Mkutano huu (picha ya juu) ulifanyika eneo la stendi, Butiama. Wapinzani wao wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) walifanya mkutano wa mwisho wa kampeni kwenye kitongoji cha Mtuzu, Butiama.
Saturday, December 13, 2014
Mwisho wa kampeni Butiama za uchaguzi wa serikali za mitaa
Viongozi na wagombea wa Chama cha Mapinduzi wa kijijini Butiama wakiomba kura mbele ya wakazi wa Butiama siku moja kabla ya uchaguzi wa serikali za mitaa utakaofanyika nchini kote kesho tarehe 14 Desemba 2014.
Friday, December 12, 2014
Mabondia na unga (sehemu ya tatu ya awamu tatu)
Promota wa ndondi za kulipwa, Ibrahim Kamwe, anaeleza kwa nini baadhi ya mabondia wanajiingiza kwenye biashara ya madawa ya kulevya.
![]() |
| Ibrahim Kamwe |
Ukiangalia umbumbumbu na maskini tulionao mabondia, hapo wajanja
wenye pesa zao, wafanyabiashara, na baadhi ya viongozi wanatumia udhaifu
tulionao mabondia kutuhadaa kwa kutupatia safari za nje za kimichezo au
matembezi ya kwenda kufanya mazoezi ughaibuni na hatimaye kutubebesha
mihadarati (madawa ya kulevya) bila kujua kwa kutuwekea katika mizigo tunayosafiri
nayo. Wakati mwingine kuna baadhi ya wafanya biashara hao wenye pesa zao
hukuweka wazi wakati unaenda pigana umbebee mzigo wake na atakulipa pesa
nyingi. Hapo ndipo tunapobanwa ukiangalia nyumbani tunalalia telemka tukaze,
tunashindia tembele mlo mmoja, msosi wa kengele tena kwa masimango,
mfukoni huna kitu na wala huna kazi itakayokupatia pesa ya kula kwa wakati huo. Hapo sijaingiza mambo ya kodi, na demu wangu namlinda vipi.
Hii njaa na umaskini tulio nao mabondia ndiyo inawapa nguvu vigogo
kututumia kwa kutubebesha madawa ya kulevya kusafirisha nje wakijua wazi
hatuwezi kataa kutokana na dhiki tuliyo nayo. Tutakubali tu kwani hakuna
apendae kulala njaa, kulala pachafu, au kuvaa midabwada.
“Siwezi acha dili la pesa kama hili wakati jina langu kubwa kila kona linatajwa mitaani na vyombo vya habari lakini mimi binafsi nauli ya daladala sina. Siku ya tatu leo nakula mlo mmoja kwa siku, watoto hawapo katika hali nzuri, mazoezi yenyewe sifanyi kwa raha nafikiria nitapata wapi mshiko. Leo unaniletea ishu ya pesa niikatae si nitakuwa kichaa?”
“Wadau wenzangu wa ngumi ,wapambe wao, na walio karibu na sisi mabondia wana nguo za bei kubwa wanapendeza, wana magari. Ukiangalia mimi bondia ndiye mtendaji wao mkuu nipo ovyo sina kitu mfukoni wala tumboni, madeni kibao yaani majanga matupu.”
Ushauri wangu kwa serikali au taasisi zinazohusika na
wanaolichukia jambo hili kiukweli - maana wengine hujifanya kulichukia mdomoni
pembeni ndiyo watendaji wakuu wa kuwatumia wanamichezo au wasanii kwa faida zao
- mabondia au wanamichezo tuboreshewe maeneo yetu ya michezo ikiwemo katika
vilabu vyetu na maeneo ya mazoezi, na vifaa viongezwe. Ikiwezekana kodi ya
vifaa vya michezo ipunguzwe ili viwe vingi nchini mabondia wasibabaike na vya
kuazima au kuangalia katika TV vifaa vya wenzetu.
Serikali iwajali mabondia, isaidie kudhamini semina za walimu wa
ngumi ili wawaongoze vyema vijana wao. Magym ya makusudi yajengwe na maeneo ya
wazi wasigawane wenye pesa na viongozi kwa faida zao. Wajenge sehemu za michezo
ya ndani, na kama pia
itatumika njia ya kutoa madarasa matupu katika mashule yetu kwa ajili ya
kutuachia sehemu ya mazoezi ya jioni itasaidia sana kukuza mchezo na walimu
wenye taaluma kufundisha vizuri kuliko mabondia kufundishana vichochoroni na
kutokuwa na nidhamu ya mchezo wala maisha.
Sunday, December 7, 2014
Mabondia na unga (sehemu ya pili ya awamu tatu)
Promota wa ndondi za kulipwa, Ibrahim Kamwe, anaeleza kwa nini baadhi ya mabondia wanajiingiza kwenye biashara ya madawa ya kulevya.
%2B(640x480).jpg)
Siku za hivi karibuni kuna vimaendeleo kidogo kwa baadhi ya
mabondia; tunafanya mazoezi katika
vilabu vya pombe kwa kuwalipa kodi ya mazoezi wenye baa. Naweza kusema Tanzania
hakuna sehemu rasmi za kufanyia mazoezi ya ndani zilizotengwa na serikali
kwa ajili ya raia wake wapenda michezo na kama zipo ni chache na ziko katika
makambi ya jeshi kwa masharti magumu kwa raia wa kawaida.
Siku za nyuma wakazi
wa mjini kama vile Kisutu, Gerezani na Kariakoo walikuwa wanafanya mazoezi pale
Arnatoglou. Siku hizi huwezi kusikia kuna mwanamichezo katokea Gerezani au
Kariakoo. Iliyobaki kwao ni kuuza na kutumia madawa ya kulevya na kukimbizana
na wafanyabiashara wa maeneo hayo. Naweza kuilaumu serikali kwa kutoendeleza
michezo bali ilishiriki kuuwa kabisa michezo maeneo hayo na mengineyo zaidi.
Kwa sisi tulioanza kukua kimichezo pambano la ngumi likiandaliwa
huwa tunalipwa kuanzia shilingi 5,000/- mpaka 20,000/- kwa mapambano haya
madogomadogo na iwapo kutakuwa na pambano kubwa na kupata bahati ya kucheza
unaweza kulipwa shilingi 40,000/- mpaka 100,000/-. Mapambano makubwa yanaweza
kuwa moja, mawili, au matatu kwa mwaka; hayazidi hapo. Haya mapambano madogo
tunaweza pata mawili mpaka sita kwa mwaka.
Msiwaone mabondia wakicheza mkadhani wana kipato kikubwa. La
hasha! Ni wale tu wachache waliobahatika kupata wadhamini au waratibu wenye
uwezo wa kipesa ndiyo kidogo hutoka.
Kwa sisi wengine ukiangalia elimu ya kusoma hatuna, kazi hakuna,
na mchezo wa ngumi tunaupenda na pengine tuna vipaji na kufanya vizuri
katika mapambano yetu. Hivyo mchezo ndiyo huwa kama ajira yetu kwa sababu
tunapata chochote kidogo kupitia mchezo huo kuliko kuiba au kukimbizana na
mapolisi katika kamari na kuishia jela.
Kwetu sisi mabondia huona ni jambo la kifahari na hufurahi mno
pale tu tunapopata pambano la nje ya nchi na hufurahia kupanda ndege na vile
vimisosimisosi tunavyopata tukiwa mahotelini ugenini. Tukihadithiana mambo ya
safari uswahilini kwetu tunahisi tunakosa mambo mengi ya raha.
Hapo ndipo mawakala wa ngumi hutupata na mabondia huwa wanadiriki
kukubali kwenda kucheza popote tukijua tutapanda ndege, tunakula raha bila
kujali na wala kuhoji tuendako tutalipwa kiasi gani cha pambano
nitakalocheza wala kujua usalama wangu.
(itaendelea
na sehemu ya tatu)
Tuesday, November 25, 2014
Mabondia na unga (sehemu ya kwanza ya awamu tatu)
Promota wa ndondi za kulipwa, Ibrahim Kamwe, anaeleza kwa nini baadhi ya mabondia wanajiingiza kwenye biashara ya madawa ya kulevya.
![]() |
| Ibrahim Kamwe |
Asili ya mabondia wengi duniani wanatoka katika familia
duni. Kwa mfano hapa kwetu ni nadra kumkuta bondia ametoka Upanga, Oysterbay,
au Masaki ushuwani, nikiwa na maana mabondia wengi wanatoka uswahilini. Ni
watu wa hali duni. Wengi wetu hatujakalia madawati ya shule na wengine
tuliojitahidi tumefika darasa la tano au sita. Kama wazazi walikomaa ndiyo
tunamaliza la saba.
Baadhi yetu tukiwa na umri wa kuanzia miaka sita nyumbani huwa tunaanza
kupewa uzowefu wa kuuza visheti, maandazi, vitumbua, karanga n.k. na vikibaki
nyumbani hauli chakula mpaka viishe. Shuleni mwalimu mkali, darasani hafundishi
mpaka usome tuisheni ndiyo unapata kufundishwa kidogo, na ukishindwa maswali
yake unapata viboko vya ghadhabu. Hapo ndipo tunapoamua kuachana na shule na
kutinga mitaani. Michezo yetu ni katika madampo na vichochoroni na tukifikia
umri wa kuanzia miaka 12 na kuendelea tunajua jinsi ya kutafuta pesa kwa kuuza
njiwa, kucheza kamari, malani, kuiba kuku na bata, na kwa wale walio watukutu
zaidi kuuza na kuvuta bangi ni sehemu ya maisha ya kawaida tu huku mitaani
kwetu.
Mara nyingi mlo kwetu ni mmoja tu kiubishoo au kuwa wageni ndiyo
tunakula milo miwili. Katika maisha yetu muda mwingi tupo huru na michezo
kuliko kusoma, hasa kolokolo, ngoma, mpira, na ngumi. Mpira tunacheza mabarabarani,
vichochoroni, na kwenye madampo, wakati ngumi tunajifundisha katika makamali,
vichochoroni, au uwani kwa kina masta. Begi au tairi linafungwa juu ya mti,
tizi linaendelea bila vifanyio vya mazoezi vilivyo rasmi. Mwendo mdundo
tunasonga na tunashinda au kufanya vizuri katika mashindano yetu tunayoshiriki
na hali yetu duni hii hii ya kimaisha, na majina yetu kutangazwa sana katika
vyombo vya habari na kupata umaarufu mkubwa nchini, nchi jirani na hata
nchi za Ulaya.
Lakini ukibahatika kututembelea na kuangalia tunapoishi na familia
zetu na umaarufu tuliyonao, utakuta maisha yetu mabovu na yanasikitisha.
Friday, November 21, 2014
Wazanaki na dini
Simulizi hii nimepewa na Mwalimu Jack Nyamwaga, kiongozi mstaafu wa kijiji cha Butiama ambaye pia anafahamu vyema baadhi ya matukio ya historia ya kabila la Wazanaki wa eneo la Butiama. Ni simulizi inayotoa picha kuhusu baadhi ya mila na desturi za Wazanaki.
| Mwalimu Jack Nyamwaga, kulia, akiongea na Dk. Thomas Molony, mtafiti na mhadhiri kutoka Chuo Kikuu cha Edinburgh. |
"Wamisionari wa kwanza waliofika hapa Butiama walikuwa Waprotestanti. Wakati huo Roman Catholic walikuwa wameshafika Nyegina [karibu na Musoma]. Hata hivyo Waprotestanti hawakuingia ndani sana kueneza dini miongoni mwa Wazanaki.
Halafu wakaja Seventh Day Adventist (SDA) na wakasema kuwa masharti ya madhehebu yao ni pamoja na wanaume kuoa mwanamke mmoja tu na waumini wao kukatazwa kunywa pombe. Hayo masharti hayakuwa rahisi kukubaliwa na Wazanaki ambao siyo tu walikuwa na desturi ya kuoa mke zaidi ya mmoja, lakini walikuwa na asili ya kunywa pombe na hata kuitumia katika mitambiko. Mwaka 1938 SDA wakahamia Busegwe [kijiji cha jirani] ambako kulikuwa na mchanganyiko wa makabila mengine zaidi ya Wazanaki.
Halafu wakaja Mennonite na wao pia walikuwa na marufuku ya kunywa pombe. Hawa wakashauriwa kwenda Bumangi [kijiji cha jirani]. Mtemi Nyerere Burito alipoambiwa kuwa anapaswa kuwa na mke mmoja akauliza: "Hawa wake zangu 13 nitawapeleka wapi?"
Walipofika wamisionari wa madhehebu ya Roman Catholic Wazanaki wa Butiama wakapendekeza kanisa lao lijengwe Magorombe, kijiji kilicho mbali na Butiama kwenye ardhi inayotitia ikitarajiwa kuwa kanisa likijengwa hapo lintaanguka. Mmisionari aliyekwenda huko alipanda mikaratusi iliyofyonza maji na akajenga kanisa imara.
Waislamu walipokuja nao walikuwa na marufuku ya kunywa pombe. Wao wakashauriwa waende Nyamuswa kwa Mtemi Makongoro Matutu, ambaye alikuwa rafiki wa Mtemi Edward Wanzagi. Yeye aliwapokea na akasilimu.
Kizingiti kikubwa cha kuwahi kuenea kwa dini miongoni mwa Wazanaki wa Butiama ilikuwa suala la marufuku ya kuoa mke zaidi ya mmoja na marufuku ya kunywa pombe."
Subscribe to:
Posts (Atom)
.jpg)
