Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Showing posts with label mila na tamaduni. Show all posts
Showing posts with label mila na tamaduni. Show all posts

Friday, March 2, 2018

Hii ndiyo mila ya Kizananki ya kurudisha mahari

Miaka ya hivi karibuni baada ya kufariki mmoja wa shangazi zangu, nilipigiwa simu na baba yangu mdogo kunipa taarifa ya msiba na kunitaka nifike kwenye msiba.

Nilichelewa kidogo kufika kwenye msiba na aliendelea kunipigia simu mara kwa mara kunihimiza nifike mapema kwenye msiba. Alisema: "huu ni msiba wenu, njoo haraka!"

Sikuelewa maana ya ule kuwa "msiba wetu" mpaka baadaye.

Katika mila ambayo ilifuatwa miongoni mwa Wazanaki, mume anaweza kurudishiwa mahari na ndugu wa mke ili kuhalalisha wanandoa wawili kuachana na mke kurudi kwa ndugu zake.

Hili hutokea kwa sababu za kutoelewana kwa wanandoa, na hasa kama ndugu wa mke wanaamini kuwa dada yao anateswa au kudhalilishwa na mume wake.

Nilichojifunza kwenye msiba ni kuwa Mwalimu Nyerere alirudisha mahari kwa mume wa shangazi yangu na shangazi akarudi kuishi miongoni mwa ndugu zake.

Kwa desturi ya enzi hizo mke anayerudi nyumbani anatunzwa na ndugu zake. Kwa huyo shangazi, Mwalimu Nyerere alimjengea nyumba na aliendelea kuishi kwenye kijiji cha Butiama mpaka alipofariki.

Kwa mila hii mahitaji yake yote makubwa pamoja na ya watoto wake yatatimizwa  na ndugu zake. Aidha, inapotokea binti zake kuolewa basi mahari yao inachukuliwa na hao waliomrudisha nyumbani. Kwa mantiki hiyo, hata unapotokea msiba gharama za msiba zinabebwa na waliomtoa kwa mume wake.

Na ndiyo hapo nikaelewa kauli ya baba yangu mdogo: "huu ni msiba wenu!" Mwalimu Nyerere ana warithi wake ambao wanapaswa kurithi pia majukumu yake.

Lakini mila na desturi zinabadilika. Wakati wa msiba uliibuka ubishi mkali kati ya wazee juu ya mila hiyo. Baadhi yao waliona kuwa haipaswi kufuatwa kwa sasa.

Sunday, March 19, 2017

Unafahamu masuala haya 5 kuhusu Mwitongo?

Unafahamu masuala haya 5 kuhusu Mwitongo?

Mwitongo ni eneo la kijiji cha Butiama alipozaliwa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, rais wa kwanza wa Tanzania tarehe 13 Aprili 1922. Aidha, ni eneo alipozikwa tarehe 23 Novemba 1999.

Yafuatayo ni masuala matano ya Mwitongo ambayo pengine huyafahamu.

1. Ajali ya ndege
Mwaka 1978, baada ya majeshi ya Idi Amin Dada kiongozi wa kijeshi wa Uganda kuvamia eneo la mkoa wa Kagera, Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) lilianza kampeni ya kuondoa majeshi ya Idi Amin kwenye ardhi ya Tanzania.

Katika harakati za kujiandaa na vita hivyo, kikosi cha anga cha JWTZ kilihamisha baadhi ya ndege zake za kivita kutoka kituo cha Ngerengere na kuzipeleka kwenye uwanja wa ndege wa Mwanza.

Kwa sababu ya kasi ya hizo ndege, marubani wawili waliorusha hizo ndege walipitiliza Mwanza na kulazimika kuzunguka kuelekea upande wa kaskazini mashariki ili warudi tena kutua Mwanza. Uamuzi huo ukasababisha waruke juu ya anga ya mji wa Musoma.

Askari wa kikosi cha mizinga kilichokuwa kinalinda eneo la Musoma, kwa kukosa taarifa juu ya ndege hizo na kudhania kuwa ni ndege za adui, walizishambulia. Moja ya ndege hizo ilianguka Musoma, na nyingine iliangukia Mwitongo, kwenye msitu wa Muhunda.

Eneo la Mwitongo ilipoanguka ndege ya pili umejengwa mnara wa kumbukumbu.
Mnara wa kumbukumbu ya ajali ya ndege kwenye msitu wa Muhunda.
2. Msitu wa Muhunda
Msitu wa Muhunda ni sehemu ya eneo la Mwitongo. Ni msitu ambao, kwa mujibu wa mila na desturi za kabila la Wazanaki wa eneo la Butiama, ndiyo makazi ya mzimu wao, Muhunda. Msitu una ukubwa wa ekari 5.

Ni marufuku kukata miti iliyopo ndani ya msitu huo. Inaruhusiwa kukusanya kuni za matawi yaliyoanguka chini tu. Wazee wa kimila hufanya mitambiko ndani ya msitu huo.

Inaaminika kuwa mzimu huo hujibadilisha kuwa mojawapo ya viumbe vifuatavyo: nyani mkubwa, chui, mbuzi mkubwa, au nyoka mkubwa.

3. Mamba Mweusi (Black Mamba)
Mwinuko wa Mwitongo upo ndani ya eneo lililozungukwa na vichaka misitu, na majabali makubwa.

Ni eneo ambalo lina viumbe wadogo wadogo, pamoja na nyoka wa aina mbalimbali. Mojawapo wa nyoka hawa ni mamba mweusi.
Picha ya Mamba Mweusi. Jina lake la kisayansi ni Dendroaspis polylepis. Picha inatumika kwa idhini ya Creative Commons License. Taarifa kamili zipo hapa: http://creativecommons.org/licenses/by-sa/3.0/deed.en
Huyu ni moingoni mwa nyoka wenye sumu kali kabisa duniani, na inasemekana kuwa nyoka pekee ambaye hushambulia binadamu kwa makusudi, tofauti na aina nyingine ya nyoka ambao hushambulia tu wanapotishiwa usalama wao.

4. Ziwa Viktoria
Mwitongo ni eneo la mwinuko wa mita 1,405 juu ya usawa wa bahari. Kwa sababu ya mwinuko huo mtu anayesimama Mwitongo anaweza kuona kingo za Ziwa Viktoria zilizopo umbali wa kilomita 40 magharibi mwa Butiama.
Ziwa Viktoria.

5. Nelson Mandela
Rais wa kwanza wa Afrika Kusini, Nelson Mandela, alitembelea Mwitongo mwezi Novemba 1999. Alifika Mwitongo kuhani kifo cha Mwalimu Nyerere aliyefariki tarehe 14 Oktoba 1999.

Mzee Mandela aliandaliwa chumba maalum cha kulala wakati wa ziara yake. Kitanda maalum kiliwekwa kwenye chumba hicho. Hata hivyo, ratiba yake haikuruhusu kulala, na akaondoka siku hiyo hiyo kurudi Afrika Kusini. Kitanda kile hakijaondolewa kwenye chumba kile hadi hii leo.

Sunday, November 20, 2016

Rais Magufuli na ngoma za Ikulu: utamaduni unadumishwa

Desturi ya kupokea mgeni mashuhuri kwa kupiga ngoma ipo miongoni mwa watawala wa makabila mengi ya Tanzania.

Enzi za tawala za kitemi, hiyo ndiyo ilikuwa desturi. Mgeni, hasa yule ambaye alikuwa na hadhi ya utawala kama mwenyeji wake, alipigiwa ngoma za mwenyeji wake. Ni ngoma ambazo zilisikika kwenye himaya ya mtemi mwenyeji na zilisambaza taarifa ya kuwepo kwa mgeni muhimu.

Baada ya uhuru wa Tanganyika, desturi hiyo ilihamia kwenye Ikulu ya Dar es Salaam na viongozi mbalimbali waliotembelea Ikulu walipokelewa kwa desturi hiyo.
Rais Nyerere akimkaribisha Rais Sekou Toure wa Guinea kupiga ngoma za kumkaribisha Ikulu, Dar es Salaam.
Kumbukumbu yangu inaweza kuwa siyo sahihi, lakini sikumbuki kama baada ya Mwalimu Nyerere desturi hii ilifuatwa sana, ingawa tunaona sasa kuwa Rais wa awamu hii ya tano, John Magufuli, ameichangamkia vyema na huwashirikisha viongozi wanaofika Ikulu kupiga ngoma zilizopo Ikulu.

Inawezekana pia kuwa siyo wageni wote wanaofika Ikulu ambao hukaribishwa kwa kupiga ngoma,

Friday, August 12, 2016

Kijijini kama mjini

Wapo wengi ambao hawakupenda uamuzi wa serikali ya awamu ya nne ya kuanzisha kwa wilaya mpya ya Butiama. Mimi ni mmojawapo.

Nimejihusisha na kazi ya kutangaza historia na utamaduni wa eneo la Butiama kwa zaidi ya miaka saba sasa, na natambua ni jinsi gani utamaduni wa eneo unavyoweza kuathirika unapotokea muingiliano wa haraka kati ya maeneo ya mijini na ya vijijini. Mawasiliano mazuri kati ya miji na vijiji yanaweza kuongeza kasi hiyo, na hali kadhalika, uamuzi wa kuanzisha wilaya mpya pia unaweza kuleta matokeo hayo hayo.

Wilaya mpya inakuja na ongezeko kubwa la wafanyakazi kutoka maeneo mbalimbali. Nao siyo kama wanakuja na tamaduni zao za asili tu, ila wanaleta zaidi tamaduni za miji, na hata sheria za miji. Matokeo yake ni kudumazwa kwa tamaduni za asili za maeneo hayo mapya ya wilaya, na hasa kama yalikuwa maeneo ya vijijini.
Mojawapo ya sehemu za burudani na starehe za Butiama zilizoibuka baada ya kuanzishwa kwa wilaya mpya ya Butiama.
Msimamo wangu haulengi kutetea suala la ukabila, bali unalenga kulinda na kutunza mila na desturi za eneo mahususi kwa madhumuni ya kuendeleza utalii wa utamaduni.

Thursday, December 24, 2015

Watu kama sisi

Mwaka jana nilishirikishwa kama mmoja wa waliohojiwa kwenye filamu juu ya albino na adha wanazopata kwenye jamii. Inaelimisha vyema.

Isambaze pia kwa wengine.

Monday, June 22, 2015

Utamaduni wa utoaji majina miongoni mwa kabila la walango wa Uganda

Nimepata fursa hivi karibuni ya kuonana tena na mmoja wa watoto wa kiume wa rais wa zamani wa Uganda, Apollo Milton Obote na tuliongelea utamaduni wa kutoa majina kwa kabila lao la walango.

Nilipenda kufahamu kwa nini jina lake halina ubini wa baba yake, Obote. Yeye anaitwa Eddy Engena-Maitum, na ni askofu wa kanisa la Bright Morningstar Ministry. Alinijibu kuwa kwa mila na desturi za kabila lao, kila mtoto anayezaliwa anapewa majina yake bila kuweka jina la baba mzazi. Alifafanua kuwa majina yote ya baba yake ni yake, hakutumia ya baba yake (babu yake Eddy).

Mdogo wake naye anafuata utaratibu huo huo: ni Jimmy Akena, ambaye ni mwanasiasa na rais wa chama cha Uganda Peoples' Congress. Aidha, ametangaza nia ya kugombea nafasi ya urais kupitia chama chake kwenye uchaguzi mkuu wa Uganda utakaofanyika 2017. Alipomuoa mbunge mwenzake Betty Amongi mwaka 2013 Rais Yoweri Museveni alihudhuria harusi hiyo.

Mimi (kulia), nikiwa pamoja na Askofu Eddy Engena-Maitum jijini Kampala hivi karibuni.
Eddy anafafanua kuwa zipo faida na hasara za kutotumia ubini wa baba yao. Wakati mwingine akijitambulisha kama mtoto wa Milton Obote wale wasiomfahamu humtilia shaka wanapoona kuwa jina lake kamili halina jina la baba yake. Faida ni kuwa pale inapokuwa siyo lazima kujitambulisha hivyo inampa fursa ya kubaki bila utambulisho huo ambao, kwa watoto ambao wazazi ni wanasiasa inaweza kuwa ni jambo linalozua hisia tofauti kwa wanaobaini hali hiyo. Inaweza kutokea kubebeshwa kesi ambayo siyo yako.

Friday, November 21, 2014

Wazanaki na dini

Simulizi hii nimepewa na Mwalimu Jack Nyamwaga, kiongozi mstaafu wa kijiji cha Butiama ambaye pia anafahamu vyema baadhi ya matukio ya historia ya kabila la Wazanaki wa eneo la Butiama. Ni simulizi inayotoa picha kuhusu baadhi ya mila na desturi za Wazanaki.
Mwalimu Jack Nyamwaga, kulia, akiongea na Dk. Thomas Molony, mtafiti na mhadhiri kutoka Chuo Kikuu cha Edinburgh.
"Wamisionari wa kwanza waliofika hapa Butiama walikuwa Waprotestanti. Wakati huo Roman Catholic walikuwa wameshafika Nyegina [karibu na Musoma]. Hata hivyo Waprotestanti hawakuingia ndani sana kueneza dini miongoni mwa Wazanaki.

Halafu wakaja Seventh Day Adventist (SDA) na wakasema kuwa masharti ya madhehebu yao ni pamoja na wanaume kuoa mwanamke mmoja tu na waumini wao kukatazwa kunywa pombe. Hayo masharti hayakuwa rahisi kukubaliwa na Wazanaki ambao siyo tu walikuwa na desturi ya kuoa mke zaidi ya mmoja, lakini walikuwa na asili ya kunywa pombe na hata kuitumia katika mitambiko. Mwaka 1938 SDA wakahamia Busegwe [kijiji cha jirani] ambako kulikuwa na mchanganyiko wa makabila mengine zaidi ya Wazanaki. 
Halafu wakaja Mennonite na wao pia walikuwa na marufuku ya kunywa pombe. Hawa wakashauriwa kwenda Bumangi [kijiji cha jirani]. Mtemi Nyerere Burito alipoambiwa kuwa anapaswa kuwa na mke mmoja akauliza: "Hawa wake zangu 13 nitawapeleka wapi?"

Walipofika wamisionari wa madhehebu ya Roman Catholic Wazanaki wa Butiama wakapendekeza kanisa lao lijengwe Magorombe, kijiji kilicho mbali na Butiama kwenye ardhi inayotitia ikitarajiwa kuwa kanisa likijengwa hapo lintaanguka. Mmisionari aliyekwenda huko alipanda mikaratusi iliyofyonza maji na akajenga kanisa imara.

Waislamu walipokuja nao walikuwa na marufuku ya kunywa pombe. Wao wakashauriwa waende Nyamuswa kwa Mtemi Makongoro Matutu, ambaye alikuwa rafiki wa Mtemi Edward Wanzagi. Yeye aliwapokea na akasilimu. 
Kizingiti kikubwa cha kuwahi kuenea kwa dini miongoni mwa Wazanaki wa Butiama ilikuwa suala la marufuku ya kuoa mke zaidi ya mmoja na marufuku ya kunywa pombe."

Tuesday, September 30, 2014

Mila na tamaduni: Watanzania ni wakarimu (sehemu ya tano)

Hivi karibuni nimemaliza mzunguko wa kazi na mazoezi nikitumia baiskeli wa takriban kilomita 174 ndani ya mikoa ya Mwanza na Mara. Imenipa fursa ya kuthibitisha kuwa utamaduni wa ukarimu miongoni mwa Watanzania bado uko imara.

Jiunge nami kwenye sehemu ya tano na ya mwisho ya msafara huu...

Agosti 5
Ni zaidi ya kilomita 40 toka Bunda kuelekea Butiama na safari inaenda vizuri tu nikiwa nimejaa shauku ya kumaliza hili zoezi.
Hata hivyo adui mkubwa wa masafa marefu kwa baiskeli ni njaa na suala la kupata chakula cha mchana ni muhimu kabisa ili kuweza kuendesha baiskeli kwa saa zaidi ya tano kwa siku ya leo. Naenda kwa wastani wa kilomita kama 11 kwa saa. Kwa hiyo nalazimika kusimama tena Nyamisisi kukamilisha mlo wangu wa mchana kabla ya kuendeela na safari hadi Butiama. Nyamisisi ni sehemu ambayo siyo mashuhuri tu kwa matunda ila ina sifa ya kuwepo wataalamu juu ya taarifa za wanasoka na wasanii maarufu.

Napumzika sehemu ambayo nilikaa na Elvis Lelo Munis miezi kadhaa iliyopita alipopita hapa akielekea Nairobi na baadaye Moshi. Elvis ni Mtanzania ambaye alizunguka nchi zaidi ya mia moja za dunia akitumia baiskeli na alimaliza ziara yake hiyo ya maelfu ya kilomita mwezi Julai 2014. Nimekula chipsi mayai na baadaye naanza ngwe ya mwisho ya mzunguko wangu.
Mimi namalizia ziara yangu ya kilomita zaidi ya 170 lakini nahisi nahitaji mapumziko baada ya safari yangu ya kutoka Ukerewe mpaka Butiama.

Saturday, September 27, 2014

Mila na tamaduni: Watanzania ni wakarimu (sehemu ya nne)

Hivi karibuni nimemaliza mzunguko wa kazi na mazoezi nikitumia baiskeli wa takriban kilomita 174 ndani ya mikoa ya Mwanza na Mara. Imenipa fursa ya kuthibitisha kuwa utamaduni wa ukarimu miongoni mwa Watanzania bado uko imara.

Jiunge nami kwenye sehemu ya nne ya msafara huu...

Agosti 4
Sijaendesha baiskeli kwa masafa marefu kwa muda mrefu kwa hiyo leo naanza kusikia mwili unapanga njama za kuanzisha mgomo wa kutoendelea na safari. Hata hivyo hii ni njia ambayo nimeshawahi kupita kwa baiskeli kuelekea Ukerewe na muda si mrefu najikuta nimefika kwenye kiwanda cha kuchambua pamba cha Bulamba.

Inanipa matumaini kuwa safari ya kwenda Bunda imepungua kwa kiasi kikubwa. Nilipokaribia Bunda nilikimbiliwa na mtoto wa miaka sita hivi akaniomba pesa. Huwa nawakanya watoto wasiwe na tabia ya kuomba pesa kwa wapita njia ili kulinda usalama wao. Hata hivyo kwa leo ninakiuka taratibu zangu mwenyewe na kufanya naye majadiliano yafuatayo:

"Unataka pesa za nini?"
"Za kununulia pipi."

Hapo nilifungua mfuko wangu na kutoa kipande cha chokoleti kilichochanganywa na karanga. Alipofungua kifungio naamini ile taswira ya alichokiona ilimfanya asite kidogo akaniuliza:

"Hiki ni nini?"
"Kula tu ni tamu sana."

Alivyoonja alicheka ghafla akiwa na furaha isiyo na kifani halafu akaniambia: "Uwe unapita hapa kila siku!"
Alipofungua chokoleti alisita kuila.
Alinisababisha mimi pia kucheka.

Taarifa inayofuata: Naagiza chipsi mayai

sehemu ya tatu ya makala hii

Wednesday, September 24, 2014

Mila na tamaduni: Watanzania ni wakarimu (sehemu ya tatu)

Hivi karibuni nimemaliza mzunguko wa kazi na mazoezi nikitumia baiskeli wa takriban kilomita 174 ndani ya mikoa ya Mwanza na Mara. Imenipa fursa ya kuthibitisha kuwa utamaduni wa ukarimu miongoni mwa Watanzania bado uko imara.

Jiunge nami kwenye sehemu ya tatu ya msafara huu...

Agosti 3
Mapema asubuhi nilianza safari yangu ya baiskeli ya kurudi Butiama kwa kuelekea kwenye kivuko cha Rugezi na ni leo ndiyo iliyodhihirisha kwangu kuwa Watanzania bado watu wakarimu. Nilipovuka upande wa pili kwenye mji mdogo wa Kisorya, nilisimama kwa muda kwenye mgahawa kuongeza mlo wa asubuhi wa chapati mbili na chai, ingawa ilikuwa inakaribia saa tano asubuhi.

Nikiwa na uhakika kidogo wa kuendelea na safari yangu mpaka njaa itakaponilazimisha kusimama na kula chakula cha mchana, nilianza safari ya kuelekea Kibara. Hata hivyo haikuchukuwa muda nikalazimika kusimama kutafuta chakula kwenye kijiji kilicho njiani.

Pembeni yangu niliona jengo linafanana na mgahawa. Alitokeza binti mmoja na mazungumzo yakawa hivi:

"Una chakula?"
"Ndiyo"
"Chakula gani?"
"Chai na chapati"
"Mimi nimeulizia chakula, siyo chai."
"Samahani, nina chai na chapati tu."

Niliendelea kudadisi:

"Kwani wewe mchana huli chakula?"
"Nitakula.
"Unapika nini?"
"Ugali na dagaa."
"Basi ongeza na cha kwangu halafu nitakulipa."

Akakubali. Chakula kilipokuwa tayari akanikaribisha kwenye mgahawa wake, akanipa maji ninawe na yeye akanawa tukakaa pamoja kula.
Niliegesha usafiri wangu, nikapiga picha, halafu nikaingia kusubiri chakula.
Wakati nakaribia kushiba nikapata nguvu za kuongea kidogo na kumwomba radhi kuwa nimempunguzia chakula chake kwa siku hiyo. Aliniambia nisijali, na kuwa labda kuna siku na yeye atanitembelea na mimi nitamkaribisha chakula.

Nikijiandaa kuondoka nilimuuliza nimlipe kiasi gani kwa kile chakula. Alinishangaa na kuniambia: "Wewe si nilikwambia kuwa hakuna tatizo? Pesa za nini?"

Nikabaki hoi. Lakini nilifungua mfuko wa baiskeli yangu na kutoa pakiti ya biskuti nikampa na kusema ni zawadi kwa watoto wake. Alifurahi sana na kuniuliza bei ya biskuti zile. Nilimwambia shilingi elfu tatu nikapanda basikeli na kuanza safari ya kuelekea Kibara.

Vijijini wema huu bado upo. Sina hakika kama mijini hali imebakia hivi.

Taarifa ijayo: Hiki ni nini?

Sehemu ya pili ya makala hii

Saturday, September 6, 2014

Mila na tamaduni: Watanzania ni wakarimu (sehemu ya pili)

Hivi karibuni nimemaliza mzunguko wa kazi na mazoezi nikitumia baiskeli wa takriban kilomita 174 ndani ya mikoa ya Mwanza na Mara. Imenipa fursa ya kuthibitisha kuwa utamaduni wa ukarimu miongoni mwa Watanzania bado uko imara.

Jiunge nami kwenye sehemu ya pili ya msafara huu...

Agosti 2
Tulitembelea makazi ya kwanza walipofikia Wakristu wa kwanza kutua kwenye kisiwa cha Ukerewe zaidi ya miaka 100 iliyopita. Hakuna maelezo mengi sana kuhusu eneo hili ila simulizi za mauaji yaliyofanyika hapo dhidi ya baadhi ya wageni hao na mtawala wa eneo hilo wa wakati huo. Ni eneo ambalo liko kwenye kilima chenye mwinuko mkubwa unaowezesha kuona umbali mkubwa juu ya Ziwa Viktoria. Mwenyeji wangu aliniambia kuwa nyakati ambapo hakuna ukungu yawezekana kuona ndege zikipaa na kutua kwenye uwanja wa ndege wa Mwanza.
Ukerewe ni kisiwa chenye mandhari za kuvutia na visiwa vingi vinavyokizunguka. Upande wa kulia wa picha kinaonekana kisiwa cha Bwiru.
Baada ya hapo tulitembelea eneo la ufukweni wa ziwa ambapo mjasiria mali mmoja wa Nansio, makao makuu ya wilaya ya Ukerewe, anajenga hoteli itakayozingatia utunzwaji wa mazingira wa eneo hilo.

Taarifa ijayo: Watanzania ni watu wakarimu

sehemu ya kwanza ya makala hii
sehemu ya tatu ya makala hii

Saturday, August 23, 2014

Mila na Tamaduni: Watanzania ni wakarimu (sehemu ya kwanza)

Hivi karibuni nimemaliza mzunguko wa kazi na mazoezi nikitumia baiskeli wa takriban kilomita 174 ndani ya mikoa ya Mwanza na Mara. Imenipa fursa ya kuthibitisha kuwa utamaduni wa ukarimu miongoni mwa Watanzania bado uko imara.

Jiunge nami kwenye msafara huu...

Agosti 1
Safari yangu ilianzia Mwanza kwa kuvuka na meli iitwayo MV Clarias kuelekea Nansio, Ukerewe. Huko nilipokelewa na muongozaji wageni maarufu wa kisiwa cha Ukerewe, Tumaini Yohana Ladislaus ambaye ni mmiliki wa Tumaini Tours.
Muda mchache kabla ya kuanza safari ya kuelekea Ukerewe kutokea Mwanza.
Siku ya kwanza alinipeleka kwenye makazi ya Mtemi Gabriel Ruhumbika, kwenye kijiji cha Bukindo ambako tulipata maelezo mafupi ya historia ya eneo hilo kutoka kwa mmoja wa waongozaji anayepokea wageni katika makazi hayo. Mtemi Ruhumbika ni baba mzazi wa Mtemi Michael Lukumbuzya ambaye alishika nyadhifa kadhaa serikalini ikiwa ni pamoja na kuwa balozi wa Tanzania nchini Canada.
Muongozaji wageni akitoa maelezo ya picha mbili za Mtemi Michael Lukumbuzya.
Tulipotoka hapo tulielekea kwenye kijiji cha Murutunguru. Hapa ilikuwa sawasawa na kufungua kurasa za kitabu cha watu mashuhuri. Niliambiwa hapa ni nyumbani kwa aliyekuwa mkuu wa walinzi binafsi wa Rais Julius Kambarage Nyerere; hapa ni nyumbani kwa aliyekuwa spika wa bunge la Afrika Gertrude Mongella; hapa ni nyumbani kwa aliyekuwa spika wa bunge la Tanzania, Pius Msekwa, na kadhalika, na kadhalika. Na ni hivyo hivyo katika sehemu nyingi ya kisiwa cha Ukerewe.

Inasemekana Ukerewe ndiyo eneo lenye mkusanyiko mkubwa zaidi kwa kilomita za mraba za wasomi wa shahada za uzamivu kuliko sehemu yoyote ile Tanzania, na pengine hata Afrika.

Itaendela na: Mjasiriamali wa Ukerewe

sehemu ya pili ya makala hii

Friday, November 29, 2013

Maajabu ya mapishi [imefanyiwa masahihisho]

Hii ni tafsiri ya makala ya lugha ya Kiingereza niliyoandika na ikachapishwa kwenye gazeti la Daily News kwenye safu yangu iliyoitwa Letter from Butiama, makala nilizoandika kati ya mwaka 2005 na 2011. Makala hiyo ilichapishwa tarehe 26 Juni 2005.
*****************************************************
Inasemekana kuwa biashara zote zinazohusu nyama ndani ya mkoa wa Mara zinadhibitiwa na Wazanaki. Utawakuta kwenye kila ngazi ya biashara hiyo kama wamiliki, kama wafanyabiashara wa kununua na kuuza ng'ombe, na muhimu zaidi, kama wamiliki wa bucha. Aidha wamepata mafanikio wakubwa kwenye biashara hiyo kwenye jiji la Mwanza.

Somo kubwa linalojitokeza katika kuchunguza masuala yanayobainisha kampuni zenye mafanikio makubwa na zile zenye mafanikio duni ni ukweli kuwa mameneja wa kampuni zenye mafanikio wamejikita kwenye shughuli za bidhaa na huduma ambazo wanazielewa vyema. Inaelekea kuwa mmoja wa wafanyabiashara wa ng'ombe niliyeonana naye anaelewa vyema ukweli huu. Alinipa somo kuhusu hali mbali mbali za nyama kutoka sehemu tofauti za mwili wa ng'ombe na kuhitimisha kuwa nyama ya ng'ombe yenye ladha bora kuliko zote ni inayopatikana sehemu ya ndani ya paja la ng'ombe. Uelewa usiyo wa kawaida kama huu pengine ndiyo chanzo cha Wazanaki kutawala biashara ya ng'ombe na nyama ndani ya mkoa wa Mara. Napata picha ya matajiri wa Kizanaki wakimiliki biashara ya nyama ya bara la Afrika kama ambavyo Wajapani wamedhibiti biashara ya magari.

Pamoja na hii hamasa ya Wazanaki juu ya ng'ombe na nyama, ukweli unabaki kuwa hisia kali ya mtu mmoja inaweza kuwa mwiko kwa mtu mwingine. Migongano mikubwa ya kitamaduni inaweza kupatikana kwenye chaguzi ambazo watu toka tamaduni mbalimbali wanafanya kuhusu chakula wanachokula na kile wasichokula. Kwa baadhi ya dini kula nyama ni mwiko. Mboga na nafaka ndiyo hutumika kama vyakula vya msingi kwa jamii hizi.

Suala la chakula lilizua taharuki kwenye ziara mojawapo ya Rais Nyerere katika miaka ya sabini kwenye nchi mojawapo ya Ulaya. Kama ilivyo desturi kwenye misafara ya viongozi wa nchi, kiongozi mwenyeji wa nchi ile aliandaa dhifa ya taifa kwa mgeni wake, na baada ya juma moja Rais Nyerere akaandaa dhifa kwa mwenyeji wake. Wakati wa dhifa ya pili, mmoja wa Watanzania waliokuwa kwenye msafara ule alimdanganya Mtanzania mwenzake kuwa miongoni mwa vyakula vilivyoandaliwa kwenye dhifa ya kwanza ilikuwa ni pamoja na vyura na kuwa yule mwenzake alikula hao vyura bila kufahamu.

Aliyetoa taarifa hiyo alikusudia yawe mazungumzo kati yao tu, lakini aliyepewa taarifa ya kula miguu ya vyura alianza kujisikia vibaya hapo hapo na akaanza kutapika wakati dhifa ikiendelea.

Nilipokuwa mwanafunzi nchini Italia mimi na rafiki yangu George kutoka Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo tulialikwa chakula cha jioni na mwenyeji wetu Mtaliani. Baada ya kutuagizia chakula alisema kuwa alikuwa ametuchagulia chakula mahususi kwa ajili yetu ambacho huandaliwa marafiki wa karibu kabisa au wageni mashuhuri. Ukweli ni kuwa alikuwa ametuagizia miguu ya vyura. Ilikuwa mara yangu ya kwanza kula miguu ya vyura na nakumbuka ladha ilikuwa kama ya samaki. Mara tulipowekewa sahani zetu mezani na mhudumu, George alishituka na alitaka kuhama kabisa ile meza tuliyokaa. Mimi na mwenyeji wetu tulipoanza kushambulia ile miguu nakumbuka George alipata shida kubwa kubaki kwenye meza moja na sisi na kuangalia kitendo ambacho ni dhahiri kilimfadhaisha sana.

Mwenyeji wetu, ambaye aliwahi kutembelea nchi kadhaa za Afrika, alishangaa sana George. Alimuuliza anawezaje kuona kinyaa kula miguu ya vyura wakati yeye ameshuhudia Waafrika wakila wale wadudu ambao hutokeza baada ya mvua kunyesha. Alikuwa anazungumzia senene. George naye alishindwa kumuelewa Giuseppe. Mtu anawezaje kulinganisha kula senene na miguu ya vyura? Alisema Giuseppe alikuwa analinganisha vitu ambavyo havipaswi kulinganishwa kabisa.

Kuacha mimi, hamna kati yao ambaye alikuwa ameshakula miguu ya vyura pamoja na senene. Kimya kimya niliwashangaa hao wawili ambao walikuwa wanabishana ubishi ambao hawakuwa na mamlaka hata kidogo ya kuuendeleza. Jambo ambalo sikuweza kulibainisha wakati ule ni chakula kipi, kati ya chura na senene, kilikuwa na ladha nzuri zaidi.

Ukweli ni kuwa yawezekana kufikia usemi kuwa ladha ya chakula ni uamuzi ambao uko kichwani mwa mtu mmoja mmoja. Nimewahi kujitwika ujasiri usiyo na mfano na nikala chakula ambacho machoni kilikuwa kinatisha kuangalia lakini nikajikuta nimeweka mdomoni chakula chenye ladha nzuri kuliko maelezo. Tofauti na mwananchi mwenzangu ambaye alikuwa kwenye ziara ya Rais Nyerere, mimi nilifahamu chakula nilichokula siku ile kwenye ule mgahawa nchini Italia, kwa hiyo jambo la kushangaza ambalo naweza kulizungumzia ni ladha nzuri tu ya miguu ya vyura.

Thursday, July 11, 2013

Mandhari mpya ya Mwitongo, Butiama

Mandhari ya eneo la Mwitongo inaendelea kupendeza kutokana na kazi ya mtaalamu wa kutengeneza vihenge, Kisyeri Magese.
Kwa miezi kadhaa sasa, mtaalamu huyu asilia kutoka kijiji cha jirani, Nyamuswa, anakarabati na kujenga upya vihenge vya kuhifadhia nafaka ambavyo viko kwenye makazi ya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere kwenye eneo la Mwitongo, kijijini Butiama na ambavyo Mwalimu Nyerere alivitumia kuhifadhia ulezi aliolima.

Baadhi ya vihenge, kama kinachoonekana kwenye picha (kulia), vimekamilika na kazi yote inatarajiwa kukamilika mwezi Agosti 2013. Hili ni eneo linalotembelewa na wageni wanaofika Butiama.

Sunday, July 7, 2013

Maana ya Mwitongo

Kwa kabila la Wazanaki Mwitongo ni jina la eneo walipoishi watu zamani na kuhama. Ni mahame.
Kwa mila za Wazanaki tukio lililofanya watu wahame eneo ilikuwa kufariki kwa mkuu wa kaya. Baada ya kuzikwa tu mali zake zote (na zama hizo hata wake walikuwa ni mali) zilirithiwa na kuhamishiwa kwa warithi.

Mwitongo kwenye kijiji cha Butiama ni eneo alipoishi na kuzikwa Mtemi Nyerere Burito, baba mzazi wa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere. Mwalimu Nyerere naye amezikwa eneo hilo hilo tarehe 23 Oktoba 1999.

Chief Nyerere alizikwa tarehe 30 Machi 1942.

Saturday, May 11, 2013

Desturi ya Wazanaki ya kupokea mahari

Siku chache zilizopita nimehudhuria sherehe ya kupokea mahari ya kitukuu wa Mtemi Edward Wanzagi wa Butiama.
Wageni wanajitambulisha.

Wageni (waliosimama), wanawasalimia wenyeji.
 Desturi inaelekeza kuwa mahari lazima ipokelewe kabla ya saa sita mchana, yaani kabla jua halijavuka na kuwa upande wa magharibi.
Kukagua mahari.
Kuna mlolongo mfupi wa matukio yanayohusiana na sherehe hiyo. Wageni wanaoleta mahari wanatambulishwa kwa wenyeji wao, na wao wanatambulisha upande wao. Halafu, wageni wanajongea walipoketi wenyeji na "kuwaamkia." Na kama ishara ya heshima wageni wote wanaamkia "shimakoo" hata kwa wale wageni ambao wanaostahili "shikamoo" zao kutoka kwa baadhi ya wenyeji. Wakati wa kusalimia wenyeji huketi wakati wageni wanasimama mbele ya wenyeji.
Kukagua mahari.
Baada ya salamu ndiyo unawadia wakati wa kukabidhiwa mahari. Mahari iliyoafikiwa ni ng'ombe sita, na mbuzi wanne. Wenyeji hukagua mahari kuhakikisha kuwa ng'ombe na mbuzi wako kwenye hali nzuri. Na hapo ilitokea mmoja wa wazee kwa upande wa wenyeji kutamka kuwa mmoja wa ng'ombe alikuwa na homa, hakuwa mzima. Na desturi ingelazimisha yule ng'ombe kurudishwa na kuletwa mwingine ambaye hana tatizo. Lakini ikaamuliwa kuwa pengine hali hiyo ya ng'ombe ilisababishwa na safari ndefu ya kuwafikisha pale Butiama na kuwa baada ya muda hali ya kawaida ya ng'ombe yule itarejea.
"Ng'ombe mmoja ana homa," alisema mzee mmoja baada ya kuwakagua ng'ombe.
Baada ya hapo msemaji wa wenyeji anatamka kuwa mahari imekamilika na kina mama wanapiga vigelegele.  Inafuata hatua ya kukabidhi zawadi ndogo kwa wazee (blanketi), na kwa mama wa bibi harusi (kitenge na sufuria). Mwisho kwenye ratiba ni chakula na baadaye wageni kuondoka.
Mzee Joseph Muhunda Nyerere anapokea blanketi kutoka kwa mwakilishi wa Bwana Harusi.
Baada ya hapo inasubiriwa siku ya kufunga ndoa. Kwa mila na destru za zamani, ndoa ingekuwa imekamilika baada ya kupokelewa mahari.

Maharusi watarajiwa hawahudhurii sherehe hii.

Wednesday, May 1, 2013

Ukarimu wa Watanzania unatoweka

Enzi zilizopita utamaduni wa Mtanzania ulihusisha pia ukarimu. Leo hii utamaduni huo unatoweka.

Nianze kwa tukio lililonitokea yapata miaka 27 iliyopita. Nilikuwa nasafiri kutoka Arusha kuelekea Butiama nikiendesha gari nikiwa peke yangu. Nilitoka kwenye lango la Ikoma la Hifadhi ya Serengeti jioni na mvua kubwa ilikuwa inanyesha. Kwa sababu kiza kilikuwa kimeingia na kwa sababu barabara ilikuwa mbaya sana kutokana na mvua na ilikuwa dhahiri gari ingeweza kuzama kwenye matope na kusababisha nilale porini, nilipofika Fort Ikoma niliamua kuelekea Mugumu ili niweze kulala huko na kuendelea na safari kesho yake.

Kutokana na mvua kubwa iliyoendelea kunyesha, barabara kati ya Fort Ikoma na Mugumu nayo ilikuwa mbaya sana lakini Landrover 109 niliokuwa naendesha ilimudu kukabiliana na hali mbaya ya barabara ingawa mara kadhaa ilielekea kunasa kwenye matope. Katikati ya safari yangu kuelekea Mugumu, ikiwa imepita saa 3:00 usiku na nikiwa katikati ya pori, nilikutana na mtu mmoja akitembea kwa mguu ambaye aliashiria kunisimamisha na kuomba nimchukue. Nilisimamisha gari kumchukua. Alikuwa anaelekea Mugumu.
File:Land Rover Series III 109.JPG
Aina ya gari niliyoendesha siku hiyo. Picha: Buckers.
Nakumbuka tulifika Mugumu baada ya saa 5:00 usiku na sikufanikiwa kupata chumba kwenye hoteli za Mugumu. Zote zilikuwa zimejaa. Yule mtu niliyemchukua porini alinuchukua mpaka anakoishi akanipisha chumba chake nikalala mpaka asubuhi na kuendelea na safari yangu ya kuelekea Butiama. Bila yeye ningelala ndani ya gari.

Hiyo ndiyo Tanzania ya zamani. Ya watu wenye kuaminiana na wenye ukarimu ambao leo hii ni vigumu kuuona. 

Pamoja na kuwa miaka 27 iliyopita nilisimamisha gari katikati ya pori na kumpa msaada mtembea kwa miguu ambaye sikuwa namfahamu, nakiri kuwa leo hii nitasita kusimamisha gari mchana kumchukuwa mtu nisiyemfahamu katika eneo lolote la Tanzania. Na hata yule mtu aliyenipisha kitanda chake sidhani kama leo hii atathubutu kukaribisha mtu asiyemfahamu alale chumbani kwake bila kuwa na hofu kuwa mgeni wake atahama na baadhi ya mali zake.

Imani inatoweka na ukarimu unafifia kutokana na mabadiliko ndani ya jamii ambayo yameleta Watanzania wasiyothamini uhai wa binadamu wenzao na hivyo kusababisha kubadilika kwa mila na desturi ambazo tulizoea zamani.

Monday, April 15, 2013

Muhunda 'aonekana' tena Butiama

Mzimu wa kabila la Wazanaki wa Butiama unaojulikana kama Muhunda 'umeonekana' Butiama siku chache zilizopita.

Taarifa kuhusu Muhunda ambazo nilizitoa kwenye makala zilizopita hizi hapa:


Kwa mujibu wa mtoa habari, Muhunda 'alionekana' jioni ya tarehe 11 Aprili 2013 jirani na eneo la msitu wa Muhunda. 'Alionekana' Butiama mara ya mwisho Julai 2011.

Friday, February 15, 2013

Wazanaki na mirathi

Kwa desturi ya kabila la Wazanaki, wapwa ndiyo walirithi mali za marehemu. Baadhi ya sababu zinazotajwa kwa jamii ya Wazanaki kufuata mila hii ni kuwa baba wa familia hakuwa na uhakika kuwa watoto waliozaliwa na mke (wake) zake walikuwa ni wa kwake.

Kwa sababu hiyo urithi walipewa wapwa kwa sababu, kupitia kwa dada yake, baba huyo alikuwa na uhakika kuwa anapofariki mali zake zinabaki kwa ndugu ambao ana uhusiano nao wa damu.

Mila hii ilianza kupungua nguvu kwenye msiba wa mmoja wa wadogo zake Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, Joseph Kizurira Nyerere aliyefariki tarehe 8 Agosti 1994.
Mzee Joseph Kizurira Nyerere, kushoto, alikuwa shabiki mkubwa wa Vijana Jazz Orchestra.
Akizungumza baada ya mazishi ya mdogo wake, Mwalimu Nyerere alisema umefika wakati kwa Wazanaki kuachana na hiyo desturi na kurudisha mirathi kwa mke na watoto wa marehemu.

Sunday, February 3, 2013

William Rutta anaandika kuhusu senene katika utamaduni wa Wahaya


William Rutta ni Meneja wa Kiroyera Tours. Hapa anatoa maelezo kuhusu utamdauni wa kabila la Wahaya wa kula senene.
*************************************************
Senene katika utamaduni wa Wahaya
William Rutta
na William Rutta

Senene (Ensenene, kwa Kihaya) ni miongoni mwa wadudu wanaotumiwa sana na kabila la Wahaya mkoani Kagera kama kitoweo, pengine kuliko kabila lolote tangu enzi za mababu.

Pamoja na wadudu hao kuheshimika katika kabila la Wahaya, historia kamili ya asili ya wadudu hao bado haijulikani.

Mwanzoni senene waliliwa na wanaume peke yake. Wanawake walionywa wawe na haya siku zote na wasivunje mwiko kwa kula senene na vitu vyote vilivyokatazwa. Wanawake wote walikuwa na utii wakiheshimu mila na desturi za kabila lao hivyo kutokana na haya hiyo waliitwa “WAHAYA”. 

Wasichana walipeleka zawadi ya senene kwa wachumba wao kama ishara ya kuonyesha upendo na utayari wa kuolewa na mchumba huyo. Msichana ambaye hakufanya hivyo uwezekano wa kuolewa na mchumba wake ulikuwa mdogo, hivyo senene walitumika kama ishara ya upendo na uaminifu.

Zipo aina nyingi za senene lakini wale wanaozungumziwa hapa wamegawanyika katika kundi lijulikanalo kama Orthopterous. Hawa ni jamii ya panzi wapole ambao hawana tabia ya kuharibu na kuteketeza makazi yao kwa chakula kama walivyo nzige wengine. Senene huzaliana kwa wingi katika mwambao wa maziwa makuu baada ya kutaga mayai yao ardhini kipindi cha kiangazi.

Baada ya kutaga mayai na kuangua mzunguko wa maisha yao huishia kati ya mwezi Oktoba na Desemba ambapo kipindi hiki huwa ni msimu wa mvua za vuli zijulikanazo kwa wahaya kama Omusenene. Hiki ni kipindi ambacho senene huruka wakiwa katika makundi wakihitimisha safari ya maisha yao.

Pamoja na kutumika kama kitoweo pia jamii imeanza kufaidika na senene kama chanzo cha kujipatia kipato, jambo ambalo limeufanya mkoa wa Kagera hasa Bukoba kujulikana sana kitaifa na kimataifa, pia kutokana na uchunguzi wa madaktari imeonekana kuwa senene wanaongeza vitamin “C”

Taarifa nyingine inayofanana na hii:
http://muhunda.blogspot.com/2011/09/lugha-yetu-kiswahili.html

Taarifa nyingine inayofanana na hii kutoka kwenye blogu yangu ya lugha ya Kiingereza
http://madarakanyerere.blogspot.com/2012/10/akamwani-traditional-welcome-gesture-in.html