Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Friday, September 24, 2010

Kisa cha kuacha kuvuta sigara: safari yangu ya kupanda Mlima Kilimanjaro (makala ya nne kati ya kumi)

Jumapili 17 Agosti 2008
Baada ya kuamua kuacha kupanda milima ya Upare niliendelea kujipa moyo kutokana na mawaidha ya Jose' akisema kuwa haina haja ya kuwa mkakamavu wa kiwango cha juu kabisa kuweza kukabili safari ya siku 7 hadi 8 ya kupanda Mlima Kilimanjaro kwa njia aliyoipendekeza, yaani Lemosho - Southern Circuit, Barafu, hadi kilele cha Uhuru. Njia hii ndefu inauandaa mwili kuzowea polepole hali ya kuwepo kwenye nyanda za juu na ndiyo njia yenye uhakika mkubwa zaidi ya kumwezesha mkweaji kufika kileleni.

Rafiki yangu Jose' ameshapanda Mlima Kilimanjaro mara 12 na angeungana nami mwaka huu kupanda tena mlima kwa mara ya kumi na tatu. Lakini kwa bahati mbaya aliumia kifundo cha mguu na hataweza kuja. Ameshawahi pia kukwea maeneo ya milima ya Himalaya hadi kufikia Mt. Everest Base Camp.

Aliniarifu kuwa Bw. Le Hu Dyuong, mhandisi mtaalam wa programu za kompyuta na raia wa Vietnam ataungana na mimi kupanda Kiliamnjaro. Le pia ameshawahi kufika Everest Base Camp na kabla ya kupanda Mlima Kilimanjaro alitoka kupanda Mlima Kenya. Le aliniomba niahirishe kuanza safari ya kupanda Kilimanjaro ili kutoa fursa kwake apumzike kwa siku chache baada ya kupanda Mlima Kenya. [Siku chache baada ya kupanda Kilimanjaro, alienda kupanda Mlima Meru]. Halafu akapumzika kwa majuma mawili na akaanza kufanya mipango ya kupanda Mlima Oldoinyo Lengai, lakini mipango haikukaa vizuri na hivyo hakuweza kupanda hiyo volkano.

Jumatatu 18 Agosti 2008
Asubuhi nilikutana na Le kwenye kituo cha basi cha mjini Moshi, akitokea Arusha. Tulifikia hoteli ya Springlands na wakati wa mlo wa mchana tulikaa meza moja na wanandoa raia wa Afrika ya Kusini waliohamia Manchester, Uingereza. Walituambia kuwa kupanda Kilimanjaro siyo mchezo, lakini ni jambo la manufaa. Walitushauri tujaribu kupitia Lava Tower tunapoelekea kileleni.

Jioni tulijumuika kwa ajili ya mkutano wa maandalizi na tukatambulishwa kwa jamaa mmoja mrefu mwembamba mwenye rasta ambaye ndiye kiongozi wetu wa msafara, anaitwa Pius. Alituarifu kuwa anajulikana pia kama "Yahoo" kwa wenzake.

Tulibishana naye kidogo alipotaka kushauri tupunguze siku za safari zilipendekezwa na Jose' na badala yake ziwe chache zaidi. Tulisisitiza kutumia muda ule ule tuliyopanga na hasa kulala kambi ya Barafu (kambi ya mwisho kabla ya safari ya kuelekea kileleni) ili kuiwezesha miili yetu kuzowea hali ya kuwa kwenye nyanda za juu na kuepuka athari ya upungufu wa oksijeni.

Nilimwambia Yahoo kuwa anaweza kuwa ana haraka ya kurudi Moshi ili aondoke na wageni wengine kueleka kileleni na kuweza kujiongezea kipato lakini, kwa bahati mbaya, alikuwa amepewa kazi ya kuongoza wakweaji wawili, mmoja asiye na uzoefu wa kutosha na mwingine ambaye alikuwa na uzoefu wa kutosha kuhusu ugonjwa wa nyanda za juu unaosababishwa na upungufu wa oksijeni na ambaye hakuwa tayari kuacha kuchukuwa tahadhari. Yahoo alikubali kwa shingo upande.

Baada ya kununua ramani ya Mlima Kilimanjaro kutoka dukani muuza duka alijaribu kuniuzia dawa ya mbu, lakini Le akamstukia na kupinga kuwepo kwa mbu kwenye Mlima Kilimanjaro. Watanzania tunatambua umahiri wa wakazi wa mkoa wa Kilimanjaro katika masuala ya kutafuta pesa. Kwa hakika, kama bado sikuwa natambua hilo, basi nilitambua leo kuwa ndugu zetu Wachaga walikuwa watu wenye ujuzi wa uuzaji usiyo wa kawaida.

Makala ijayo: Napiga hatua ya kwanza kuelekea kileleni

Bonyeza hapa kuisoma makala hii kwa Kiingereza

Makala zinazohusiana na hii:

No comments: