Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Thursday, October 25, 2012

Msanii Kingkapita ametoa nyimbo mpya

Msanii wa Hip Hop, Kingkapita, ametoa kibao kipya chenye jina: Shikamoo pesa.



Taarifa aliyoisambaza mwenyewe inaeleza:
"Nilimshirikisha Tash, mzee wa chapia mulemule kutoka Arachuga. Nyimbo imerekodiwa katika studio za Rocanna Basemennt chini ya producer Jimmy Jizze na master kumaliziwa Home Town Record chini ya master Traveller."

Sikiliza kibao hicho hapa: http://www.hulkshare.com/7u4tpclsbwu8

Tuesday, October 23, 2012

Huduma ya bure kufasiri Kiswahili kwa Kiingereza*

*Vigezo na viwango kuzingatiwa: kutokana na kuwa na majukumu mengine naweza kupokea kazi kidogo tu kwa siku.

Nimechunguza kiwango cha watu wengi kumudu uandishi wa lugha ya Kiingereza - na hata lugha yetu ya Kiswahili - na, kwa maoni yangu, picha inayojitokeza ni kuwa kiwango hakiridhishi. Hapa nazungumzia Watanzania wa kada mbali mbali, kuanzia wasomi na wale ambao hawakupata fursa ya kupata elimu ya juu.

Kwa bahati mbaya imejengeka tabia inayohusisha uongo kuwa mtu anayeongea au kuandika kwa lugha ya Kiingereza ndiyo anadhihirisha kuwa ana elimu nzuri. Kwa sababu hii, watu wengi ambao wangeweza kufanya mawasiliano kwa lugha ya Kiswahili hung'ang'ana kuongea au kuandika kwa Kiingereza pasipo kuwepo uwezo mzuri wa kufanya hivyo. Kama ambavyo kutofahamu Kichina haihusiani na kutokuwa na elimu, vivyo hivyo kutofahamu Kiingereza hakuashirii kutokuwa na elimu.

Hata hivyo kuna ukweli kuwa yapo mazingira yanayolazimu mtu kuandika au kuwasilisha mada kwa lugha ya Kiingereza. Hapa naamini naweza kusaidia kutokana na uwezo wangu wa zaidi ya miaka 20 wa uandishi kwa lugha za Kiingereza na Kiswahili na uandishi kwa ujumla.

Najitolea kufasiri maandishi kutoka lugha ya Kiswahili kwenda kwenye lugha ya Kiingereza iwapo maandishi hayo hayatazidi kurasa moja ya ukubwa wa A-4. Lakini nikiri kuwa nikiona dalili kuwa kazi ni kubwa nitatoza ada kuanzia kurasa ya pili na kuendelea.

Mimi si mtaalamu wa lugha kwa hiyo siwezi kutoa tafsiri rasmi, ila nina uzoefu wa kutosha wa uandishi katika lugha za Kiswahili na Kiingereza kiasi cha kuweza kutoa tafsiri zinazokidhi viwango vya kuridhisha vya uandishi.

Nitumie maandishi yako kwa barua pepe na nitakurudishia tafsiri siku inayofuata:

kiswahilikwakiingereza@gmail.com

Monday, October 1, 2012

Mwanafunzi wa kidato cha nne afika kilele cha Mlima Kilimanjaro

Mwanafunzi Placidia Prudence wa Shule ya Sekondari ya Wasichana Loreto ya jijini Mwanza ambaye alikuwa kwenye msafara wa kukwea Mlima Kilimanjaro amefanikiwa kufika kilele cha mlima huo tarehe 28 Septemba 2012.

Nami nilikuwa kwenye msafara huo ambao ulishirikisha wanafunzi wengine 15 toka shule hiyo pamoja na walimu watatu. Katika wote tulioshiriki ni yeye peke yake alifanikiwa kufika kileleni ambako alifika akiongozana na muongozaji Entold Mpunga.
Placidia Prudence akiwa kwenye kambi ya Horombo baada ya kufika kwenye kilele cha Mlima Kilimanjaro. Kushoto, juu, unaonekana Mlima Kilimanjaro.
Mwanafunzi Nusra Alkarim, mwalimu wa michezo Isack Katambi, na mimi tulifanikiwa kufika Gillman's Point, mita 5,685 juu ya usawa wa bahari na kiasi cha mwendo wa kama saa moja na nusu toka kilele cha Uhuru alikofika Placidia. Kilele cha Mlima Kilimanjaro kina urefu wa mita 5,895 juu ya usawa wa bahari.

Msafara huo ulipangwa kwa madhumuni ya kuchangisha pesa za mradi wa kuboresha na kufikisha maji safi na salama kwenye shule ya Loreto.

Placidia ana umri wa miaka 20 na ameniarifu anakusudia kuwa mhandisi.

Sunday, September 23, 2012

Pambano la ndondi Oktoba 14 kumuenzi Mwalimu Nyerere

Mabingwa wa uzito wa kati (kilo 72.5) wa Uganda na Tanzania wanaotambuliwa na Tanzania Professional Boxing Organization (TPBO) watapambana tarehe 14 Oktoba mwaka huu Friends Corner Bar, Manzese, Dar es Salaam katika pambano lilioandaliwa kumuenzi Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, aliyefariki zaidi ya miaka 12 iliyopita.

Pambano hilo litawapambanisha bingwa wa Tanzania Thomas Mashali, juu, na bingwa wa Uganda, Med Sebyala, chini.


Mchezo huo utakuwa wa kuwania ubingwa wa Afrika Mashariki.

Bondia Sebyala ameshawahi kupambana na kushindwa kwa pointi na bondia Francis Cheka, bingwa wa mabara wa Afrika anayetambuliwa na International Boxing Federation (IBF). Aidha, ameshawahi kupambana na Rashidi Matumla na ingawa mapambano yote alishindwa kwa pointi, alitoa upinzani mkali kwa mabondia hao Watanzania.

Bondia Mashali anayo sifa ya kutoa vichapo vikali kwa wapinzani wake na kuwapumzisha kwa knock-out za mapema.

Taarifa kutoka TPBO zinaeleza kuwa kwa kumuenzi Mwalimu Nyerere na kuthamini juhudi zake za kuendeleza michezo TPBO itaandaa mapambano ya ngumi kwenye kila maadhimisho ya kifo chake tarehe 14 Oktoba.

Friday, September 21, 2012

Twist mpaka chini: harusi za Tanzania zinafanana sana

Sijui ni hisia zangu tu, lakini nahisi kama mtiririko wa ratiba za harusi ninazohudhuria siku hizi zinafanana sana.

Kwenye harusi nilizohudhuria hivi karibuni nimeshuhudia kuna wakati wa kuita kamati iliyoandaa harusi na kila mwanakamati hujitambulisha. Salama ipo kama wanakamati bado hawajachangamka kwa vinywaji vinavyoondoa aibu mbele ya kadamnasi. Lakini kama wanakamati wameshachagamka mambo huwa hayatabiriki.
Mara wanapomaliza kujitambulisha na kueleza mambo waliyofanya kufanikisha harusi, basi muongozaji wa sherehe anaagiza DJ aweke twist ya uhakika.

Na mara zote nimeshuhudia kuwa wimbo unaopigwa ni ule ule. Uchezaji nao ni ule ule, haujabadilika tangu miaka ya hamsini ingawa silalamikii uchezaji nao ubadilike.