Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Tuesday, July 12, 2011

Siasa ya Tanzania: chama na sera zake, au mtu?


Kwenye picha ya hapa chini anaonekana diwani wa kata ya Muleba, Hassan Milanga wa Chama cha Wananchi (CUF), mwenye fulana nyekundu, akiteta jambo na wapiga kura wake wa mjini Muleba, ambao pia ni wafanyabiashara wa samaki. Milanga aliingia kwenye siasa mwaka 2000 na akachaguliwa kuwa diwani kwa tiketi ya Chama cha Mapinduzi (CCM).
Kutokana na kile anachokieleza kuwa ‘mizengwe’ilizomzuwia kubaki CCM wakati wa uchaguzi mkuu wa mwaka 2005 alihamia CUF, na wapiga kura wakahama naye na kumchagua kwa mara ya pili kuwaongoza kama diwani wao.

Wapiga kura wakarudia tena kufanya hivyo hivyo mwaka 2010. Ni dhahiri kuwa kwa sehemu nyingi za Tanzania wapiga kura wanachagua mtu na siyo chama. Swali: Ina maana wagombea wanapoteza muda kunadi sera wakati wa kampeni?

Saturday, July 9, 2011

Wageni wa Butiama: Kwaya ya Uamsho ya Musoma yafika Mwitongo kutengeneza video


Kwaya ya Uamsho ya Dayosisi ya Musoma ya Kanisa la Anglikana ilizuru Mwitongo juzi kuandaa video ya nyimbo ambazo inakusudia kutoa katika kipindi cha mwezi mmoja kuanzia sasa. 
 Katika ya miaka ya hivi karibuni kwaya kadhaa zimetembelea Butiama kwa madhumuni ya kutengeneza video kutokana na mandhari murua iliyopo kwenye eneo la Mwitongo.

Wednesday, July 6, 2011

Kituo cha redio kwenye Mtandao chaanzishwa

Taarifa hizi nimepata hivi punde toka kwa  Sillah Mbuya:
JINA LA WEBSITE: TONE INTERNET RADIO

LINK: 
http://www.toneinternetradio.blogspot.com

Tunapenda kuwatambulisha Watanzania wote waishio popote Duniani kwamba kuanzia sasa wanaweza sikiliza redio kupitia mtandao yani "Internet" Buree. Tumeona tufanye hivi kwa kutambua kwamba pamoja na kuwa Watanzania wengi wapo hapa nchini na wengi wao kwa sasa wanatumia Mtandao na wanapenda sikiliza redio kupitia Mtandao, lakini pia tumezingatia na Watanzania wenzetu wanaoishi nje ya nchi wapate burudani, habari na mambo mengine mengi kutoka Tanzania. Kupitia Tone  Internet Radio watakuwa hawajisikii upweke na kuona kama wapo Tanzania. Pia Tone Radio inawapa nafasi wasanii wa muziki wa aina yoyote Tanzania kuleta nyimbo zao hapa studio na sisi kutangaza kazi zao bure kwa kututumia nyimbo zao kupitia toneinternentradio@yahoo.com .
Karibuni sana
Tunatanguliza shukurani zetu za dhati na karibuni sana...
Tone Internet Radio Pamoja Tutafika

Sillah Mbuya

Tuesday, July 5, 2011

Machinga wa Dar es Salaam


Kabla ya mwaka 1999 niliishi na kufanya kazi jijini Dar es Salaam, halafu baada ya hapo nikahamia kijijini Butiama.

Kuna mabadiliko makubwa yanaonekana jijini Dar es Salaam kwa mtu ambaye anakuwa nje ya jiji hilo kwa muda. Siyo rahisi kwa wakazi wa Dar kuona hayo mabadiliko kulinganisha na anayetokea nje ya Dar. Nakiri huwa “nashangaa” kwa mabadiliko makubwa ninayoyaona Dar kila ninapotembelea huko. Mfano, hivi karibuni nilienda sehemu ambapo ilikuwepo Sno Cream, jirani na Shule ya Forodhani, nikakuta jengo lile ilipokuwa Sno Cream limebomolewa na kuna jengo jipya linajengwa. Niliambiwa Sno Cream walishahama pale siku nyingi.

Kundi la watu wenye uzoefu wa kuwasoma watu “wanaoshangaa” ni machinga wanaorandaranda jijni Dar es Salaam wakiuza bidhaa mbalimbali. Miaka kadhaa iliyopita nilitembelea Dar es Salaam na nilikuwa nimekaa na rafiki zangu wa siku nyingi sehemu ya vinywaji na chakula inayoitwa George’s Grill. Machinga aliingia pale akiuza vitu na alikuja moja kwa moja kwangu akijaribu kuniuzia bidhaa. Nilimuuliza: ‘”Mimi fala? Katika watu wote waliokaa hapa umeona mimi ndiyo nafaa kuwa mteja wako?”

Yule machinga alijibu: “Hapana, siyo hivyo mzee”, akionekana kujizuwia kucheka.

Baada ya kuondoka Dar na kuisha kijijini kwa muda mrefu ni dhahiri kuwa nina mueleko ambao ni tofauti na wa wakazi wa Dar es Salaam, hasa  wale niliokaa nao meza moja. Yule machinga aliiona hiyo tofauti (labda kwa mavazi yangu) na akanilenga mimi moja kwa moja. Hainisumbuwi, lakini ndiyo hali halisi.

Mwanzoni mwa mwaka huu nilionana na mwanafunzi mwenzangu wa siku nyingi tuliyesoma naye Chuo cha Elimu ya Biashara (Shycom) miaka iliyopita. Anasema enzi hizo, miaka 33 iliyopita, sisi wanafunzi wa Shycom kutoka Dar tulionekana wajanja sana kuliko wanafunzi wengine ambao walitokea maeneo mengine ya Tanzania. Leo nimegeuka mawindo ya machinga.

Monday, July 4, 2011

"Wagumu" wa Mlima Kilimanjaro

Mgeni yoyote anayepanda mlima Kilimanjaro anahitaji huduma ya waongoza msafara, wapishi, na wabeba mizigo. Hili kundi la mwisho wanajulikana kama “wagumu” kwa sababu ya ugumu wa kazi wanayofanya ya kumbebea mgeni vitu muhimu vinavyohitajika: mahema, chakula, maji, na vifaa vingine vya lazima.
Mgumu (kushoto) akiwa na mzigo wake baada ya kumpita Muongoza Msafara (mwenye kofia nyekundu) anayeongoza mgeni aliye nyuma yake.
Asubuhi wao huamka mapema kuandaa kifungua kinywa kwa wageni wakishirikiana na mpishi. Baada ya kifungua kinywa Muongoza Msafara (ambaye naye huanza kazi kama mbeba mizigo kwa miaka kadhaa) huongoza msafara wa wageni kuelekea kwenye kambi inayofuata. Msafara wa kukwea Mlima Kilimanjaro unaweza kuchukuwa kati ya siku 5 hadi 12, kutegemea na njia inayotumika.

Baada ya msafara kuondoka kambini, wagumu huvunja kambi na kufungasha mahema na mizigo mingine yote na kuanza safari ya kuelekea kambi inayofuata. Kwa kuwa ni wazoefu wa kubebea mzigo, huupita msafara wa wageni na Muongoza Msafara na msafara unapofika kwenye kambi wageni wanakuta wagumu wameshasimika upya mahema yote, na mpishi anakuwa tayari ameshapika chakula cha wageni. Wanafanya hivi kila siku ya msafara.
 
Wagumu wanayo sifa ya kutumia pesa inayotokana na kazi yao ya kusindikiza wageni kupanda Mlima Kilimanjaro kwa fujo. Dada mmoja mhudumu wa baa moja ya mjini Moshi aliniambia baadhi yao wanapolipwa pesa yao huhamia baa mpaka pesa iishe. Pesa inapoishia kwenye pombe, wengine hujisababishia majeraha ya mwili na kudanganywa wake zao kuwa wameporwa malipo yao na vibaka.
Wagumu wa Kilimanjaro wakifurahia siku ya mwisho ya msafara katika Kambi ya Mweka.
 Hii ndiyo baadhi ya mikasa ya wagumu wa Kilimanjaro.
Wagumu wa Kilimanjaro wakifurahia siku ya mwisho ya msafara katika Kambi ya Mweka.