Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Monday, March 28, 2016

Viongozi wabaguzi ambao wanaendelea kuenziwa

Wapo viongozi wa dunia ambao wamejijengea sifa kubwa, pamoja na ukweli kuwa wanabeba kasoro kubwa za kibaguzi kwenye matamshi au maamuzi yao. Viongozi wawili ambao wanayo sifa hii ni Winston Churchill, na Mahatma Gandhi.
Sir Winston S Churchill.jpg
Winston Churchill (Picha: Wikipedia)

Churchill alikuwa kiongozi wa Uingereza ambaye aliwahi pia kuwa waziri mkuu wa nchi hiyo. Katika nyadhifa zake mbalimbali amenukuliwa akitoa matamshi na kuchukua hatua za kibaguzi dhidi ya watu mbalimbali, ikiwa ni pamoja na Waafrika, Wahindi, na Waarabu. Kwa ujumla, alikuwa mbaguzi wa rangi ha kiwango cha Hitler aliyeamini kuwa binadamu mwenye ngozi nyeupe anapaswa kutawala binadamu wengine wote. Pamoja na ukweli huu, Churchill anakumbukwa kwenye historia kama kiongozi aliyefanikiwa kuiongoza Uingereza vyema wakati wa vita vya pili vya dunia.

Gandhi naye haachwi mbali kwa matamshi yake ya kibaguzi. Akiwa anafanya kazi Afrika ya Kusini aliandika kuhusu kupinga kwake kwa wahindi kufananishwa na Waafrika, akiamini kuwa Mwafrika alikuwa na hadhi ya chini kuliko Mhindi. Gandhi ni mmoja wa wanaharakati wa India ambaye anaheshimika sana katika ulimwenguni wa mapambano dhidi ya ukoloni, haki, na usawa.

Wanataaluma wanafahamu kuwa, kwa kutumia mifumo ya habari na mawasiliano ambayo inamilikiwa na kampuni chache sana duniani, inawezekana kujenga taswira juu ya kiongozi ambayo haifanani kabisa na hali halisi. Mwizi anaweza kuonekana ni muadilifu, na mhalifu akaonekana asiye na hatia. Hali kadhalika, muadilifu na asiye kuwa na hatia akatambulishwa kuwa tofauti kabisa na hali halisi.
File:Portrait Gandhi.jpg
Mahatma Gandhi (Picha: Wikipedia)
Haipingiki kuwa historia ya kiongozi inapaswa kuakisi mazuri na mabaya yake, lakini nafikiri inapofikia suala la ubaguzi wa binadamu kwa misingi ya rangi ya ngozi, basi kinga hiyo inapotea kwa viongozi wa aina hiyo. Kiongozi asiye mbaguzi na aliyetumbukia kwenye makosa ya kiutendaji anaweza kuvumiliwa kidogo, lakini kiongozi mbaguzi hasafishiki na hapaswi kuvumiliwa hata kidogo.

Hata hivyo, uandishi wa historia unaoficha mabaya ya viongozi wa aina hii pamoja na mifumo ya habari na mawasiliano ambayo inaendelea kudhibitiwa na wamiliki wachache haitoi fursa ya kuwaanika viongozi wa aina hii pamoja na maovu yao.

Thursday, December 24, 2015

Watu kama sisi

Mwaka jana nilishirikishwa kama mmoja wa waliohojiwa kwenye filamu juu ya albino na adha wanazopata kwenye jamii. Inaelimisha vyema.

Isambaze pia kwa wengine.

Tuesday, December 1, 2015

Kufanikisha falsafa ya Sasa Kazi tu! ni kazi kweli kweli!

Tunajifunza mengi kwa kusikiliza. Leo nimemsikiliza mama wa kijijini Butiama akilalamika kwangu tena kuhusu binti yake kuondoka nyumbani na kuhamia kwa mtu aliyezaa naye.

Tatizo ni kuwa binti mwenyewe ana umri wa miaka 15 tu, na aliyempa ujauzito ni mtu mzima. Alimpa hiyo mimba binti akiwa shuleni, na kwa mujibu wa sheria zilizopo angestahili kuchukuliwa hatua za kisheria. Hayo hayakutokea.

Nahisi hayakutokea kwa sababu mama wa binti, badala ya kupeleka hilo suala mbele ya sheria, alifikia makubaliano na huyo jamaa na inawezekana kuwa alikuwa anapewa pesa ili kutulia.

Sasa leo kalalamika tena kuwa binti karudi kule kule na akaniambia kuwa sasa anakusudia kufikisha suala hilo polisi. Lakini njia anayotumia haijanyooka vizuri. Kaniambia kuwa ana jirani yake polisi ambaye amemuomba aende kumkamatia yule mhalifu.

Jirani yake kakubali lakini amemwambia ampe shilingi elfu kumi ili amfanyie hiyo kazi. Yeye alisema hana hizo pesa, na akamwambia yule jirani kuwa amfanyie tu hiyo kazi kwa kuwa wanahusiana pia kiukoo. Jirani polisi hakusumbuliwa sana na hoja ya uhusiano wa kiukoo, na amemwambia mlalamikaji atafute angalau shilingi elfu tano ili afanye hiyo kazi.
 
Rais John Magufuli (wa pili kutoka kushoto), akiwa na marais wastaafu (kutoka kushoto kwenda kulia) Ali Hassan Mwinyi, Jakaya Mrisho Kikwete, na Benjamini William Mkapa. (Picha kwa hisani ya CCM Blog)

Miongoni mwa vielelezo kuwa uongozi ni kazi kubwa ni pamoja na tukio hili. Kwenye ngazi hii ya chini, kujenga imani kuwa falsafa ya Sasa Kazi tu! itafanikiwa ili mradi yupo rais na waziri mkuu wachapa kazi ni ndoto tu. Mabadiliko chanya yatapatikana iwapo wote tutashiriki kwa namna tunavyoweza kuleta mafanikio tunayotarajia.

Wednesday, November 11, 2015

Adha za Mwenge wa Uhuru

Sina tatizo na madhumuni ya mbio za Mwenge wa Uhuru, lakini ninaona kasoro kubwa katika baadhi ya vipengele vya mchakato wa mbio hizo unavyoendeshwa.

Mwenge unapohamishwa kutoka sehemu moja kwenda nyingine, barabara zote huwa au hazipitiki au zinapitika kwa shida. Barabara zinafungwa mpaka Mwenge upite. Wale wenye shida za dharura wanakuwa hawawezi kutumia usafiri wa barabara kufuatilia shida zao.

Hata mgonjwa mahututi ambaye anapelekwa hospitali au kwenye kituo cha afya anaweza kujikuta ndani ya gari akisubiri Mwenge upite kwanza, ndipo gari alilopanda (kama siyo la kubeba wagonjwa) liweze kuruhusiwa na kuendelea na safari yake.

Gari zikiwa zimesimamishwa eneo la Kisesa, Mwanza, zikisubiri msafara wa Mwenge wa Uhuru upite.
Na isingekuwa vibaya sana iwapo watu wangelazimika kusubiri kwa muda kidogo tu kupisha Mwenge upite. Tatizo ni kuwa wakati mwingine watu husubirishwa kwa muda mrefu sana ili msafara wa Mwenge upite, hata pale ambapo msafara huo unaelekea njia tofauti. Ili mradi tu unapishana nao, basi utalazimika kusimama.

Mwenge wa Taifa ni nembo ya Taifa na nadhani maana ya kusimamishwa watu njiani ni kutoa heshima kwa hiyo nembo ya Taifa. Sijui kama hii ndiyo mantiki ya hatua hizi, lakini inawezekana pia kuwa watu husimamishwa kwa sababu ya kipengele kimoja ambacho nadhani kipo kwenye Sheria ya Usalama Barabarani ambacho kinatamka kuwa msafara rasmi ni lazima upishwe.

Nadhani msafara wa Mwenge unapewa hadhi ya msafara rasmi, kama msafara wa rais au viongozi wengine wa ngazi ya juu. Hatari iliyopo ni kuwa msafara wa Mwenge unaweza kumsubirisha mgonjwa mahututi na asiwahi kupata huduma ya matibabu ambayo inaweza kuokoa maisha yake.

Tuesday, November 10, 2015

Mwalimu Nyerere na nguzo ya uwajibikaji kwa wote katika uongozi

Kwenye kijitabu chake, Ujamaa ni Imani 1: Moyo kabla ya silaha, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere anasema:

Alinijia Mzanaki mmoja mwaka 1961, mara tu baada ya kupata uhuru. Anataka kazi; anasema, "Mzanaki ndiye Rais, basi sisi Wazanaki tutainuka." Nikamwambia, "Nenda, uko utaratibu wa kupata kazi." Akaniambia, "Na mimi vilevile niende huko?" Nikamwambia, "Kwa nini usiende huko?" Akasema, lazima nije kwako; sasa Mwalimu wewe umekwisha pata, ndugu zako wengine vile vile wapate. Sasa tusipoanza sisi Wazanaki waanze nani? Na wakubwa ndio wa kula, na wakati wa kula umefika; basi tule!"
            (Uk. wa 40)

Yameharibika mengi kwenye nchi hii kwa sababu viongozi wengi wanaamini kuwa uongozi ni sehemu ya kujineemisha wao na familia zao. Na kwa wale ambao hawana ndugu au marafiki kwenye sehemu muhimu za uongozi, uwezekano wa kupata ajira au haupo kabisa au ni finyu sana.
Mwalimu Nyerere

Kurudisha mfumo ambao unatoa fursa sawa kwa wote inawezekana kabisa.