Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Wednesday, March 21, 2012

Lugha yetu Kiswahili

Hii ni sehemu ya hotuba niliyotoa kwenye mahafali ya kidato cha sita katika Shule ya Sekondari ya Wasichana ya Loreto, Mwanza, tarehe 18 Februrai 2012.
***********************************
Napenda kugusia pia matumizi sahihi ya lugha kwa sababu kama tukirejea kwenye ile nukuu ya Mwalimu Nyerere kuwa shabaha ya elimu ni:

 “...kurithisha kutoka kizazi kimoja hadi kizazi kingine maarifa na mila za taifa, na kuwaandaa vijana wawe tayari kuchukua nafasi zao katika kulitumikia na kuliendeleza taifa.”

basi utakuta kuwa lugha ni kipengele muhimu sana cha mila za Taifa. Lakini kinachotokea kwenye lugha siku hizi kinatisha. Mifano ni mingi lakini nitataja mfano toka kwenye sanaa.

Kuna msanii mmoja wa siku hizi anaimba wimbo mmoja na kutumia neno “hakunaga”. Sasa sitaki kuanzisha ubishi kati yangu na nyinyi kuhusu kama huyu ni msanii mzuri au siyo kwa sababu tunaweza tusifikie muafaka. Lakini kuna mtu nimesikia akisema kuwa katika masuala ya sanaa siyo muhimu kuzungumza lugha sahihi kwa sababu ukilazimisha hivyo unaua kipaji cha ubunifu, au utunzi.

Inawezekana haya ninayosema yanapingana na mliyofundishwa na walimu zenu, lakini kwa maoni yangu ni afadhali tuache kusikia nyimbo kama “hakunaga” lakini tuzungumze lugha ambayo ni sahihi. Huyu msanii anasikilizwa na watoto ambao baada ya miaka ishirini wataamini kuwa “hakunaga” ni neno sahihi la lugha ya Kiswahili.

Hapa sizungumzii Kiswahili tu, ila lugha yoyote ile ambayo wewe umejifunza au ambayo utajifunza. Hakuna lugha ambayo ni muhimu kuliko lugha nyingine. Mimi naongea Kiswahili, Kiingereza, na Kitaliani, lakini nafahamu Kizanaki kidogo sana. Kwa wazee wa Kizanaki ambao hawaongei Kiswahili hizo lugha nyingine hazinisaidii kitu chochote. Kwanza ni aibu kuwa kuna wakati mwingine nalazimika kutumia mkalimani kuongea na mzee wa Kizanaki.

Kwa hiyo ushauri wangu ni kuwa jiufunzeni lugha kwa kadiri inavyowezekana lakini jifunzeni hizo lugha vizuri.

Labda ni vyema kuanza kuzungumza Kiswahili vizuri kwanza, halafu kuendelea na lugha nyingine. Nyie ndiyo wazazi wa kesho, ndiyo viongozi wa kesho. Na mnao wajibu wa kulinda na kuhifadhi Kiswahili kama urithi wetu.

Siku hizi, kwa bahati mbaya, wale wanoongea Kiswahili kwa kuchanganya na maneno ya Kiingereza ndiyo wanaonekana wafahamu zaidi kuliko wale wanaoongea Kiswahili peke yake. Wengine wanachanganya lugha kwa kufikiria wataonekana bora zaidi ya wengine, lakini kuna wengine wanafanya hivyo kwa sababu baadhi ya maneno wamejifunza kwa Kiingereza halafu ndiyo wanatafuta maana yake katika Kiswahili.

Ninawaomba nyinyi mjifunze lugha vizuri kwa sababu nyinyi ndiyo mtakuwa mnaotazamwa na watoto wenu kama walimu wao. Msipojifunza vizuri lugha yenu mtachangia kupoteza kabisa lugha yetu au kuibadilisha.

Naomba niwape mfano mmoja. Zamani wakati Watanzania tukisafiri kwenda Kenya tulikuwa tunaagiza “nyama ya kuchoma” ; Wakenya walivyokuja Tanzania waliagiza “nyama choma”. Sasa naogopa kuanza mjadala na Sr. Judy kuhusu usemi upi ni sahihi lakini ukweli ni kuwa naamini sasa hivi ni Watanzania wachache sana wanaotumia msemo “nyama ya kuchoma”. Karibu kila mtu anasema ”nyama choma”, na hii naamini imechochewa na matumizi na hasa matangazo kwenye vyombo vya habari.

Maana yake ni kuwa jambo linalorudiwa mara kwa mara linaweza kubadilisha matumizi kwenye lugha.

Na huu ndiyo aina ya mfano wa mabadiliko ya matumizi ambayo tunaweza kuona baada ya miaka kadhaa kwa watoto wanaoendelea  kusikiliza “hakunaga”.

No comments: