Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Saturday, September 11, 2010

John Mnyika wa CHADEMA anajibu hoja dhidi ya sera ya majimbo (sehemu ya kwanza)

Katika taarifa iliyopita, Amani Millanga, akiandika kuhusu uchaguzi mkuu 2010, alitoa hoja dhidi ya sera ya majimbo. Ingawa hakutaja chama moja kwa moja, nilihisi anazungumzia sera ya majimbo ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA). Niliwaomba CHADEMA wajibu hoja.



Kama nilivyoahidi, naleta hapa sehemu ya kwanza ya makala mbili za Naibu Katibu Mkuu wa CHADEMA, John Mnyika, alizowahi kuandika juu ya sera hiyo.
-----------------------------------------------------------------------------------------------------------

John Mnyika, Naibu Katibu Mkuu wa CHADEMA
Sera ya Majimbo ni siri ya maisha bora kwa kila Mtanzania

na

John Mnyika
Mkurugenzi wa Mambo ya Nje

Hivi karibuni pameanza tena mjadala kuhusu 'majimbo' na masuala kadhaa yameibuliwa.


Huu ni wakati muafaka nami nichangie hoja kadhaa katika mjadala huu muhimu.


Nikumbushe tu kwamba mjadala huu ulishika kasi sana wakati wa Uchaguzi Mkuu mwaka 2005 kwa vijembe vya majukwaani.


Hoja kuu ya kufahamu ni kwamba chimbuko la sera ya majimbo nchini ni falsafa ya CHADEMA ya nguvu ya umma.


Kwani umma ndio unapaswa kuwa na mamlaka lakini pia umma ndio unapaswa kunufaika na rasilimali za nchi.


Niweke pia bayana kwamba katika uchaguzi CHADEMA haikuwa na ajenda ya majimbo kama ajenda inayosimama peke yake. Ilikuwa ni sehemu ya ajenda nyingine.


Tulisema wazi kwamba tatizo la CCM ni kwamba huwa inakuja na ilani ya kuahidi kila kitu na hatimaye kutofanya chochote.


Sisi tulisema pamoja na kuwa na sera nyingi lakini tutakuwa na vipaumbele vitano tu:

Mosi, mfumo mpya wa utawala, pili; elimu, tatu; kilimo, nne; uchumi; na tano afya. Na hata katika vipaumbele hivi bado tulichagua maeneo machache mahususi.


Mathalani katika uchumi tulilenga kodi (kupunguza ukubwa wa kodi na kuhakikisha kuwa kodi zinakusanywa ipasavyo).


Ajira na rasilimali hususan madini katika mfumo wa utawala.

Hapa tulikuwa na masuala matatu, kwanza, uongozi mpya kwa maana ya wananchi kuwaondoa viongozi walioko madarakani kwa maana wameshiriki ufisadi wa nyuma, hivyo hawawezi kufanya mabadiliko yoyote ya maana.


Pili; kusafisha mfumo wa utawala kwa maana ya kupambana na rushwa na ufisadi, na tatu, kutengeneza muundo mpya wa utawala ikiwamo kuanzisha muundo wa majimbo.


Lakini kwa kuwa suala la majimbo lilipata ladha zaidi na mashambulizi mengi; sera, ajenda, maana ya mfumo mpya wa utawala ikafunikwa kabisa.


Sina nia ya kujadili makala ya leo kwa nini hali hii ilijitokeza.


Kwa kuwa wengi wamezoea kutumia jina "sera ya majimbo' nami katika mjadala huu nitatumia jina hili ili twende pamoja.


Suala la sera ya majimbo ni suala la kikatiba. Chama chochote cha siasa kinauza kwa wananchi matakwa yake kama kikipewa ridhaa na wananchi.


Matakwa hayo yanaweza kutokana na misingi ya chama husika ama matakwa ya wananchi ama matakwa ya viongozi wa chama husika.


Lakini baada ya uchaguzi zipo sera ambazo utekelezaji wake lazima urudi tena kwa wananchi kupata ridhaa ya pamoja, mathalani CCM wamejikuta suala la mahakama ya kadhi linapaswa kurudi kwa wananchi, ingawa liko katika ilani ya chama chao.


Lakini mambo mengi ya chama hutekelezwa kwa kwenda kwa wawakilishi wa wananchi yaani Bunge.


Kadhalika, suala la kuundwa kwa majimbo ni suala la mabadiliko ya katiba hivyo kwa vyovyote vile CHADEMA ingepaswa kurudi kwa wananchi.


Hata ndani ya chama kwenyewe, misingi na sera ilikubaliwa kwa pamoja lakini tafsiri ya kina kila mtu alikuwa anaifanya kwa mujibu wa mahali.


Kwa vyovyote vile, kama tungechukua dola tungepaswa kukubaliana kuhusu masuala kadhaa kwa undani kabisa kabla ya kwenda kwa wananchi kuomba ridhaa.


Je, hii ni ishara ya kutoifanyia kazi sera kwa undani? Hapana. Ni kawaida ya ilani ya uchaguzi. Huwa inatoa ahadi ya ujumla. Mathalani, tutahakikisha kila mwanafunzi anapata nafasi ya kusoma shule ya msingi - suala la nani atafanya nini kutekeleza ahadi hii linakuwapo kwenye programu ya utekelezaji ambayo inaingia kwa kina kuweka mikakati na shughuli mbalimbali.


Suala la sera ya majimbo siyo geni duniani. Nchi kadhaa za Afrika zinafuata mfumo huu, mathalani Afrika Kusini, Nigeria, Ethiopia na nyinginezo. Ulaya nchi nyingi zinafuata mfumo huu.


Marekani ya Kaskazini, Australia. Kwa kweli dunia kwa ujumla wake inatambua umuhimu wa majimbo.


Wengine wamekuwa na majimbo kutokana na tofauti za kimbari/kinasaba (ethnic federalism), wengine ni sababu tu za kurahisisha utendaji (functional federalism) na wengine ni umbali tu wa jiografia (geographical federalism).


Kwa hiyo, wote wanaochambua majimbo ni vyema wakachambua pia ufiderali unafanyaje kazi katika nchi hizi, faida na hasara zake.


Ukiangalia hata muungano wa Tanganyika na Zanzibar ni aina ya ufiderali, ingawa ni ufiderali tenge!


Kwa hiyo cha msingi hapa ni kujadili misingi ya Sera ya majimbo ya CHADEMA na kuangalia vipi ni sehemu ya falsafa ya nguvu ya umma na kwa vipi inaendana na misingi ya CHADEMA, kwa vipi inaweza kusaidia utekelezaji wa sera za CHADEMA na kwa ujumla ni namna gani ni silaha ya nyongeza katika kukabiliana na ujinga, umaskini na maradhi na hatimaye kuleta maisha bora kwa kila Mtanzania.


Kwa mtazamo wangu, hii ni misingi ya "Sera ya majimbo".


Msingi wa kwanza ni kujenga uwezo wa kisiasa, uongozi na uwajibikaji. Sera ya majimbo inaelekeza taifa kuwa na viongozi wa kuchaguliwa moja kwa moja na wananchi katika ngazi mbalimbali.


Hii ina maanisha kwamba kwa muktadha wa sera ya majimbo, ofisi na vyeo vya mkuu wa mkoa, mkuu wa wilaya, katibu tarafa vitafutwa.


Uzoefu unaonyesha kwamba wamekuwa wakiongeza mzigo wa gharama kutokana na mwingiliano kati yao na wakurugenzi, mathalani wa halmashauri ambao ni wataalamu wanaofanya kazi chini ya viongozi wa kuchaguliwa.


Uzoefu unaonyesha kwamba kwa kuwa mikono ya mhimili wa serikali ngazi ya chini viongozi hawa wamekuwa sababu ya serikali kuu kuingilia serikali zingine na kimaamuzi na kimwelekeo.


Matokeo yake ni kuwa nchi nzima inaendeshwa na Ikulu Dar es Salaam hata katika mambo ya kawaida kabisa.


Urasimu huu umekuwa kikwazo kwa maendeleo. Nguvu ambayo viongozi hawa wamepewa toka wakati wa muundo wa kikiloni wa kutawala kwa kutumia mawakala umewafanya wawe miungu watu na wanyanyasaji.


Kwa kifupi ni watu wasiohitajika. Kwa upande mwingine, sera ya majimbo inataka mameya wachaguliwe na wananchi moja kwa moja badala ya mabaraza ya madiwani ili kuongeza uawajibikaji.


Kwa kifupi, msingi huu wa sera unachochea hamasa ya uongozi na kuweka viongozi wenye kuwajibika kwa watu. Hii ndiyo falsafa ya nguvu ya umma katika vitendo.


Msingi wa pili ni kushusha na kugawanya madaraka (Devolving and separation of powers). Kwamba uzoefu unaonyesha kuwa majimbo yanapopewa madaraka nayo yanatoa madaraka kwa ngazi za chini yake mpaka chini kabisa.


Serikali kuu inapohodhi mamlaka kadhalika ngazi za chini zinahodhi mamlaka ya ngazi za chini.


Hoja itatolewa kwamba je, kwa nini njia isingekuwa serikali huru za mitaa? Hiyo ni njia moja lakini mamlaka (mandate) ya serikali ya mtaa huwa katika maeneo machache, tena ya utekelezaji zaidi tofauti na mfumo wa majimbo.


Mfumo wa majimbo unahusisha masuala gani ambayo majimbo yanaweza kuyashughulikia moja kwa moja kama ambavyo masuala yanavyogawanywa kwa misingi ya muungano na yasiyo ya muungano.[?]


Lengo ni kufanya serikali ya fideresheni ishughulike na mambo machache na kila eneo lisimamie mambo yake kwa mujibu wa mazingira ya eneo husika. Hiyo ndiyo nguvu ya umma!


Msingi wa tatu ni kupanua umoja na mshikamano miongoni mwa Watanzania na kuvunja dhana ya ukabila.


Mfumo wa sasa wa kugawa wilaya pamoja na sababu zingine zinazotolewa na serikali umekuwa ukilalamikiwa kuwa umejikita katika kugawa wilaya kwa mujibu wa makabila - mfano Rombo ya Warombo, Ukerewe ya Wakerewe - mifano ni mingi kweli kweli.


Sera ya majimbo imelenga kuvunja mshikamano wa kiwilaya na badala yake kutengeneza fungamano la kimajimbo - mathalani Jimbo la Kaskazini linajumuisha mikoa ya Arusha, Kilimanjaro, Manyara na Tanga - hili ni jimbo la Wamasai, Wairaq, Wabarabaig, Wachaga, Wapare, Wabondei n.k.


Jimbo la Ziwa, ni mikoa ya Kagera, Mara, Mwanza n.k., hii ina maanisha Wasukuma, Wahaya, Wakurya, n.k.


Lengo ni kutengeneza kizio (unit) kipya cha utambulisho chini ya taifa (Tanzania), yaani wakazi wa jimbo fulani kufanya watu wajinasibishe kabisa na majimbo yao.


Hii ni kwa sababu majimbo yanakuwa na upekee wake ambao mtu anapenda 'kujinasibisha' nao.


Mathalani jimbo moja linaweza kuwa na sheria za ajira zenye kuvutia zaidi, n.k. Hii ndiyo nguvu ya umma!


Msingi wa nne ni kuweka utamaduni wa ushindani na upekee ndani ya nchi. Kama ambavyo nchi zinavyoshindana ndivyo ambavyo majimbo yenye taratibu tofauti za kibisahara, ajira, uwekezaji, makazi na kadhalika yatakavyoshindana.


Serikali ya majimbo inatoa mwanya wa majimbo kujiamulia mwelekeo wake katika masuala fulani fulani.


Mathalani jimbo moja linaweza kupiga marufuku uvutaji sigara; majimbo mengine yanaweza kuiga ama yanaweza kutofuata.


Hata katika michezo na kadhalika, ushindani utaongezeka maradufu. Kila jimbo litataka kujinufaisha na mafanikio fulani fulani.


Dhana ya ushindani na upekee imeshindikana katika mazingira ya sasa ambapo kila halmashauri inaongozwa na maelekezo ya Dar es Salaam na inajivunia mafanikio ya nchi kwa ujumla wake.


Hata binadamu, ukipewa uhuru wa kujiamulia una uwezo wa kufanya vitu vya pekee zaidi kuliko ukiwa sehemu ya mfumo mpana.


Hii ni saikolojia ya maendeneleo. Hii ndiyo falsafa ya nguvu ya umma!


Msingi wa sita ni kupanua vyanzo vya mapato. Pia majimbo yanapopaswa kujitegemea kwa aina fulani, moja kwa moja yanapaswa kuanza kutaufta njia za kujitegemea.


Hii itasaidia vyanzo vya mapato kupatikana. Hii ni kutokana na kanuni ya mwitu (The law of the jungle).


Sasa hivi kila mahali wanaitazama Dar es Salaam ikusanye pesa nchi nzima na kutoka kwa wahisani na kila eneo lina achama mdomo kwa ajili ya kupokea.


Wapinzani wa hoja hii wanatoa hoja kwamba lipo jimbo ambalo halina rasilimali na wanatolea mfano wa jimbo la kusini.


Hawa ni watu ambao pengine hawajui kwamba Tanzania ina rasilimali kila mahali. Wananchi wengi wamekuwa wakilalamika kuwa mikoa ya kusini haina maendeleo.


Ukweli ni kwamba tafiti zinaonyesha kuwa mikoa ya kusini ina rasilimali na mali asili nyingi sana, tatizo kubwa ni miundo mbinu.


Jimbo la Pwani ya Kusini kwa mfano lina mikoa ya Lindi, Mtwara na wilaya a Kisarawe na Kibiti.


Jimbo hili lina rasilimali kama madini, bandari, uvuvi, nishati ya gesi, kilimo cha korosho, mikoko pamoja na utalii. CHADEMA ina kila sababu ya kuwaeleza wananchi umuhimu wa majimbo kwani kila jimbo lina rasilimali za kutosha, ila kwa kuwa serikali ya CCM imekuwa ikiwahadaa wananchi na kuwafanya wabweteke kisaikolojia ili wasijeletee maendeleo, imekuwa ikipinga vikali serikali ya majimbo.


Hata kama kungekuwa hakuna maliasili: ukweli unabaki kwamba zipo nchi duniani ambazo hazina maliasili lakini zimeneemeka kutokana na kutoa huduma tu!


Lakini kwa upande mwingine kama sehemu ya sera ya majimbo, lipo pato ambalo litakusanywa serikali kuu na kusaidia katika maeneo ambayo yana upungufu.


Msingi wa saba ni wananchi kunufaika kutokana na matunda ya rasilimali za eneo lao.


Mfumo wa sasa ambapo rasilimali zote zinamilikiwa na "Dar es Salaam" kwa maana ya serikali kuu, unafanya wananchi wasinufaike na rasilimali za maeneo yao kikamilifu.


Mathalani kodi za madini, mbuga za wanyama n.k., sehemu kubwa inakuja serikali kuu ama kugawanywa katika mfumo ambao haunufaishi maeneo husika ama kutumika katika matumizi ya anasa ya serikali kuu.


Mathalani, pamoja na kuchimba madini yenye thamani, Geita ni moja ya wilaya maskini kabisa. Wanaofaidi madini ya Geita wako Dar es Salaam.


Serikali ya majimbo itakuwa na sehemu ya mamlaka ya ugawanyaji wa mapato yanayotoka katika eneo husika.


Pamoja na kukusanya mapato ya pamoja ya serikali kuu. Hii ndiyo nguvu ya umma.


Msingi wa nane ni kupunguza ukubwa wa gharama za uendeshaji wa serikali. Serikali ya majimbo haiongezi ngazi yoyote ya utendaji kwa kuwa inavunja ngazi za mkoa (ambayo ni mikoa mingi zaidi - takriban 26) na kutengeneza ngazi ya jimbo (majimbo ni machache, manne mpaka manane, kutegemea na makubaliano ya kikatiba).


Wakati huo huo ukubwa wa serikali kuu utapunguzwa kwa kuwa wizara zitabaki chache za mambo ya federesheni mathalani ulinzi, mambo ya nje, fedha.


Wizara nyingine zote zinakuwa katika ngazi ya majimbo husika kwa mujibu wa utaratibu wa majimbo husika.


Kutokana na ukaribu wa utoaji huduma na utendaji, mwishowe gharama za utendaji zitakuwa ndogo kuliko Dar es Salaam inavyoendesha nchi nzima katika kila jambo.


Mathalani utaoaji wa pasi za kusafiria (passport), vibali vya elimu na mambo mengine mengi.


Serikali ya majimbo itahakikisha mfumo wa utendaji unakuwa mdogo kwa kujenga mifumo iliyokaribu zaidi. Hii ndio nguvu ya umma!


Msingi wa tisa ni muundo mpya unaosaidia utekelezaji wa majukumu. Hapa ni mjadala wa kipi kinaanza - muundo ama majukumu (structure or function).


Sera ya majimbo inachukua mtazamo wa kwamba yote yanakwenda pamoja. Wachambuzi wengi wamekuwa wakitoa hoja kwamba matatizo ya msingi ya mwananchi ni hali mbaya ya maisha, kipato duni, uchumi mbovu, elimu duni n.k. Na wanachotaka wananchi ni suluhisho la haya matatizo ya msingi si 'porojo' za sera ya majimbo.


Lakini ukweli ni kuwa kuna uhusiano wa moja kwa moja kimatokeo baina ya masuala haya (direct and causality relationship).


Kwa mfano, asili ya wananchi wa Geita kuwa na uchumi mbovu ni sera mbovu ya madini iliyopitishwa Dar es Salaam lakini pia mfumo mbovu wa mgawanyo wa mapato unaosimamiwa kutoka Dar es Salaam na kwa halalishwa na sheria na mikataba mibovu.


Pengine wananchi wa Geita na jimbo lao wanajua zaidi nini ambacho wanataka; sehemu ya tiba ni kuwapa sehemu ya mamlaka ya kujiamulia mambo yao. Wajikaange kwa mafuta yao! Tatizo la elimu pengine ni maagizo ya waziri kutoka Dar es Salaam ambaye hajui kabisa kuwa hali ya Mwanza ni tofauti na Mtwara.


Sasa, hata elimu aamue waziri Dar es Salaam? Changamoto ya nchi yetu ni wananchi kukosa motisha (motivation) na hisia za umiliki (sense of ownership).


Ujinga, umaskini na maradhi ni matokeo tu, chanzo ni uongozi. Kuweka uongozi bora ni suala moja. Kushughulikia mfumo na muundo wa uongozi/utawala ni sehemu ya suluhisho.


Upo wasiwasi wa kufanya hivi kwamba kuna kutengeneza matabaka. Hata sasa matabaka katika nchi yetu yapo, tena mabaya zaidi.


Maana haya ni ya mtu na mtu.Afadhali utofauti wa kisera kati ya jimbo na jimbo kuliko mtu na jirani yako.


Kuna hofu kwamba yapo majimbo yatakayojitenga. Katika muundo wa Tanzania ya jimbo lenye makabila mbalimbali haliwezi kujitenga, ilhali jeshi, mambo ya nje na masuala kadhaa nyeti yako kwenye kapu moja.


Huku ni kuhofia kivuli. Huku ni kuyaficha majimbo ambayo ni siri ya maisha bora kwa kila Mtanzania.


Ndiyo maana nasisitiza, tunapaswa kukubali mabadiliko ya kweli na uhuru wa kweli. Hakuna kulala, mpaka kieleweke.

No comments: