Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Friday, August 12, 2016

Kijijini kama mjini

Wapo wengi ambao hawakupenda uamuzi wa serikali ya awamu ya nne ya kuanzisha kwa wilaya mpya ya Butiama. Mimi ni mmojawapo.

Nimejihusisha na kazi ya kutangaza historia na utamaduni wa eneo la Butiama kwa zaidi ya miaka saba sasa, na natambua ni jinsi gani utamaduni wa eneo unavyoweza kuathirika unapotokea muingiliano wa haraka kati ya maeneo ya mijini na ya vijijini. Mawasiliano mazuri kati ya miji na vijiji yanaweza kuongeza kasi hiyo, na hali kadhalika, uamuzi wa kuanzisha wilaya mpya pia unaweza kuleta matokeo hayo hayo.

Wilaya mpya inakuja na ongezeko kubwa la wafanyakazi kutoka maeneo mbalimbali. Nao siyo kama wanakuja na tamaduni zao za asili tu, ila wanaleta zaidi tamaduni za miji, na hata sheria za miji. Matokeo yake ni kudumazwa kwa tamaduni za asili za maeneo hayo mapya ya wilaya, na hasa kama yalikuwa maeneo ya vijijini.
Mojawapo ya sehemu za burudani na starehe za Butiama zilizoibuka baada ya kuanzishwa kwa wilaya mpya ya Butiama.
Msimamo wangu haulengi kutetea suala la ukabila, bali unalenga kulinda na kutunza mila na desturi za eneo mahususi kwa madhumuni ya kuendeleza utalii wa utamaduni.

Saturday, July 30, 2016

Mada yangu ya leo: mwizi ni mwizi tu

Sikumbuki niliisoma wapi habari hii, lakini kuna kichwa cha habari cha toleo la gazeti la hivi karibuni liliarifu kuwa yule mtuhumiwa wa kuiba milioni 7 kwa dakika "mwenye asili ya Kiarabu" amefikishwa mahakamani.

Kwanza, nitamke wazi kuwa hili suala liko mahakamani na mimi simhukumu mtuhumiwa. Namtetea kwa kubaguliwa. Akikutwa na hatia, nitazungumzia hilo.

Mwizi ni mwizi tu, hata kama ni kabila yako. Uandishi wa aina hii wa kubainisha kuwa mtuhumiwa ana asili ya Uarabu ni hatua ya wazi ya kubagua mtu kwa rangi yake ya ngozi. Maana inayojitokeza ya makala hii ni kuwa kama angekuwa Mbantu akutwe na hatia ya kuiba milioni 7 kwa dakika, tatizo lingekuwa dogo zaidi. Labda milioni 7 ingekuwa 2 tu kwa sababu tu mwizi alikuwa ana rangi tofauti ya ngozi.

Monday, March 28, 2016

Viongozi wabaguzi ambao wanaendelea kuenziwa

Wapo viongozi wa dunia ambao wamejijengea sifa kubwa, pamoja na ukweli kuwa wanabeba kasoro kubwa za kibaguzi kwenye matamshi au maamuzi yao. Viongozi wawili ambao wanayo sifa hii ni Winston Churchill, na Mahatma Gandhi.
Sir Winston S Churchill.jpg
Winston Churchill (Picha: Wikipedia)

Churchill alikuwa kiongozi wa Uingereza ambaye aliwahi pia kuwa waziri mkuu wa nchi hiyo. Katika nyadhifa zake mbalimbali amenukuliwa akitoa matamshi na kuchukua hatua za kibaguzi dhidi ya watu mbalimbali, ikiwa ni pamoja na Waafrika, Wahindi, na Waarabu. Kwa ujumla, alikuwa mbaguzi wa rangi ha kiwango cha Hitler aliyeamini kuwa binadamu mwenye ngozi nyeupe anapaswa kutawala binadamu wengine wote. Pamoja na ukweli huu, Churchill anakumbukwa kwenye historia kama kiongozi aliyefanikiwa kuiongoza Uingereza vyema wakati wa vita vya pili vya dunia.

Gandhi naye haachwi mbali kwa matamshi yake ya kibaguzi. Akiwa anafanya kazi Afrika ya Kusini aliandika kuhusu kupinga kwake kwa wahindi kufananishwa na Waafrika, akiamini kuwa Mwafrika alikuwa na hadhi ya chini kuliko Mhindi. Gandhi ni mmoja wa wanaharakati wa India ambaye anaheshimika sana katika ulimwenguni wa mapambano dhidi ya ukoloni, haki, na usawa.

Wanataaluma wanafahamu kuwa, kwa kutumia mifumo ya habari na mawasiliano ambayo inamilikiwa na kampuni chache sana duniani, inawezekana kujenga taswira juu ya kiongozi ambayo haifanani kabisa na hali halisi. Mwizi anaweza kuonekana ni muadilifu, na mhalifu akaonekana asiye na hatia. Hali kadhalika, muadilifu na asiye kuwa na hatia akatambulishwa kuwa tofauti kabisa na hali halisi.
File:Portrait Gandhi.jpg
Mahatma Gandhi (Picha: Wikipedia)
Haipingiki kuwa historia ya kiongozi inapaswa kuakisi mazuri na mabaya yake, lakini nafikiri inapofikia suala la ubaguzi wa binadamu kwa misingi ya rangi ya ngozi, basi kinga hiyo inapotea kwa viongozi wa aina hiyo. Kiongozi asiye mbaguzi na aliyetumbukia kwenye makosa ya kiutendaji anaweza kuvumiliwa kidogo, lakini kiongozi mbaguzi hasafishiki na hapaswi kuvumiliwa hata kidogo.

Hata hivyo, uandishi wa historia unaoficha mabaya ya viongozi wa aina hii pamoja na mifumo ya habari na mawasiliano ambayo inaendelea kudhibitiwa na wamiliki wachache haitoi fursa ya kuwaanika viongozi wa aina hii pamoja na maovu yao.

Thursday, December 24, 2015

Watu kama sisi

Mwaka jana nilishirikishwa kama mmoja wa waliohojiwa kwenye filamu juu ya albino na adha wanazopata kwenye jamii. Inaelimisha vyema.

Isambaze pia kwa wengine.

Tuesday, December 1, 2015

Kufanikisha falsafa ya Sasa Kazi tu! ni kazi kweli kweli!

Tunajifunza mengi kwa kusikiliza. Leo nimemsikiliza mama wa kijijini Butiama akilalamika kwangu tena kuhusu binti yake kuondoka nyumbani na kuhamia kwa mtu aliyezaa naye.

Tatizo ni kuwa binti mwenyewe ana umri wa miaka 15 tu, na aliyempa ujauzito ni mtu mzima. Alimpa hiyo mimba binti akiwa shuleni, na kwa mujibu wa sheria zilizopo angestahili kuchukuliwa hatua za kisheria. Hayo hayakutokea.

Nahisi hayakutokea kwa sababu mama wa binti, badala ya kupeleka hilo suala mbele ya sheria, alifikia makubaliano na huyo jamaa na inawezekana kuwa alikuwa anapewa pesa ili kutulia.

Sasa leo kalalamika tena kuwa binti karudi kule kule na akaniambia kuwa sasa anakusudia kufikisha suala hilo polisi. Lakini njia anayotumia haijanyooka vizuri. Kaniambia kuwa ana jirani yake polisi ambaye amemuomba aende kumkamatia yule mhalifu.

Jirani yake kakubali lakini amemwambia ampe shilingi elfu kumi ili amfanyie hiyo kazi. Yeye alisema hana hizo pesa, na akamwambia yule jirani kuwa amfanyie tu hiyo kazi kwa kuwa wanahusiana pia kiukoo. Jirani polisi hakusumbuliwa sana na hoja ya uhusiano wa kiukoo, na amemwambia mlalamikaji atafute angalau shilingi elfu tano ili afanye hiyo kazi.
 
Rais John Magufuli (wa pili kutoka kushoto), akiwa na marais wastaafu (kutoka kushoto kwenda kulia) Ali Hassan Mwinyi, Jakaya Mrisho Kikwete, na Benjamini William Mkapa. (Picha kwa hisani ya CCM Blog)

Miongoni mwa vielelezo kuwa uongozi ni kazi kubwa ni pamoja na tukio hili. Kwenye ngazi hii ya chini, kujenga imani kuwa falsafa ya Sasa Kazi tu! itafanikiwa ili mradi yupo rais na waziri mkuu wachapa kazi ni ndoto tu. Mabadiliko chanya yatapatikana iwapo wote tutashiriki kwa namna tunavyoweza kuleta mafanikio tunayotarajia.