Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Tuesday, September 4, 2012

Katiba mpya itamke lugha rasmi ya bunge kuwa Kiswahili

Kama kuna kundi liliojijengea utaalamu wa kuvuruga lugha ya Kiswahili, kundi hilo ni la viongozi wa kada mbalimbali hapa Tanzania. Na vinara zaidi wa kuivuruga lugha ya Taifa ni wabunge wetu.

Ukisikiliza mjadala wa Bunge la Muungano ni vigumu kupita dakika kumi bila anayeongea kutumia neno la Kiingereza ndani ya mjadala unaoendeshwa kwa lugha ya Kiswahili. Baadhi ya watu wameipachika jina tabia hii ya kuchanganya lugha za Kiingereza na Kiswahili kuwa ni kuongea kiswanglish, neno lisilo rasmi kwenye lugha zote mbili.

Kuna dhana potofu miongoni mwa viongozi wetu wa sasa kuwa unapochanganya mazungumzo kwa kutumia maneno ya Kiingereza kwenye mazungumzo yako, basi wewe unaonekana kuwa ni mtu msomi. Na utakuta viongozi hawa hawa hata kwenye maandishi yao wanaweza kutumia neno la Kiswahili halafu kwenye mabano wanatoa fasili ya neno hilo hilo kwa lugha ya Kiingereza, kama vile kuwakumbusha wale wanaosoma maelezo yao kuwa wasisahau kuwa wao ni wasomi.

Jambo moja dhahiri ni kuwa ni Watanzania wachache sana wanaoelewa hayo maneno ambayo viongozi wetu, katika jitihada za kukogana wao kwa wao, wanayoyatumia kwenye maandishi na matamshi ikiwa ni pamoja na kwenye mijadala, mikutano, na kwenye vyombo vya habari.

Naamini umewadia wakati kwa lugha ya Kiswahili kutamkwa kuwa ndiyo lugha rasmi ya kutumika ndani ya Bunge la Muungano. Haileti mantiki kwa mwananchi aliyepiga kura kumchagua mbunge asielewe anachojadili mbunge wake.

No comments: