Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Tuesday, September 21, 2010

Kisa cha kuacha kuvuta sigara: safari yangu ya kupanda Mlima Kilimanjaro (makala ya tatu kati ya kumi)

Ijumaa 15 Agosti 2008
Niliondoka Butiama alfajiri, nikikusudia kuendesha gari hadi Mwanza kabla askari wa usalama barabarani hawajafika barabarani kukagua bima ya gari ambayo muda wake ulikuwa umeisha siku chache zilizopita. Tatizo langu ni kuwa niligundua wakati muda umeshapita kuhusu gharama kubwa za kupanda Mlima Kilimanjaro, na sikuwa na uhakika iwapo ningeweza kumudu kwa pamoja gharama za kupanda mlima na kulipia bima ya gari.

Nilipofika Mwanza nilipita ofisi ya Air Tanzania kuchukuwa tiketi yangu ya bei nafuu niliyopewa na Air Tanzania Corporation Limited (ATCL) ikiwa ni mchango wao kwa The Mwalimu Nyerere Charity Climb 2008 kwa kunisafirisha toka Mwanza hadi Kilimanjaro, na kurudi Mwanza. Nahisi kama mzaha kuwa masikioni tukio lenyewe linasikika kama tukio moja kubwa sana la kuchangisha pesa, lakini ukweli ni kuwa ni mimi peke yangu tu, mtu mmoja ambaye nimejiingiza kwenye utata wa kukwea Mlima Kilimanjaro. Mimi ndiyo nilkuwa kampeni nzima. Nilipanda ndege kuelekea Uwanja wa Kimataifa wa Kilimanjaro jioni.

Jumamosi 16 Agosti 2008
Niliamka mapema kutuma makala yangu kwenye gazeti la Sunday News nikiwa nimechelwa tena, kama kawaida. Ninalo tatizo kubwa la kupata mada mpya ya kuandika kila juma kwa ajili ya makala yangu. Natumia sehemu kubwa ya juma kufikiria jambo ambalo naweza kuandika kwenye makala yangu na inapofikia wakati wa kukaa chini na kuandika makala yenyewe, nakuwa nimeshavuka muda uliyowekwa wa kuwasilisha makala. Faida mojawapo ya kupanda Mlima itakuwa nitafanikiwa kukamua mada zaidi ya moja kwa ajili ya kuandikia kwenye makala yangu.

Niliongea na Zainab Ansell, mmiliki wa Zara Tanzania Adventures na kaniambia kuwa kamuni yake imeamua kunilipia gharama zote za siku nane za kupanda Mlima Kilimanjaro zinazofikia dola za Marekani 1,500. Nilifurahi sana.

Jioni, rafiki yangu toka Mwanga alinitumia gari kunichukuwa Moshi na nikalala kwenye chumba ambacho kilikuwa na takriban mbu mia moja. Nilitumia zaidi ya saa nzima kuwapunguza wale mbu kwa kutumia mbinu inayojulikana kama kombora la nguo. Mbinu hiyo inahusisha kusubiri mbu atue kwenye ukuta halafu kufurumisha dhidi ya ukuta nguo na kumbamiza ukutani na kumuua. Kwa kadiri ninayofahamu, ndiyo njia iliyo rafiki zaidi kwa mazingira ya kumaliza mbu.

Taarifa ijayo: Nakutana na Le, mtu aliyebobea kupanda milima, na Yahoo, muongozaji wetu wa mlimani.
Makala zinazohusiana na hii:

Sunday, September 19, 2010

Kisa cha kuacha kuvuta sigara: safari yangu ya kupanda Mlima Kilimanjaro (makala ya pili kati ya kumi)

Mwaka 2007 ilivyoonekana kuwa nilikuwa nimepoteza fursa nyingine ya kupanda Mlima Kilimanjaro niliamua kuweka nguvu ya ziada, ama sivyo ningeendelea kuota tu kufika kilele cha Uhuru. Nilipaswa kujiweka katika hatua ya kutorudi nyuma. Niliamua kuwaambia watu wachache kuwa nitapanda Mlima Kilimanjaro mwaka huu kuchangisha pesa kwa ajili ya elimu. Wa kwanza kumueleza hayo alikuwa mwalimu mkuu wa Sekondari ya Wasichana ya Chief Edward Wanzagi iliyo jirani na Butiama na akaniambia, "Kwa nini usichange pesa kwa ajili yetu? Tunahitaji mabweni ya wanafunzi."

Aidha, niliandika barua pepe kwa Howard Chinner, mkazi wa Sevenoaks, England, ambaye nimekuwa nawasiliana nae baada ya yeye kusoma moja ya makala zangu. Alipendekeza naweza pia kuchangisha pesa kwa ajili ya Village Education Project Kilimanjaro (VEPK) iliyopo Mshiri, Marangu, kwenye miteremko ya Mlima Kiliamnajro.

Ilikuwa ni kutokana pia na pendekezo lake kuwa tukio ambalo lingekuwa halina hata jina, likihusisha kupanda mlima mrefu kuliko yote duniani inayosimama pekee (milima mirefu zaidi ya Kilimanjaro, kwa mfano Mlima Everest, ni mkusanyiko wa milima zaidi ya mmoja), lilipata jina la The Mwalimu Nyerere Charity Climb. Baada ya kuanza safari ya kuelekea kileleni, na kadiri nilivyoendelea kujenga matumaini yangu kuwa nitafika kileleni, niliamua kupachika "2008" kwenye jina hilo, nikiashiria kuwa litakuwa ni tukio la kila mwaka.

Kwa ahadi hizo mbili (moja kwa Skondari ya Chief Edward na nyingine kwa VEPK) haikuwezekana tena kutafuta sababu  ya kutopanda mlima. Baada ya hapo nilituma barua pepe kwa wote niliyofikiri wangekuwa na utashi wa kuchangia mojawapo wa walengwa wa mchango huo wa hisani. Nilipokea majibu ya kutumainia, na hiyo ikanizuwia zaidi kupanga mipango yoyote isiyojumuisha kipengele cha kupanda Mlima Kilimanjaro.

Kabla ya kupanda, nilitumia muda kidogo kuongeza uwezo wangu wa kuhimili kwata kwa kufanya mazoezi ya kutembelea baadhi ya vilima vya Butiama. Nilibadilisha mpango wangu wa awali wa kutembea kilomita tano nikizunguka msitu wa Muhunda, msitu wa nasaba wa Butiama, na kuanza kufanya safari ndefu zaidi za kwenda Mlima Mtuzu, nikiongeza kiasi cha kilomita tatu za ziada. Wakati nilipoanza kuzoea mazoezi yangu haya ya ziada, niliaanza kujenga imani kuwa mwili wangu ulianza kubadilika kuwa kifaa cha kutisha cha kupanda mlima.

Rafiki yangu mmoja anayeishi jirani na Mlima Kilimanjaro aliniambia kuwa imani yangu hiyo ilikuwa haina msingi, kwamba Butiama haina milima ila ina vichuguu tu, na kuwa ningetaka kupata picha halisi ya kupanda Mlima Kilimanjaro ningeipata kwa kumtembelea Mwanga na kukaa pale kwa muda nikikwea milima ya Upare.

Nilienda Mwanga na kukaa siku mbili, lakini sikupanda mlima wowote. Badala yake nilipumzika na kuomba kuwa nilikuwa imara kiasi cha kutosha kupanda Mlima Kilimanjaro.

Makala ijayo: Naondoka kijijini, na kuelekea mlimani.


Makala inayohusiana na makala hii:

Saturday, September 18, 2010

Mwenge umepita Butiama leo

Mbio za Mwenge wa Uhuru leo zimefika Butiama. Kama desturi ya mbio za mwenge katika miaka tangu kufariki Mwalimu Nyerere mwaka 1999, ratiba ya mwenge kila mwaka inahusisha kupitisha mwenge kwenye makazi ya Mwalimu Nyerere yaliyopo Mwitongo, Butiama.

Kukaribisha mwenge leo Mwitongo alikuwa Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi Mkoa wa Mara, Makongoro Nyerere, akiongoza baadhi ya wakazi wa kijiji cha Butiama.
Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Mara, Makongoro Nyerere, (mwenye shati la kijani) akimkaribisha Mkuu wa Wilaya ya Musoma, Geoffrey Ngatuni, kwenye tukio la mwenge kupita Mwitongo, Butiama.

Mwenge ukiingia Mwitongo, Butiama.

Makongoro Nyerere akipokea mwenge toka kwa mkimbizaji mwenge, Flatei Massay

Ulinzi wa mwenge siyo wa kawaida.

Ulinzi wa mwenge siyo wa kawaida.

Kiongozi wa mwenge, Dk. Nassoro Matuzya, akipandisha mwenge eneo la mwenge wa Mwitongo.
Kabla ya risala iliyotolewa na kiongozi wa mbio za mwenge, Dk. Nassoro Matuzya, Mwenge wa Uhuru ulipandishwa kwenye eneo ulipo mwenge wa Mwitongo ili kuwasha mwenge wa Mwitongo kwa kutumia Mwenge wa Uhuru.

Wakimbizaji mwenge baadaye walizuru kaburi la Mwalimu Nyerere lililopo Mwitongo.

Friday, September 17, 2010

Kisa cha kuacha kuvuta sigara: safari yangu ya kupanda Mlima Kilimanjaro (makala ya kwanza kati ya kumi)

Sikumbuki ni lini nilianza kupata wazo la kupanda Mlima Kilimanjaro, lakini inaweza kuwa ni miaka minane iliyopita.* Bila sababu yoyote ya msingi, niliamua nataka kupanda Mlima Kilimanjaro.

Kufikia uamuzi huo ilikuwa ni jambo rahisi kuliko yote, lakini kuetekeleza azma hiyo ilikuwa jambo tofauti kabisa. Miaka kadhaa ikapita na nikatambua kuwa bila kuchukuwa hatua madhubuti, kamwe nisingepanda huu mlima.

Miaka ilivyopita, niliibua sababu zaidi za kunisukuma kupanda huu mlima. Niliendelea kukutana na watu kutoka pembe zote za dunia ambao walikuwa wameshapanda Mlima Kilimanjaro na nikajihisi kunyimwa kufaidi hazina kubwa ya Watanzania ambayo watu toka nje wameweza kuivumbua wakati Watanzania wachache mno wanapanda Mlima Kilmanjaro. Nilifikia hatua nikaamua sitaweza kuvumilia tena hali ya kukutana na mgeni toka nje ambaye ameshapanda Kilimanjaro na nishindwe kumwambia kuwa hata mimi nimeshaupanda huo mlima.

Katika muongo uliyopita mengi yamesemwa na kuandikwa kuhusu ongezeko la joto duniani na athari zake kwa mazingira. Baadhi ya wataalamu wanatabiri kuwa kwa sababu ya ongezeko la joto duniani theluji za Kilimanjaro zitayeyuka katika muda siyo mrefu ujayo. Nilipata msukumo kupanda kilele kirefu kabisa cha Afrika kuona hiyo theluji kabla athari za maendeleo ya binadamu hayajaifuta toka kwenye uso wa dunia.

Lazime itamkwe kuwa kuna mtazamo tofauti unaoashiria kuwa barafu za Mlima Kilimanjaro zinapunguwa siyo kutokana na ongezeko la joto duniani, ila kwa sababu ya mkusanyiko wa sababu nyingine. [Bonyeza hapa kusoma makala ya Kiingereza yenye mtazamo huo tofauti].

Mwezi Agosti 2005 nilikutana na Jenerali (Mstaafu) Mirisho Sarakikya, aliyewahi kuwa mkuu wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) na ambaye amebobea kwa kupanda Kilimanjaro. Ameshapanda Kilimajaro mara 46. Nilimuahidi kuwa ningeungana naye mwezi Septemba 2006 lakini sikuweza sikuweza kutimiza ahadi, na nikaendelea kusumbuliwa na maneno yake tulivyoona mwaka 2005: "Nitasikitika sana kama wewe ni kati ya wale Watanzania ambao hukutana nao mara moja na hatuonani tena."

Sababu moja inayoweza kuchangia Watanzania wachache kufika kwenye kilele ni gharama. Inagharimu wastani wa dola za Marekani 1,500 kulipia safari ya siku nane, gharama ambayo Watanzania wengi hawaimudu. Kuna idadi kubwa ya Watanzania wanaoweza kulipa gharama hizo, lakini swali ni iwapo wanayo azma ya kukabili kibarua cha kupanda ambacho, kwa binadamu yoyote wa kawaida, ni kibarua kigumu.

Nilishangazwa kugundua kuwa, mbali na waongozaji na wabeba mizigo, ilikuwa ni kama hamna kabisa Mtanzania kwenye Mlima Kilimanjaro. Yawezekana nilikutana na zaidi ya wageni 100 nilipopanda Mlima, lakini kati ya hao nilionana naMtanzania mmoja tu akielekea kileleni wakati nashuka. Kwa masikitiko, aliathiriwa na ugonjwa wa mwinuko unaoletwa na upungufu wa oksijeni na aliteremshwa kutoka mlimani kwa machela.

Makala ijayo: Maandalizi ya kupanda


* Hii makala ilichapishwa kwanza tarehe 18/10/2008, kwenye wavuti yangu ya lugha ya Kiingereza, From Butiama and Beyond

Wednesday, September 15, 2010

Mlima Kilimanjaro Novemba

Mwezi Novemba, mwaka huu, natarajia kupanda Mlima Kilimanjaro kwa mara ya tatu chini ya mpango wa kuchangisha pesa za hisani katika tukio ambalo linaitwa The Mwalimu Nyerere Charity Climb 2010.

Mwaka 2008 nilifanikiwa kuchangisha zaidi ya Sh.20/- milioni ambazo zilichangia ujenzi wa mabweni ya wanafunzi wa Shule ya Sekondari ya Wasichana ya Chief Edward Wanzagi iliyopo Buturu, Mkoa wa Mara.

Wanafunzi wa Sekondari ya Wasichana ya Chief Edward Wanzagi, mbele ya shule yao.

Mwaka 2009 nilipanda tena Kilimanjaro nikikusudia kuchangisha pesa kwa ajili ya asasi ya mjini Musoma, Community Alive, inayojishughulisha na kutoa msaada kwa watoto yatima ambao wazazi wao wamekufa kwa UKIMWI. Pamoja na kupata msaada mkubwa wa vyombo vya habari katika kuhamasisha uchangiaji, pesa zilizoahidiwa zilivuka kwa kiasii kidogo tu Sh.2/- milioni. Na sehemu yote ya hizo ahadi haikulipwa.

Mwaka huu bado haijaamuliwa mchango utakuwa kwa ajili ya madhumuni gani.

Mwaka 2008 nilipanda Kilimanjaro na raia wa Vietnam, Le Huyn. Mwaka jana nilipanda na Watanzania wawili: Notburga Maskini wa Ofisi ya Waziri Mkuu (Tawala za Mikoa), pamoja na Gerald Hando wa Clouds FM.

Mwaka huu Gerald Hando amesema atashiriki tena. Kundi zima litashirikisha wafuatao:

1. Jaffar Amin 
Jaffar Amin, akijaribisha miwani ya kuvaa wakati wa kupanda Mlima Kilimanjaro
2. Muhidini Issa Michuzi wa Blogu ya Jamii & 3. Fred Fredwaa wa Radio Free Africa
Muhidini Michuzi, na Fred Fredwaa Fidelis

4. Philipp Kissanga, raia wa Austria

Phillipp Kissanga, kulia
5. Matare Nyerere
Matare (wa tano kutoka kushoto) akiwa na timu yake ya mpira ambayo kiwanja cha nyumbani ni kwenye klabu ya Tazara, Dar es Salaam 
6. Amrani Batenga (Mfanyabiashara wa Mwanza)
7. Cutlat Mazengo (National Insurance Corporation)
8. Gerald Hando (Clouds FM)
9. Prof. Khoti Kamanga (Chuo Kikuu cha Dar es Salaam)
10. Mustafa Othim (kutoka Nakuru, Kenya)
11. Salum Mwaimu (wa Channel10)
12. Mary Kalikawe (Mkurugenzi wa Kiroyera Tours)
13. Stefan Joham (raia wa Austria)
14. Makongoro Nyerere (Mwenyekiti wa CCM, Mkoa wa Mara)
15. William Rutta (Meneja, Kiroyera Tours) 

William Rutta
Katika taarifa zijazo, nitatoa maelezo na picha ya safari yangu ya mwaka 2008 kupanda Mlima Kilimanjaro.

Makala inayohusiana na hii:
http://muhunda.blogspot.com/2010/09/kisa-cha-kuacha-kuvuta-sigara-ari-yangu.html