Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Monday, December 20, 2010

Mchango wa kwanza wa hisani umepatikana kwa Sekondari ya Wasichana ya Chief Edward Wanzagi

Mchango wa kwanza wa thamani ya Sh.500,000/- (laki tano) kuchangia jitihada za The Mwalimu Nyerere/Mt. Kilimanjaro Charity Climb 2010 kusaidia Shule ya Sekondari ya Chief Edward Wanzagi umetolewa na Tanzania Gatsby Trust.

Shukurani za dhati ziende kwa Tanzania Gatsby Trust (TGT), na kwa Afisa Mtendaji Mkuu wa TGT, Mama Olive Luena.

Unayesoma habari hizi unaombwa kuchangia mojawapo ya walengwa wafuatao wawili wa mwaka huu (au walengwa wote wawili):

Jina la Akaunti:
Chief Edward Wanzagi Girls' Secondary School Fundraising

Benki:
National Bank of Commerce, Tawi la Musoma

Namba ya Akaunti:
030201191529

Pamoja na:

Jina la Akaunti:
Budap

Benki:
National Bank of Commerce, Tawi la Bukoba

Namba ya Akaunti:
027201092625

Sunday, December 19, 2010

Masahihisho kwenye namba ya akaunti ya BUDAP

Nilifanya makosa katika taarifa ya awali niliyotoa juu ya namba ya akaunti ya Budap, mmoja wa walengwa wa The Mwalimu Nyerere/Mt. Kilimanjaro Charity Climb iliyomalizika hivi karibuni mjini Moshi.
Juu ya kilele cha Mlima Kilimanjaro. Kulia unaonekana Mlima Meru.
Taarifa sahihi ni hizi:


Jina la Akaunti:
Budap

Benki:
National Bank of Commerce, Tawi la Bukoba

Namba ya Akaunti:
027201092625

Wednesday, December 15, 2010

CCM wafungua tawi Uingereza, CHADEMA juu ya Mlima Kilimanjaro

Taarifa zilizonifikia hivi punde zinaeleza kuwa baadhi ya Watanzania waishiyo katika mji wa Luton Uingereza walijumuika 12 Desemba 2010 kwa ajili ya ufunguzi wa tawi jipya katika mji wa Luton, ufunguzi uliyofanyika katika hoteli ya Chiltern UK.

Taarifa hiyo, kwa hisani ya Tawi la CCM Uingereza inaendelea:
Wengi wao wanasema wana imani kubwa na CCM katika kuiongoza Tanzania kwa kuonyesha muelekeo wa kuwa na imani na vijana wasomi wachapakazi waliyoko ndani na nje ya nchi.



Ufunguzi huo ambao uliongozwa na mwenyekiti wa tawi la CCM - UK, Maina Owino, kwa kushirikiana na viongozi wengine wa CCM akiwemo Katibu Mwenezi wa Siasa, Moses Katega. Pia viongozi kutoka mashina ya Reading, Birmingham na sehemu zote za London walijumuika.


Katika hotuba yake fupi Ndugu Maina Owino alitoa changamoto nyingi za mafanikio  yaliyopatikana katika kipindi cha miaka mitano iliyopita chini ya uongozi wa Mwenyekiti wa CCM Taifa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Jakaya Mrisho Kikwete katika nyanja mbalimbali kama madini, elimu, ukusanyaji wa mapato ya serikali, waajiriwa wenye sifa za kukidhi nafasi za uongozi serikalini katika nyanja zote, na ujasiriamali kwa Watanzania wanaojitafutia maendeleo bila bugudha.


Changamoto kuhusu ushiriki wa vijana wasomi hapa Uingereza kuingia katika mchakato wa siasa ndani ya Chama ili kuleta mabadiliko yatakayozidi kukiimarisha Chama kisera na kuzidi kuwaletea Watanzania maendeleo katika nyanja mbalimbali kupambana na umasikini yalitolewa na katibu wa shina jipya la Luton aliyechaguliwa siku hiyo, Ndugu Abraham Sangiwa, na kuungwa mkono na wajumbe wote waliyohudhuria ufunguzi huo.


Viongozi waliochaguliwa ni:


Albert Ntmi - Mwenyekiti
Abraham Sangiwa - Katibu Mkuu
John Mbwete - Mjumbe
Sammy Martin - Mjumbe
Norman Wage - Mjumbe

Wakati huo huo, siku mbili zilizopita, nikielekea kilele cha Mlima Kilimanjaro, katika kambi ya Barafu, ambayo ni kituo cha mwisho kabla ya safari ya kufika kilele cha Uhuru niliona bendera ya CHADEMA ikipepea.


Kwa mujibu wa taarifa nilizopata toka kwa wapagazi wanaosindikiza wageni kupanda Mlima Kilimanjaro wanaojulikana miongoni mwao kama "wagumu", kutokana na kazi ngumu wanayofanya kusindikiza wageni juu ya mlima huu maarufu, shughuli za CHADEMA zimeanza juu ya Mlima Kilimanjaro miaka mitatu iliyopita.

CHADEMA hawana tawi juu ya Mlima Kilimanjaro ila nilichoshuhudia mimi na jitihada za wana-CHADEMA kupeperusha bendera ya chama chao kwenye sehemu iliyo juu kuliko zote Tanzania. Kambi ya Barafu ipo urefu wa mita 4,600 juu ya usawa wa bahari.

Sunday, December 5, 2010

Jaffar Amin amewasili Moshi kupanda Mlima Kilimanjaro

Bwana Jaffar Amin amewasili Moshi leo mchana tayari kwa kushiriki nami kupanda Mlima Kilimanjaro kwa madhumuni ya kuchangisha pesa za hisani kwa ajili ya Sekondari ya Wasichana ya Chief Wanzagi ya mkoani Mara, pamoja na kuchangia asasi ya mjini Buoka inayoitwa BUDAP inayojishughulisha na miradi ya kusaidia walemavu kwa njia ya mafunzo na ajira.
Jaffar Amin, pichani, mara baada ya kuwasili Moshi mjini leo mchana, akiwa na hamasa kubwa ya kupambana na Mlima Kilimanjaro ambao unaonekana nyuma yake.
Baada ya kumpokea katika uwanja wa ndege wa kimataifa wa Kilimanjaro, Jaffar alisema amejitayarisha vyema kupanda Mlima Kilimanjaro kuanzia Jumanne, 7 Desemba 2010 kwa muda wa siku nane.

Ni mara yangu ya tatu kupanda huo mlima, na mara ya kwanza kwa Jaffar. Matarajio na maombi kwa wadau mbalimbali ni kuchangia mojawapo ya walengwa wa tukio hili ambalo linajulikana kama The Mwalimu Nyerere/Mt. Kilimanjaro Charity Climb 2010.

Tafadhali changia mojawapo ya hawa wafuatao (au wote):

Jina la Akaunti:
Chief Edward Wanzagi Girls' Secondary School Fundraising

Benki:
National Bank of Commerce, Tawi la Musoma

Namba ya Akaunti:
030201191529

Pamoja na:

Jina la Akaunti:
Budap

Benki:
National Bank of Commerce, Tawi la Bukoba

Namba ya Akaunti:
027201092625
##################################

Saturday, December 4, 2010

Hardmad amerudi tea ulingoni

Baadaya ya kimya kirefu na kujifua kisawasawa, Hardmad amerudi tena kwa kishindo. Na safari hii amekuja na albamu inayokwenda kwa jina Imebaki Story ambayo ina jumla ya nyimbo 11.

zilizorekodiwa katika studio za 41 Records, Tatoo Records, na Maisha Studios za Dar es Salaam, na Click Studio ya Copenhagen, Denmark.

Usanifu umefanywa katika Studio za C4 nchini Denmark. Kwa kipindi cha mwezi mmoja Hardman alikuwa amejichimbia kambini kwa ajili ya mazoezi kwa kushirikiana na Kaka Zao Band atakayokuwa akifanya nayo maonyesho.

Picha na habari kutoka kwa Kwame Mchauru wa Maisha Music.

Thursday, November 4, 2010

Uchaguzi Mkuu 2010 katika picha

Shabiki wa Chama cha Wananchi (CUF) wa jijini Mwanza akielekea kwenye mkutano wa kampeni za uchaguzi mkuu uliyohitimishwa tarehe 31 Oktoba. Mkutano huo ulihutubiwa na Prof. Ibrahim Lipumba, mgombea urais wa CUF.

Monday, November 1, 2010

Vincent Nyerere wa CHADEMA ashinda ubunge Musoma Mjini

Taarifa rasmi iliyotangazwa na msimamizi wa uchaguzi wa Musoma Mjini, saa 11:30 alfajiri hii, imethibitisha ushindi wa Vincent Nyerere wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kuwa mbunge mpya baada ya kumshinda aliyekuwa mbunge, Vedasto Mathayo Manyinyi wa Chama cha Mapinduzi (CCM).
Vincent Nyerere, mbunge mteule wa jimbo la Musoma Mjini, akihutubia mkutano wa uchaguzi uliyofanyika Musoma wakati wa kampeni za uchaguzi za zilizoisha juzi.
Matokeo rasmi ni haya:

Jina la Mgombea
Chama
Kura  Alizopata
Asilimia ya Kura
Zote Zilizopigwa
Vincent K. Nyerere
CHADEMA
              21,225
                   59.71
Vedasto  M. Manyinyi
CCM
              14,072
                   39.38
Mustapha J. Wandwi
CUF
                   253
                     0.71
Chrisant N. Nyakitita
DP
                     53
                     0.15
Tabu S. Machibya
NCCR - Mageuzi
                     19
                     0.05

Sunday, October 31, 2010

Amani Millanga bado anahoji Sera ya Majimbo ya CHADEMA (sehemu ya kwanza)

Katika taarifa ya Septemba 5 nilitoa maelezo ya Amani Millanga akifafanua hoja zake kupinga Sera ya Majimbo ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA). Nilifanikiwa kupata maelezo katika mfumo wa makala zilizoandikwa na John Mnyika, Kaimu Katibu Mkuu wa CHAEMA na mgombea ubunge wa chama hicho kwa jimbo la Ubungo, akiweka msimamo wa CHADEMA kuhusu sera hiyo ya majimbo.


Baada ya kusoma maelezo ya CHADEMA, Amani Millanga anaendelea kufafanua hoja zake dhidi ya Sera ya Majimbo ya CHADEMA.


Pamoja na kwamba sikufanikiwa kutoa taarifa hizi kabla ya uchaguzi, bado nafikiri kuna umuhimu wa wasomaji kusikia hoja za Amani Millanga.

Sera za Majimbo: Utaifa na Hatima ya Amani Yetu
Na Amani Millanga
Amani Millanga (kulia), akiongea na Afisa Kilimo wa Kijiji cha Butiama, David Sanagara.
Kote duniani tumeshuhudia vita na mauwaji ya kikatili yanavyoendelea kizitafuna nchi changa zenye serikali za majimbo na hata zile zisizokuwa na majimbo. Zipo sababu nyingi za ndani na nje za hali ilivyo katika nchi hizi kukosa amani na umoja lakini miongoni mwa sababu kubwa kabisa ni ukabila na udini ambao unachochewa na umkoa na umajimbo. Mtanzania yoyote mwenye kuchukua kila tahadahari ya kuilinda amani yetu hawezi kukubaliana na sera ya majimbo. Hili si suala la "watu kuwa na hofu, na woga au kubisha," bali ni suala la hatima ya utaifa na umoja wetu. Wahenga wetu walisema, mwenzio akinyolewa wewe tia maji. Kwa nini tujitege bomu ili hali tunajua kuwa likilipuka litatumaliza.


Kuiga, Historia na Maslahi ya Taifa
Yapo mambo mengi ya kujifunza kutoka sehemu mbalimbali duniani lakini si yote yanayotufaa. Miongoni mwa yasiyotufaa ni hili la serikali za majimbo. Sababu za kutokutufaa ziko wazi kabisa: ni kuvunjika kwa umoja wa kitaifa na hatimaye amani yetu. Umoja, amani na utaifa ndiyo maslahi yetu ya kwanza kabla ya jambo lolote.


Sera yoyote inayolenga kuyaua mambo haya haitufai. Kupoteza amani na umoja ni jambo la siku moja tu. Lakini kuirejesha amani na umoja katika nchi yoyote ni gharama kubwa ni inachukua muda mrefu sana. Mifano iko wazi. Marekani kwa mfano ilikuwa na vita ya wenyewe kwa wenyewe miaka ya 1860 ambapo majimbo ya kaskazini yalizuia majimbo ya kusini mwa nchi hiyo yasijitenge. Athari za vita hiyo ilikuwa ni kubwa mno. Nigeria hali kadhalika ukianzia na Biafra, majimbo ya kasakzini na delta ya mto Niger. Je tuna uhakika gani kwamba Tanzania haiwezi kuingia katika mgogoro wa baadhi ya majimbo kutaka kujitenga? Mmejiandaa vipi kuidhibiti hali hii kwa Tanzania? Je mnataka tuwe kama Nigeria? Hakuna umoja wala amani pale. Tukumbuke kuwa kuwepo kwa serikali za majimbo huko Marekani ya kaskazini, baadhi ya nchi za Ulaya, Afrika Kusini na Australia si kigezo cha sisi Tanzania kuwa na serikali za majimbo kwani wao wana historia yao inayowapa mwanya wa kuwa na majimbo. Tanzania ina historia yake. Historia yetu haituruhusu kuwa na majimbo kwani yataua utaifa wetu. Yataua nchi yetu.


Majimbo ni Ufa
Katika kitabu cha Nyufa, Mwalimu Nyerere anatukumbusha Tanzania bado ni taifa changa sana na kwamba kuna mambo ambayo tunapaswa kuendelea kuyasimamia na kuyalinda kama mboni za macho yetu. Mwalimu anatahadharisha kwa kusema: "Lakini mambo haya ya msingi yanataka yasimamiwe katika nchi changa. Lazima yasimamiwe.


Ukiacha, watu wanarudi kule kule kwenye mawazo ya kijinga jinga. Ukabila, kama ukabila, sisi bado wakabila sana. Kwa hiyo la ukabila lazima liendelee kupigwa vita mpaka life. Halijafa. Ukiwaminya hawa kidogo utakuta ukabila uko pale pale tu!" Mwalimu anaongeza kuwa: "Ukabila bado upo. Kwa hiyo, ukabila lazima uendelee kupigwa vita. Hapana kukaa na kusema 'Tanzania hatuna ukabila'. Hapana. Watu hatujawa Watanzania bado. Kwa hiyo lazima tuendelee kuupiga vita. Na watu wana udini udini" (uk 28).


Serikali za majimbo ni hatari kwani zitatugawa Watanzania kimakabila na hata kidini. Na kwa mgawanyo huu hauwezi kuleta maendeleo ya kweli kwa Tanzania yote kwa pamoja. Kutakuwa na upendeleo fulani kwa majimbo fulani kutoka serikali ya shirikisho na kutakuwa na upendeleo kutoka serikali ya jimbo kwenda wilayani kutegemea ni kabila gani au ni nani kashika uongozi wa taifa au jimbo. Haya mambo yapo hasa kwa nchi changa, tusijifanye hatuyajui.


Hivyo utaifa wetu unapaswa kulindwa kwa kuepuka kila sera au jambo lolote linaloweza kuuweka hatarini. Ukweli ni kwamba umoja na utaifa wetu utayumba iwapo tutakuwa na serikali za majimbo. Huo ni mwanzo wa kuparaganyika kwa Tanzania na hizo ajenda nyingine mlizonazo hazitafanya kazi yoyote kwani taifa halitakuwepo tena. Sera yenu hii itaweka ufa mkubwa na kubomoa taifa letu. Tutakuwa na serikali yenye nchi isiyokuwa na taifa. Nigeria iko hivyo, isomeni historia yake jinsi ambavyo majimbo yamongeza mgawanyiko.


Muungano Kuvunjika
Suala la majimbo ni hatari kwa Muungano wetu. Mnataka kuifanya Zanzibar iwe jimbo? Na kama Zanzibar wakikataa serikali za majimbo, jambo ambalo ni wazi kwamba watakataa kuwa jimbo, je mnatuhakikishia vipi kuwa mtaulinda Muungano wetu?


Sera ya majimbo ni silaha ya kuuvunja Muungano. Na mara tu Tanzania ikigawika huwezi kuondoa umaskini, ujinga na maradhi. Huwezi kuleta maisha bora bali utaleta ubaguzi na hatimaye machafuko na kumwaga damu.


Muungano wa Tanganyika na Zanzibar si Ufederali au shirikisho. Ndio maana tunayo Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, si Jamhuri ya Shirikisho la Tanzania. Pia Muungano wetu si tenge na mafanikio yake ni makubwa. Hatupaswi kuubeza na kuuita "Tenge". Ndiyo, zipo kero lakini kero hizo hazimaanishi kuwa Muungano ni 'tenge'. Kama ungekuwa tenge kwa maana halisi ya neno tenge basi ungeishavunjika. Leo hii Watanzania tunatembea kifua mbele kwa kujivunia Muungano wetu ambao una faida nyingi kwetu (hii ni mada nyingine).


Serikali za Mitaa
Haya mambo mnayoyataja kuwa yatafanywa na serikali za majimbo tayari yanafanywa na serikali za mitaa nchini. Falsafa ya nguvu ya umma ndiyo msingi mkubwa wa serikali za mitaa. Hoja iwe ni kuziboresha zaidi serikali za mitaa kwa kuzipa mamlaka zaidi ya sasa na si kuziondoa na kuleta serikali za majimbo.


Tuangalie zimeshindwa wapi, kwa nini na nini kifanyike ili ziwahudumie wananchi kwa ufanisi zaidi. Kimsingi kupitia serikali za mitaa ni rahisi zaidi kutoa maamuzi na kusimamia shughuli za maendeleo kuliko katika jimbo litakalokuwa ni kubwa mno na utajikuta unakwama. Mfano katika jimbo la kanda ya ziwa Kagera, Mara na Mwanza kuna watu wenye mahitaji mbali bali. Kwa mfumo wa jimbo si rahisi kuwafikia watu hawa na kutatua matatizo yao. Lakini kwa serikali za mitaa katika kila wilaya ni rahisi zaidi kwani utakuwa unaiongelea Muleba tu na si jimbo zima.


Kimantiki unaliona suala hili kwa uawzi kabisa. Kwanini mambo ya Muleba yaamuliwe katika bunge la jimbo litakalo kuwa pale Mwanza, kwa mfano, badala ya kuamuliwa na baraza la madiwani wa Muleba wanaoijua uzuri Muleba na mahitaji yake? Kwanini niifuate huduma Mwanza badala ya Muleba? Hapa mbona utakuwa unaturudisha kwenye urasimu ule ule ambao serikali ya CCM inauondoa kwa kuzipa serikali za mitaa mamlaka zaidi? Kama hoja ni kuvifuta vyeo vya mkuu wa mkoa, mkuu wa wilaya na katibu tarafa hili ni suala ambalo linaweza kujadiliwa kwa kuangalia faida na hasara zake kwetu. Lakini uwepo wa viongozi hawa usitumiwe kama hoja ya kutaka serikali za majimbo kwani hakuna uhusiano sisisi wa kimantiki kati ya wakuu hawa na kuwa na serikali za majimbo.


Mzigo Mkubwa
Serikali za majimbo zina utitiri wa viongozi zaidi ya mfumo tulionao sasa. Na huu ndio ukweli. Gharama za kuziendesha serikali za majimbo na shirikisho zitaongeza mzigo mkubwa zaidi kwa wananchi badala ya kuupunguza. Utakuwa na bunge katika kila jimbo na bunge la shirikisho, gavana wa jimbo na mawaziri wake na makatibu wa wizara au idara, wakurugenzi n.k. Msululu ni mrefu mno hadi kuja kufika kwa mkurugenzi mtendaji wa wilaya. Hiyo yote ni pesa ya umma inatafunwa. Hivi kwa nini tupoteze mabilioni yote hayo katika kaunzisha majimbo na kuudurusu upya utendaji wake ili kuuboresha zaidi? Kwanini tuwatwishe wananchi mzigo mkubwa zaidi?


Ikulu Lazima Iongoze Taifa-Nchi
Suala la Ikulu au serikali kuu kuingilia serikali za mitaa lina mapana yake katika kilijadili. Inategemea wanaingilia katika lipi na sheria inasemaje. Hapo ndipo tunapaswa kuziangalia kanuni, taratibu na sheria zetu za mitaa. Kama zina mapungufu tuyaondoe ili seikali za mitaa ziwe huru zaidi. Lakini ni ukweli usio na kificho kuwa Ikulu na serikali kuu ni lazima ziwe na mamlaka ya kiutawala na kiutendaji kwa serikali za mitaa. Kinyume chake Tanzania itakuwa haina serikali kwa maana halisi ya 'serikali ya taifa-nchi' na hivyo basi hakuna sababu ya kuwa na Ikulu. Taifa-nchi ni pamoja na serikali za mitaa.


Sasa tujiulize: Ikulu ni ya nini ikiwa haiwezi kuingilia na kusimamia uendeshaji wa taifa na nchi?


Katika mfumo wetu wa sasa, kwa mfano, kila halmashauri ina vyanzo vyake vya mapato na bajeti. Ni kweli kwamba serikali za mitaa zinapokea pesa kutoka serikali kuu lakini si pesa zote zinazoendesha halmashauri zinatoka Dar es Salaam. Huu ni uwongo na uzushi. Juu ya hayo si kweli kwamba kila jambo katika kila halmashauri linaongozwa na maelekezo ya Ikulu ya Dar es Salaam. Hivi Ikulu inaamua hata ushuru au kodi ya halmashauri itozwe vipi na mapato yatumikeje? Hii ni nguvu ya kuupotosha umma!


(sehemu ya mwisho ya makala ya Amani Millanga itatolewa kesho.

Wakala wa CCM kituo cha hospitali ya Butiama yuko ngangari

Nilivyotembelea kituo cha kupiga kura cha Hospitali ya Butiama leo asubuhi nilibaini mtu mmoja amekaa pembezoni, akiwa anaangalia kwa makini mienendo ya kila mmoja pale kituoni. Mwanzo nilifikiri labda ni afisa wa Usalama wa Taifa.
Wakala wa CCM kushoto, akinitupia jicho nilipopiga picha hii leo asubuhi kwenye kituo cha kupigia kura cha Hospitali ya Butiama.
Nilipata ujasiri wa kumuuliza yeye ni nani na akaniambia kuwa ni wakala wa Chama cha Mapinduzi (CCM). Sijashangaa kuwa hakuwepo wakala wa chama kingine kwa sababu mbili: Kwanza, mbunge wa CCM wa jimbo la Musoma Mjini, Nimrod Mkono, amepita bila kupingwa; na pili, nguvu ya upinzani, hata kwenye ngazi ya udiwani, siyo kubwa sana.

Kwenye chaguzi za serikali za mitaa, ni mgombea wa CCM ndiyo aliyeibuka mshindi na kuchaguliwa kuwa mwenyekiti wa kijiji.

Butiama wanapiga kura

Picha hii, chini, inaonyesha mpiga kura wa kijiji cha Butiama akipiga kura leo asubuhi kwenye kituo kilichopo Hospitali ya Butiama.

Nimeshuhudia mstari mrefu wa wapiga kura kwenye kituo hicho, muda mfupi baada ya kituo kufunguliwa, saa 1 asubuhi.

Watanzania nchini kote wanapiga kura leo katika uchaguzi mkuu utakaochagua rais, wabunge, na madiwani. Huu ni uchaguzi mkuu wa nne chini ya mfumo wa vyama vingi.

Monday, October 18, 2010

Lugha yetu Kiswahili

Nilitembelewa Butiama hivi karibuni na Andrea Wobmann, raia wa Uswisi, ambaye alikuwa Tanzania kwa miezi kadhaa akifanya kazi ya kujitolea katika kuendeleza shughuli za utalii jijini Mwanza.

Alisindikizwa na mwenyeji wake toka Mwanza (ambaye jina lake nitaliweka hapa baada ya muda kwa sababu silikumbuki kwa sasa) aliyevaa fulana iliyoandikwa "mzungu."

Awali nilihisi kuwa ile fulana angeivaa Andrea, lakini nilivyopekuwa kwenye kamusi nikagundua kuwa yawezekana sifahamu vizuri tu Kiswahili. Neno hilo, kama lilivyoandikwa kwenye fulana lina maana nyingine zifuatazo, zaidi ya ile maana ambayo wazungumzaji wengi wa Kiswahili tunaifahamu:

1. jambo lisilo la kawaida
2. mafunzo yanayotolewa kwa wanafunzi wa ngazi ya awali
3. ujanja; uerevu

Ingekuwa maandishi ya kwenye fulana yalikuwa "Mzungu", yaani na herufi kubwa ya mwanzo, basi ile maana niliyoidhania mimi ndiyo ingekuwa sahihi, kwa mujibu wa Kamusi ya Kiswahili-Kiingereza ya Taasisi ya Uchunguzi wa Kiswahili (TUKI) ya mwaka 2001.

Sunday, October 17, 2010

Kumbukumbu ya siku ya kufariki Mwalimu Julius Kambarage Nyerere

Alhamisi iliyopita tuliadhimisha kumbukumbu 11 ya kufariki Mwalimu Julius Kambarage Nyerere hapa kijijini Butiama. Maadhimisho yalianza na misa iliyoongozwa na Askofu Michael Msonganzila wa Jimbo Kuu la Kanisa Katoliki, Musoma.
Mama Maria Nyerere (kulia), akisalimiana na Mkurugenzi wa Mkoa wa Mwanza wa Chuo Kikuu Huria, Ben Kapaya (aliyembeba mwanaye, James), akiwa na mkewe (wa pili toka kulia). Siku hiyo ya maadhimisho James alitimiza umri wa mwaka mmoja.

Baada ya misa ilifanyika sala fupi kwenye kaburi la Mwalimu Nyerere katika eneo la Mwitongo, Butiama.
Makongoro Nyerere (kushoto), mwenyekiti wa mkoa wa Mara wa Chama cha Mapinduzi (CCM), akiwa na Askofu Michael Msonganzila wa Dayosisi ya Kanisa Katoliki ya Musoma (kushoto), pamoja na mgeni toka Uganda, Ssalongo Katumba (katikati).  
Na baada ya sala ya kwenye kaburi wageni walipata chakula cha mchana kwenye makazi ya Mwalimu Nyerere iliyopo Mwitongo.
Makongoro Nyerere (katikati), akiwa na Kisheri Kyanzi Mchere, kiongozi wa Umoja wa Vijana wa Chama cha Mapinduzi (UV-CCM), tawi la IFM
Baadhi ya wageni waliyofika kwenye maadhimisho hayo ni pamoja na Waziri Mkuu mstaafu, Jaji Joseph Sinde Warioba na Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Mara ambaye pia ni Mkuu wa Wilaya ya Musoma, Godfrey Ngatuni na mkewe. 
Mgombea ubunge wa jimbo la Musoma Mjini kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Vincent Nyerere (kulia), akisalimiana na Mkuu wa Wilaya ya Musoma, Godfrey Ngatuni wakati wa maadhimisho ya kumbukumbu ya kifo cha Mwalimu Nyerere yaliyofanyika Butiama, tarehe 14 Oktoba 2010.

Kisa cha kuacha kuvuta sigara: safari yangu ya kupanda Mlima Kilimanjaro (makala ya kumi kati ya kumi)

Kumradhi kwa kuchelewa kuleta makala hii ya mwisho katika mtiririko wa makala hizi za safari ya kupanda Mlima Kilimanjaro kutokana na kutingwa na shughuli mbalimbali.

Jumanne 26 Agosti 2008
Baada ya kupata kifungua kinywa tulipiga picha ya pamoja na kuanza safari ambayo kwangu ilikuwa ni ngumu kushuka kueleka lango la Mweka. Njiani kundi la wasichana lilitupita na mmoja akasema, "sirudii tena." Nilimuelewa vyema kwa nini alitamka maneno yale.

Kiasi cha mita 200 kabla ya kufika kwenye lango la Mweka tulikutana na madereva toka Zara Tanzania Adventures ambao walitufuata kwa mguu ili kufahamu iwapo tulikuwa tumechoka sana kiasi cha kushindwa kutembea hatua zile za mwisho. Tulikataa wazo lao la kupanda gari. Ingetia doa tukio ambalo halikuwa la kawaida.

Kuruhusu mwili kuanza kuzowea hali ya kuwa katika nyanda za chini ni suala la umuhimu ule ule kama la kuuzowesha mwili hali ya kuwa nyanda za juu wakati wa kupanda mlima. Yasemekana athari za kuwa katika nyanda za juu zinachukuwa muda kuisha. Kwenye duka la vitu vya ukumbusho lililopo lango la Mweka Le aliinua kofia iliyoandikwa "Hifadhi za Taifa" na akaniomba nifasiri. Sikuweza kukumbuka tafsiri ya Kiingereza na niligeukia maafisa wa Hifadhi ya Kilimanjaro kuomba wanisaidie.

Mmojawapo alisema, "National Parks", na mimi nikasema, "ni kweli! Nimewezaje kusahau hilo!" Mmoja akanijibu, "Usijali, ni kawaida. Akili zako bado zimeganda. Alinipa hoja ya nguvu ya kutolala tena kwenye Kambi ya Crater safari ijayo.

Sasa kuhusu kichwa cha habari cha hii makala: Niliacha kuvuta sigara mwaka wa kwanza nilipoamua kupanda Mlima Kilimanjaro kwa sababu nilikuwa na hofu uvutaji sigara ungenipunguzia nafasi ya kuweza kufika kwenye kilele.

Pesa zilizokusanywa mpaka sasa:

Paundi za Uingereza 440
Dola za Marekani 16,180
Shilingi za Tanzania 2,570,000

Bonyeza hapa kuisoma makala hii kwa Kiingereza

Makala zinazohusiana na hii:
http://muhunda.blogspot.com/2010/10/kisa-cha-kuacha-kuvuta-sigara-safari_05.html

Tuesday, October 5, 2010

Kisa cha kuacha kuvuta sigara: safari yangu ya kupanda Mlima Kilimanjaro (makala ya tisa kati ya kumi)

Jumatatu 25 Agosti 2008
Le na Yahoo walianza safari ya kuelekea Kilele cha Uhuru saa 10:00 alfajiri kuwahi mawio. Baada ya kupambazuka nilitembea juu ya eneo la tambarare la kasoko (shimo la katikati ya volkano) nikiwa pamoja na muongozaji msaidizi hadi Stella Point ambako nilituma ujumbe wa maandishi wa simu niliyokusudia kuutuma jana tokea kileleni: "Salamu toka Kilele cha Uhuru, kilele cha Mlima Kilimanjaro (mita 5,896)..."

Baadhi ya majibu niliyoyapata yalikuwa yanapendeza. Joseph Ibanda, rubani, aliandika: "..kwa hakika mandhari itakuwa ya kustaajabisha hapo ulipo..." Asingeweza kutumia msemo uliyo bora zaidi kuelezea hisia zangu na hapakuwa na sehemu bora zaidi kupata hizo hisia kuliko pale niliposimama wakati nasoma ujumbe wake. 
Hema langu mbele ya barafu katika Kambi ya Crater
Kushoto kwangu kulikuwa na eneo pana la wazi kati ya Kibo na Mawenzi, mbali lakini kukionekana vizuri kabisa. Chini zaidi kulikuwa na mandhari nzuri kwa kiasi cha mita 1,500 halafu utando mzito wa mawingu. Siwezi kuelezea msisimko wa kusimama juu ya ardhi na wakati huo huo kuwa uko juu ya mwaingu, zaidi ya mita 1,500 juu ya mawingu. Ni rubani tu anaweza kutamka alivyotamka Joseph.

Baada ya kuutangazia ulimwengu kuwa nimefanikiwa kufika kileleni, tulianza kuteremka kuelekea Kambi ya Barafu. Wabeba mizigo wanaotupita kwa kasi wanaleta mkanganyiko katika ugumu unaowakabili watu wanaopanda mlima kwa mara ya kwanza. Na hakuna sehemu ambapo ugumu huu unajitokeza kwa kiasi kikubwa kama kipande kati ya Kambi ya Barafu na Stella Point. Ni hapa ambapo wengi ambao wanashindwa kuendelea kutokana na athari za kuwepo katika hali ya uwanda wa juu pamoja na matumizi ya nguvu wanajitenga na wale wazoefu wa kupanda milima. Katika mazingira haya, mzee wa takribani miaka 70 alitupita kama vile anakimbia akiwa na muongozaji wake akijitahidi kwenda kwa kasi ya yule mzee. Michezo ya Olimpiki ya Beijing ikiwa iko mbioni nahisi kuwa huyu mzee anaweza kuwa anatumia madawa ya kuongeza nguvu. Anaweza kuwaadhiri hata wale wenye umri wa kuwa wajukuu zake.

Tunavyozidi kuteremka baada ya kupita Kambi ya Barafu tunakutana na wanaoelekea kileleni. Wanauliza, "Hali ilikuwaje? Jibu langu la mwanzo nasema "kasheshe". Le anatoa jibu ambalo la kutia moyo zaidi. Anasifia mandhari na kusema, "Nzuri sana, ya kustaajabisha." Halafu nakumbuka kuwa hata mimi nilipanda Kilimanjaro kwa madhumuni ya kuona mandhari: mandhari ya kuvutia ya Mawenzi jua lilipochomoza; taswira  za umbali mrefu na muonekano wa njia zenye mizungukuko zilizopo kwenye kipande kati ya Mawenzi na Kibo; na hali ya kujisikia kama niko kwenye Ncha ya Kaskazini nilipokuwa kwenye Kambi ya Crater. Lakini, baba lao, kusimama juu ya ardhi na kutazama mawingu yakiwa chini yako. Nilisimama pale nikivuta hewa ya ubaridi ya mlimani na nilichoweza kusema tu ni "kasheshe."

Leo tulitembea kutoka Kambi ya Crater (iliyopo mita 5,790 juu ya usawa wa bahari), kupita Kambi ya Barafu (iliyopo mita 4,600 juu ya usawa wa bahari), kupita Kambi ya Millenium ya Juu (iliyopo mita 3,797 juu ya usawa wa bahari), mpaka Kambi ya Mweka (iliyopo mita 3,100 juu ya usawa wa bahari) ambako tulilala kwa siku ya mwisho. Hii ilikuwa ni safari moja ngumu sana, na nilihisi misuli yangu ya miguu ikianza kufikia kikomo kutokana na kutembea mara kwa mara kwa siku sita.

Makala ijayo: akili zilizoganda na sababu ya kuacha kuvuta sigara


Makala zinazohusiana na hii:

Friday, October 1, 2010

Kisa cha kuacha kuvuta sigara: safari yangu ya kupanda Mlima Kilimanjaro (makala ya nane kati ya kumi)

Jumapili Agosti 2008
Ingawa nilikuwa najiamini kwa kiasi kikubwa leo (kwa sababu ya kunywa Red Bull moja jana usiku, na nyingine asubuhi), wenzangu walikuwa na hofu juu yangu. Njia mbadala ambayo tulijadili katika siku chache zilizopita ilikuwa ni kwamba, badala ya kufanya jaribio moja la kufika kileleni toka Kambi ya Barafu kuanzia saa sita usiku, tuliamua kuanza asubuhi. Aidha, kwa njia hiyo mbadala tuliyoijadili, iwapo tutafika Stella Point (baada ya mpando mmoja mkali sana wa leo), na nitajisikia bado naweza kumalizia kilomita moja kufika kilele cha Uhuru ambayo inahusisha mpando mwepesi kwenye sehemu ya juu ya Mlima Kilimanjaro, basi nitamalizia kipande cha kutoka Stella Point mpaka kielele cha Uhuru.

Lakini kama nguvu ya Red Bull itakuwa imeisha mwilini baada ya kufika Stella Point, iliyopo urefu wa mita 5,756 juu ya usawa wa bahari, basi tutaelekea Kambi ya Crater, iliyopo urefu wa mita 5,790 juu ya usawa wa bahari, na tutajaribu kufika kileleni kesho asubuhi. Tulikubaliana pia iwapo Le ataona kama mwendo wangu ni wa polepole sana, yeye na Saidi, msaidizi wa Yahoo, watatuacha na kutangulia. Kila mmoja alihisi begi langu lilikuwa na uzito wa ziada na nilishauriwa kupunguza nguo kutoka kwenye begi na kubaki na vitu muhimu tu.
Kabla tu ya mawio, Kilele cha Mawenzi kinavyoonekana.
Kulinganisha na siku zilizopita, leo kulikuwa na wakweaji wachache zaidi waliyotupita njiani. Na kwa hakika, hata wapagazi, ambao walikuwa wana kawaida ya kutupita kama tumesimama, leo walitembea polepole zaidi wakati tukielekea Stella Point. Wengine walishindwa hata kutupita na waliendelea kutembea nyuma yetu. Tuliona taswira ya kuvutia kabisa ya Mawenzi, kilele cha pili cha Mlima Kilimanjaro, na sehemu ya katikati ya Kibo na Mawenzi, inayoitwa saddle kwa Kiingereza.

Kadiri saa zilivyozidi kupita, wote waliyokuwa na hofu juu yangu walianza kukubali kuwa tulikuwa tunasonga mbele kwa kasi nzuri kabisa. Tulivyowasili Stella Point nilihisi kuwa nina nguvu za kutosha kuelekea kilele cha Uhuru. Nilishangaa kuona kuwa ile kilomita moja ya mwisho iligeuka kuwa sehemu moja ngumu kuliko zote. Yawezekana kabisa kuwa nilikuwa nimeishiwa Red Bull. Kutokea Stella Point, Le alieleka Kambi ya Crater, akikusudia kupanda kileleni baadaye kwa ajili ya machweo na kwa mara ya pili kesho kwa ajili ya mawio.

Nilifika kilele cha Uhuru na Yahoo muda kidogo baada ya saa 9 alasiri, na muda mfupi baadaye raia wa Ujerumani na msindikizaji wake walifika pale kileleni. Tuliwapiga picha, na wao wakatupiga sisi picha. Nilijaribu kutuma ujumbe mfupi wa maandishi kwa simu lakini sikuweza kupata mawasiliano. Kwa mbali kidogo, niliona waya ambao nilihisi kama ulikuwa kwenye sehemu ya juu kidogo kuliko Kilele cha Uhuru. Yahoo na yule muongozaji mwingine walikubaliana nami kuwa sehemu ile ilionekana iko juu zaidi ya pale tulipokuwa, na wakasema kuwa chombo kinachopima urefu kutoka usawa wa bahari huonyesha kuwa kuna sehemu moja kati ya Stella Point na Kilele cha Uhuru ambayo huashiria kuwa ni juu zaidi ya Kilele cha Uhuru. Nikitafakari yaliyopita na hasa baada ya ile fatiki kati ya Stella Point na kilele cha Uhuru, najiuliza iwapo kilele kinaweza kuwa "kimesogezwa" chini kidogo kupunguza idadi ya watu wanaoshindwa kufika kilele halisi.
Yahoo (kushoto) na mimi (kulia) kileleni.
Tulilala Kambi ya Crater mbele ya mwamba mkubwa wa barafu. Nilijihisi kama niko kwenye duara la Ncha ya Kaskazini. Ulikuwa ni usiku wa mhangaiko mkubwa kwangu. Wakati wa mpando wa kuelekea Stella Point nilivuta vumbi nyingi kwa sababu ya kuwa nyuma ya Pius, Le, na Saidi na hali hiyo ilinisababishia kupata shida kubwa kupumua usiku ule. Ilikuwa ni usiku wa baridi kali. Kwa mara ya kwanza, nililala nikiwa nimevaa koti zito la baridi.

Makala ijayo: Kuna mtu anatumia madawa ya kuongeza nguvu?


Makala zinazohusiana na hii:

Thursday, September 30, 2010

Tuma taarifa za uchaguzi kwa njia ya mtandao na simu

Taarifa hizi nimepata toka kwa Steven Nyabero wa Vijana FM na inaelezwa kuwa ni njia ya kutumua taarifa mbalimbali ambazo zinahusiana na uchaguzi mkuu wa mwaka huu.

Kwa mujibu wa maelezo yake:

"Vijana FM inatumia Crowdmap, chombo kilichotengenezwa na Ushahidi, kukusanya taarifa, mawazo na uzoefu wakati wa Uchaguzi Mkuu Tanzania. Ni matarajio yetu kwamba chombo hiki kitawapa jukwaa watu kutoa taarifa, maoni, kuanzisha mijadala na kueneza ujuzi wa mchakato wa uchaguzi na matukio mbalimbali."
Anaendela:

Taarifa zinaweza kuwasilishwa kwa njia tatu:

  1. Kwa kutuma barua pepe: TZelect (at) gmail (dot) com
  2. Kwa Twitter hashtags #TZelect au #uchaguzitz (Shukrani Jamii Forums)
  3. Kwa kujaza fomu kwenye tovuti

Wednesday, September 29, 2010

Kisa cha kuacha kuvuta sigara: safari yangu ya kupanda Mlima Kilimanjaro (makala ya saba kati ya kumi)


Jumamosi 23 Agosti 2008
Tuliamka kukiwa na hali nzuri ya jua na tukaanza mpando mmoja mkali kuelekea Kambi ya Barafu. Nagundua mabadiliko kidogo; najihisi kama nina nishati ya ziada kidogo. Hii itakuwa ni Red Bull. Nilijadiliana kwa kirefu na Yahoo uwezekano wa kuleta watu wengine kupanda Mlima Kilimanjaro mwakani iwapo nitafanikiwa kufika kileleni. Hii itakuwa Red Bull iliyonipa ujasiri wa kufikiri kuwa upo uwezekano kwangu wa kufika kileleni.

Tulifika Kambi ya Barafu (iliyopo mita 4,600 juu ya usawa wa bahari) ikikaribia wakati wa mlo wa mchana na tukala saa 8 mchana. Najihisi kama, kadiri siku zinavyopita, mwili wangu unaanza kuzowea hali ya kuwa kwenye nyanda za juu. Yahoo, pamoja na kuwa kila wakati anazungumzia mikakati ya kujitoa iwapo nitashnidwa kuukabili Mlima, amesema kuwa naonekana mwenye hali nafuu leo.

Kwenye kambi ya wahifadhi kuna mtu alikuwa anauza makopo ya bia ya Kilimanjaro kwa Sh.3,000 kila moja, na bei hiyo hiyo kwa Coca Cola. Ukilinganisha ni jinsi gani tulivyo juu kutoka usawa wa bahari, unaweza kusema kuwa bei hizo ja juu ni muafaka kabisa.

Tulikutana tena na kundi la wale vijana wa Kijerumani, waliyotupita karibu na Lava Tower jana, wakiteremka kutoka kileleni. Niliambiwa kuwa walipitiliza Kambi ya Karanga [kambi ambayo sisi tulilala] na yawezekana kuwa walilala kwa saa chache tu kwenye Kambi ya Barafu kabla ya kuanza kuelekea kileleni.

Leo hii nina uzoefu wa kutosha wa kupanda milima kiasi cha kuweza kutoa ushauri kwa wanafunzi wasiyo wazoefu. Siwezi kupendekeza kupanda Mlima huu kwa mtu ambaye:
  • hafanyi mazoezi mara kwa mara
  • hawezi kustahimili hali ya baridi
  • hukaa ofisini kuanzia Jumatatu hadi Ijumaa na kuhamia kwenye kaunta ya baa kati ya Ijumaa na Jumapili
  • saa chache baada ya kuanza kutembea atafikiri, "Hivi huku nimefuata nini? Naweza kuwa kwenye chumba chenye joto, napata laga yangu moja baridi, na nikiangalia kwenye luninga ligi ambayo hupendelea sana kuangalia."

Ukikusudia kupanda huu mlima lazima uwe unasukumwa na jambo moja zito sana. Mimi nimechagua kuchangisha pesa kwa ajili ya elimu. Nimekuwa najaribu kufikiria kwa nini mtu yoyote awe tayari kulipa pesa na ajiingize kwenye fatiki kubwa kiasi hiki na bado nakosa jawabu. Naweza kuandika orodha ndefu ya marafiki zangu, wanafamilia, na washirika wangu ambao hawatakuwa tayari hata kulipwa pesa kuja kupanda mlima huu.

Kesho, nitafahamu iwapo ninazo sifa za kuweza kufika kwenye kilele kirefu kuliko vyote vya bara la Afrika. Leo, tunauona mlima vizuri kabisa na naanza kuhisi kuwa kesho nitapambana na kasheshe isiyo ya kawaida. 
Naanza kutafakari msemo niliyousikia kuwa "kupanda Mlima Kilimanjaro ni mtihani wa kisaikolojia zaidi kuliko wa maguvu." Ninavyautazama mpando mkali wa kesho, naanza kuelewa uzito wa usemi huo:
Nimesimama mbele ya Mlima Kilimanjaro katika safari ya kuelekea Kambi ya Barafu

 inawezekana vipi kwa mtu yoyote ambaye anapanda mlima huu kwa mara ya kwanza kushindwa kuelewa uzito huo.

Wakati najiandaa kulala joini namwambia Le kuwa mpaka sasa sehemu ngumu kabisa ya kupanda mlima huu inanikumba ninapokwenda chooni. Nikiwa nyumbani ninayo fursa, ambaye nadra kuitumia, ya kufungua gazeti na kulisoma nikiwa maliwatoni; hapa Kilimanjaro nalazimika kuchuchumaa. Mimi napata shida kubwa kuchuchumaa sehemu yoyote, wacha mlimani. Kwa hiyo kuchuchumaa mita 4,600 juu ya usawa wa bahari ni mtihani mkubwa sana kwangu.

Kwenye nyanda za juu hata kufunga kamba za viatu inahitaji kuhenyeka kwa hali ya juu. Asubuhi nafunga kamba ya kiatu kimoja halafu inabidi nipumzike na kuvuta pumzi kwa kama dakika tano hivi kabla ya kufunga kamba ya kiatu cha pili. Kwenda chooni inahitaji mara mbili ya nguvu inayotumika kufunga kamba za viatu.

Leo nilishuhudia wakweaji watatu wakiwasili Kambi ya Barafu na nikaona nyusa zao zilizogubikwa uchovu mkubwa na nikawaza: kama hivi ndivyo na mimi huonekana kila ninapofika kambini baada ya kutembea kwa siku nzima, basi kupanda huu mlima siyo mchezo hata kidogo.

Nimeshaamua kuwa huu mlima ni wa kupendezesha macho tu na wa kusifiwa kwa mbali, na pengine wa kusifiwa na kutazamwa kwenye picha lakini, kwa hakika, siyo mlima wa kukwea hata kidogo.

Makala ijayo: Kilele cha Uhuru na Kambi ya Crater


Makala zinazohusiana na hii:

Tuesday, September 28, 2010

Kisa cha kuacha kuvuta sigara: safari yangu ya kupanda Mlima Kilimanjaro (makala ya sita kati ya kumi)

Alhamisi 21 Agosti 2008
Tulianza na mpando wa taratibu kutoka Kambi ya Shira (iliyopo mita 3,400 kutoka usawa wa bahari) na tutafika na kupita Lava Tower (iliyopo mita 4,600 juu ya usawa wa bahari). Wenye nishati ya ziada wanaweza kukwea Lava Tower ambayo nilikadiria ina urefu wa mita 500 juu ya njia ya kuelekea Kambi ya Barranco, kikomo cha safari yetu kwa siku ya leo. Tulikutana na kundi la vijana wa Kijerumani wakiteremka toka Lava Tower.
Taswira ya Mlima Kilimanjaro kutoka upande wake wa mashariki

Ilikuwa ni mteremko mmoja mrefu na wa kuchosha kutoka Lava Tower kuelekea Barranco (iliyopo mita 3,950 kutoka usawa wa bahari) ambako nilikutana na wahifadhi wawili, wote wakiwa wanamazingira, na ambao walionyesha shauku kubwa kujua kusudio la msafara wangu. Kwanini nilikuwa napanda Mlima Kilimanjaro? Nikifanikiwa kufika kileleni nitapanda milima mingine, kama Meru, au Oldoinyo Lengai? Mmojawapo aliniambia kuwa yeye ni Mmasai na aliniambia kuwa ana jina refu kama langu. Aliniambia kuwa mwenzie ni kutoka wa kabila la Wairaqi.

Jioni wakati wa tathmini ya siku nilihisi kama Yahoo alihisi kuwa ninapata shida kupanda mlima baada ya yeye kushauri kuwa mimi nitumie njia tofauti ya kuteremka badala ya ile njia ambayo Jose' alipendekeza na ambayo Le alikuwa na shauku ya kuitumia. Yahoo alisema pengine itabidi nichukue njia ya moja kwa moja kuelekea lango la Mweka badala ya kutumia njia ya Machame iliyopendekezwa na Jose'.

Nilikubali. Kiongozi wa msafara ndiyo hufanya maamuzi yote ya mwisho kwa kuzingatia tathmini yake kwa kila moja na ingawa sikujihisi kuwa nimefikia kikomo cha uwezo wangu, sikuwa na nguvu ya kutosha kuanza kubishana nae baada ya kutembea kwa siku nzima. Labda nitakuwa na maoni tofauti kesho asubuhi.

Ijumaa 22 Agisti 2008
Nimeamka nikijisikia na hali nzuri zaidi leo. Tulianza kutembea tukiwa mbele ya jabali ambalo nakisia lilikuwa na urefu wa mita 750. Hii, Pius alituambia, ndiyo inaitwa "Mpando wa Kifungua Kinywa" Kutokana na ugumu wa mpando huu alisema mara tutakapofika kule juu tutajihisi kuwa tunahitaji kupata tena kifungua kinywa. Alituambia kuwa wakweaji wengi huwa wakifika hapa hukata tamaa na kuteremka kurudi Moshi. Na cha kustaajabisha ni kuwa hii ni njia ambayo mwasisi mmoja aliamua kuwa, kama ambavyo Le anapenda sana kutamka, inawezekana kupita.

Pius alituambia kuwa alikaribia kuacha kazi yake kama muongozaji wa misafara ya kupanda Mlima Kilimanjaro alipoambiwa kwa mara ya kwanza kuwa Mpando wa Kifungua Kinywa ndiyo njia pekee ya kuelekea kileleni kutokea hapa. Katikati ya kupambana na Mpando wa Kifungua Kinywa tulifika eneo linaloitwa Busu la Mwamba ambapo unakumbatia uso wa jabali ili kujinusuru kuanguka na kuepuka mauti.

Sehemu ya mwisho tulipokaribia Kambi ya Karanga (iliyopo mita 3,963 juu ya usawa wa bahari) ilikuwa ni mpando mwingine mrefu na wa kuchosha. Kutokea Karanga tuliweza kuuona Mlima Kilimanjaro kama ambavyo wengi tumozoea kuuona. Kadiri tunavyozidi kuelekea mashariki, tunapata taswira tofauti ya mlima kila siku. Kabla ya kulala, nilikunywa mojawapo ya kopo moja ya Red Bull na nilisumbuka sana karibu usiku mzima. Asubuhi Pius alituambia kuwa yawezekana kuwa usiku nyuzi joto zilishuka chini ya kiwango cha kugandisha maji.

Makala ijayo: Athari za Red Bull


Makala zinazohusiana na hii:

Monday, September 27, 2010

Kisa cha kuacha kuvuta sigara: safari yangu ya kupanda Mlima Kilimanjaro (makala ya tano kati ya kumi)

Jumanne 19 Agosti 2008
Tulipanda gari kutoka Moshi tukielekea upande wa Arusha halafu tukakatiza kuelekea Machame kwenda eneo la kuanzia safari yetu. Nilisikitika kuwa mawingu yalituzuwia kuuona vizuri Mlima Kilimanjaro. Wahifadhi 

Le, akiwa nje ya mahema yetu ya kulala
Kilimanjaro walikagua vifaa vya wasindikizaji wetu kwenye lango la Londorossi. Kundi letu lilikuwa na wabeba mizigo 9, Yahoo, na msaidizi wake.

Wabeba mizigo wa Mlima Kilimanjaro wanafanya kazi katika mazingira magumu na wanabeba mizigo mizito  ya mahema, mifuko ya kulalia, chakula, na maji ili kutuwezesha sisi kufika kilele cha Uhuru katika mazingira ya starehe. Hata hivyo, mazingira yao magumu yanasababisha athari siyo tu kwa afya zao ila na hata kwa maisha yao. Tulisimuliwa hadithi ya wabeba mizigo waliokuta mauti kutokana na kutokuwa na mavazi muafaka ya kuhimili baridi.

Mlima Kilimanjaro unaonekana kwa mara ya kwanza baada ya kutoka eneo la msitu.
Tuliteremshwa mwisho wa barabara mbaya, aina ya barabara ambayo inapitika na magari yaliyotengenezwa mahususi kukabili barabara za aina hiyo. Tulianza na mwendo wa kutembea wa kasi ndogo kabisa ambayo sijawahi kuona tangu nianze kujifunza kutembea. Yahoo, akiwa mbele yetu, ndiye aliyepanga hiyo kasi ambayo tuliendelea nayo kwa muda wa saa nne. Katika siku zilizofuata, tulivyoanza kupambana na maeneo magumu ya mpando nilielewa umuhimu wa kasi ile ndogo ambayo inasaidia sana kupiga hatua ya wastani wakati wote. Usiku wa kwanza tulilala kambi ya Big Tree, tukiwa kati ya mbega kadhaa.

Tatizo kuu la usiku wa kwanza ni kulala mapema. Kujaribu kulala saa mbili usiku ilikuwa mateso, lakini kwa usiku wa kwanza tu. Katika siku saba zilizofuata nilikuwa na uchovu mkubwa sana kutokana na kutembea kila siku kiasi ambapo ningeweza kulala hata saa 6 mchana. Mtihani mwingine ulikuwa kulala ndani ya mfuko wa kulalia. Jaribu kufikiria kulala ndani ya zulia lililoviringishwa na uweze kupata usingizi. Wakati tukikaribia kumaliza safari yetu Le alipendekeza kuwa nitafute mfuko wa kulalia toka Australia ambao unatengenezwa na nafasi kubwa zaidi kwa mtumiaji.

Niliona ajabu sana kuwa wakati nahangaika kutafuta usingizi nilisikia jamaa anakoroma kutoka hema la jirani yangu.

Jumatano 20 Agosti 2008
Leo, naamini nilifanikiwa kutembea kwa mwendo mrefu kuliko yote ambayo nimewahi kutembea. Siamini hata Neslon Mandela amewahi kutembea kwa mwendo mrefu zaidi. Kuachilia saa moja ya mlo wa mchana katika kambi ya Shira, tulitembea kuanzia saa 1 asubuhi mpaka karibia saa 2 usiku, tukiwa tumepambanishwa na mpando mmoja mkali baada ya kumaliza eneo la msitu na kuelekea kwenye Uwanda wa Shira.

Sehemu ngumu kuliko yote kwa leo ilikuwa baada ya machweo wakati Yahoo alipotuonyesha mwanga uliyokuwa mbali juu ya safu ya kilima na akasema ndiyo kikomo cha safari yetu kwa leo. Ilikuwa ni mpando mgumu ambao ulikuwa kama hauelekei kwisha. Ilifika wakati nilimpa Yahoo mfuko wangu wa mgongoni na nilimalizia safari bila mzigo. Baada ya hapa nilianza kuwa na hofu kuwa pengine sitaweza kufika kileleni.

Ingawa sikusumbuliwa na baridi nilihisi kupungukiwa pumzi, na Yahoo aliniambia kuwa hizo zilikuwa dalili za ugonjwa wa nyanda za juu unaosababishwa na upungufu wa oksijeni. Alisema baadhi ya dalili za mgonjwa mahututi ni pamoja na rangi ya ulimi kugeuka kijani.

Makala ijayo: Tunaelekea kambi ya Barranco na "mpando wa kifungua kinywa".


Makala zinazohusiana na hii:

Sunday, September 26, 2010

Kikwete ahutubia Musoma Mjini kwenye kampeni za uchaguzi

Jana, mgombea urais wa Chama cha Mapinduzi (CCM) na Rais wa Tanzania, Jakaya Mrisho Kikwete, alihutubia umati wa wananchi wa Musoma Mjini katika ratiba yake ya kampeni ya kuwania kiti cha urais katika uchaguzi mkuu wa mwezi Oktoba mwaka huu.


Mgombea urais wa CCM akihutubia mkutano wa kampeni za uchaguzi kwenye kiwanja cha Shule ya Msingi Mukendo jana mjini Musoma 
Katika hotuba ambayo ilitanguliwa na hotuba fupi za mbunge aliyemaliza muda wake wa CCM kwa jimbo la Bunda, Stephen Wassira, na ya mbunge mwingine wa CCM aliyemaliza muda wake katika jimbo la Musoma Mjini, Vedasto Mathayo, na ya Mwenyekiti wa CCM mkoa wa Mara, Makongoro Nyerere, Rais Kikwete alitoa ahadi mbalimbali za chama chake kwa wapiga kura iwapo atachaguliwa kuongoza tena kuanzia Oktoba.

Aidha, aliorodhesha yale aliyoyataja kama mafanikio ya serikali yake katika kipindi cha miaka mitano iliyopita kwenye sekta za afya, maji, umeme, barabara, kilimo na ufugaji.

Ahadi nazo zilikuwa nyingi tu katika sekta zote muhimu, zikiwa ni pamoja na kumalizia ujenzi wa hospitali ya Kwangwa iliyopo Musoma; mpango wa kuongeza matumizi ya serikali kupambana na ugonjwa wa Malaria kwa matumizi ya chandarua, pamoja na kunyunyuzia dawa za kuua mbu. Alitaja pia mpango wa ushirikiano na nchi ya Cuba, nchi ambayo ilifanikiwa kufuta malaria kwa dawa zinazoshambulia mbu katika maeneo ya kuzalia.


Mgombea urais wa CCM alisema:
Nimekuja tena kuwaomba CCM iendelee kuongoza nchi yetu. Sababu ziko nyingi, nitataja mambo matatu. La Kwanza, hakuna chama kama CCM. Vyama vya siasa viko vingi, lakini kwa muundo, kwa mtandao, kwa sera, kwa mipango, mipangilio na uendelezaji hakuna hata kimoja kitaikaribia CCM.
Pili, tunaingoza vizuri nchi hii. Nchi imetulia, mafanikio yanaonekana dhahiri. Tanzania ilivyokuwa mwaka 1961 sivyo ilivyo leo, ilivyokuwa mwaka 2005 sivyo ilivyo leo. Na katika miaka mitano hii tumefanya mambo mengi ambayo huko nyuma yalionekana hayawezekani, tumeyaweza.
Tatu, sisi waaminifu.

Katika hotuba yake hawakusahau kina mama:
Wakipewa nafasi kina mama wanaweza. Kina mama niliahidi tutawapeni nafasi, mawaziri wengi katika baraza langu kuliko wakati mwingine wowote katika historia, majaji wengi. Kila mahali, tuliahidi [asilimia] hamsini kwa hamsini. Bunge lijalo wanawake watakuwa [asilimia] hamsini, na kina baba watakuwa [aslimia] hamsini.
Aliendelea:
Tuliahidi kuborehsa upatikanaji wa huduma mbalimbali: elimu, afya, maji, barabara, umeme, mitandao ya simu, na kadhalika.

Mwaka 2005, sekondari za Musoma zilikuwa na vijana 3,000. Leo sekondari zina vijana 10,777. Ameeleza mheshimiwa mbunge kuwa ziko changamoto za walimu, vitabu, maabara, na nyumba za walimu. Ni kweli. Lakini ni changamoto za maendeleo. Lakini sisi tumejiandaa kuikabili changamoto hiyo na tumepata mafanikio makubwa.

Tuliamua kupanua mafunzo ya ualimu katika vyuo vikuu, na vyuo vya ualimu kwa ngazi ya diploma. Mwaka 2005 tulikuwa tunapata kutoka vyuo vikuu walimu wasiozidi 600. Mwaka huu tutatoa walimu 12,124. Si mafanikio madogo. Ni mambo yanayofanywa na watu makini kama sisi, na yanatekelezwa na serikali makini kama serikali ya CCM.

Mwakani kila shule ya sekondari itapata walimu wasiopungua watano. Chuo Kikuu tulichojenga Dodoma kitatoa wanafunzi 40,000. Kati ya hao 15,000 ni wanafunzi waliyosomea ualimu. Tatizo la ualimu lipo?
Waliyomtangulia walisema yafuatayo:

Alianza Stephen Wassira:

Stephen Wassira, mgombea ubunge wa CCM kwa jimbo la Bunda, akihutubia wakazi wa Musoma jana
Watu wengine nao wamesema wanataka tuwachague. Lakini kilichonishangaza wakati nafuatilia maneno yao, nikagundua wanawadanganya Watanzania kwa ahadi za uongo. Mmoja anasema, 'mkinichagua mabati yatakuwa shilingi elfu tano.' Sasa mimi namuuliza: pale Ikulu kuna kiwanda cha mabati? Maana mabati ni bidhaa, inatengenezwa katika mazingira fulani ya uchumi. Kuna masuala ya gharama ya kuzalisha mabati hayo. Kuna gharama ya kusafirisha. Kuna mambo ambayo yako nje kabisa hata ya uwezo wa rais wa Watanzania. Bei ya mafuta ikipanda, huyo rais wa mabati ya shilingi elfu tano atayafanyaje? Anaongopa....Huyu anadanganya, tena anadanganya mchana.
Akafuatia Makongoro Nyerere:
Leo amekuja mgombea wetu wa urais, na kila harusi huwa haikosi wasindikizaji.Ukifika kwenye stendi ya mabasi kuna watu kadha wa kadha ambao wanashughulikia shughuli ya usafiri. Wapiga debe wapo, makonda wapo, na madereva wa magari wapo. Wewe ukifika pale stendi, hela yako unampa mpiga debe? Utafika? Usimpe hela yako mpiga debe, maana yeye ni mpiga debe tu. Mpe hela yako konda.
Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Mara, Makongoro Nyerere, akiwa jukwaani muda mfupi kabla ya kumkaribisha mgombea urais wa CCM, Jakaya Kikwete, kwenye mkutano wa jana.
Leo mtu anataka kuwa raisi wetu aende akauweke mwenge [wa Uhuru] stoo. Halafu anakuja hapa anadanganya wana Musoma wenzangu eti yeye anamuenzi Nyerere. Wewe unamuenzi Nyerere mwenge wake unataka kwenda kuuweka stoo, ndiyo ujanja wako huo?


Akamalizia Vedasto Mathayo:

Katika kipindi cha miaka mitano...ilani ya uchaguzi tumeweza kuitekeleza barabara, tumeitekeleza kwa asilimia tisini. Mwaka 2005, tulisema kwamba lazima tuendelee kuboresha huduma za kijamii, na tukasema: kipaumbele chetu cha kwanza tutakipeleka kwenye elimu. Ilani yetu ya uchaguzi ilikuwa inatuagiza 2005 - 2010 kila kata iwe na sekondari moja. Kazi hiyo tumeifanya vizuri...tunazo sekondari 15.

Rais Kikwete, kushoto, akiwa na mgombea ubunge wa CCM kwa jimbo la Musoma Mjini, Vedasto Mathayo, kulia, kwenye mkutano wa jana 
Hakuna mtoto wa Musoma Mjini hata mmoja aliyefaulu akashindwa kwenda sekondari. Pale ambapo wazazi hawana uwezo, Serikali ya Chama cha Mapinduzi kila mwaka kwa  Musoma Mjini, inasomesha watoto zaidi ya 250 bure.

Aliendelea kutaja mafanikio kwenye ujenzi wa barabara, sekta ya afya, na maji. Alimuomba mgomea urais wa chama chake aweke nguvu katika ujenzi wa barabara.

Friday, September 24, 2010

Kisa cha kuacha kuvuta sigara: safari yangu ya kupanda Mlima Kilimanjaro (makala ya nne kati ya kumi)

Jumapili 17 Agosti 2008
Baada ya kuamua kuacha kupanda milima ya Upare niliendelea kujipa moyo kutokana na mawaidha ya Jose' akisema kuwa haina haja ya kuwa mkakamavu wa kiwango cha juu kabisa kuweza kukabili safari ya siku 7 hadi 8 ya kupanda Mlima Kilimanjaro kwa njia aliyoipendekeza, yaani Lemosho - Southern Circuit, Barafu, hadi kilele cha Uhuru. Njia hii ndefu inauandaa mwili kuzowea polepole hali ya kuwepo kwenye nyanda za juu na ndiyo njia yenye uhakika mkubwa zaidi ya kumwezesha mkweaji kufika kileleni.

Rafiki yangu Jose' ameshapanda Mlima Kilimanjaro mara 12 na angeungana nami mwaka huu kupanda tena mlima kwa mara ya kumi na tatu. Lakini kwa bahati mbaya aliumia kifundo cha mguu na hataweza kuja. Ameshawahi pia kukwea maeneo ya milima ya Himalaya hadi kufikia Mt. Everest Base Camp.

Aliniarifu kuwa Bw. Le Hu Dyuong, mhandisi mtaalam wa programu za kompyuta na raia wa Vietnam ataungana na mimi kupanda Kiliamnjaro. Le pia ameshawahi kufika Everest Base Camp na kabla ya kupanda Mlima Kilimanjaro alitoka kupanda Mlima Kenya. Le aliniomba niahirishe kuanza safari ya kupanda Kilimanjaro ili kutoa fursa kwake apumzike kwa siku chache baada ya kupanda Mlima Kenya. [Siku chache baada ya kupanda Kilimanjaro, alienda kupanda Mlima Meru]. Halafu akapumzika kwa majuma mawili na akaanza kufanya mipango ya kupanda Mlima Oldoinyo Lengai, lakini mipango haikukaa vizuri na hivyo hakuweza kupanda hiyo volkano.

Jumatatu 18 Agosti 2008
Asubuhi nilikutana na Le kwenye kituo cha basi cha mjini Moshi, akitokea Arusha. Tulifikia hoteli ya Springlands na wakati wa mlo wa mchana tulikaa meza moja na wanandoa raia wa Afrika ya Kusini waliohamia Manchester, Uingereza. Walituambia kuwa kupanda Kilimanjaro siyo mchezo, lakini ni jambo la manufaa. Walitushauri tujaribu kupitia Lava Tower tunapoelekea kileleni.

Jioni tulijumuika kwa ajili ya mkutano wa maandalizi na tukatambulishwa kwa jamaa mmoja mrefu mwembamba mwenye rasta ambaye ndiye kiongozi wetu wa msafara, anaitwa Pius. Alituarifu kuwa anajulikana pia kama "Yahoo" kwa wenzake.

Tulibishana naye kidogo alipotaka kushauri tupunguze siku za safari zilipendekezwa na Jose' na badala yake ziwe chache zaidi. Tulisisitiza kutumia muda ule ule tuliyopanga na hasa kulala kambi ya Barafu (kambi ya mwisho kabla ya safari ya kuelekea kileleni) ili kuiwezesha miili yetu kuzowea hali ya kuwa kwenye nyanda za juu na kuepuka athari ya upungufu wa oksijeni.

Nilimwambia Yahoo kuwa anaweza kuwa ana haraka ya kurudi Moshi ili aondoke na wageni wengine kueleka kileleni na kuweza kujiongezea kipato lakini, kwa bahati mbaya, alikuwa amepewa kazi ya kuongoza wakweaji wawili, mmoja asiye na uzoefu wa kutosha na mwingine ambaye alikuwa na uzoefu wa kutosha kuhusu ugonjwa wa nyanda za juu unaosababishwa na upungufu wa oksijeni na ambaye hakuwa tayari kuacha kuchukuwa tahadhari. Yahoo alikubali kwa shingo upande.

Baada ya kununua ramani ya Mlima Kilimanjaro kutoka dukani muuza duka alijaribu kuniuzia dawa ya mbu, lakini Le akamstukia na kupinga kuwepo kwa mbu kwenye Mlima Kilimanjaro. Watanzania tunatambua umahiri wa wakazi wa mkoa wa Kilimanjaro katika masuala ya kutafuta pesa. Kwa hakika, kama bado sikuwa natambua hilo, basi nilitambua leo kuwa ndugu zetu Wachaga walikuwa watu wenye ujuzi wa uuzaji usiyo wa kawaida.

Makala ijayo: Napiga hatua ya kwanza kuelekea kileleni

Bonyeza hapa kuisoma makala hii kwa Kiingereza

Makala zinazohusiana na hii: