Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Friday, September 17, 2010

Kisa cha kuacha kuvuta sigara: safari yangu ya kupanda Mlima Kilimanjaro (makala ya kwanza kati ya kumi)

Sikumbuki ni lini nilianza kupata wazo la kupanda Mlima Kilimanjaro, lakini inaweza kuwa ni miaka minane iliyopita.* Bila sababu yoyote ya msingi, niliamua nataka kupanda Mlima Kilimanjaro.

Kufikia uamuzi huo ilikuwa ni jambo rahisi kuliko yote, lakini kuetekeleza azma hiyo ilikuwa jambo tofauti kabisa. Miaka kadhaa ikapita na nikatambua kuwa bila kuchukuwa hatua madhubuti, kamwe nisingepanda huu mlima.

Miaka ilivyopita, niliibua sababu zaidi za kunisukuma kupanda huu mlima. Niliendelea kukutana na watu kutoka pembe zote za dunia ambao walikuwa wameshapanda Mlima Kilimanjaro na nikajihisi kunyimwa kufaidi hazina kubwa ya Watanzania ambayo watu toka nje wameweza kuivumbua wakati Watanzania wachache mno wanapanda Mlima Kilmanjaro. Nilifikia hatua nikaamua sitaweza kuvumilia tena hali ya kukutana na mgeni toka nje ambaye ameshapanda Kilimanjaro na nishindwe kumwambia kuwa hata mimi nimeshaupanda huo mlima.

Katika muongo uliyopita mengi yamesemwa na kuandikwa kuhusu ongezeko la joto duniani na athari zake kwa mazingira. Baadhi ya wataalamu wanatabiri kuwa kwa sababu ya ongezeko la joto duniani theluji za Kilimanjaro zitayeyuka katika muda siyo mrefu ujayo. Nilipata msukumo kupanda kilele kirefu kabisa cha Afrika kuona hiyo theluji kabla athari za maendeleo ya binadamu hayajaifuta toka kwenye uso wa dunia.

Lazime itamkwe kuwa kuna mtazamo tofauti unaoashiria kuwa barafu za Mlima Kilimanjaro zinapunguwa siyo kutokana na ongezeko la joto duniani, ila kwa sababu ya mkusanyiko wa sababu nyingine. [Bonyeza hapa kusoma makala ya Kiingereza yenye mtazamo huo tofauti].

Mwezi Agosti 2005 nilikutana na Jenerali (Mstaafu) Mirisho Sarakikya, aliyewahi kuwa mkuu wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) na ambaye amebobea kwa kupanda Kilimanjaro. Ameshapanda Kilimajaro mara 46. Nilimuahidi kuwa ningeungana naye mwezi Septemba 2006 lakini sikuweza sikuweza kutimiza ahadi, na nikaendelea kusumbuliwa na maneno yake tulivyoona mwaka 2005: "Nitasikitika sana kama wewe ni kati ya wale Watanzania ambao hukutana nao mara moja na hatuonani tena."

Sababu moja inayoweza kuchangia Watanzania wachache kufika kwenye kilele ni gharama. Inagharimu wastani wa dola za Marekani 1,500 kulipia safari ya siku nane, gharama ambayo Watanzania wengi hawaimudu. Kuna idadi kubwa ya Watanzania wanaoweza kulipa gharama hizo, lakini swali ni iwapo wanayo azma ya kukabili kibarua cha kupanda ambacho, kwa binadamu yoyote wa kawaida, ni kibarua kigumu.

Nilishangazwa kugundua kuwa, mbali na waongozaji na wabeba mizigo, ilikuwa ni kama hamna kabisa Mtanzania kwenye Mlima Kilimanjaro. Yawezekana nilikutana na zaidi ya wageni 100 nilipopanda Mlima, lakini kati ya hao nilionana naMtanzania mmoja tu akielekea kileleni wakati nashuka. Kwa masikitiko, aliathiriwa na ugonjwa wa mwinuko unaoletwa na upungufu wa oksijeni na aliteremshwa kutoka mlimani kwa machela.

Makala ijayo: Maandalizi ya kupanda


* Hii makala ilichapishwa kwanza tarehe 18/10/2008, kwenye wavuti yangu ya lugha ya Kiingereza, From Butiama and Beyond

No comments: