Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Wednesday, September 24, 2014

Mila na tamaduni: Watanzania ni wakarimu (sehemu ya tatu)

Hivi karibuni nimemaliza mzunguko wa kazi na mazoezi nikitumia baiskeli wa takriban kilomita 174 ndani ya mikoa ya Mwanza na Mara. Imenipa fursa ya kuthibitisha kuwa utamaduni wa ukarimu miongoni mwa Watanzania bado uko imara.

Jiunge nami kwenye sehemu ya tatu ya msafara huu...

Agosti 3
Mapema asubuhi nilianza safari yangu ya baiskeli ya kurudi Butiama kwa kuelekea kwenye kivuko cha Rugezi na ni leo ndiyo iliyodhihirisha kwangu kuwa Watanzania bado watu wakarimu. Nilipovuka upande wa pili kwenye mji mdogo wa Kisorya, nilisimama kwa muda kwenye mgahawa kuongeza mlo wa asubuhi wa chapati mbili na chai, ingawa ilikuwa inakaribia saa tano asubuhi.

Nikiwa na uhakika kidogo wa kuendelea na safari yangu mpaka njaa itakaponilazimisha kusimama na kula chakula cha mchana, nilianza safari ya kuelekea Kibara. Hata hivyo haikuchukuwa muda nikalazimika kusimama kutafuta chakula kwenye kijiji kilicho njiani.

Pembeni yangu niliona jengo linafanana na mgahawa. Alitokeza binti mmoja na mazungumzo yakawa hivi:

"Una chakula?"
"Ndiyo"
"Chakula gani?"
"Chai na chapati"
"Mimi nimeulizia chakula, siyo chai."
"Samahani, nina chai na chapati tu."

Niliendelea kudadisi:

"Kwani wewe mchana huli chakula?"
"Nitakula.
"Unapika nini?"
"Ugali na dagaa."
"Basi ongeza na cha kwangu halafu nitakulipa."

Akakubali. Chakula kilipokuwa tayari akanikaribisha kwenye mgahawa wake, akanipa maji ninawe na yeye akanawa tukakaa pamoja kula.
Niliegesha usafiri wangu, nikapiga picha, halafu nikaingia kusubiri chakula.
Wakati nakaribia kushiba nikapata nguvu za kuongea kidogo na kumwomba radhi kuwa nimempunguzia chakula chake kwa siku hiyo. Aliniambia nisijali, na kuwa labda kuna siku na yeye atanitembelea na mimi nitamkaribisha chakula.

Nikijiandaa kuondoka nilimuuliza nimlipe kiasi gani kwa kile chakula. Alinishangaa na kuniambia: "Wewe si nilikwambia kuwa hakuna tatizo? Pesa za nini?"

Nikabaki hoi. Lakini nilifungua mfuko wa baiskeli yangu na kutoa pakiti ya biskuti nikampa na kusema ni zawadi kwa watoto wake. Alifurahi sana na kuniuliza bei ya biskuti zile. Nilimwambia shilingi elfu tatu nikapanda basikeli na kuanza safari ya kuelekea Kibara.

Vijijini wema huu bado upo. Sina hakika kama mijini hali imebakia hivi.

Taarifa ijayo: Hiki ni nini?

Sehemu ya pili ya makala hii

No comments: