Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Sunday, April 14, 2013

Tathmini ya muziki wa Tanzania mwaka 2012 (sehemu ya nne kati ya nne)

Katika makala hii nitakayoitoa katika sehemu nne, mwanamuziki mashuhuri John Kitime, anafanya tathmini ya hali ya muziki Tanzania mwaka 2012.
******************************************
Tathmini ya muziki wa Tanzania mwaka 2012

makala ya John Kitime

(Sehemu ya nne kati ya sehemu nne)

Ikiwa kulikuwa na mchango wa serikali katika muziki, basi ulikuwa mdogo au ulikuwa ni kwa shughuli maalumu lakini si kwa kutengeneza mazingira ya kuwezesha unafuu kwa wanamuziki kwa ujumla. Idara ya Utamaduni imeendelea kupata bajeti ndogo ambayo imefanya Baraza La Sanaa La Taifa kuendelea kubaki Dar es Salaam tu, likibangaiza kuweko kwa kutegemea kutoa vibali mbalimbali kwa wasanii, na nguvu zake kuonekana Dar es Salaam tu. Na kwa kuwa hakuna Maafisa Utamaduni Mkoa, na Maafisa Utamaduni Wilaya na Manispaa wako chini ya serikali za mitaa hivyo kuwa wizara tofauti na Waziri wa Utamaduni, nguvu za serikali katika utamaduni ni 0.

COSOTA, chombo ambacho shughuli yake ilikuwa ni kulinda hakimiliki za wasanii na ambacho kilikuwa chini ya wasanii, kwa kinyemela kabisa kimerudishwa katika mikono ya serikali, lakini bado kinakusanya mirabaha 'kwa niaba ya wasanii' huku kukiwa na bodi isiyo na uwakilishi wa wasanii kuanzia 2007. Swali: utakusanyaje pesa kwa niaba yangu lakini huniruhusu kujua ni kiasi gani umekusanya, unazitumiaje na ukiulizwa unakuwa mkali!!!!!!? Kuna wasanii wamekuwa wakidai kurudishiwa COSOTA, ushauri wangu wasanii wakae wajipange  na kuelewa vizuri sheria ya Hakimiliki kabla ya kujitwishwa zigo hilo la miba.

Katika miezi sita ya mwisho ya 2012 kumejitokeza spidi kali ya Mamlaka ya Ukusanyaji wa Mapato kutengeneza mazingira ya kukusanya mapato kutokana na mauzo ya kazi za muziki na filamu. Kimsingi kulipa kodi ni wajibu wa kila mwananchi na wasanii ni wananchi pia, lakini taratibu zake ndiyo zinanipa utata, hasa pale ambapo kwa muda mrefu imekuwa ikitangazwa kuwa njia hii itasaidia wasanii kwa kupunguza kuibiwa. 

Sentensi hii inaonyesha wazi anayeiongelea au hajui mfumo wa biashara ya kazi muziki, au kwa makusudi anapotosha ili kuficha kitu. Wasanii wengi huwa wamekwishalipwa kwa kazi ambazo zimesambaa na ziko barabarani zinaibiwa, wanaoibiwa ni wasambazaji. Hivyo kulinda kazi hizo unamlinda msambazaji si msanii. Pia kuanza kukusanya kodi kwa kazi hizi kumepewa jina ‘kurasimishwa  kwa kazi ya usanii’. 

Kuna mabilioni wasanii wanatakiwa walipwe na watumiaji wa kazi za sanaa, kama redio na TV, mapromota, waajiri na kadhalika lakini hakuna anaeliongelea hilo wala hakuna anaetamka takwimu hizo. Kuna kazi ya kurudisha mitaala ya masomo ya sanaa mashuleni, kurudisha vyuo vya walimu wa sanaa, kurudisha maafisa utamaduni kuwa chini ya Wizara ya Utamaduni kuwawezesha kufanya kazi zao kadiri ya Sera ya Utamaduni, na mengine mengi ya aina hiyo ndiyo ningeona kurasimisha kazi za sanaa. Lakini kukusanya kodi tu kwa kazi ambazo hata hivyo mikataba yake mingi inautata na kuita urasimishaji si sahihi.

Katika nchi nyingi critics au watu ninaoweza kuwaita Kiswahili wakosoaji, huwa ni muhimu katika maendeleo ya sanaa. Watu hawa hupata heshima kutokana na kuweza kuangalia mapungufu katika kazi za sanaa na kuyasema, jambo ambalo hupelekea wasanii kujirekibisha na kutengeneza kazi bora zaidi. Hapa kwetu kutoa ushauri ni kutafuta matusi, toka kwa wasanii wenye kazi husika, vyombo vya habari na hata sehemu ya jamii. Umefika muda wahusika kuchukua uchambuzi kama changamoto za kuboresha kazi.

Niliyoyataja hapa yote yako wazi. Ninachotegemea ni kuona 2013 hatua zinaanza kupigwa kurekebisha ili wanamuziki wa nchi hii nao wapate nafasi sawa na wengine wa nchi nyingine.

John Kitime
31.12.2012
Sinza, Dar es Salaam 

Taarifa zinazohusiana na hii:

No comments: