Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Sunday, October 27, 2013

Wageni toka Kagera wamtembelea Mama Maria Nyerere

Viongozi wa kikundi cha wajane na yatima kutoka mkoa wa Kagera walimtembelea Mama Maria Nyerere, kijijini Butiama hivi karibuni.
Grace Mahambuka, mwenyekiti wa kikundi cha Wajane na Yatima Kagera akitoa zawadi ya "akamwani" (kahawa ya kutafuna) kwa Mama Maria Nyerere (kushoto) Mwitongo, Butiama.
Msafara uliongozwa na mwenyekiti wao, Mama Grace Mahambuka, ambaye aliongozana na Mama Agnes Paulo Mukuta ambaye ni mdau wa maendeleo anayeunga mkono kikundi hicho. Mwingine katika msafara huo alikuwa Sittiwarth Mugasha ambaye ni yatima na msanii muimbaji wa kikundi cha Umoja wa Wanawake Wajane na Yatima Band.

Taarifa zinazohusiana na hii:
http://muhunda.blogspot.com/2011/07/wageni-wa-butiama-ujumbe-wa-veta.html
http://muhunda.blogspot.com/2011/07/wageni-wa-butiama-ujumbe-wa-veta.html
http://muhunda.blogspot.com/2010/10/kumbukumbu-ya-siku-ya-kufariki-mwalimu.html

Saturday, October 26, 2013

Madaraka Nyerere: Niliwahi kumsaidia baba pesa

Madaraka Nyerere: Niliwahi kumsaidia baba pesa

Mahojiano haya nilifanya na Stella Nyemenohi wa gazeti la Habari Leo. Yamechapishwa tena hivi karibuni wakati wa maadhimisho ya miaka 14 tangu kufariki Mwalimu Julius Kambarage Nyerere.

Bofya hapo juu kusoma mahojiano yote.

Friday, October 25, 2013

Msiofahamu vyema Kiingereza zungumzeni na andikeni kwa Kiswahili, mtafanya makosa machache zaidi

Hili nimeshalisema sana lakini naona kuna umuhimu kulirudia: tofauti na Watanzania wengi tunavyoamini, kufahamu vyema lugha ya Kiingereza siyo ishara kuwa anayeifahamu vyema lugha hiyo ni mtu aliyesoma kwa kiwango cha juu. Inasemekana kuwa John Major, waziri mkuu wa zamani wa Uingereza, alikuwa na elimu ndogo sana lakini hatuna shaka kuwa alifahamu Kiingereza vizuri sana.

Tunang’ang'ania lugha ya Kiingereza tunapoongea au kuandika kwa kuamini kuwa kwa kufanya hivyo tutaonekana ni wasomi sana. Kiingereza ni lugha kama lugha nyingine: Kichina, Kijapani, Kifaransa, na hata Kizanaki.
Ni kweli mtu anapoongea au kuandika lugha vyema inaashiria kuwa yeye ni msomi kwa maana ya kwamba yawezekana amekaa kwenye mfumo wa elimu kwa miaka mingi na bila shaka amejifunza misingi ya hiyo lugha anayoongea. Lakini ukweli unabaki kuwa hakuna uhusiano wowote wa moja kwa moja kati ya kuongea na kuandika lugha yoyote kwa ufahasaha na kiwango cha elimu cha mhusika.

Naona mara kadhaa mwenye mitandao ya jamii watu wakijaribu kujipambanua kuwa waandikaji wazuri wa lugha ya Kiingereza lakini kinachojitokeza ni kuwa hawana uwezo huo.

Unaweza kujiuliza: kwanini baadhi ya hawa wanaoamini kuwa kufahamu vyema matumizi ya lugha ya Kiingereza ni ishara ya usomi wasitumie lugha yao mama, Kiswahili, kwa sababu wengi wanaowaandikia wanafahamu lugha hiyo? Kama jamii nzima inaamini kuwa kufahamu Kiingereza ndiyo hali ya kujivunia basi ni vigumu kuona mabadiliko.

Jambo la msingi ingekuwa kwa wale wasiofahamu lugha vyema – siyo Kiingereza tu – wajifunze hizo lugha vyema ili pale wanapoongea au kuandika basi wafanye hivyo kwa ufasaha na kuweza kuwa walimu wa wengine. Ukweli ni kuwa kama hufahamu lugha ya Kiswahili vyema ni vigumu kujifunza lugha nyingine kwa ufasaha.

Lakini kuna suala moja la msingi linajitokeza: iwapo hufahamu kuwa hufahamu basi tatizo ni kubwa zaidi. Kuna mwanahabari mmoja mwandamizi aliwahi kuandika makala akisema kuwa ili mtu apate uwezo wa kufahamu kuwa hafahamu anahitaji kiwango fulani cha elimu. Kwa maana nyingine, inahitaji kuwa msomi kidogo kubaini kuwa huna uwezo na jambo fulani.

Inawezekana kuwa mfumo wetu wa elimu umekuwa duni kwa muda mrefu sana kiasi ambapo limejengeka tabaka kubwa la Watanzania ambao wako kwenye kundi hilo la kuwa watu wasiofahamu kuwa hawafahamu na basi hujikuta wakiandika na kusema vitu ambavyo siyo sahihi kwa Kiingereza wala Kiswahili.

Jambo lingine ambalo linatuangamiza kabisa ni kuwa Watanzania ni wagumu sana kusahihisha wenzao pale wanapokosea kwenye matamshi na maandishi. Mkosoaji anaonekana siyo mstaarabu au huonekana anataka kujipambanua kuwa yeye anafahamu zaidi ya wenzake. Matokeo yake ni kuwa matumizi yasiyo sahihi ya lugha yanaendelea kushamiri kwenye jamii.

Nimesikiliza mara nyingi tangazo linalosikika hivi karibuni kwenye vyombo vya habari ambapo binti anatamka namba za simu na anataja “zilo zilo” akimaanisha “ziro ziro” au “sifuri sifuri.” Hilo tangazo limepitiwa na wahusika na hawakuona kasoro yake. Matokeo yake mamilioni ya watoto wanalisikiliza na kuamini kuwa kutamka “zilo” ni sahihi. Najiuliza: hawa wahusika ndiyo wale wale waliopoteza uwezo wa kutofahamu kuwa hawafahamu, au ndiyo ule ustaarabu wetu wa kutosahihisha makosa?


Maoni yangu ni kuwa tujifunze Kiswahili vyema kwanza kabla ya kujaribu kujifunza lugha nyingine. Ni kazi ndogo zaidi kumfundisha Kiswahili mtu ambaye Kiswahili ni lugha yake mama kuliko kumfundisha Kiingereza (au lugha nyingine) mtu ambaye Kiswahili ni lugha yake mama. Na hili ni kweli hata kwa yule ambaye Kiswahili ni lugha yake mama na anayetamka “zilo zilo.”

Taarifa zinazofanana na hii:

Monday, October 7, 2013

Msafara mwingine wa Mlima Kilimanjaro wamalizika, safari hii kuchangia pesa kwa shule ya Kichalikani

Ndiyo kwanza nimemaliza kukwea Mlima Kilimanjaro katika mwaka wa 6 wa The Mwalimu Nyerere/Mt. Kilimanjaro Charity Climb kuchangisha pesa kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa shule iliyopo kwenye kijiji cha Kichalikani, wilayani Mkinga, mkoa wa Tanga.

Pamoja nami katika msafara wa Mlima Kilimanjaro alikuwa E. Gassana. Tulifika kwenye kilele cha Mlima Kilimanjaro asubuhi ya tarehe 5 Oktoba, saa 2:30 asubuhi.
Kwenye kilele cha Mlima Kilimanjaro, mita 5,895 juu ya usawa wa bahari na sehemu iliyo juu kuliko zote katika bara la Afrika, kutoka kushoto: Pius Yahoo, muongozaji wetu; E. Gassana; mwandishi wa blogu hii; na Musa Juma, muongozaji msaidizi.
Wakazi wa kijiji cha Kichalikani walianza ujenzi wa shule mwaka 2009 kwa kutumia sehemu ya ushuru uliokusanywa kwenye soko la samaki. Baada ya kuona jitihada hizi, Saidi Masimango, aliyekuwa Mkurugenzi wa Idara ya Teknolojia na Habari ya Shirika la Hifadhi ya Jamii alichangia shilingi milioni moja. Masimango alifariki mwezi Julai 2013.

Aidha, Mkuu wa Wilaya ya Rufiji, Nurdin Babu, naye alichanga mabati 33, wakati Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Mwantumu Mahiza alitoa mabati 100.

Kiasi cha shilingi milioni 7 zinahitajika kumalizia kazi za ujenzi ambazo hazijakamilika pamoja na kununua madawati.
Tafadhali changa kwa njia zifuatazo:

Jina la Akaunti: Kijiji cha Kichalikani
Benki: National Microfinance Bank
Namba ya Akaunti: 4193300163
Tawi: Mkwakwani, Tanga.

Wanaochangia wanaombwa kutuma majina kamili na viwango vilivyotolewa (kwa madhumuni ya kuchapisha orodha kamili kwenye gazeti la Jamhuri) kwa:


Hata wasiopenda majina yao yachapishwe nao wanaombwa kuwasilisha hizo taarifa kwa njia hiyo ya barua pepe (majina hayatachapishwa).

Kuchangia kwa njia ya simu tumia namba ifuatayo (pesa zitakusanywa na kuwekwa kwenye akaunti ya benki iliyotajwa juu):
+255 755 570 795

Saturday, September 14, 2013

Asikwambie mtu, Mtanzania mwenye simu siyo maskini

Baadhi ya matumizi ya simu yanaashiria kuwa Watanzania wanao uwezo mkubwa.

Nimekuwa msikilizaji wa mazungumzo ya simu ninapokuwa mitaani au safarini na katika utafiti usiyo rasmi ambao nimefanya, watu wengi wanaotumia simu hawazitumii kama nyenzo za kuongeza ufanisi katika shughuli zao, bali huzitumia kama chombo cha kupiga porojo zisizo na manufaa kwao au kwa wanaoongea nao.

Sina mamlaka kuhoji ambavyo mtu aliye huru anaamuaje kutumia salio lako kwenye simu, lakini kukosa mamlaka hayo hakufuti ukweli kuwa Watanzania wengi tunapoteza pesa zetu za mawasiliano kupiga porojo na kutuma ujumbe wa maandishi ambao hauleti maendeleo yoyote kwetu na kwa Taifa. Wanaochekelea ni wamiliki wa kampuni za simu ambao bila shaka wanatunisha mifuko yao kwa kila sekunde inayopita.

Chukua mfano huu: nimeketi ndani ya ndege iliyowasili kwenye uwanja wa ndege halafu abiria kadhaa wanawasha simu zao na kuwapigia simu watu ambao wamefika kuwapokea uwanjani wakiwaambia kuwa kuwa ndege imeshatua. Hii nimeshuhudia mara nyingi. "Vipi, umeshafika? Na sisi ndiyo tumetua."

Kwangu ingekuwa inaleta maana zaidi iwapo baada ya kutoka uwanjani na asimuone aliyempokea ndiyo apige simu kumuuliza kilichomsibu mwenyeji wake mpaka asifike uwanjani.

Siku za hivi karibuni nimeshuhudia mtu anayeongea kwenye simu karibu siku nzima. Akimaliza simu moja anapiga na kuongea na nyingine. Sijui anaongea nini kwa sababu anaongea Kizanaki (lugha ambayo siifahamu vizuri) lakini pamoja na kutofahamu lugha hiyo bado sipati picha ya suala ambalo litanifanya niongee kwa siku nzima. Hoja yangu hapa ni kuwa siyo rahisi kuongea mfululizo kwa karibu siku nzima na ukawa unapanga masuala ya kuleta maendeleo kwako au kwa jamii inayokuzunguka. Asilimia kubwa ya mazungumzo itakuwa porojo ambayo matokeo yake itakufanya kupungukiwa tu pesa ambazo ungeweza kuzitumia kwa jambo la maana zaaidi na lenye manufaa. Dakika chache kwenye simu kila siku zinafikia pesa nyingi baada ya muda mrefu.

Naweza kuwa nitatofautiana na wengi lakini ule woga wa serikali hivi karibuni kutoza shiling elfu moja kwa mwezi kwa kila mtumiaji wa simu ulikuwa woga wa kisiasa kwa sababu baadhi ya makundi ya jamii yalilivalia njuga suala hilo na kodi hiyo ya mawasiliano ilionekana kuwa ingeipunguzia serikali ushawishi kwa Watanzania. Inawezekana kuwa serikali inayo matatizo mengi 

Ukweli ni kuwa watumiaji wengi wa simu wanatumia pesa nyingi kwa mwezi kuongea na kuandika ujumbe wa maandishi usiyo na manufaa yoyote lakini ambao unawagharimu kiasi kikubwa kuliko hiyo shilingi elfu moja.