Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Monday, September 10, 2012

Wageni wa Butiama

Bi Victoria Gilago Bache kutoka Makumbusho ya Taifa alitembelea Butiama hivi karibuni akifanya utafiti juu ya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere.

Bi Victoria ni msimamizi wa nyumba aliyoishi Mwalimu Nyerere iliyopo eneo la Magomeni, Dar es salaa, Mtaa wa Ifunda.
Bi Victoria akiwa ndani ya maktaba yenye mkusanyiko wa vitabu zaidi ya 8,000 vya Mwalimu Nyerere kwenye nyumba ya Mwalimu Nyerere iliyopo eneo la Mwitongo, Butiama.
Utafiti wake ulijikita juu ya maisha ya Mwalimu na familia yake wakati wanaishi kwenye nyumba hiyo ya Magomeni kabla ya uhuru, mwaka 1961.

Saturday, September 8, 2012

Wachawi wa siku hizi

Hii taarifa ni tasfiri ya makala ya lugha ya Kiingereza niliyoiandika mwaka 2005 kwenye gazeti la Sunday News.

Amini au usiamini kuhusu uchawi lakini ukweli unabaki kuwa uchawi ni suala lisiloepukika kwenye jamii za Kiafrika. Butiama nayo haiwezi kukwepa ukweli huu.

Mwezi Mei mtuhumiwa wa uchawi ambaye nitamuita Pepe alitimuliwa Butiama na wanakijiji waliyomtuhumu kufuga na kufanya biashara ya mazuu. Inaaminikia mazuu ni binadamu ambao huzikwa wakiaminika wamekufa lakni hufufuliwa kwa njia za kichawi na hufanyishwa kazi kwenye mashamba na pia kutoa huduma kadhaa za weledi.

Mfanyakazi wa hospitali ambaye mfanyakazi mwenzake aliyekuwa daktari alifariki hivi karibuni amesema kuwa yule mfanyakazi mwenzake, ambaye wote tunajua kuwa ni marehemu, sasa hivi anaendesha hospitali kwenye ulimwengu wa siri wa mazuu. Hospitali hiyo ina upungufu wa wafanyakazi na "mchawi" aliyetimuliwa ndiyo anasadikiwa kupeleka watu wa kuziba nafasi zilizo wazi.

Pepe alijijengea desturi ya kufanya shughuli za kawaida katika mida ambayo siyo ya kawaida. Wanakijiji wenzake wakijiandaa kulala yeye ndiyo kwanza aliwaelekeza mafundi kuendelea na ujenzi wa nyumba yake katika mida ambayo pia inajulikana ndiyo mida wale ambapo wale wanaominika kuwa wasaidizi mahiri wa wachawi, yaani fisi na bundi, wanakuwa na pirika pirika nyingi na mizunguko ya huku na kule.

Jambo moja la kushangaza ni kuwa fundi mmojawapo ambaye alishiriki kwa kipindi kifupi nyakati za usiku kujenga nyumba ya Pepe alikiri kuwa hajaona muda mzuri wa kujenga nyumba kuliko usiku kwa sababu usiku hakuna wale wapiga porojo wa mchana ambao hupunguza kasi ya kazi. Huyo fundi aliacha ujenzi wa nyumba ya Pepe baada ya kupata onyo kali kutoka kwa wazee wa kimila, wanyikura.

Baada ya hapo wanyikura walituma wito kwa Pepe kumtaka aeleze sababu ya kujenga nyumba usiku. Alielekezwa kuendeleza ujenzi wake mchana kama wengine na akafuata kwa muda lakini baadaye akarudia tena ujenzi wa usiku. Alipata wito mwingine kuonana na wanyikura lakini safari hii badala ya kuitika wito, siyo tu hakuhudhuria kikao kilichoitishwa kwa ajili yake, lakini akatuma onyo kwa wazee kuwa wakiendelea kumfuata fuata atawafungulia mashitaka mahakamani na wangeweza kujikuta jela. Kama hii ni kweli basi alikuwa amefanya kosa kubwa sana. Wazee wa jadi ni taasisi muhimu sana ya kimila. Ni dhahiri kuwatishia huku kuliibua tafrani kubwa zaidi.

Wanyikura ni kama serikali. Pepe alikuwa anachochea moto. Kwa kulipiza kisasi wanyikura wakaanza kuweka vikwazo. Hakuna aliyeruhusiwa kuongea naye. Yoyote ambaye angekiuka hiyo amri angeweza kutozwa faini, aghalabu ng'ombe mzima, kutegemea na mazingira ya ukiukwaji uliyofanyika. Athari za ukiukwaji wa aina hii kwenye mazingira ya mjini yanaweza kuwa ni madogo sana, lakini kwenye kijiji, ambapo ushrikiano na wengine ni muhimu sana katika kila nyanja, vikwazo vinaweza kuwa na athari kubwa sana. Nilipata taarifa kuwa mmiliki mmoja wa duka alipewa onyo kali na wazee wa kimila baada ya kumuuzia Pepe vocha za simu.

"Angekubali tu amri ya wazee, akakubali kulipa faini, na kuendela kujenga mchana, angekuwa bado yupo," alisema fundi. Kusingezuka kisingizio cha kumfukuza. Aliwadharau wazee akawapa mwanya wale waliyokuwa wanamshuku kwa uchawi kufanya njama za kumtimua kijijini.

Ukichukulia kuwa mtu yoyote anayeaminiwa kuwa ni mchawi anachukuliwa kuwa hawezi kuwa na woga wa aina yoyote na kuwa ni mkatili mmmoja ambaye hurandaranda usiku akitafuta binadamu wa kuwadhuru akitumia fisi kama usafiri wake, mimi nilifikia uamuzi kuwa Pepe hakufanana asilani na taswira hii. Jioni moja, nilikuwa naendesha gari nikitokea Musoma na nilisimamishwa na kundi la watu waliyokuwa wamesimama pembeni ya gari nyingine ndogo. Miongoni mwao alikuwa Pepe. Alinijulisha kuwa walikuwa wakielekea Musoma lakini baada ya kukuta mawe makubwa yameegeshwa katikati ya barabara niliyopita mimi muda ule ule kabla ya kuwafikia, waligeuza gari haraka wakihofu kushambuliwa na majambazi wenye silaha.

Niliwaambia sikuona mawe yoyote barabarani na kuongeza kuwa yawezekana kuwa baada ya wao kugeuza gari na "majambazi" nao wakatawanyika wakihofia nia yao mbaya imegundulika.

Kutokana na maelezo yangu baadhi ya abiria wa ile gari walifarijika na wakaanza jitihada za kumshawishi dereva apite palepale na kuendelea na safari kwenda Musoma. Mtu pekee aliyeamua kuwa kuendelea na safari ya Musoma ni hatari alikuwa mtuhumiwa wa uchawi, Pepe. Aliniomba lifti tukarudi naye Butiama.

Tuesday, September 4, 2012

Katiba mpya itamke lugha rasmi ya bunge kuwa Kiswahili

Kama kuna kundi liliojijengea utaalamu wa kuvuruga lugha ya Kiswahili, kundi hilo ni la viongozi wa kada mbalimbali hapa Tanzania. Na vinara zaidi wa kuivuruga lugha ya Taifa ni wabunge wetu.

Ukisikiliza mjadala wa Bunge la Muungano ni vigumu kupita dakika kumi bila anayeongea kutumia neno la Kiingereza ndani ya mjadala unaoendeshwa kwa lugha ya Kiswahili. Baadhi ya watu wameipachika jina tabia hii ya kuchanganya lugha za Kiingereza na Kiswahili kuwa ni kuongea kiswanglish, neno lisilo rasmi kwenye lugha zote mbili.

Kuna dhana potofu miongoni mwa viongozi wetu wa sasa kuwa unapochanganya mazungumzo kwa kutumia maneno ya Kiingereza kwenye mazungumzo yako, basi wewe unaonekana kuwa ni mtu msomi. Na utakuta viongozi hawa hawa hata kwenye maandishi yao wanaweza kutumia neno la Kiswahili halafu kwenye mabano wanatoa fasili ya neno hilo hilo kwa lugha ya Kiingereza, kama vile kuwakumbusha wale wanaosoma maelezo yao kuwa wasisahau kuwa wao ni wasomi.

Jambo moja dhahiri ni kuwa ni Watanzania wachache sana wanaoelewa hayo maneno ambayo viongozi wetu, katika jitihada za kukogana wao kwa wao, wanayoyatumia kwenye maandishi na matamshi ikiwa ni pamoja na kwenye mijadala, mikutano, na kwenye vyombo vya habari.

Naamini umewadia wakati kwa lugha ya Kiswahili kutamkwa kuwa ndiyo lugha rasmi ya kutumika ndani ya Bunge la Muungano. Haileti mantiki kwa mwananchi aliyepiga kura kumchagua mbunge asielewe anachojadili mbunge wake.

Sunday, September 2, 2012

Dk. Kenneth Kaunda, rais mstaafu wa Zambia

Mwezi Juni 2007 nilialikwa jijini London, Uingereza, kwenye uzinduzi mpya wa Azimio la Arusha na nikafikia kwa wenyeji wangu, Selma James na Nina Lopez, wote ambao hawali nyama. Nikiwa natokea kwenye kabila ambalo ukizungumzia "chakula" ni sawa sawa na kutamka "nyama" na ambapo mboga za majani zinaliwa na mifugo peke yake, zile siku kumi nilizokaa London nikila mboga za majani zilikuwa ni mtihani mkubwa kwangu.

Nilimudu kwa jitihada kubwa kuishi hizo siku kumi bila kula nyama na niliporudi Tanzania watu walioniona walisema kuwa nilionekana kijana kuliko ninavyostahili. Nilihisi kuwa yawezekana kuwa kulishwa mboga za majani kwa siku kumi bila hiari yangu nikiwa London ndiyo kulisababisha mimi kuonekana kijana.

Imani yangu kuwa ulaji wa mboga za majani kwa siku kumi ndiko kulisababisha kupunguza kuzeeka kwangu ilinisukuma kuacha kula nyama na nikaanza jitihada ya kuwa mlaji mboga za majani tu na kuacha kula aina zote za nyama.

Mwaka mmoja baada ya hapo, nikiwa kwenye mkutano jijini Maputo, Msumbiji, nilipata fursa ya kuonana na  Dk. Kenneth Kaunda, rais mstaafu wa Zambia ambaye ni maarufu pia kuwa mtu ambaye hali nyama.
Rais mstaafu wa Zambia, Dk. Kenneth Kaunda, kulia.
Aliniambia aliacha kula nyama mwaka 1952 kupinga sera za kibaguzi za serikali ya kikoloni ya Waingereza iloyoelekeza wamiliki wa bucha kuweka madirisha mawili tofauti ya kuwauzia nyama Waafrika na wazungu. Yeye hanywi pombe, kahawa, wala chai lakini anakunywa maji ya matunda kila siku.

Kitendo hicho cha upinzani wa kisiasa kinaelekea kufanikisha kupunguza idadi kubwa ya miaka ya huyu rais mstaafu mwenye umri wa miaka 88. Ni mwingi wa nguvu na mchangamfu sana. Kwenye mkutano Maputo kila alipoitwa kwenye jukwaa alienda kwa mchakamchaka.

Mtanziko mkubwa unaonikabili, mkubwa zaidi kuliko uamuzi wa kuacha kula nyama, ni kipi kitakachofuata kuacha kula kati ya samaki na kuku.

Tuesday, August 28, 2012

Hatimaye, watu wa sensa hawa hapa

Jumapili, tarehe 26 Agosti, nilikaa nyumbani siku nzima nikisubiri kuhesabiwa kwenye Sensa ya Taifa lakini sikuona mtu hata mmoja kuja kuniuliza swali. Hatimaye leo maafisa wa sensa ya Taifa wamefika kunihoji maswali yao 62, ambayo kila mshiriki anapaswa kuyajibu.

Wengi wetu hatukukumbuka kuwa ni zoezi la juma zima.
Mimi, kushoto, nikijibu maswali ya Sensa ya Taifa leo asubuhi. 
Ndani ya muda wa dakika kumi zoezi lilimalizika na wakaondoka.

Pamoja na kwamba wengine tulikuwa na shauku kubwa ya kukamilisha kazi hii kuna Watanznia wenzetu ambao kabla ya zoezi hili kuanza wamekuwa wakiendesha kampeni ya wazi kuhimiza Waislamu wasishiriki kwenye sensa kwa sababu maswali yale 62 hayaulizi dini ya anayehesabiwa.

Nimejaribu kuuliza hili swali lakini mpaka leo sijasikia jibu lake: tunataka kujua kuna Watanzania wangapi wa dini mbalimbali ili tutumie hizo takwimu kufanya nini? Mwenye jibu naomba anifahamishe.