Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Tuesday, February 26, 2013

Lugha yetu Kiswahili

Hivi majuzi katika sherehe mojawapo niliandaa mtiririko wa nyimbo mbalimbali za muziki wa dansi za kusikiliza kwenye sherehe hiyo kwa kutumia kompyuta yangu ambayo inahifadhi mkusanyiko wa nyimbo nyingi ambazo nimezikusanya kwa miaka mingi. Baada ya hapo kompyuta inaunganishwa na vipaza sauti na nyimbo zilizochaguliwa zinaanza kusikika moja baada ya nyingine kwa muda mrefu tu.

Nyingi ya nyimbo hizo ni za wanamuziki wa zamani, wengi ambao hawako hai kwa sasa. Baadhi ya hizo Watanzania tunaziita "zilipendwa" au nyimbo za zamani ambazo vijana wengi wa siku hizi hawasikilizi.

Mmoja wa waliohudhuria sherehe hiyo alizipenda nyimbo zile sana na hakutulia sana kwenye kiti chake, akiinuka mara kwa mara kwenda kucheza muziki mmoja baada ya mwingine.

Nilivyotambua jinsi nilivyomsumbua huyo mtu nikajisifia kwa kumuuliza: Umenikubali? Na hapo nikazua mjadala na mtu mwingine aliyehudhuria sherehe hiyo akihoji iwapo ilikuwa sahihi kwangu kutumia neno hilo. Alisisitiza kuwa hawezi kunikubali mimi bali anaweza kukubali nyimbo ambazo nilizichagua kusikilizwa kwenye sherehe hiyo.

Mimi nilisisitiza kuwa "kunikubali" ulikuwa ni msemo tu lakini ukimaanisha alikubali uwezo wangu wa kuchagua nyimbo nzuri na siyo kunikubali mimi binafsi. Hoja yangu ilikuwa hata asingefahamu ni nani aliyechagua zile nyimbo angeweza kusema: "namkubali aliyepanga hizo nyimbo."

Ni kweli kuwa msemo wa "kumkubali" mtu umeibuka kwenye matumizi yasiyo rasmi ya lugha ya Kiswahili, hasa kwa vijana wa Tanzania, ukimaanisha kutoa sifa isiyo ya kawaida kwa mtu kwa uwezo wake wa kufanya jambo fulani.

Lakini siyo kweli pia kuwa tunaweza kuzungumzia kuwa wapiga kura "wamemkubali" mgombea mmoja na kumchagua kuwa kiongozi wao na kwa maana hiyo matumizi hayo yakaleta maana rasmi?

Wewe unasemaje?

Sunday, February 17, 2013

Wageni wa Butiama: mkuu wa Idhaa ya Kiswahili ya BBC

Hizi ni habari za zamani kidogo ambazo nilizitoa kwenye blogu yangu ya lugha ya Kiingereza. Nazirudia hapa kwa manufaa ya wale ambao hawakuzisoma.
******************************************
Kabla ya kufika kwa Jaffar Amin kijijini Butiama mwezi Aprili [2009] ziara yake, ambayo iliandaliwa na Idhaa ya Kiswahili ya shirika la utangazaji la BBC, ilitanguliwa na kufika Butiama kwa baadhi ya miamba ya utangazaji ya Idhaa ya Kiswahili ya BBC, ikiwa ni pamoja na Solomon Mugera, mkuu wa Idhaa hiyo, na Vicky Ntetema, kiongozi wa ofisi ya BBC iliyopo Tanzania.
Wengine toka BBC waliyofika Butiama walikuwa ni muongozaji vipindi Charles Hilary ambaye kwa desturi hutangaza akiwa London, Caroline Karobia anayefanya kazi kutokea Nairobi, na jina lenye kufahamika na wengi wa wasikilizaji wa Idhaa ya Kiswahili ya BBC, Eric David Nampesya, mtangazaji wa BBC wa eneo la Maziwa Makuu, ambaye anaonekana hapo juu, kulia, pamoja na Solomon Mugera. 

Nikiwa mmoja wa wasikilizaji wa mara kwa mara wa BBC nilijisikia mwenye furaha kuwa miongoni mwa watu mashuhuri kama hawa toka Idhaa ya Kiswahili ya BBC.

Friday, February 15, 2013

Wazanaki na mirathi

Kwa desturi ya kabila la Wazanaki, wapwa ndiyo walirithi mali za marehemu. Baadhi ya sababu zinazotajwa kwa jamii ya Wazanaki kufuata mila hii ni kuwa baba wa familia hakuwa na uhakika kuwa watoto waliozaliwa na mke (wake) zake walikuwa ni wa kwake.

Kwa sababu hiyo urithi walipewa wapwa kwa sababu, kupitia kwa dada yake, baba huyo alikuwa na uhakika kuwa anapofariki mali zake zinabaki kwa ndugu ambao ana uhusiano nao wa damu.

Mila hii ilianza kupungua nguvu kwenye msiba wa mmoja wa wadogo zake Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, Joseph Kizurira Nyerere aliyefariki tarehe 8 Agosti 1994.
Mzee Joseph Kizurira Nyerere, kushoto, alikuwa shabiki mkubwa wa Vijana Jazz Orchestra.
Akizungumza baada ya mazishi ya mdogo wake, Mwalimu Nyerere alisema umefika wakati kwa Wazanaki kuachana na hiyo desturi na kurudisha mirathi kwa mke na watoto wa marehemu.

Wednesday, February 13, 2013

Francis Cheka kutetea ubingwa wa Afrika dhidi ya Thomas Mashali Mei Mosi


Taarifa kwa vyombo vya habari toka Shirikisho la Ngumi la Kimataifa Afrika (IBF/Africa) linaarifu kuidhinishwa kwa pambano la utetezi la ubingwa wa IBF Africa unaoashikiliwa na Mtanzania Francis Cheka. Habari kamili hizi hapa:
********************************************
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
FEBRUARY 13, 2013
   Francis Cheka (kushoto) akiwa na Adam Tanaka (katikatia) na Thomas Mashali (kulia)
Shirikisho la Ngumi la Kimataifa Afrika (IBF/Africa) limetoa kibali kwa bondia Francis Cheka ambaye ni bingwa wa Afrika katika uzito wa Super Middle kutetea ubingwa wake dhidi ya bondia Thomas Mashali wa Tanzania. 

Mabondia hao wawili leo tarehe 13 February walikutana katika hoteli ya Ndekha, iliyoko Magomeni Kondoa na kutia sahihi mkataba wa kupigana pambano hilo ambalo limepangwa kufanyika siku ya Mei Mosi katika ukumbi wa PTA jijini Dar es Salaam.

Thomas Mashali ambaye ndiye bingwa wa Afrika ya Mashariki na Kati (ECAPBF) katika uzito wa Middle ana kiwango kizuri cha kushindana na Francis Cheka katika pambalo hilo.

Hii itakuwa mara ya pili kwa bondia Francis Cheka kutetea mkanda alioushinda tarehe 29 April 2012 dhidi ya bondia machachari Mada Maugo wa Tanzania. Cheka aliutetea vyema mkanda wa ubingwa wa IBF/Afrika dhidi ya bondia Chiotcha Chimwemwe ambaye ni Afisa katika jeshi la Malawi siku ya Boxing Day (26 Decewmber 2012) katika jiji la Arusha.

Kama Francis Cheka atashinda tena pambano hili, atapewa nafasi ya kupigana kugombea mkanda wa IBF wa mabara (IBF I/C) .

Pambano hili linaandaliwa na kampuni ya Mumask Investment and Gebby Pressure ya jijini Dar es Salaam chini ya uratibu wa Adam Tanaka.

Imetumwa na:

UONGOZI
Shirikisho la Ngumi la Kimataifa Africa (IBF/Africa)
Dar-Es-Salaam, Tanzania 

Taarifa nyingine inayohusiana na hii
http://muhunda.blogspot.com/2012/05/ngowi-kusamamia-pambano-la-ubingwa-wa.html

Monday, February 11, 2013

Mapigano kati ya Wakristu na Waislamu Katoro, Geita, 7 wafa

Kuna taarifa nimepata kuwa watu saba wamekufa kutokana na mapigano kati ya Wakristu na Waislamu huko Katoro, Geita.

Kwa mujibu wa mtoa habari vurugu zilianza kutokana na mmiliki wa bucha kuuza nyama ya ng'ombe aliyechinjwa na Mkristu.

Baadhi ya Waislamu walifika kwenye bucha hiyo na kuichoma moto na kusababisha kuzuka hayo mapigano.

Taarifa zinasema pia kuwa raia wa kigeni ambaye alipita kwenye eneo la vurugu kwa gari alishambuliwa na kuchinjwa.

Hivi karibuni Serikali mkoani Mwanza iliagiza kuwa Waislamu pekee ndiyo waruhusiwe kuchinja wanyama ambao nyama yao inauzwa kwenye bucha.