Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Saturday, March 31, 2012

Gumzo za Nyamisisi

Muda si mrefu uliopita nilikuwa Nyamisisi kwenye barabara kuu inayounganisha Manispaa ya Musoma na jiji la Mwanza.

Wakati nikisubiri basi la kuelekea Mwanza nilisikia mazungumzo ya baadhi ya wakazi wa eneo lile.

Kwanza mmoja wao alianza kuwaarifu wenzake kuhusu mtu ambaye wanamfahamu ambaye alikuwa amehamia Urusi na ambaye kwa mujibu wa mtoa taarifa huyo mtu alikuwa anapata kipato kikubwa huko Urusi.

Nilitafakari sababu ya kumhamisha mtu kutoka Nyamisisi hadi Urusi na sikuipata. Hata hivyo nilivyoendelea kusikiliza yale mazungumzo nikagundua sikuwa nimeelewa vizuri. Aliyekuwa akizungumziwa alikuwa Malouda, mcheza kandanda maarufu ambaye anacheza soka ya kulipwa nchini Urusi.

Mazungumzo yalihamia kuhusu malipo makubwa ya wacheza mpira na wanamuziki. Mchangiaji mmoja alisisitiza kuwa wanamuziki wanalipwa pesa nyingi zaidi kuliko wacheza mpira na katika kusisitiza hoja yake alisimulia yaliyomkuta David Beckham.

Alieleza Beckham, akiwa Marekani, aliingia kwenye duka la nguo kwa madhumuni ya kununua nguo na akamwambia mwenye duka afunge duka kwa sababu sehemu ile haikuwa salama, na yeye alikusudia kununua nguo zenye thamani iliyo sawa na shilingi milioni 50.

Mwenye duka akamuuliza Beckham: "Wewe ni nani mpaka nifunge duka?"
Beckham: "Mimi ni David Beckham."
Mwenye duka: "Unafanya shughuli gani?"
David Beckham: "Ni mchezaji wa mpira."

Kwa mujibu wa mtoa taarifa wa Nyamisisi, yule mmiliki wa duka alimwambia Beckham: "toka hapa!" na akamfukuza dukani kwake.

Mtoa maelezo aliendelea kuwahadithia wenzake kuwa wasanii maarufu ulimwenguni ni matajiri zaidi kuliko wachaeza mpira wa miguu ingawa kuna baadhi ya waliyomsikiliza walipinga hiyo hoja.

Baada ya muda basi la Mwanza likafika na kuninyima fursa ya kuendelea kusikiliza gumzo za Nyamisisi.
posted from Bloggeroid

2 comments:

Anonymous said...

Mkuu story imetulia sana hiyo,




Madaraka said...

Karibu sana.