Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Friday, August 25, 2017

Umuhimu wa wagombea huru sasa umejidhihirisha

Hii ni makala yangu ya tarehe 11 Agosti 2015 kwenye safu yangu inayoitwa Ujumbe toka Muhunda ndani ya gazeti la Jamhuri linalochapishwa kila Jumanne.
******************************************
Kama unahitajika ushahidi kuwa upo umuhimu wa kuruhusiwa kwa wagombea huru ndani ya Katiba ya Tanzania, basi huo ushahidi umejitokeza baada ya matukio ya hii karibuni yaliyomo ndani ya siasa za Tanzania.

Tukio lililohitimisha ukweli huo ni kuhama kwa Waziri Mkuu mstaafu Edward Lowassa kutoka Chama cha Mapinduzi (CCM) na kujiunga na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA). Kwa maelezo yake, amehama kutoka CCM kwenda CHADEMA kwa sababu “…mchakato wa kuteua wagombea uligubikwa na mizengwe, ukiukwaji wa maadili, uvunjifu wa Katiba, na taratibu za uchaguzi ndani ya CCM.”

Aliendelea kusema: “Zaidi ya hayo uchaguzi ulisimamiwa kwa upendeleo zaidi na chuki iliyokithiri dhidi yangu.” Kilichotokea Dodoma, kwa mujibu wa maelezo yake, ni kubaka Demokrasia.

Amehamia CHADEMA akiamini kuwa yale yaliyomkuta ndani ya CCM hayawezi kutokea ndani ya CHADEMA. Na dalili ni nzuri kwake mpaka sasa kwa sababu CHADEMA hawakuchukua muda mrefu na walimpa nafasi ya kugombea urais kwenye uchaguzi mkuu wa mwaka huu, nafasi ambayo CCM haikumpa. Hatimaye amepitishwa kuwa ni mgombea urais wa muungano wa vyama vya siasa vinavyojulikana kama UKAWA.

Mwalimu Nyerere amenukuliwa na Lowassa akitamka kuwa Chama cha Mapinduzi siyo baba yake [Mzee Nyerere Burito], wala mama yake [Mugaya wa Nyang’ombe] na kuwa akikosa mabadiliko ndani ya chama hicho, basi atayatafuta nje ya chama hicho. Mheshimiwa Lowassa amekosa mabadiliko ndani ya CCM na anaamini atayapata ndani ya CHADEMA na UKAWA. Swali ambalo halijaulizwa ni hili: asiyeona mabadiliko ndani na nje ya CCM anakuwa mtoto wa nani?

Kwangu mimi haipo sababu ya msingi ya kuwepo yatima wa kisiasa nchini. Jawabu ni kuwepo kwa mfumo wa kikatiba unaoruhusu wagombea huru kama nguzo ya tatu kwenye siasa. Wagombea huru watatoa fursa kwa wanachama waliokosa macho ya kuona na masikio ya kusikia fursa za mabadiliko zilizomo ndani ya chama tawala na ndani ya vyama vya upinzani kutafuta mabadiliko hayo kwingineko kama wagombea huru, au kama watetezi wa wagombea huru.

Kuna mengi ambayo mtu anaweza kuunga mkono ndani ya sera za vyama tofauti vya siasa, lakini akawa pia hakubaliani na kipengele cha sera kwenye vyama hivyo hivyo. Aidha, kuna maamuzi ambayo yanaweza kupitishwa na chama anachokiunga mkono ambayo hayaafiki. Mtu wa aina hii anapaswa kupewa fursa ya kikatiba ya kupenyeza mawazo yake bila kulazimika kuchukua uamuzi ambao tunaousikia kwa baadhi ya watu wa kustaafu siasa au kuachia wadhifa wake ndani ya chama cha siasa, kwa sababu tu haoni chama ambacho kinawakilisha matakwa yake kwa wakati huo.

Kinadharia, chama kinachotawala au chama cha upinzani kinachobaini hali hiyo kitatambua ukomo wa kile ambacho mimi naita jeuri ya chama, au uhakika wa chama cha siasa kuwa kile kinachoidhinishwa na maamuzi rasmi au yasiyo rasmi ya chama ndiyo mwisho wa mjadala na kufungwa kwa kikao. Mfumo wa wagombea huru unaweza kuwa kama sehemu ya mwisho ya kukata rufaa kwa wananchi kwa sababu hiyo ya uwepo wa kukinzana kwa mitazamo baina ya mtu na mienendo ya chama alichokiunga mkono.

Woga mkubwa wa washiriki wa siasa za siku hizi ni kushindwa uchaguzi, siyo kung’ang'ania misimamo ambayo nyakati hizi inaitwa imepitwa na wakati.

Kwenye nadharia ya siasa chama cha siasa kinapaswa kuwa tayari kushindwa kwenye uchaguzi kwa sababu ya kushikilia misimamo mbalimbali ambayo kimekuwa kikiunga mkono kwa mujibu wa sera zake. Kwenye miaka ya mwanzo baada ya Tanganyika kupata uhuru, Mwalimu Nyerere, akiwa Waziri mkuu wa wakati ule, alipingana na baadhi ya wawakilishi wa chama cha TANU bungeni na wa serikali yake, ambao wakati wa kujadili muswada wa uraia wa Tanganyika walidai kuwa uraia wa Tanganyika uwe haki ya Watanganyika wenye ngozi nyeusi tu. Katika kupinga msimamo wa wenzake na akiwa anatetea hoja kuwa kila Mtanganyika anayo haki ya kuwa raia bila kubaguliwa kwa rangi ya ngozi yake, Mwalimu Nyerere alisema kuwa serikali yake itakuwa tayari kushindwa kwenye kura bungeni na kuondoshwa madarakani lakini haiwezi kukiuka misingi ya haki na usawa ambayo yenyewe iliipigania na kuitetea.

Leo hii ndani ya siasa tunashuhudia kuwa misimamo ni kama mashati ambayo hubadilishwa kwa mujibu wa mahitaji yanayojitokeza.

Kwa mtazamo wangu, vyama vyote siasa vinaweka mikakati ya kufika Ikulu tu, kwa kushinda uchaguzi mkuu ujao. Kwa CCM ni kupigana kufa na kupona kuhakikisha kuwa Edward Lowassa hawi rais wa tano wa Tanzania.

Kwa UKAWA hali hii ni dhahiri kuliko kwa CCM. Hatutarajii kuwa jambo rahisi kwa vyama vinne vya siasa kukubaliana kwa yote yaliyomo kwenye sera zao. Kwao jambo la msingi itakuwa “Rais wetu akishaapishwa tutajua la kufanya.”

Ukweli haupingiki kuwa lipo pengo ndani ya siasa ambalo linalazimisha sehemu fulani ya wapiga kura ya Watanzania kuwepo kwenye siasa za vyama ambazo haziwakilishi kikamilifu matakwa yao. Suluhisho ni wagombea huru. Wagombea huru hawatamaliza hitilafu zilizopo lakini watazipunguza kwa kiasi kikubwa.

Taarifa nyingine kama hii:
https://muhunda.blogspot.com/2017/07/afrika-tunaibiwa-sana-tena-sana.html

Saturday, August 19, 2017

Simulizi za Samora Machel, rais wa kwanza wa Msumbiji

Miaka kadhaa iliyopita nilihudhuria mkutano uliyoandaliwa jijini Maputo Msumbiji na muungano wa vyama vya wanajeshi na wapiganaji wa zamani walioshiriki vita mbalimbali duniani. Chama chao kinaitwa Worlds Veterans Federation.

Katika moja ya hafla zilizoandaliwa na Rais wa Msumbiji wa wakati huo Armando Guebuza, nilipata fursa ya kukaa na mzee mmoja mpiganaji wa zamani wa jeshi la ukombozi la FRELIMO ambaye alishiriki kwenye vita ya ukombozi ya Msumbiji.

Alinisimulia mengi juu ya maisha yao walivyokuwa kwenye kambi za FRELIMO zilizokuwa Tanzania, na baadhi ya matukio katika vita iliyoshiriki.

Alisema kuna wakati Kamati ya Ukombozi ya Umoja wa Nchi Huru za Afrika (OAU) ilitembelea baadhi ya maeneo yaliyokombolewa ndani ya Msumbiji na kupokelewa na Samora Machel, wakati huo akiwa rais wa FRELIMO aliyeshiriki mwenyewe katika mapambano.

Waliandaa chakula kwa ujumbe ulioyoongozwa na Katibu Mtendaji wa kamati, Hashim Mbita. Lakini walipokuwa tayari kuanza kula tu, hapo hapo ndege za jeshi la Ureno zilianza kushambulia kambi ile na chakula kikaachwa ili kunusuru maisha yao.

Inaelekea jeshi la Ureno lilipata taarifa ya ziara ile.

Mwalimu Nyerere na Samora Machel kwenye moja ya mikutano ya hadhara.

Niliambiwa kuwa Samora mwenyewe aliongoza mikakati ya kulinda usalama wa ule ujumbe, akiwatanguliza wageni wakikimbia mbele na wakiwa wamezungukwa na ulinzi mkali wa wapiganaji wa FRELIMO. Nikaambiwa Samora mwenyewe alikuwa wa mwisho, nyuma ya kila mtu, akiwa ameshika bastola yake mkononi.

Ni kielelezo cha ushujaa wa baadhi ya viongozi wetu wa zamani. Yule mzee alinitolea simulizi hii huku akicheka kuwa wageni hawakuweza kula siku ile.

Taarifa nyingine ambazo unaweza kupendelea kusoma:
https://muhunda.blogspot.com/2016/12/redio-ya-Mwalimu-Nyerere.html
https://muhunda.blogspot.com/2012/09/wageni-wa-butiama.html

Saturday, August 5, 2017

Baraka Elias, Mtanzania mrefu kuliko Watanzania wote

Nimewahi kuonana na Baraka Elias, Mtanzania mrefu kuliko Watanzania wote, alipotembelea Butiama mwaka 2012. Ana urefu wa mita 2.20 na umri wa miaka 27.
Kwenye picha juu ni yeye pamoja na Notburga Maskini anayeongea naye, kushoto. Notburga tumewahi kuongozana naye kwenye moja ya misafara yangu ya kukwea Mlima Kilimanjaro.

Taarifa nyingine za Baraka Elias hizi hapa (kwa Kiingereza):

Taarifa nyingine za Notburga Maskini hizi hapa (kwa Kiingereza):