Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Thursday, March 1, 2012

Nyoka wa kumwaga

Wale ambao wamepata fursa ya kusoma makala zangu za Kiingereza kwenye gazeti la Sunday News watagundua kuwa, mara kwa mara, naandika kuhusu nyoka. Nakutana na nyoka mara kwa mara kiasi ambapo inakuwa vigumu kukwepa hii mada. Wapo kila mahali. Natazama nje ya dirisha langu na naona nyoka anatambaa ukutani (picha ya hapa chini). Kuna mmoja aliingia chumbani kwangu usiku, na nikamkuta sehemu ambapo ninakanyaga niamkapo kitandani.
Kuna safari moja, wakati natoka chumbani kwangu, ikiwa kuna giza kidogo, nilimruka nyoka bila kutambua na nikafunga mlango wa chumba na kumbana nyoka mlangoni. Nilivyorudi chumbani nikamkuta yuko hai, sehemu ya kiwiliwili chake kikiwa nje ya chumba na sehemu ikiwa chumbani kwangu, ingawa alikuwa bado hai. Nilimchota na mti mrefu nikamtoa nje ya nyumba na kumuachia. Kuna mtu aliniuliza: "Kwa nini hukumuua?" Jibu nililipata kwenye asili ya kabila langu: Wazanaki.

Kwanza, angeweza kuwa Muhunda, nilimuarifu, mzimu wa Kizanaki (sisi tunaita musambwa) unaolinda kabila la Wazanaki wa Butiama (kila eneo kati ya maeneo nane ya Uzanaki lina musambwa wake). Tunaamini kuwa Muhunda anaweza kujibadilisha na kuwa nyoka, au chui, au nyani dume. Kwa imani za Wazanaki Muhunda siyo Muumba; Wazanaki wana imani kuwa yupo Muumba na mbingu.

Mimi najiita Mzanaki, japokuwa sina uwezo wa kuongea Kizanaki. Aidha, kwa mujibu wa mila zetu, mimi ni mmoja wa walinzi au wasimamizi wa msitu wa mitambiko ambao nao unaitwa Muhunda, sehemu ambayo Muhunda anaaminika kutembelea mara kwa mara. Kwa hali siyo siwezi kuua kiumbe ambacho napaswa kukilinda, hasa ukizingatia kuwa jukumu kubwa la Muhunda ni kulinda jamii nzima ya wakazi wa Butiama, Watyama.

Mimi naungana na wale wanaoamini kuwa kuna viumbe wachache sana ambao wananaweza kushambulia viumbe wengine bila kuwa na hisia kuwa usalama wao uko hatarini. Ni binadamu pekee ndiyo mwenye hulka ya kushambulia binadamu mwenzake, hata pale ambapo usalama wake hauko hatarini. Nyoka wengi hawashambulii binadamu isipokuwa tu pale wanapohisi kuwa usalama wao unatishiwa, kwa hiyo naamini kuwa sina sababu ya kuua kila nyoka ninayemuona.

Ni nyoka aina ya Mamba Mweusi tu ambaye inasemekana anaweza kumshambulia binadamu pasipo sababu ya msingi.

No comments: