Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Sunday, December 7, 2014

Mabondia na unga (sehemu ya pili ya awamu tatu)

Promota wa ndondi za kulipwa, Ibrahim Kamwe, anaeleza kwa nini baadhi ya mabondia wanajiingiza kwenye biashara ya madawa ya kulevya.
Siku za hivi karibuni kuna vimaendeleo kidogo kwa baadhi ya mabondia; tunafanya mazoezi katika vilabu vya pombe kwa kuwalipa kodi ya mazoezi wenye baa. Naweza kusema Tanzania hakuna sehemu rasmi za kufanyia mazoezi ya ndani zilizotengwa na serikali kwa ajili ya raia wake wapenda michezo na kama zipo ni chache na ziko katika makambi ya jeshi kwa masharti magumu kwa raia wa kawaida. 

Siku za nyuma wakazi wa mjini kama vile Kisutu, Gerezani na Kariakoo walikuwa wanafanya mazoezi pale Arnatoglou. Siku hizi huwezi kusikia kuna mwanamichezo katokea Gerezani au Kariakoo. Iliyobaki kwao ni kuuza na kutumia madawa ya kulevya na kukimbizana na wafanyabiashara wa maeneo hayo. Naweza kuilaumu serikali kwa kutoendeleza michezo bali ilishiriki kuuwa kabisa michezo maeneo hayo na mengineyo zaidi.

Kwa sisi tulioanza kukua kimichezo pambano la ngumi likiandaliwa huwa tunalipwa kuanzia shilingi 5,000/- mpaka 20,000/- kwa mapambano haya madogomadogo na iwapo kutakuwa na pambano kubwa na kupata bahati ya kucheza unaweza kulipwa shilingi 40,000/- mpaka 100,000/-. Mapambano makubwa yanaweza kuwa moja, mawili, au matatu kwa mwaka; hayazidi hapo. Haya mapambano madogo tunaweza pata mawili mpaka sita kwa mwaka.

Msiwaone mabondia wakicheza mkadhani wana kipato kikubwa. La hasha! Ni wale tu wachache waliobahatika kupata wadhamini au waratibu wenye uwezo wa kipesa ndiyo kidogo hutoka.

Kwa sisi wengine ukiangalia elimu ya kusoma hatuna, kazi hakuna, na mchezo wa ngumi tunaupenda na pengine tuna vipaji na kufanya vizuri katika mapambano yetu. Hivyo mchezo ndiyo huwa kama ajira yetu kwa sababu tunapata chochote kidogo kupitia mchezo huo kuliko kuiba au kukimbizana na mapolisi katika kamari na kuishia jela.

Kwetu sisi mabondia huona ni jambo la kifahari na hufurahi mno pale tu tunapopata pambano la nje ya nchi na hufurahia kupanda ndege na vile vimisosimisosi tunavyopata tukiwa mahotelini ugenini. Tukihadithiana mambo ya safari uswahilini kwetu tunahisi tunakosa mambo mengi ya raha.

Hapo ndipo mawakala wa ngumi hutupata na mabondia huwa wanadiriki kukubali kwenda kucheza popote tukijua tutapanda ndege, tunakula raha bila kujali  na wala kuhoji tuendako tutalipwa kiasi gani cha pambano nitakalocheza wala kujua usalama wangu.


(itaendelea na sehemu ya tatu)

No comments: