Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Tuesday, September 21, 2010

Kisa cha kuacha kuvuta sigara: safari yangu ya kupanda Mlima Kilimanjaro (makala ya tatu kati ya kumi)

Ijumaa 15 Agosti 2008
Niliondoka Butiama alfajiri, nikikusudia kuendesha gari hadi Mwanza kabla askari wa usalama barabarani hawajafika barabarani kukagua bima ya gari ambayo muda wake ulikuwa umeisha siku chache zilizopita. Tatizo langu ni kuwa niligundua wakati muda umeshapita kuhusu gharama kubwa za kupanda Mlima Kilimanjaro, na sikuwa na uhakika iwapo ningeweza kumudu kwa pamoja gharama za kupanda mlima na kulipia bima ya gari.

Nilipofika Mwanza nilipita ofisi ya Air Tanzania kuchukuwa tiketi yangu ya bei nafuu niliyopewa na Air Tanzania Corporation Limited (ATCL) ikiwa ni mchango wao kwa The Mwalimu Nyerere Charity Climb 2008 kwa kunisafirisha toka Mwanza hadi Kilimanjaro, na kurudi Mwanza. Nahisi kama mzaha kuwa masikioni tukio lenyewe linasikika kama tukio moja kubwa sana la kuchangisha pesa, lakini ukweli ni kuwa ni mimi peke yangu tu, mtu mmoja ambaye nimejiingiza kwenye utata wa kukwea Mlima Kilimanjaro. Mimi ndiyo nilkuwa kampeni nzima. Nilipanda ndege kuelekea Uwanja wa Kimataifa wa Kilimanjaro jioni.

Jumamosi 16 Agosti 2008
Niliamka mapema kutuma makala yangu kwenye gazeti la Sunday News nikiwa nimechelwa tena, kama kawaida. Ninalo tatizo kubwa la kupata mada mpya ya kuandika kila juma kwa ajili ya makala yangu. Natumia sehemu kubwa ya juma kufikiria jambo ambalo naweza kuandika kwenye makala yangu na inapofikia wakati wa kukaa chini na kuandika makala yenyewe, nakuwa nimeshavuka muda uliyowekwa wa kuwasilisha makala. Faida mojawapo ya kupanda Mlima itakuwa nitafanikiwa kukamua mada zaidi ya moja kwa ajili ya kuandikia kwenye makala yangu.

Niliongea na Zainab Ansell, mmiliki wa Zara Tanzania Adventures na kaniambia kuwa kamuni yake imeamua kunilipia gharama zote za siku nane za kupanda Mlima Kilimanjaro zinazofikia dola za Marekani 1,500. Nilifurahi sana.

Jioni, rafiki yangu toka Mwanga alinitumia gari kunichukuwa Moshi na nikalala kwenye chumba ambacho kilikuwa na takriban mbu mia moja. Nilitumia zaidi ya saa nzima kuwapunguza wale mbu kwa kutumia mbinu inayojulikana kama kombora la nguo. Mbinu hiyo inahusisha kusubiri mbu atue kwenye ukuta halafu kufurumisha dhidi ya ukuta nguo na kumbamiza ukutani na kumuua. Kwa kadiri ninayofahamu, ndiyo njia iliyo rafiki zaidi kwa mazingira ya kumaliza mbu.

Taarifa ijayo: Nakutana na Le, mtu aliyebobea kupanda milima, na Yahoo, muongozaji wetu wa mlimani.
Makala zinazohusiana na hii:

No comments: