Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Tuesday, December 13, 2016

Lugha yetu Kiswahili

Kiswahili lugha nzuri, lakini hutatanisha wengi.

Siku moja nikiwa safarini nilijikuta kwenye mgahawa wa Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro. Nilikuwa nimewahi asubuhi mapema siku hiyo nikaondoka Arusha bila kupata staftahi, au kifungua kinywa.

Nilipovuka eneo la ukaguzi la maafisa usalama na kuingia kwenye ukumbi wa abiria wanaojiandaa kupanda ndege nikawahi kwenye mgahawa na kuagiza kahawa. Aidha, hupendelea kula mayai asubuhi, kwa hiyo nikamuita mhudumu ili nimuagize mayai kuwahi kabla ya abiria kutangaziwa kuingia ndani ya ndege.

Mazungumzo yakawa hivi:

Mimi: Nitapata mayai?
Yeye: Ndiyo.
Mimi: Naomba jicho la ng'ombe.
Yeye: Hapa hatuna jicho la ng'ombe.

Sikumuelewa. Huyo huyo aliyekubali kuwa mayai yapo akaniambia hawana jicho la ng'ombe. Nilibaini naongea na mtu ambaye Kiswahili kinampiga chenga. Nilihisi alikuwa mwenyeji wa Kenya. Nikamwambia anipeleke kwa mpishi niongee naye, na huko kwa mpishi nikaagiza mayai jicho la ng'ombe na yakakaangwa vizuri tu.
Jicho la ng'ombe.
Nilivyoelewa mimi, mhudumu alidhani nimeagiza nipikiwe jicho hasa la ng'ombe.

Taarifa inayofanana na hii:
http://muhunda.blogspot.com/2013/10/msiofahamu-vyema-kiingereza-zungumzeni.html

Sunday, November 20, 2016

Rais Magufuli na ngoma za Ikulu: utamaduni unadumishwa

Desturi ya kupokea mgeni mashuhuri kwa kupiga ngoma ipo miongoni mwa watawala wa makabila mengi ya Tanzania.

Enzi za tawala za kitemi, hiyo ndiyo ilikuwa desturi. Mgeni, hasa yule ambaye alikuwa na hadhi ya utawala kama mwenyeji wake, alipigiwa ngoma za mwenyeji wake. Ni ngoma ambazo zilisikika kwenye himaya ya mtemi mwenyeji na zilisambaza taarifa ya kuwepo kwa mgeni muhimu.

Baada ya uhuru wa Tanganyika, desturi hiyo ilihamia kwenye Ikulu ya Dar es Salaam na viongozi mbalimbali waliotembelea Ikulu walipokelewa kwa desturi hiyo.
Rais Nyerere akimkaribisha Rais Sekou Toure wa Guinea kupiga ngoma za kumkaribisha Ikulu, Dar es Salaam.
Kumbukumbu yangu inaweza kuwa siyo sahihi, lakini sikumbuki kama baada ya Mwalimu Nyerere desturi hii ilifuatwa sana, ingawa tunaona sasa kuwa Rais wa awamu hii ya tano, John Magufuli, ameichangamkia vyema na huwashirikisha viongozi wanaofika Ikulu kupiga ngoma zilizopo Ikulu.

Inawezekana pia kuwa siyo wageni wote wanaofika Ikulu ambao hukaribishwa kwa kupiga ngoma,

Thursday, November 10, 2016

Mbuga ya Serengeti inavyoonekana juu ya Mlima Balili

Mkoa wa Mara una vivutio vingi vya utalii, na mojawapo ya vivutio hivi ni Mlima Balili uliyopo Wilaya ya Bunda.
Kutoka juu ya Mlima Balili kuna mojawapo ya mandhari nzuri katika eneo hili. Kwenye picha, upande wa kushoto ni Hifadhi ya Taifa ya Serengeti. Juu kidogo ya picha hii unaoenakana Mto Grumeti ambao ni mojawapo ya mito inayotiririka ndani ya Hifadhi ya Serengeti na kuishia ndani ya Ziwa Victoria.

Ziwa Victoria linaonekana juu kulia. Upande wa kulia ni barabara kuu inayotoka Musoma hadi Mwanza.

Friday, August 12, 2016

Kijijini kama mjini

Wapo wengi ambao hawakupenda uamuzi wa serikali ya awamu ya nne ya kuanzisha kwa wilaya mpya ya Butiama. Mimi ni mmojawapo.

Nimejihusisha na kazi ya kutangaza historia na utamaduni wa eneo la Butiama kwa zaidi ya miaka saba sasa, na natambua ni jinsi gani utamaduni wa eneo unavyoweza kuathirika unapotokea muingiliano wa haraka kati ya maeneo ya mijini na ya vijijini. Mawasiliano mazuri kati ya miji na vijiji yanaweza kuongeza kasi hiyo, na hali kadhalika, uamuzi wa kuanzisha wilaya mpya pia unaweza kuleta matokeo hayo hayo.

Wilaya mpya inakuja na ongezeko kubwa la wafanyakazi kutoka maeneo mbalimbali. Nao siyo kama wanakuja na tamaduni zao za asili tu, ila wanaleta zaidi tamaduni za miji, na hata sheria za miji. Matokeo yake ni kudumazwa kwa tamaduni za asili za maeneo hayo mapya ya wilaya, na hasa kama yalikuwa maeneo ya vijijini.
Mojawapo ya sehemu za burudani na starehe za Butiama zilizoibuka baada ya kuanzishwa kwa wilaya mpya ya Butiama.
Msimamo wangu haulengi kutetea suala la ukabila, bali unalenga kulinda na kutunza mila na desturi za eneo mahususi kwa madhumuni ya kuendeleza utalii wa utamaduni.

Saturday, July 30, 2016

Mada yangu ya leo: mwizi ni mwizi tu

Sikumbuki niliisoma wapi habari hii, lakini kuna kichwa cha habari cha toleo la gazeti la hivi karibuni liliarifu kuwa yule mtuhumiwa wa kuiba milioni 7 kwa dakika "mwenye asili ya Kiarabu" amefikishwa mahakamani.

Kwanza, nitamke wazi kuwa hili suala liko mahakamani na mimi simhukumu mtuhumiwa. Namtetea kwa kubaguliwa. Akikutwa na hatia, nitazungumzia hilo.

Mwizi ni mwizi tu, hata kama ni kabila yako. Uandishi wa aina hii wa kubainisha kuwa mtuhumiwa ana asili ya Uarabu ni hatua ya wazi ya kubagua mtu kwa rangi yake ya ngozi. Maana inayojitokeza ya makala hii ni kuwa kama angekuwa Mbantu akutwe na hatia ya kuiba milioni 7 kwa dakika, tatizo lingekuwa dogo zaidi. Labda milioni 7 ingekuwa 2 tu kwa sababu tu mwizi alikuwa ana rangi tofauti ya ngozi.