Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Sunday, October 31, 2010

Amani Millanga bado anahoji Sera ya Majimbo ya CHADEMA (sehemu ya kwanza)

Katika taarifa ya Septemba 5 nilitoa maelezo ya Amani Millanga akifafanua hoja zake kupinga Sera ya Majimbo ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA). Nilifanikiwa kupata maelezo katika mfumo wa makala zilizoandikwa na John Mnyika, Kaimu Katibu Mkuu wa CHAEMA na mgombea ubunge wa chama hicho kwa jimbo la Ubungo, akiweka msimamo wa CHADEMA kuhusu sera hiyo ya majimbo.


Baada ya kusoma maelezo ya CHADEMA, Amani Millanga anaendelea kufafanua hoja zake dhidi ya Sera ya Majimbo ya CHADEMA.


Pamoja na kwamba sikufanikiwa kutoa taarifa hizi kabla ya uchaguzi, bado nafikiri kuna umuhimu wa wasomaji kusikia hoja za Amani Millanga.

Sera za Majimbo: Utaifa na Hatima ya Amani Yetu
Na Amani Millanga
Amani Millanga (kulia), akiongea na Afisa Kilimo wa Kijiji cha Butiama, David Sanagara.
Kote duniani tumeshuhudia vita na mauwaji ya kikatili yanavyoendelea kizitafuna nchi changa zenye serikali za majimbo na hata zile zisizokuwa na majimbo. Zipo sababu nyingi za ndani na nje za hali ilivyo katika nchi hizi kukosa amani na umoja lakini miongoni mwa sababu kubwa kabisa ni ukabila na udini ambao unachochewa na umkoa na umajimbo. Mtanzania yoyote mwenye kuchukua kila tahadahari ya kuilinda amani yetu hawezi kukubaliana na sera ya majimbo. Hili si suala la "watu kuwa na hofu, na woga au kubisha," bali ni suala la hatima ya utaifa na umoja wetu. Wahenga wetu walisema, mwenzio akinyolewa wewe tia maji. Kwa nini tujitege bomu ili hali tunajua kuwa likilipuka litatumaliza.


Kuiga, Historia na Maslahi ya Taifa
Yapo mambo mengi ya kujifunza kutoka sehemu mbalimbali duniani lakini si yote yanayotufaa. Miongoni mwa yasiyotufaa ni hili la serikali za majimbo. Sababu za kutokutufaa ziko wazi kabisa: ni kuvunjika kwa umoja wa kitaifa na hatimaye amani yetu. Umoja, amani na utaifa ndiyo maslahi yetu ya kwanza kabla ya jambo lolote.


Sera yoyote inayolenga kuyaua mambo haya haitufai. Kupoteza amani na umoja ni jambo la siku moja tu. Lakini kuirejesha amani na umoja katika nchi yoyote ni gharama kubwa ni inachukua muda mrefu sana. Mifano iko wazi. Marekani kwa mfano ilikuwa na vita ya wenyewe kwa wenyewe miaka ya 1860 ambapo majimbo ya kaskazini yalizuia majimbo ya kusini mwa nchi hiyo yasijitenge. Athari za vita hiyo ilikuwa ni kubwa mno. Nigeria hali kadhalika ukianzia na Biafra, majimbo ya kasakzini na delta ya mto Niger. Je tuna uhakika gani kwamba Tanzania haiwezi kuingia katika mgogoro wa baadhi ya majimbo kutaka kujitenga? Mmejiandaa vipi kuidhibiti hali hii kwa Tanzania? Je mnataka tuwe kama Nigeria? Hakuna umoja wala amani pale. Tukumbuke kuwa kuwepo kwa serikali za majimbo huko Marekani ya kaskazini, baadhi ya nchi za Ulaya, Afrika Kusini na Australia si kigezo cha sisi Tanzania kuwa na serikali za majimbo kwani wao wana historia yao inayowapa mwanya wa kuwa na majimbo. Tanzania ina historia yake. Historia yetu haituruhusu kuwa na majimbo kwani yataua utaifa wetu. Yataua nchi yetu.


Majimbo ni Ufa
Katika kitabu cha Nyufa, Mwalimu Nyerere anatukumbusha Tanzania bado ni taifa changa sana na kwamba kuna mambo ambayo tunapaswa kuendelea kuyasimamia na kuyalinda kama mboni za macho yetu. Mwalimu anatahadharisha kwa kusema: "Lakini mambo haya ya msingi yanataka yasimamiwe katika nchi changa. Lazima yasimamiwe.


Ukiacha, watu wanarudi kule kule kwenye mawazo ya kijinga jinga. Ukabila, kama ukabila, sisi bado wakabila sana. Kwa hiyo la ukabila lazima liendelee kupigwa vita mpaka life. Halijafa. Ukiwaminya hawa kidogo utakuta ukabila uko pale pale tu!" Mwalimu anaongeza kuwa: "Ukabila bado upo. Kwa hiyo, ukabila lazima uendelee kupigwa vita. Hapana kukaa na kusema 'Tanzania hatuna ukabila'. Hapana. Watu hatujawa Watanzania bado. Kwa hiyo lazima tuendelee kuupiga vita. Na watu wana udini udini" (uk 28).


Serikali za majimbo ni hatari kwani zitatugawa Watanzania kimakabila na hata kidini. Na kwa mgawanyo huu hauwezi kuleta maendeleo ya kweli kwa Tanzania yote kwa pamoja. Kutakuwa na upendeleo fulani kwa majimbo fulani kutoka serikali ya shirikisho na kutakuwa na upendeleo kutoka serikali ya jimbo kwenda wilayani kutegemea ni kabila gani au ni nani kashika uongozi wa taifa au jimbo. Haya mambo yapo hasa kwa nchi changa, tusijifanye hatuyajui.


Hivyo utaifa wetu unapaswa kulindwa kwa kuepuka kila sera au jambo lolote linaloweza kuuweka hatarini. Ukweli ni kwamba umoja na utaifa wetu utayumba iwapo tutakuwa na serikali za majimbo. Huo ni mwanzo wa kuparaganyika kwa Tanzania na hizo ajenda nyingine mlizonazo hazitafanya kazi yoyote kwani taifa halitakuwepo tena. Sera yenu hii itaweka ufa mkubwa na kubomoa taifa letu. Tutakuwa na serikali yenye nchi isiyokuwa na taifa. Nigeria iko hivyo, isomeni historia yake jinsi ambavyo majimbo yamongeza mgawanyiko.


Muungano Kuvunjika
Suala la majimbo ni hatari kwa Muungano wetu. Mnataka kuifanya Zanzibar iwe jimbo? Na kama Zanzibar wakikataa serikali za majimbo, jambo ambalo ni wazi kwamba watakataa kuwa jimbo, je mnatuhakikishia vipi kuwa mtaulinda Muungano wetu?


Sera ya majimbo ni silaha ya kuuvunja Muungano. Na mara tu Tanzania ikigawika huwezi kuondoa umaskini, ujinga na maradhi. Huwezi kuleta maisha bora bali utaleta ubaguzi na hatimaye machafuko na kumwaga damu.


Muungano wa Tanganyika na Zanzibar si Ufederali au shirikisho. Ndio maana tunayo Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, si Jamhuri ya Shirikisho la Tanzania. Pia Muungano wetu si tenge na mafanikio yake ni makubwa. Hatupaswi kuubeza na kuuita "Tenge". Ndiyo, zipo kero lakini kero hizo hazimaanishi kuwa Muungano ni 'tenge'. Kama ungekuwa tenge kwa maana halisi ya neno tenge basi ungeishavunjika. Leo hii Watanzania tunatembea kifua mbele kwa kujivunia Muungano wetu ambao una faida nyingi kwetu (hii ni mada nyingine).


Serikali za Mitaa
Haya mambo mnayoyataja kuwa yatafanywa na serikali za majimbo tayari yanafanywa na serikali za mitaa nchini. Falsafa ya nguvu ya umma ndiyo msingi mkubwa wa serikali za mitaa. Hoja iwe ni kuziboresha zaidi serikali za mitaa kwa kuzipa mamlaka zaidi ya sasa na si kuziondoa na kuleta serikali za majimbo.


Tuangalie zimeshindwa wapi, kwa nini na nini kifanyike ili ziwahudumie wananchi kwa ufanisi zaidi. Kimsingi kupitia serikali za mitaa ni rahisi zaidi kutoa maamuzi na kusimamia shughuli za maendeleo kuliko katika jimbo litakalokuwa ni kubwa mno na utajikuta unakwama. Mfano katika jimbo la kanda ya ziwa Kagera, Mara na Mwanza kuna watu wenye mahitaji mbali bali. Kwa mfumo wa jimbo si rahisi kuwafikia watu hawa na kutatua matatizo yao. Lakini kwa serikali za mitaa katika kila wilaya ni rahisi zaidi kwani utakuwa unaiongelea Muleba tu na si jimbo zima.


Kimantiki unaliona suala hili kwa uawzi kabisa. Kwanini mambo ya Muleba yaamuliwe katika bunge la jimbo litakalo kuwa pale Mwanza, kwa mfano, badala ya kuamuliwa na baraza la madiwani wa Muleba wanaoijua uzuri Muleba na mahitaji yake? Kwanini niifuate huduma Mwanza badala ya Muleba? Hapa mbona utakuwa unaturudisha kwenye urasimu ule ule ambao serikali ya CCM inauondoa kwa kuzipa serikali za mitaa mamlaka zaidi? Kama hoja ni kuvifuta vyeo vya mkuu wa mkoa, mkuu wa wilaya na katibu tarafa hili ni suala ambalo linaweza kujadiliwa kwa kuangalia faida na hasara zake kwetu. Lakini uwepo wa viongozi hawa usitumiwe kama hoja ya kutaka serikali za majimbo kwani hakuna uhusiano sisisi wa kimantiki kati ya wakuu hawa na kuwa na serikali za majimbo.


Mzigo Mkubwa
Serikali za majimbo zina utitiri wa viongozi zaidi ya mfumo tulionao sasa. Na huu ndio ukweli. Gharama za kuziendesha serikali za majimbo na shirikisho zitaongeza mzigo mkubwa zaidi kwa wananchi badala ya kuupunguza. Utakuwa na bunge katika kila jimbo na bunge la shirikisho, gavana wa jimbo na mawaziri wake na makatibu wa wizara au idara, wakurugenzi n.k. Msululu ni mrefu mno hadi kuja kufika kwa mkurugenzi mtendaji wa wilaya. Hiyo yote ni pesa ya umma inatafunwa. Hivi kwa nini tupoteze mabilioni yote hayo katika kaunzisha majimbo na kuudurusu upya utendaji wake ili kuuboresha zaidi? Kwanini tuwatwishe wananchi mzigo mkubwa zaidi?


Ikulu Lazima Iongoze Taifa-Nchi
Suala la Ikulu au serikali kuu kuingilia serikali za mitaa lina mapana yake katika kilijadili. Inategemea wanaingilia katika lipi na sheria inasemaje. Hapo ndipo tunapaswa kuziangalia kanuni, taratibu na sheria zetu za mitaa. Kama zina mapungufu tuyaondoe ili seikali za mitaa ziwe huru zaidi. Lakini ni ukweli usio na kificho kuwa Ikulu na serikali kuu ni lazima ziwe na mamlaka ya kiutawala na kiutendaji kwa serikali za mitaa. Kinyume chake Tanzania itakuwa haina serikali kwa maana halisi ya 'serikali ya taifa-nchi' na hivyo basi hakuna sababu ya kuwa na Ikulu. Taifa-nchi ni pamoja na serikali za mitaa.


Sasa tujiulize: Ikulu ni ya nini ikiwa haiwezi kuingilia na kusimamia uendeshaji wa taifa na nchi?


Katika mfumo wetu wa sasa, kwa mfano, kila halmashauri ina vyanzo vyake vya mapato na bajeti. Ni kweli kwamba serikali za mitaa zinapokea pesa kutoka serikali kuu lakini si pesa zote zinazoendesha halmashauri zinatoka Dar es Salaam. Huu ni uwongo na uzushi. Juu ya hayo si kweli kwamba kila jambo katika kila halmashauri linaongozwa na maelekezo ya Ikulu ya Dar es Salaam. Hivi Ikulu inaamua hata ushuru au kodi ya halmashauri itozwe vipi na mapato yatumikeje? Hii ni nguvu ya kuupotosha umma!


(sehemu ya mwisho ya makala ya Amani Millanga itatolewa kesho.

Wakala wa CCM kituo cha hospitali ya Butiama yuko ngangari

Nilivyotembelea kituo cha kupiga kura cha Hospitali ya Butiama leo asubuhi nilibaini mtu mmoja amekaa pembezoni, akiwa anaangalia kwa makini mienendo ya kila mmoja pale kituoni. Mwanzo nilifikiri labda ni afisa wa Usalama wa Taifa.
Wakala wa CCM kushoto, akinitupia jicho nilipopiga picha hii leo asubuhi kwenye kituo cha kupigia kura cha Hospitali ya Butiama.
Nilipata ujasiri wa kumuuliza yeye ni nani na akaniambia kuwa ni wakala wa Chama cha Mapinduzi (CCM). Sijashangaa kuwa hakuwepo wakala wa chama kingine kwa sababu mbili: Kwanza, mbunge wa CCM wa jimbo la Musoma Mjini, Nimrod Mkono, amepita bila kupingwa; na pili, nguvu ya upinzani, hata kwenye ngazi ya udiwani, siyo kubwa sana.

Kwenye chaguzi za serikali za mitaa, ni mgombea wa CCM ndiyo aliyeibuka mshindi na kuchaguliwa kuwa mwenyekiti wa kijiji.

Butiama wanapiga kura

Picha hii, chini, inaonyesha mpiga kura wa kijiji cha Butiama akipiga kura leo asubuhi kwenye kituo kilichopo Hospitali ya Butiama.

Nimeshuhudia mstari mrefu wa wapiga kura kwenye kituo hicho, muda mfupi baada ya kituo kufunguliwa, saa 1 asubuhi.

Watanzania nchini kote wanapiga kura leo katika uchaguzi mkuu utakaochagua rais, wabunge, na madiwani. Huu ni uchaguzi mkuu wa nne chini ya mfumo wa vyama vingi.

Monday, October 18, 2010

Lugha yetu Kiswahili

Nilitembelewa Butiama hivi karibuni na Andrea Wobmann, raia wa Uswisi, ambaye alikuwa Tanzania kwa miezi kadhaa akifanya kazi ya kujitolea katika kuendeleza shughuli za utalii jijini Mwanza.

Alisindikizwa na mwenyeji wake toka Mwanza (ambaye jina lake nitaliweka hapa baada ya muda kwa sababu silikumbuki kwa sasa) aliyevaa fulana iliyoandikwa "mzungu."

Awali nilihisi kuwa ile fulana angeivaa Andrea, lakini nilivyopekuwa kwenye kamusi nikagundua kuwa yawezekana sifahamu vizuri tu Kiswahili. Neno hilo, kama lilivyoandikwa kwenye fulana lina maana nyingine zifuatazo, zaidi ya ile maana ambayo wazungumzaji wengi wa Kiswahili tunaifahamu:

1. jambo lisilo la kawaida
2. mafunzo yanayotolewa kwa wanafunzi wa ngazi ya awali
3. ujanja; uerevu

Ingekuwa maandishi ya kwenye fulana yalikuwa "Mzungu", yaani na herufi kubwa ya mwanzo, basi ile maana niliyoidhania mimi ndiyo ingekuwa sahihi, kwa mujibu wa Kamusi ya Kiswahili-Kiingereza ya Taasisi ya Uchunguzi wa Kiswahili (TUKI) ya mwaka 2001.

Sunday, October 17, 2010

Kumbukumbu ya siku ya kufariki Mwalimu Julius Kambarage Nyerere

Alhamisi iliyopita tuliadhimisha kumbukumbu 11 ya kufariki Mwalimu Julius Kambarage Nyerere hapa kijijini Butiama. Maadhimisho yalianza na misa iliyoongozwa na Askofu Michael Msonganzila wa Jimbo Kuu la Kanisa Katoliki, Musoma.
Mama Maria Nyerere (kulia), akisalimiana na Mkurugenzi wa Mkoa wa Mwanza wa Chuo Kikuu Huria, Ben Kapaya (aliyembeba mwanaye, James), akiwa na mkewe (wa pili toka kulia). Siku hiyo ya maadhimisho James alitimiza umri wa mwaka mmoja.

Baada ya misa ilifanyika sala fupi kwenye kaburi la Mwalimu Nyerere katika eneo la Mwitongo, Butiama.
Makongoro Nyerere (kushoto), mwenyekiti wa mkoa wa Mara wa Chama cha Mapinduzi (CCM), akiwa na Askofu Michael Msonganzila wa Dayosisi ya Kanisa Katoliki ya Musoma (kushoto), pamoja na mgeni toka Uganda, Ssalongo Katumba (katikati).  
Na baada ya sala ya kwenye kaburi wageni walipata chakula cha mchana kwenye makazi ya Mwalimu Nyerere iliyopo Mwitongo.
Makongoro Nyerere (katikati), akiwa na Kisheri Kyanzi Mchere, kiongozi wa Umoja wa Vijana wa Chama cha Mapinduzi (UV-CCM), tawi la IFM
Baadhi ya wageni waliyofika kwenye maadhimisho hayo ni pamoja na Waziri Mkuu mstaafu, Jaji Joseph Sinde Warioba na Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Mara ambaye pia ni Mkuu wa Wilaya ya Musoma, Godfrey Ngatuni na mkewe. 
Mgombea ubunge wa jimbo la Musoma Mjini kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Vincent Nyerere (kulia), akisalimiana na Mkuu wa Wilaya ya Musoma, Godfrey Ngatuni wakati wa maadhimisho ya kumbukumbu ya kifo cha Mwalimu Nyerere yaliyofanyika Butiama, tarehe 14 Oktoba 2010.

Kisa cha kuacha kuvuta sigara: safari yangu ya kupanda Mlima Kilimanjaro (makala ya kumi kati ya kumi)

Kumradhi kwa kuchelewa kuleta makala hii ya mwisho katika mtiririko wa makala hizi za safari ya kupanda Mlima Kilimanjaro kutokana na kutingwa na shughuli mbalimbali.

Jumanne 26 Agosti 2008
Baada ya kupata kifungua kinywa tulipiga picha ya pamoja na kuanza safari ambayo kwangu ilikuwa ni ngumu kushuka kueleka lango la Mweka. Njiani kundi la wasichana lilitupita na mmoja akasema, "sirudii tena." Nilimuelewa vyema kwa nini alitamka maneno yale.

Kiasi cha mita 200 kabla ya kufika kwenye lango la Mweka tulikutana na madereva toka Zara Tanzania Adventures ambao walitufuata kwa mguu ili kufahamu iwapo tulikuwa tumechoka sana kiasi cha kushindwa kutembea hatua zile za mwisho. Tulikataa wazo lao la kupanda gari. Ingetia doa tukio ambalo halikuwa la kawaida.

Kuruhusu mwili kuanza kuzowea hali ya kuwa katika nyanda za chini ni suala la umuhimu ule ule kama la kuuzowesha mwili hali ya kuwa nyanda za juu wakati wa kupanda mlima. Yasemekana athari za kuwa katika nyanda za juu zinachukuwa muda kuisha. Kwenye duka la vitu vya ukumbusho lililopo lango la Mweka Le aliinua kofia iliyoandikwa "Hifadhi za Taifa" na akaniomba nifasiri. Sikuweza kukumbuka tafsiri ya Kiingereza na niligeukia maafisa wa Hifadhi ya Kilimanjaro kuomba wanisaidie.

Mmojawapo alisema, "National Parks", na mimi nikasema, "ni kweli! Nimewezaje kusahau hilo!" Mmoja akanijibu, "Usijali, ni kawaida. Akili zako bado zimeganda. Alinipa hoja ya nguvu ya kutolala tena kwenye Kambi ya Crater safari ijayo.

Sasa kuhusu kichwa cha habari cha hii makala: Niliacha kuvuta sigara mwaka wa kwanza nilipoamua kupanda Mlima Kilimanjaro kwa sababu nilikuwa na hofu uvutaji sigara ungenipunguzia nafasi ya kuweza kufika kwenye kilele.

Pesa zilizokusanywa mpaka sasa:

Paundi za Uingereza 440
Dola za Marekani 16,180
Shilingi za Tanzania 2,570,000

Bonyeza hapa kuisoma makala hii kwa Kiingereza

Makala zinazohusiana na hii:
http://muhunda.blogspot.com/2010/10/kisa-cha-kuacha-kuvuta-sigara-safari_05.html

Tuesday, October 5, 2010

Kisa cha kuacha kuvuta sigara: safari yangu ya kupanda Mlima Kilimanjaro (makala ya tisa kati ya kumi)

Jumatatu 25 Agosti 2008
Le na Yahoo walianza safari ya kuelekea Kilele cha Uhuru saa 10:00 alfajiri kuwahi mawio. Baada ya kupambazuka nilitembea juu ya eneo la tambarare la kasoko (shimo la katikati ya volkano) nikiwa pamoja na muongozaji msaidizi hadi Stella Point ambako nilituma ujumbe wa maandishi wa simu niliyokusudia kuutuma jana tokea kileleni: "Salamu toka Kilele cha Uhuru, kilele cha Mlima Kilimanjaro (mita 5,896)..."

Baadhi ya majibu niliyoyapata yalikuwa yanapendeza. Joseph Ibanda, rubani, aliandika: "..kwa hakika mandhari itakuwa ya kustaajabisha hapo ulipo..." Asingeweza kutumia msemo uliyo bora zaidi kuelezea hisia zangu na hapakuwa na sehemu bora zaidi kupata hizo hisia kuliko pale niliposimama wakati nasoma ujumbe wake. 
Hema langu mbele ya barafu katika Kambi ya Crater
Kushoto kwangu kulikuwa na eneo pana la wazi kati ya Kibo na Mawenzi, mbali lakini kukionekana vizuri kabisa. Chini zaidi kulikuwa na mandhari nzuri kwa kiasi cha mita 1,500 halafu utando mzito wa mawingu. Siwezi kuelezea msisimko wa kusimama juu ya ardhi na wakati huo huo kuwa uko juu ya mwaingu, zaidi ya mita 1,500 juu ya mawingu. Ni rubani tu anaweza kutamka alivyotamka Joseph.

Baada ya kuutangazia ulimwengu kuwa nimefanikiwa kufika kileleni, tulianza kuteremka kuelekea Kambi ya Barafu. Wabeba mizigo wanaotupita kwa kasi wanaleta mkanganyiko katika ugumu unaowakabili watu wanaopanda mlima kwa mara ya kwanza. Na hakuna sehemu ambapo ugumu huu unajitokeza kwa kiasi kikubwa kama kipande kati ya Kambi ya Barafu na Stella Point. Ni hapa ambapo wengi ambao wanashindwa kuendelea kutokana na athari za kuwepo katika hali ya uwanda wa juu pamoja na matumizi ya nguvu wanajitenga na wale wazoefu wa kupanda milima. Katika mazingira haya, mzee wa takribani miaka 70 alitupita kama vile anakimbia akiwa na muongozaji wake akijitahidi kwenda kwa kasi ya yule mzee. Michezo ya Olimpiki ya Beijing ikiwa iko mbioni nahisi kuwa huyu mzee anaweza kuwa anatumia madawa ya kuongeza nguvu. Anaweza kuwaadhiri hata wale wenye umri wa kuwa wajukuu zake.

Tunavyozidi kuteremka baada ya kupita Kambi ya Barafu tunakutana na wanaoelekea kileleni. Wanauliza, "Hali ilikuwaje? Jibu langu la mwanzo nasema "kasheshe". Le anatoa jibu ambalo la kutia moyo zaidi. Anasifia mandhari na kusema, "Nzuri sana, ya kustaajabisha." Halafu nakumbuka kuwa hata mimi nilipanda Kilimanjaro kwa madhumuni ya kuona mandhari: mandhari ya kuvutia ya Mawenzi jua lilipochomoza; taswira  za umbali mrefu na muonekano wa njia zenye mizungukuko zilizopo kwenye kipande kati ya Mawenzi na Kibo; na hali ya kujisikia kama niko kwenye Ncha ya Kaskazini nilipokuwa kwenye Kambi ya Crater. Lakini, baba lao, kusimama juu ya ardhi na kutazama mawingu yakiwa chini yako. Nilisimama pale nikivuta hewa ya ubaridi ya mlimani na nilichoweza kusema tu ni "kasheshe."

Leo tulitembea kutoka Kambi ya Crater (iliyopo mita 5,790 juu ya usawa wa bahari), kupita Kambi ya Barafu (iliyopo mita 4,600 juu ya usawa wa bahari), kupita Kambi ya Millenium ya Juu (iliyopo mita 3,797 juu ya usawa wa bahari), mpaka Kambi ya Mweka (iliyopo mita 3,100 juu ya usawa wa bahari) ambako tulilala kwa siku ya mwisho. Hii ilikuwa ni safari moja ngumu sana, na nilihisi misuli yangu ya miguu ikianza kufikia kikomo kutokana na kutembea mara kwa mara kwa siku sita.

Makala ijayo: akili zilizoganda na sababu ya kuacha kuvuta sigara


Makala zinazohusiana na hii:

Friday, October 1, 2010

Kisa cha kuacha kuvuta sigara: safari yangu ya kupanda Mlima Kilimanjaro (makala ya nane kati ya kumi)

Jumapili Agosti 2008
Ingawa nilikuwa najiamini kwa kiasi kikubwa leo (kwa sababu ya kunywa Red Bull moja jana usiku, na nyingine asubuhi), wenzangu walikuwa na hofu juu yangu. Njia mbadala ambayo tulijadili katika siku chache zilizopita ilikuwa ni kwamba, badala ya kufanya jaribio moja la kufika kileleni toka Kambi ya Barafu kuanzia saa sita usiku, tuliamua kuanza asubuhi. Aidha, kwa njia hiyo mbadala tuliyoijadili, iwapo tutafika Stella Point (baada ya mpando mmoja mkali sana wa leo), na nitajisikia bado naweza kumalizia kilomita moja kufika kilele cha Uhuru ambayo inahusisha mpando mwepesi kwenye sehemu ya juu ya Mlima Kilimanjaro, basi nitamalizia kipande cha kutoka Stella Point mpaka kielele cha Uhuru.

Lakini kama nguvu ya Red Bull itakuwa imeisha mwilini baada ya kufika Stella Point, iliyopo urefu wa mita 5,756 juu ya usawa wa bahari, basi tutaelekea Kambi ya Crater, iliyopo urefu wa mita 5,790 juu ya usawa wa bahari, na tutajaribu kufika kileleni kesho asubuhi. Tulikubaliana pia iwapo Le ataona kama mwendo wangu ni wa polepole sana, yeye na Saidi, msaidizi wa Yahoo, watatuacha na kutangulia. Kila mmoja alihisi begi langu lilikuwa na uzito wa ziada na nilishauriwa kupunguza nguo kutoka kwenye begi na kubaki na vitu muhimu tu.
Kabla tu ya mawio, Kilele cha Mawenzi kinavyoonekana.
Kulinganisha na siku zilizopita, leo kulikuwa na wakweaji wachache zaidi waliyotupita njiani. Na kwa hakika, hata wapagazi, ambao walikuwa wana kawaida ya kutupita kama tumesimama, leo walitembea polepole zaidi wakati tukielekea Stella Point. Wengine walishindwa hata kutupita na waliendelea kutembea nyuma yetu. Tuliona taswira ya kuvutia kabisa ya Mawenzi, kilele cha pili cha Mlima Kilimanjaro, na sehemu ya katikati ya Kibo na Mawenzi, inayoitwa saddle kwa Kiingereza.

Kadiri saa zilivyozidi kupita, wote waliyokuwa na hofu juu yangu walianza kukubali kuwa tulikuwa tunasonga mbele kwa kasi nzuri kabisa. Tulivyowasili Stella Point nilihisi kuwa nina nguvu za kutosha kuelekea kilele cha Uhuru. Nilishangaa kuona kuwa ile kilomita moja ya mwisho iligeuka kuwa sehemu moja ngumu kuliko zote. Yawezekana kabisa kuwa nilikuwa nimeishiwa Red Bull. Kutokea Stella Point, Le alieleka Kambi ya Crater, akikusudia kupanda kileleni baadaye kwa ajili ya machweo na kwa mara ya pili kesho kwa ajili ya mawio.

Nilifika kilele cha Uhuru na Yahoo muda kidogo baada ya saa 9 alasiri, na muda mfupi baadaye raia wa Ujerumani na msindikizaji wake walifika pale kileleni. Tuliwapiga picha, na wao wakatupiga sisi picha. Nilijaribu kutuma ujumbe mfupi wa maandishi kwa simu lakini sikuweza kupata mawasiliano. Kwa mbali kidogo, niliona waya ambao nilihisi kama ulikuwa kwenye sehemu ya juu kidogo kuliko Kilele cha Uhuru. Yahoo na yule muongozaji mwingine walikubaliana nami kuwa sehemu ile ilionekana iko juu zaidi ya pale tulipokuwa, na wakasema kuwa chombo kinachopima urefu kutoka usawa wa bahari huonyesha kuwa kuna sehemu moja kati ya Stella Point na Kilele cha Uhuru ambayo huashiria kuwa ni juu zaidi ya Kilele cha Uhuru. Nikitafakari yaliyopita na hasa baada ya ile fatiki kati ya Stella Point na kilele cha Uhuru, najiuliza iwapo kilele kinaweza kuwa "kimesogezwa" chini kidogo kupunguza idadi ya watu wanaoshindwa kufika kilele halisi.
Yahoo (kushoto) na mimi (kulia) kileleni.
Tulilala Kambi ya Crater mbele ya mwamba mkubwa wa barafu. Nilijihisi kama niko kwenye duara la Ncha ya Kaskazini. Ulikuwa ni usiku wa mhangaiko mkubwa kwangu. Wakati wa mpando wa kuelekea Stella Point nilivuta vumbi nyingi kwa sababu ya kuwa nyuma ya Pius, Le, na Saidi na hali hiyo ilinisababishia kupata shida kubwa kupumua usiku ule. Ilikuwa ni usiku wa baridi kali. Kwa mara ya kwanza, nililala nikiwa nimevaa koti zito la baridi.

Makala ijayo: Kuna mtu anatumia madawa ya kuongeza nguvu?


Makala zinazohusiana na hii: