Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Tuesday, May 8, 2012

Ngowi kusimamia pambano la ubingwa wa IBF nchini Ghana


Shirikisho la Ngumi la Kimataifa (IBF) limemteua Rais wa Shirikisho hilo katika bara la Afrika, Onesmo Alfred Ngowi kusimamia pambano la ubingwa wa mabara linalotambuliwa na IBF.



Mpambano huo utafanyika katika jiji la Accra nchini Ghana tarehe 26 Mei kati ya bingwa wa mabara wa IBF Emmanuel Tagoe wa Ghana na mpinzani wake Antonio De Vitis wa Italy katika uzito wa Junior Lightweight.
Katika mpambano huo wa kutetea mkanda wa ubingwa wa IBF ambao unashikiliwa na Tagoe Ngowi atasaidiwa na waamuzi wengine kama ifuatavyo: Refarii: Roger Barnor (Ghana). Majaji: Francisco de Ruvo, (Italy), Andre Pasquier (France) na Shadrack Acquaye (Ghana).

Mpambano huo uliopewa jina la “Ni Sasa au Hakuna Tena”, bondia Joseph Agbeko wa Ghana atagombea mkanda wa dunia wa Organizesheni ya Ngumi ya Kimataifa (IBO) akichuana na bondia Michael Domingo wa Ufilipino katika uzito wa Bantam.

Bondia Joseph Agbeko anayeishi katika mji wa Bronx katika jiji la New York nchini Marekani atakumbukwa kwenye mpambano wake mkali wa kugombea ubingwa wa IBF katika uzito wa Bantam kati yake na bondia Abner Mares wa Mexico tarehe 3 mwezi Agosti 2011 katika jiji la Las Vegas, Nevada, nchini Marekani ambako ilibidi warudiane mara ya pili baada ya kutokea malalamiko ya kuonewa kwa Agbeko.

Hata hivyo bondia Abner Mares alimshinda tena Joseph Agbeko waliporudiana tarehe 18 Novemba 2011 katika jiji la California, nchini Marekani.

Naye bondia Joshua Okine wa Ghana ambaye alikuwa bingwa wa mabara wa IBF katika uzito wa Middle kabla ya kupoteza ubingwa wake kwa kupandisha uzito atapambana na bondia Theofiilus Teteh pia wa Ghana kugombea mkanda wa WBO Africa.

Bondia Sammuel Amaoko, anayejulikana pia kama Bruno wa Ghana, atapambana na bondia Sidney Siqueira wa 
Brazil kugombea mkanda wa WBO Africa katika uzito wa Heavyweight.   

Mapambano haya yaliyoandaliwa na Golden Mike Boxing Promotions ya Ghana yatafanyika katika uwanja wa kimataifa wa El-Wak, jijini Accra nchini Ghana chini ya usimamizi wa Mamlaka ya Ngumi za Kulipwa ya Ghana (Ghana Boxing Authority, GBA).

Usimamizi wa Ngowi katika mpambano huu unakuja kipindi kifupi baada ya Francis Cheka wa Tanzania kuunyakua mkanda wa IBF Continental Africa Title katika uzito wa Super Middle tarehe 28 April mwaka huu.

No comments: