakini pia vyama vingi vimejenga pia imani kwa mwananchi wa kawaida kuwa kila mtu ni mwizi. Juzi juzi nimetoka kupanda Mlima Kilimanjaro na wanafunzi wa Shule ya Sekondari ya Wasichana ya Loreto na nilimsikia mmoja wao akisema kuwa "kila mtu ni mwizi."

Hatuwezi kuacha kulaumu mienendo ya baadhi ya viongozi wetu ambayo inawafanya raia waamini kuwa viongozi wa umma waaminifu hawapo tena.

Elimu hafifu inapunguza uwezo wa raia wa kuchambua masuala mbali mbali, lakini siasa ya vyama vingi imefanya kazi nzuri ya kumfanya raia ashuku kila kitu na kila mtu. Kwa taratibu za kisheria za mfumo wa sheria unaojulikana kama civil law ni wajibu wa yule anayetuhumiwa kuthibitisha kuwa siyo mwizi, au hafanyi janja janja ya aina fulani anapokuwa kiongozi au mtumishi wa umma.

Hatari ya hali hii ni kuwa hata pale jambo linapokuwa halina mizengwe ni vigumu kwa raia kuamini hivyo. Raia wanapokuwa hawana tena imani na viongozi na mfumo wa utawala, misingi ya amani itaanza kupata nyufa. Na matukio ya miaka ya hivi karibuni yanaashiria kuwa miaka ijayo haitakuwa na amani ambayo Watanzania wamekuwa nayo kwa muda mrefu.

Sunday, September 16, 2012

Mada yangu ya leo: polisi na waandamanaji

Kuna mambo mawili muhimu yanajitokeza baada ya kuuwawa kwa mwandishi wa habari wa Channel Ten wa Iringa, Daudi Mwangosi, tarehe 2 Septemba 2012. Kwanza, Jeshi la Polisi, ambalo mmoja wa askari wake ameshafikishwa mahakamani kwa tuhuma za kuhusika na mauaji hayo, linahitaji kutoa mafunzo maalum ya namna polisi waliyopo kwenye eneo la maandamano wanavyopaswa kusimamia suala la amani katika maandamano.

Siyo kila tukio la mkusanyiko wa watu linahatarisha mali au maisha ya raia, kwa hiyo ni dhahiri pia kuwa siyo lazima kila mara kutumia nguvu zisizokuwa za lazima dhidi ya raia. Polisi wanafunzi wanapaswa kupewa elimu inayojenga taswira kuwa anaepinga serikali iliyoko madarakani siyo lazima pia awe ni adui wa Taifa au anaetishia usalama wa Taifa.

Picha inayojitokeza baada ya baadhi ya matukio ambapo polisi wameua raia ni kama vile kazi kuu ya polisi ni kuhakikisha kuwa upinzani halali wa kisiasa unaminywa kiasi cha kutosha na kuondoa kabisa uwezekano wa serikali iliyopo madarakani kuondolewa madarakani kwa njia za kidemokrasia.

Polisi wapate mafunzo kuwaelimisha kuwa kazi yao siyo kulinda maslahi ya kisiasa ya serikali iliyopo madarakani, na wafunzwe kukubali uwezekano kuwa chama chochote kilichopo upande wa upinzani kinaweza hatimaye kushinda uchaguzi na kuongoza serikali.

Jambo la pili na ambalo ni muhimu sana ni kuwa sasa waandishi wa habari wapate mafunzo ya namna ya kukusanya habari kwenye maeneo yenye usalama mdogo ili kupunguza tishio kwa usalama na maisha yao. Polisi anafanya kazi kwa amri, na kuna mazingira mengi ya kisheria yanayomruhusu polisi kutumia silaha kwa jinsi ambavyo anaona ni sawa kutokana na mazingira yanayomkabili. Polisi anayefukuzwa na kundi la waandamanaji ambao anaamini wanakusudia kumuua hatasita kutumia silaha yake dhidi ya kundi hilo. Huu ni mfano tu; haya sidhani kama ni mazingira yaliyotokea kwenye tukio lilisobabisha kifo cha Daudi Mwangosi.

Jambo la msingi ni kuwa, hata pale ambapo tunajua tunayo haki, si busara hata kidogo kubishana na mtu ambaye ameshika silaha na anaamini kuwa anatekeleza amri halali aliyopewa na mkubwa wake. Na hili haliwezi kubadilika mpaka itolewe elimu ambayo itambadilisha polisi Mtanzania ili atumie mbinu tofauti kukabiliana na waandamanaji.

Thursday, September 13, 2012

Mada yangu ya leo: kufahamu Kiingereza siyo kuwa msomi

Mada yangu leo si ndefu sana, lakini naamini ni muhimu.

Nianze na tukio moja la zamani. Niliwahi kufahamiana na raia mmoja wa Uingereza ambaye aliishi na kufanya kazi Dar es Salaam kwenye miaka ya tisini, akiwa mwajiriwa wa kampuni moja ya ulinzi. Huyu alikuwa mtu mmoja mcheshi, na mchangamfu kwa wengi aliyefahamiana nao ingawa kwa aliyewaongoza kazini alikuwa mkali sana.

Kuna Mtanzania mwenzangu ambaye naye alikuwa akifahamiana naye na alimheshimu sana, siyo tu kama binadamu mwenzake lakini naamini kwa wadhifa wake muhimu wa kuongoza kampuni yenye wafanyakazi wengi wenye jukumu la kulinda mali na makazi ya wateja wa hiyo kampuni.

Miaka kadhaa ilipita na yule Mtanzania mwenzangu siku moja aliniambia: "Unafahamu? Kumbe yule jamaa amesoma mpaka darasa la nne tu!"

Mtanzania mwenzangu, ambaye alikuwa na shahada ya chuo kikuu, hakuamini kuwa mtu aliyemdhania ni msomi mwenzake kumbe alikuwa amesoma mapaka darasa le nne tu, pamoja na kupewa jukumu la kuongoza kampuni moja mashuhuri ya Tanzania.

Tatizo nililoliona mimi lilikuwa la lugha. Kwa kipimo cha Mtanzania mwenzangu yule Mwingereza alikuwa anazungumza Kiingereza safi kabisa kuliko ambacho yeye alikuwa anamudu kuongea na kwa mantiki aliyofikia ingekuwa ni dhahiri kuwa yule jamaa alikuwa ni msomi. Kwa sababu tu anaongea Kiingereza kizuri kuliko cha kwake.

Nilimuuliza: "Sasa utamdharau kwa sababu ya ya elimu yake, wakati wote huo ukimwona ni mtu wa maana sana?"

Haya yalitokea zaidi ya miaka 20 iliyopita lakini tatizo la kumpa mtu uzito mkubwa zaidi kwa sababu anaongea Kiingereza vizuri bado lipo mpaka leo.

Friday, August 24, 2012

Mada yangu ya leo: Muungano una manufaa

Pamoja na kuwepo malalamiko mengi juu ya muungano uliounganisha Unguja na Tanganyika na kutoa Tanzania, tushukuru kuwepo kwa muungano huu kwa kutuepusha na majanga mengi.

Na wanaopaswa kushukuru zaidi ni Watanzania wa upande ulioitwa Tanganyika kabla ya tarehe 26 Aprili 1964, siku ulipozaliwa Muungano.

Bila Muungano kusingekuwepo Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ). Bila shaka ingekuwepo JWTZ lakini labda ingekuwa ni Jeshi la Wananchi wa Tanganyika.

Leo hii, makamanda wa Jeshi la Wananchi wa Tanganyika wangekuwa wakikuna vichwa kutafakari namna ya kupambana na nchi mbili: Malawi na Zanzibar. Yote hii kutokana na kutokuafikiana kwa pande mbili za Muungano kuhusu mgawanyo wa mapato yatakayotokana na mafuta yanayokisiwa kuwepo ndani ya mipaka ya Tanzania kwenye eneo la Bahari ya Hindi, na pia kutokana na madai ya Malawi kuwa eneo lote la Ziwa Nyasa ni mali ya Malawi, ikiwa ni suala linaloibuliwa na kuwepo kwa uwezekano kuwa kuna shehena kubwa ya mafuta chini ya Ziwa Nyasa. Tanzania haitambui madai hayo ya Malawi na kubainisha kuwa mpaka kati yao upo katikati ya Ziwa Nyasa.

Kwa bahati nzuri Amiri Jeshi Mkuu wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania, Rais Jakaya Kikwete, ametamka hivi karibuni kuwa mgogoro kati ya Malawi na Tanzania juu ya mpaka wa Ziwa Nyasa hautahusisha vita na kuwa utamalizwa kwa njia za kidiplomasia.

Lakini hapa tusisahau kuwa hata majeshi ya Idi Amin yalipovamia maeneo ya Tanzania mwaka 1978 Serikali ya Tanzania ilifanya jitihada kubwa za kutatua ule mgogoro kwa njia za kidiplomasia. Zile jitihada hazikufaulu kumaliza mgogoro na matokeo yake Tanzania na Uganda zikaingia kwenye vita ambayo ilileta madhara makubwa kwa pande zote mbili.

Hasara ya Uganda: gari la kijeshi lililoteketezwa na majeshi ya Tanzania ndani ya eneo la Tanzania kwenye mji mdogo wa Mutukula.
Na kwa uhakika kwa sababu ya Muungano, mgogoro kati ya Tanzania Visiwani na Tanzania Bara hautahusisha vita. Bila hivyo zingepigwa mpaka mmoja aelewe hoja ya mwenzake. Anaesema Muungano hauna faida yoyote atafakari tena.

Monday, April 16, 2012

Mada yangu ya leo

Nilikuwa katikati ya Jiji la Dar es Salaam tarehe 14 Aprili 2012 niliposikia taarifa kuwa tetemeko kubwa la ardhi lilitokea nchini Indonesia na limesababisha kuzuka kwa wimbi la Tsunami kwenye Bahari ya Hindi na kuwa wimbi hilo lilitarajiwa kufika kwenye fukwe za Afrika Mashariki jioni ya siku hiyo hiyo.

Wakazi wa Dar es Salaam walitahadharishwa kuhama maeneo yaliyo karibu na bahari, na nilishuhudia wengi wao ikiwa ni pamoja na wafanyakazi wa maofisini kwenye majengo yaliyopo katikati ya Jiji wakiondoka kwa wingi kwenye majengo hayo na kuelekea maeneo ambayo yangewaepusha na janga la kukumbwa na Tsunami.

Ilikuwa ni siku ya mvua kubwa, na kama ilivyo kawaida jijini Dar es Salaam inaponyesha mvua kubwa, kulikuwa na msongamano mkubwa sana wa magari katikati ya Jiji na maeneo ya Upanga, maeneo ambayo nilipita nikitembea kwa mguu. Naamini hali ya msongamano ilikuwa hivyo hivyo kwenye maeneo karibu yote ya Jiji ikiwa ni pamoja na kwenye barabara kuu zinazopita kandokando ya Bahari ya Hindi, sehemu ambayo ilikuwa na hatari kubwa zaidi kukumbwa na Tsunami.

Baadaye siku hiyo niliamini kuwa Mwenyezi Mungu ana upendeleo mkubwa kwa wakazi wa Dar es Salaam baada ya kusikia taarifa kuwa tishio la Tsunami halikuwa kubwa kama ilivyotabiriwa awali na hatari yoyote kwa maisha ya watu na mali ilitoweka.

Ukweli ni kuwa wimbi hilo lingefika Dar es Salaam kwa kishindo kile kile tulichoshuhudia nchini Japan basi kwa hakika tungeshuhudia maafa makubwa sana. Wakazi wengi wa Jiji hilo wangekutwa ndani ya magari yao au ndani ya daladala kutokana na msongamano mkubwa wa magari ambayo yalikuwa yakisogea hatua chache tu baada ya muda mrefu.
posted from Bloggeroid

Tuesday, September 20, 2011

Mada yangu ya leo: Kumekucha


Wakati majadiliano ya madai ya katiba mpya yanaanza niliwahi kuandika makala kwenye safu yangu ya Letter from Butiama, iliyopo kwenye gazeti la Serikali, Daily News, nikitabiri kuwa yatatokea makundi tusiyoyatarajia katika mchakato huu wa kudai haki ndani ya katiba mpya.

Baadhi ya makundi hayo yameanza kuibuka, gazeti la Majira linaripoti. Toleo lake la Septemba 16, 2011 linanmnukuu mwakilishi wa kundi la mashoga akidai nao watambuliwe ndani ya katiba mpya ili kulinda haki zao kama raia. Alinukuliwa akisema kuwa hubaguliwa wanapoomba kazi na kwa kukosa ajira wanaendelea na tabia ambazo hazikubaliki ndani ya jamii.

Hoja yangu, ambayo niliitoa kwenye makala yangu ya Kiingereza kwenye gazeti la Daily News ni kuwa suala zima la mabadiliko ya kikatiba linajikita kwenye kumpa fursa kila raia kufurahia uraia wake bila bugudha toka kwa mtu, taasisi, au kundi lingine lolote la raia. Katiba pia inaainisha wajibu wa raia katika masuala mbalimbali.

Lakini tatizo ni kuwa kwenye nchi nyingi huwa hakuna makubaliano ya mipaka ya haki hizi, na wakati nchi nyingine zinaainisha haki kwa makundi fulani ya raia wake, nchi nyingine zinaweza kuweka marufuku kwa haki hizo hizo kwa makundi ya aina hiyo.

Mfano niliotoa kwenye makala yangu ni kuwa baadhi ya nchi zimepitisha sheria zinazoruhusu ndoa za jinsia moja wakati suala hilo ni ukiukwaji wa sheria kwenye nchi nyingi duniani. Rais Robert Mugabe, ambaye ni mpinzani mkubwa wa sera hizi akihutubia nchini Zimbabwe alisema kuwa sheria hizi zinataka kuruhusu "bibi yangu (nyanya) mzazi kuona na bibi yako."

Kwetu sisi migongano hiyo sasa imefika. Raia shoga anadai haki za kikatiba. Kwa misingi ya wale wanaotufundisha kuwa kila raia anapaswa kuwa na haki chini ya katiba ya nchi ni dhahiri kuwa raia huyu anapaswa kupewa haki zake ndani ya mabadiliko mapya ya katiba.

Iko hoja itakayotolewa na waumini wa dini kadhaa, kuwa suala la ushoga ni kinyume na mafundisho ya dini. Lakini misingi ya kikatiba na haki kwa raia inakinzana na maadili kama haya ya kidini. Kwa mitazamo hiyo hiyo ya haki kwa kila raia, raia wote – wenye dini na wasiyo nayo – wanapaswa kupata haki ile ile ya msingi chini ya katiba.

Kwa mantiki hiyo, yoyote anayepinga ushoga kwa misingi ya dini anaweza kujibiwa kuwa suala la dini haliwezi kuwa kigezo kwa raia ambaye hana dini na anayedai haki zake chini ya katiba.

Maadili, mila na desturi, na tamaduni vimekuwa vigezo vinavyoongoza jamii zetu tangu enzi za mababu na bado zinaongoza jamii katika sehemu nyingi za Tanzania ambapo vigezo hivi vinatumika. Lakini maingiliano na wageni yameleta na yanazidi kuleta vigezo vipya ambavyo vitaleta mkanganyiko mkubwa ndani ya jamii kwa ujumla, na hususani ndani ya huu mjadala wa katiba mpya.

Ni dhahiri kuwa kuna mengi yatapingwa kuhusu hivi vigezo vipya na kuna uwezekano mkubwa kuwa Watanzania wengi hawatakubali kuingizwa kwa haki za mashoga kwenye katiba. Lakini litakapokataliwa ina maana kuwa tutakuwa tumeamua kuchagua 'yanayotufaa' na 'yasiyotufaa'. Na uamuzi kuwa hili linafaa na hili halifai unakinzana na azma ya kumpa kila raia uhuru wa kuwa kile anachotaka kuwa. Kwa maana nyingine, kuna mipaka ya kitamaduni inayoshinikiiza kuwa siyo kila uhuru utakubalika ndani ya jamii ya Kitanzania.

Siyo kazi rahisi kuongoza Serikali katika nyakati hizi za sasa. Zamani ilikuwa rahisi kusema hili halifai, na hili linafaa. Siku hizi kila mtu ana haki. Siku hizi tunaambiwa hata watoto ambao bado wanajikojolea kitandani wanapaswa kupewa uhuru wa kuamua wanayoyataka wao.

Ni mkanganyiko usio mdogo. Ndio maana nasema, kumekucha.

Sunday, June 5, 2011

Mada yangu ya leo: Umaskini mbaya

Mojawapo ya habari ambazo zimeandikwa kwa kina sana kwenye kipindi cha hivi karibuni ni nia ya Serikali ya kujenga Barabara ya lami kuunganisha mikoa ya Arusha na Mara kupitia mbuga ya Serengeti.

Ni habari ambayo pia imeleta mvutano mkubwa baina ya pande mbili. Upande moja ina wale wanaopinga kuwepo kwa barabara hiyo, wakidai kuwa ujenzi wake utaathiri majaliwa ya wanyamapori waliyopo Serengeti. Upande wa pili ni wale ambao wanadai kuwa ujenzi wa barabara hiyo ni kiungo muhimu cha mawasiliano kati ya wakazi wa mkoa wa Mara na mkoa wa Arusha na kuwa umefika wakati kwao pia kufaidikia ni ujenzi wa barabara kama maeneo mewngine ya Tanzania.

Wanamazingira wa ndani ya nchi na nje ya nchi wameungana kupinga kwa nguvu kabisa ujenzi wa barabara hiyo wakidai kuwa Serikali ya Tanzania imeweka sahihi mikataba ya kimataifa ya kutunza na kulinda mazingira na kuwa ujenzi wa barabara hiyo utakiuka mikataba hiyo. Aidha hifadhi ya Serengeti imeorodheshwa na Shirika la Umoja wa Kimataifa la Elimu na Sayansi (UNESCO) kama eneo la urithi wa Dunia na ujenzi wa barabara hiyo unaweza kusababisha kufutwa hadhi hiyo na kuleta athari mbalimbali kwa nchi, ikiwa ni pamoja na kupunguka kwa watalii watakaotembelea Serengeti na hivyo kuathiri biashara ya utalii na mapato yanayotokana na utalii. Na vitisho siyo vidogo, ikiwa ni pamoja na tishio la Tanzania kunyimwa misaada mbalimbali kutoka nje.

Hoja ya kwamba kwa kujenga barabara hiyo Tanzania itakuwa inakiuka mikataba ya kimataifa ambayo imeweka sahihi ni hoja yenye nguvu. Lakini tunayo mifano mingi ya nchi ambazo zinafanya maamuzi yanayokiuka sheria za kimataifa kwa misingi ya kulinda maslahi ya nchi hizo. Sisi tunaathirika na tatizo la kuwa omba omba. Maslahi ya nchi yetu tunapangiwa na nchi nyingine kwa hiyo hatuna ubavu wa kujenga hoja kuwa jambo fulani linaathiri maslahi yetu, na hivyo basi kudai mapitio ya vipengele ambavyo vitazingatia mahitaji yetu kwenye mikataba ya Kimataifa ya aina hiyo.

Hoja kuwa barabara ya lami inaweza kufuta misafara ya msimu ya wanyama kuhama kutoka upande mmoja kwenda upande mwingine nina wasiwasi nayo. Kwamba nyumbu na pundamilia wanaovuka  mbuga zenye wanyama hatari kama simba, na chui, na wanaovuka mto Grumeti uliyojaa mamba watashindwa kuvuka barabara ya lami ni mojawapo ya yale masuala ambayo wengine tunayakubali kwa shingo upande kwa sababu tu wanayoyasema ni watu ambao wanasemekana ni wataalamu wa wanyamapori na mazingira. Lakini ni hoja ya kitoto, kwa maoni yangu. Inawezekana ipo athari ya kiasi fulani itakayosababishwa na barabara ya lami, lakini siamini kuwa athari hiyo itafuta kabisa uwepo wa wanyama hao kwenye sura ya dunia kama inavyodaiwa na hawa wataalamu.

Umaskini ni tatizo, lakini wenye hoja inayounga mkono ujenzi wa barabara ya lami kupita ndani ya mbuga ya Serengeti tungekuwa na uwezo wa kifedha ingewezekana kabisa kupata wataalamu wetu wakatufanyia utafiti utakaoonyesha kuwa athari ya barabara ya lami kwa nyumbu na pundamlia siyo ya kutisha. Huu ndiyo utaratibu uliyopo nchi zilizoendelea pande zinazokinzana zinapotaka kuvunja hoja ya upande mwingine. Umesikia hivi karibuni kuna tafiti zinaonyesha kuwa matumizi ya simu za kiganja yanaweza kuleta ugonjwa wa saratani, wakati miaka yote tafiti zimeonyesha kuwa matumizi ya simu hizo hayana athari zozote?

Barabara zilizopo kwenye hifadhi za wanyama katika mataifa mengi yaliyoendelea kunakotoka shinikizo kubwa dhidi ya ujenzi wa hii barabara zimewekwa lami. Tungekuwa tuna uwezo wa kuweka msimamo tungeomba wale wote wanaopinga barabara za lami kwenye mbuga za wanyama kwanza wafumue lami zilizopo kwenye barabara zinazopita kwenye mbuga zao halafu ndiyo waje tukae meza moja kupanga namna ya kuepusha kuweka lami ndani ya mbuga ya Serengeti.

Sishabikii kumaliza wanyama, lakini naamini mahitaji ya binadamu yanawekwa nyuma ya mahitaji ya wanyama. Tatizo ni kuwa wanaharakati wa mazingira hawaambiliki, na hawana muafaka. Tunaamrishwa kusikiliza wanaosema wao, na hawasikilizi hoja nyingine zozote. Ni baadhi ya hao ambao katika jitihada za kuzuwia kuuwawa kwa baadhi ya wanyama kwa ajili ya kutengeneza makoti ya baridi kwa ajili ya binadamu, wako tayari kuua binadamu hao hao wanaovaa hayo makoti.

Hakuna tusi kubwa kwa Watanzania kama kusema kuwa mnyama ni muhimu kuliko mwanadamu. Ni kweli kwa baadhi ya wenzetu, wanyama ni muhimu sana hata kuliko binadamu. Na tumeshuhudia wanyama kufanyiwa upasuaji na madaktari bingwa kuwatibu maradhi wakati binadamu wenzao wanalala nje bila kufahamu wapi watakula, wacha kupata huduma ya matibabu.

Hoja yangu ya leo ni kuwa umasikini si sifa nzuri, na ina athari kubwa kwa nchi ambayo inajaribu kuwahudumia raia wake lakini inapata shinikizo kutoka kwa wahisani ambao kauli yao ina nguvu kuliko ile ya raia Watanzania.

Monday, May 10, 2010

Mada yangu ya leo: Kuchelewa kufika kwenye ahadi imekuwa desturi

Mada yangu ya leo siyo ndefu, lakini naamini ni ya muhimu sana.

Ni kwanini watu wengi huwa wagumu sana kutimiza ahadi za muda? Ni kwanini hawawahi kwenye ahadi wanazopanga na watu wengine? Nakiri kuwa tatizo hili hata mimi hunikuta mara moja moja, nikiwa mmojawapo wa watu wanaochelewa kwenye ahadi. Lakini nikijilinganisha na wengine, naona kuna tofauti mkubwa.

Mimi nimeishi kijijini Butiama kwa muda mrefu sasa, na nimeshuhudia kuwa suala la muda halipewi kipaumbele hata kidogo. Nimewahi kupanga mikutano na wanakijiji wenzangu mara kadhaa na pale tulipokubaliana kuwa mkutano utakuwa saa kumi jioni, watu wachache ambao unaweza kusema waliwahi kufika walianza kuingia kwenye ukumbi saa 10:45. Nilipolalamika kwanini wamechelewa kwenye kikao, waliniambia kuwa saa kumi ilimaanisha ni muda wote kati ya saa 10:01 had saa 10:59. Aidha, waliniambia kuwa ningetaka kikao kianze saa kumi basi ningewaarifu watu kuwa kikao ni saa 9:00.

Mimi sikubaliani na wanaosema kuwa hili ni tatizo la Waafrika. Ni Uafrika gani huo ambao hujitokeza siku moja na kujificha siku nyingine? Mwaafrika huyo huyo ukimwambia kuwa basi la kwenda Arusha litapita Butiama saa 11:30 alfajiri atawahi kituoni nusu saa kabla, lakini kwenye ahadi nyingine anachelewa.

Kuwahi katika vikao ni muhimu sana kwa sababu muda ule unaopotezwa kwa kusubiri wachelewaji ungeweza kutumika kufanya mambo kadhaa ya uzalishaji na maendeleo. Nina hakika kuwa hizo dakika ambazo tunazipoteza Tanzania katika mwaka mmoja zinaleta hasara kubwa sana kwenye uchumi.

Saturday, March 27, 2010

Mada yangu ya leo: biashara ya fedha za kigeni

Jambo moja ambalo napata shida sana kulielewa ni taratibu za kuendesha biashara ya fedha za kigeni nchini Tanzania.

Unapokwenda kubadliisha fedha za kigeni kwenye mabenki au maduka ya fedha za kigeni baadhi ya sehemu hizo hazipokei fedha za Marekani zenye tarehe kabla ya mwaka fulani (nadhani ni 2003). Hivi karibuni niliposindikiza wageni kubadilisha fedha zao na nilipouliza ni kwanini kuna utaratibu kama huu, niliambiwa na mfanyakazi mmoja wa tawi la benki moja iliyopo Musoma kuwa Benki Kuu ya Tanzana inaelekeza kuwa pesa hizo zisibadilishwe na badala yake zichukuliwa pesa zenye miaka ya hivi karibuni, yaani kuanzia 2004 na kuendelea.

Hili ni jambo la ajabu sana, kwa sababu Tanzania ndiyo inaweza kuwa moja ya nchi chache duniani ambayo inakataa fedha ambazo wenyewe waliyozitengeneza hawana tatizo nazo. Nadhani Wamarekani wanaofika Tanzania na dola zao wakiambiwa kuwa hapa hazina thamani, hubaki kushangaa tu. Hapa Tanzania mteja anapunjwa kwa kupewa thamani ndogo ya fedha anazobadilisha wakati wanaobadilisha wanapata thamani ile ile ya fedha ya kigeni huko nje.

Jambo lingine ambalo linaruhusiwa na taratibu za Benki Kuu ni kuweka viwango taofauti kwa noti zenye thamani kubwa (mfano za mia, na za hamsini), na viwango vya chini kwa noti zenye thamani ya chini (mfano za ishirini, na kwenda chini).

Kwa kuweka viwango viwili tofauti, ni kama vile vile mteja anafanyiwa hisani kubadilishiwa zile noti za thamani ndogo. Aidha ni kama vile huko nje noti hamsini zenye thamani ya dola moja moja zina thamani ndogo zaidi kuliko noti moja ya dola hamsini. Wanaobadilisha noti zenye thamani ndogo kwa kiwango cha chini wanapata thamani ile ile ya pesa ya kigeni wanapoipeleka nje, lakini mteja anapunjwa.

Hivi karibuni nilimsindikiza rafiki yangu Mtanzania anayesoma Uingereza kubadilisha fedha kwenye benki mojawapo ya Musoma na alipopewa viwango tofauti, hakuelewa somo. Aling'ang'ania kiwango cha juu mpaka benki wakakubali yaishe na kumbadilishia paundi zake za Uingereza kwa kiwango kile cha juu.

Kuna wakati nilipolalamika kwa mfanyakazi wa kampuni ya simu na kutaka kufahamu sababu ya kuruhusu mawakala wao kuuza vocha kwa bei inayozidi thamani iliyochapishwa juu ya vocha yenyewe (mfano, kuuza vocha ya sh.1,000/- kwa sh.1,100/-), niliambiwa kuwa hawawezi kuingilia kwa kuwa tuko kwenye mfumo wa biashara huria. Sikuelewa. Naamini pia jibu kama hilo linaweza kutumika kutetea huu utaratibu wa viwango tofauti vya kubadilisha fedha za kigeni.

Maoni yangu: hii siyo biashara huria; ni ujambazi tu uliyoidhinishwa na sheria na taratibu.