Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Monday, November 12, 2012

Uchaguzi nafasi 10 za wajumbe wa NEC - CCM Tanzania Bara, Wassira aongoza

Matokeo ya chaguzi za nafasi 10 za wajumbe wa NEC Tanzania Bara wa Chama cha Mapinduzi zinazoendela Dodoma yametoka. Matokeo haya hapa:

1.  Stephen Wassira                  - 2,135
2.  January Makamba               - 2,093
3.  Mwigulu Nchemba             - 1,967
4.  Martine Shigela                  - 1,824
5.  William Lukuvi                  - 1,805
6.  Bernard Membe                 - 1,455
7.  Mathayo David Mathayo   - 1,414
8.  Jackson Msome                  - 1,207
9.  Wilson Mukama                 - 1,174
10. Fenela Mukangara            -     984

Saturday, November 10, 2012

Konyagi watoa ala za muziki kwa Msondo Ngoma

Kampuni inayotengeneza kinywaji Konyagi imetoa zawadi ya ala za muziki kwa bendi kongwe ya muziki wa dansi nchini, Msondo Ngoma.
Msondo Ngoma jukwaani.
Akikabidhi hizo ala, Mkurugenzi Mkuu wa Tanzania Distilleries Limited ambao ndiyo watangenezaji wa Konyagi, alisema vifaa hivyo vimetolewa kwa ajili ya kuenzi utamaduni wa Mtanzania na kuiwezesha Msondo Ngoma kuwa imara katika kutoa burudani kwa Watanzania.

Alisema, "Msondo ni bendi kongwe tangu kuanzishwa kwake mwaka 1964. Imesimama imara katika kutoa burudani ya uhakika kwa Watanzania na kutumia nyimbo zake katika kuelimisha, na kufunza jamii ya Watanzania walio wengi."

Alisema kwa kuwapatia vyombo hivyo, Msondo Ngoma itakuwa moto wa kuotea mbali katika kutoa burudani ya uhakika, hali itakofanya bendi nyingine kuwa wasindikizaji katika tasnia ya muziki wa dansi nchini.

Mkurugenzi wa bendi hiyo, Maalim Gurumo, alisema kwa sasa wana deni kubwa kwa Watanzania na kampuni ya Konyagi katika kutoa burudani ya uhakika baada ya kupatiwa vifaa hivyo.
Mkurugenzi wa Tanzania Distilleries Limited David Mgwasa, wa pili kutoka kulia, akikabidhi ala kwa wanamuziki wa Msondo Ngoma.
"Tunaamini baada ya leo kupata vifaa hivi tutatoa burudani ya uhakika sanjari na kukijenga vyema kikosi chetu kwa lengo la kukiimarisha," alisema Gurumo.

Kiongozi wa bendi, Saidi Mabela, alitoa shukurani kwa kampuni ya Konyagi kwa kuwapatia vyombo na aliahidi kuendelea kutoa burudani safi kwa Watanzania na Afrka kwa ujumla.
Habari kamili ziko hapa.

Tuesday, November 6, 2012

Mlima Kilimanjaro unapendeza zaidi tokea Tanzania au Kenya?

Kuna mdau hapa anauliza swali: Mlima unaonekana vizuri tokea Tanzania au Kenya? Huyu mdau anahisi kuna hujuma inafanywa na jirani zetu kuvutia wageni wengi zaidi waende Kenya na ndiyo maana hoja hii inaibuliwa.

Hili swali halipaswi hata kuulizwa. Mlima Kilimanjaro unavyoonekana kutokea Kenya ni tofauti kidogo na unavyoonekana upande wa Tanzania. Kama kuna mtu kapendezewa na taswira ya mlima tokea Kenya huwezi kumlazimisha afurahie taswira ya mlima huo kutoka upande wa Tanzania.

Lakini huu utaratibu wa kulalamikia jirani zetu wa Kenya kunufaika na Mlima Kilimanjaro wakati sisi wenyewe tumekaa na kuongea tu pia hauna manufaa yoyote kwa maendeleo yetu.

Ninavyoamini mimi, mgeni yoyote aliyetoka nje ambaye amekuja kukwea mlima huu maarufu hajali kama uko Kenya, Tanzania, au kwenye sayari ya Zuhura. Mgeni anavutiwa na mlima wenyewe na siyo mipaka ya nchi.

Mimi nimeshakwea Mlima Kilimanjaro mara kadhaa na ukweli ni kuwa ni Watanzania wachache sana wanakwenda huko kulinganisha na wageni wa nje. Kwa kweli kule mlimani Mtanzania ndiyo mgeni na wageni ndiyo wenyeji kwa sababu idadi yao ni kubwa sana. Hivi karibuni nimekutana na Wakenya kibao kwenye njia ya Marangu wakielekea kileleni.

Mimi ningefurahi sana kuona hawa wenye uchungu na mlima huu kusemwa uko Kenya basi wawe wanajitokeza mara moja moja nao kukwea huu mlima. Hiyo itawawezesha kuzungumzia mlima wao kwa kujiamini badala ya kuuliza maswali tu na kulalamika.
Mlima Kilimanjaro unavyoonekana kutoka upande wa Tanzania.
Kitu ambacho watajifunza ni kuwa mandhari nzuri kuliko zote za mlima huu ziko huko huko mlimani. Lakini haya ni maoni yangu tu.

Sunday, November 4, 2012

Lugha yetu Kiswahili

Jana kwenye redio nimesikia marudio ya majadiliano kutoka kwenye vikao vya Bunge la Muungano vinavyoendelea sasa hivi. Alisikika mbunge mmoja, akiwa anatetea hoja kuwa lugha ya Kiswahili itumike kwenye uendeshaji wa shughuli za mahakama, akisema yafuatayo (siyo nukuu halisi kwa maana ya neno kwa neno lakini ni sahihi kwa maana ya nukuu yenyewe):

"...mienendo yote ya shughuli za mahakama iendeshwe kwa lugha ya Kiswahili tu, na kusiwe na option ya Kiswahili au Kiingereza, iwe ni Kiswahili tu."

Anayesisitiza matumizi ya Kiswahili pekee kwenye shughuli za mahakama za Tanzania anajenga hoja yake kwa kutumia neno la Kiingereza.

Ni kazi kweli kweli.

Kwenye kamusi neno option lina maana kadhaa, ikiwa ni pamoja na: uchaguzi, na hiari.

Thursday, November 1, 2012

Mada ya yangu ya leo: aliyeikashifu Kurani aadhibiwe

Kwa hali ya kawaida, mtoto aliyedhalilisha kitabu kitukufu cha dini ya Kiislamu angeweza kuadhibiwa kwa kuchapwa bakora na mzazi wake au kupewa adhabu nyingine nzito ambayo watoto wote wanaokosea hupewa.

Lakini tukio liliotokea siyo la kawaida, kama ambavyo tumeshuhudia madhara yaliyofuata na vurugu zilizotokana na kitendo kile. Makanisa yalivamiwa na mali nyingi kuporwa na kuharibiwa. Uporaji wa mali haufanani hata kidogo na Uislamu kwa hiyo ni dhahiri kuwa katika kundi la watuhumiwa wa matukio haya ambalo linasemekana kuwa ni la waumini wa dini ya Kiislamu walishiriki pia watu ambao hawakusukumwa na hasira ya kudhalilishwa kwa Kurani na dini ya Kiislamu bali ni watu waliyoona fursa ya kuharibu na kupora mali.

Tanzania inayo sheria inayosimamia watuhumiwa ambao wako chini ya umri wa miaka 18. Ni dhahiri hakuna ubishi kuwa huyo mtoto alifanya kosa hilo. Jambo moja ambalo linaweza kuepusha manung'uniko ya dhati ya waumini wa dini ya Kiislamu kulalamikia kile kitendo ni kufikisha suala la yule mtoto mahakamani bila uchelewesho. Kufanya hivyo kutaondoa kabisa kisingizio cha wale ambao wanatafuta fursa ya kufanya fujo kwa kisingizio cha kutetea hadhi na heshima ya dini ya Kiislamu.

Nina hakika yule mtoto tayari anajutia kitendo chake, lakini suala la kutafuta suluhu baina ya waumini wa dini mbalimbali, na suala la kulinda amani nchini linahitaji hatua za kisheria zichukuliwe haraka dhidi yake.