Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Sunday, September 23, 2012

Pambano la ndondi Oktoba 14 kumuenzi Mwalimu Nyerere

Mabingwa wa uzito wa kati (kilo 72.5) wa Uganda na Tanzania wanaotambuliwa na Tanzania Professional Boxing Organization (TPBO) watapambana tarehe 14 Oktoba mwaka huu Friends Corner Bar, Manzese, Dar es Salaam katika pambano lilioandaliwa kumuenzi Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, aliyefariki zaidi ya miaka 12 iliyopita.

Pambano hilo litawapambanisha bingwa wa Tanzania Thomas Mashali, juu, na bingwa wa Uganda, Med Sebyala, chini.


Mchezo huo utakuwa wa kuwania ubingwa wa Afrika Mashariki.

Bondia Sebyala ameshawahi kupambana na kushindwa kwa pointi na bondia Francis Cheka, bingwa wa mabara wa Afrika anayetambuliwa na International Boxing Federation (IBF). Aidha, ameshawahi kupambana na Rashidi Matumla na ingawa mapambano yote alishindwa kwa pointi, alitoa upinzani mkali kwa mabondia hao Watanzania.

Bondia Mashali anayo sifa ya kutoa vichapo vikali kwa wapinzani wake na kuwapumzisha kwa knock-out za mapema.

Taarifa kutoka TPBO zinaeleza kuwa kwa kumuenzi Mwalimu Nyerere na kuthamini juhudi zake za kuendeleza michezo TPBO itaandaa mapambano ya ngumi kwenye kila maadhimisho ya kifo chake tarehe 14 Oktoba.

Friday, September 21, 2012

Twist mpaka chini: harusi za Tanzania zinafanana sana

Sijui ni hisia zangu tu, lakini nahisi kama mtiririko wa ratiba za harusi ninazohudhuria siku hizi zinafanana sana.

Kwenye harusi nilizohudhuria hivi karibuni nimeshuhudia kuna wakati wa kuita kamati iliyoandaa harusi na kila mwanakamati hujitambulisha. Salama ipo kama wanakamati bado hawajachangamka kwa vinywaji vinavyoondoa aibu mbele ya kadamnasi. Lakini kama wanakamati wameshachagamka mambo huwa hayatabiriki.
Mara wanapomaliza kujitambulisha na kueleza mambo waliyofanya kufanikisha harusi, basi muongozaji wa sherehe anaagiza DJ aweke twist ya uhakika.

Na mara zote nimeshuhudia kuwa wimbo unaopigwa ni ule ule. Uchezaji nao ni ule ule, haujabadilika tangu miaka ya hamsini ingawa silalamikii uchezaji nao ubadilike.

Monday, September 17, 2012

Msondo Ngoma bado wanatamba

Wapiga gitaa wa bendi ya Msondo Ngoma Abdul Ridhiwani, kushoto, na Zahoro Bangwe, kulia,
wakiburudisha mashabiki wao hivi karibuni wakati bendi hiyo ilipotumbuiza kwenye ukumbi wa Max Bar, Ilala Bungoni, Dar es Salaam.

Msondo Ngoma ni moja ya bendi kongwe za muziki wa dansi za Tanzania. Zamani ilikuwa inaitwa NUTA Jazz.

Picha na habari zimetolewa na Rajabu Mhamila.

Sunday, September 16, 2012

Mada yangu ya leo: polisi na waandamanaji

Kuna mambo mawili muhimu yanajitokeza baada ya kuuwawa kwa mwandishi wa habari wa Channel Ten wa Iringa, Daudi Mwangosi, tarehe 2 Septemba 2012. Kwanza, Jeshi la Polisi, ambalo mmoja wa askari wake ameshafikishwa mahakamani kwa tuhuma za kuhusika na mauaji hayo, linahitaji kutoa mafunzo maalum ya namna polisi waliyopo kwenye eneo la maandamano wanavyopaswa kusimamia suala la amani katika maandamano.

Siyo kila tukio la mkusanyiko wa watu linahatarisha mali au maisha ya raia, kwa hiyo ni dhahiri pia kuwa siyo lazima kila mara kutumia nguvu zisizokuwa za lazima dhidi ya raia. Polisi wanafunzi wanapaswa kupewa elimu inayojenga taswira kuwa anaepinga serikali iliyoko madarakani siyo lazima pia awe ni adui wa Taifa au anaetishia usalama wa Taifa.

Picha inayojitokeza baada ya baadhi ya matukio ambapo polisi wameua raia ni kama vile kazi kuu ya polisi ni kuhakikisha kuwa upinzani halali wa kisiasa unaminywa kiasi cha kutosha na kuondoa kabisa uwezekano wa serikali iliyopo madarakani kuondolewa madarakani kwa njia za kidemokrasia.

Polisi wapate mafunzo kuwaelimisha kuwa kazi yao siyo kulinda maslahi ya kisiasa ya serikali iliyopo madarakani, na wafunzwe kukubali uwezekano kuwa chama chochote kilichopo upande wa upinzani kinaweza hatimaye kushinda uchaguzi na kuongoza serikali.

Jambo la pili na ambalo ni muhimu sana ni kuwa sasa waandishi wa habari wapate mafunzo ya namna ya kukusanya habari kwenye maeneo yenye usalama mdogo ili kupunguza tishio kwa usalama na maisha yao. Polisi anafanya kazi kwa amri, na kuna mazingira mengi ya kisheria yanayomruhusu polisi kutumia silaha kwa jinsi ambavyo anaona ni sawa kutokana na mazingira yanayomkabili. Polisi anayefukuzwa na kundi la waandamanaji ambao anaamini wanakusudia kumuua hatasita kutumia silaha yake dhidi ya kundi hilo. Huu ni mfano tu; haya sidhani kama ni mazingira yaliyotokea kwenye tukio lilisobabisha kifo cha Daudi Mwangosi.

Jambo la msingi ni kuwa, hata pale ambapo tunajua tunayo haki, si busara hata kidogo kubishana na mtu ambaye ameshika silaha na anaamini kuwa anatekeleza amri halali aliyopewa na mkubwa wake. Na hili haliwezi kubadilika mpaka itolewe elimu ambayo itambadilisha polisi Mtanzania ili atumie mbinu tofauti kukabiliana na waandamanaji.

Friday, September 14, 2012

Biashara ya vyuma chakavu na ufisidi (ni ufisidi, siyo ufisadi)

Miaka kadhaa iliyopita, mafundi toka Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) walijenga mnara mdogo wa kumbukumbu kijijini Butiama, sehemu ambapo ilianguka ndege ya kivita aina ya Mig, mara baada ya kuanza vita vya Kagera mwaka 1978.

Ujenzi huo uliambatana na njia ya kupita kwa miguu iliyojengewa mabomba ya chuma kuanzia barabara kuu mpaka sehemu ilipoanguka ndege, umbali wa kama mita 100 hivi.


Manara wa kumbukumbu ilipoanguka ndege ya JWTZ, eneo la Mwitongo, Butiama. Vyuma vyote vilivyo pembeni vimenyofolewa na wachuuzi wa vyuma chakavu.
Haikupita muda mrefu, wachuuzi wa biashara ya vyuma chakavu walikata mabomba yote na kuyapeleka kwa wanunuzi wa vyuma chakavu. Mnunuzi mmoja mkku wa vyuma chakavu yuko Mwanza.

Ni hawa hawa unaweza kuwasikia wakipigia makelele kuwepo kwa ufisidi (ni ufisidi, siyo ufisadi) nchini, wakinyoosha vidole kwa baadhi ya viongozi wetu, wakati hata wao wanayoyafanya hayapishani sana na yale wanayoyakemea.