Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Sunday, September 19, 2010

Kisa cha kuacha kuvuta sigara: safari yangu ya kupanda Mlima Kilimanjaro (makala ya pili kati ya kumi)

Mwaka 2007 ilivyoonekana kuwa nilikuwa nimepoteza fursa nyingine ya kupanda Mlima Kilimanjaro niliamua kuweka nguvu ya ziada, ama sivyo ningeendelea kuota tu kufika kilele cha Uhuru. Nilipaswa kujiweka katika hatua ya kutorudi nyuma. Niliamua kuwaambia watu wachache kuwa nitapanda Mlima Kilimanjaro mwaka huu kuchangisha pesa kwa ajili ya elimu. Wa kwanza kumueleza hayo alikuwa mwalimu mkuu wa Sekondari ya Wasichana ya Chief Edward Wanzagi iliyo jirani na Butiama na akaniambia, "Kwa nini usichange pesa kwa ajili yetu? Tunahitaji mabweni ya wanafunzi."

Aidha, niliandika barua pepe kwa Howard Chinner, mkazi wa Sevenoaks, England, ambaye nimekuwa nawasiliana nae baada ya yeye kusoma moja ya makala zangu. Alipendekeza naweza pia kuchangisha pesa kwa ajili ya Village Education Project Kilimanjaro (VEPK) iliyopo Mshiri, Marangu, kwenye miteremko ya Mlima Kiliamnajro.

Ilikuwa ni kutokana pia na pendekezo lake kuwa tukio ambalo lingekuwa halina hata jina, likihusisha kupanda mlima mrefu kuliko yote duniani inayosimama pekee (milima mirefu zaidi ya Kilimanjaro, kwa mfano Mlima Everest, ni mkusanyiko wa milima zaidi ya mmoja), lilipata jina la The Mwalimu Nyerere Charity Climb. Baada ya kuanza safari ya kuelekea kileleni, na kadiri nilivyoendelea kujenga matumaini yangu kuwa nitafika kileleni, niliamua kupachika "2008" kwenye jina hilo, nikiashiria kuwa litakuwa ni tukio la kila mwaka.

Kwa ahadi hizo mbili (moja kwa Skondari ya Chief Edward na nyingine kwa VEPK) haikuwezekana tena kutafuta sababu  ya kutopanda mlima. Baada ya hapo nilituma barua pepe kwa wote niliyofikiri wangekuwa na utashi wa kuchangia mojawapo wa walengwa wa mchango huo wa hisani. Nilipokea majibu ya kutumainia, na hiyo ikanizuwia zaidi kupanga mipango yoyote isiyojumuisha kipengele cha kupanda Mlima Kilimanjaro.

Kabla ya kupanda, nilitumia muda kidogo kuongeza uwezo wangu wa kuhimili kwata kwa kufanya mazoezi ya kutembelea baadhi ya vilima vya Butiama. Nilibadilisha mpango wangu wa awali wa kutembea kilomita tano nikizunguka msitu wa Muhunda, msitu wa nasaba wa Butiama, na kuanza kufanya safari ndefu zaidi za kwenda Mlima Mtuzu, nikiongeza kiasi cha kilomita tatu za ziada. Wakati nilipoanza kuzoea mazoezi yangu haya ya ziada, niliaanza kujenga imani kuwa mwili wangu ulianza kubadilika kuwa kifaa cha kutisha cha kupanda mlima.

Rafiki yangu mmoja anayeishi jirani na Mlima Kilimanjaro aliniambia kuwa imani yangu hiyo ilikuwa haina msingi, kwamba Butiama haina milima ila ina vichuguu tu, na kuwa ningetaka kupata picha halisi ya kupanda Mlima Kilimanjaro ningeipata kwa kumtembelea Mwanga na kukaa pale kwa muda nikikwea milima ya Upare.

Nilienda Mwanga na kukaa siku mbili, lakini sikupanda mlima wowote. Badala yake nilipumzika na kuomba kuwa nilikuwa imara kiasi cha kutosha kupanda Mlima Kilimanjaro.

Makala ijayo: Naondoka kijijini, na kuelekea mlimani.


Makala inayohusiana na makala hii:

No comments: