Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Tuesday, March 21, 2017

Tanzania ni nchi nzuri sana

Tanzania ni nchi nzuri sana. Hakuna ubishi juu ya hoja hii.

Lakini inahitaji fursa ya kutoka sehemu moja na kuzunguka maeneo mbalimbali ya Tanzania ambayo yanavutia kwa mandhari na vivutio mbalimbali vya asili. Ukibaki sehemu moja tu huwezi kufahamu juu ya ukweli huu.

Kama huna hiyo fursa siyo kosa lako, lakini kama unayo fursa na uwezo basi huna budi kuzunguka na kuifahamu vyema nchi yako. Utalii wa ndani unajenga uchumi, na wale ambao tunao uwezo wa kutembelea maeneo ya Tanzania tunapaswa kuchangia kwa kadiri tunavyoweza.



Moja ya sehemu ambazo zinavutia nchini Tanzania ni maeneo yanayozunguka Ziwa Viktoria. Video hii imechukuliwa kwenye kivuko cha Busisi kwenye njia kuu inayotumika na wasafiri kati ya Mwanza na Geita, Chato, hadi Kagera.

Sunday, March 19, 2017

Unafahamu masuala haya 5 kuhusu Mwitongo?

Unafahamu masuala haya 5 kuhusu Mwitongo?

Mwitongo ni eneo la kijiji cha Butiama alipozaliwa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, rais wa kwanza wa Tanzania tarehe 13 Aprili 1922. Aidha, ni eneo alipozikwa tarehe 23 Novemba 1999.

Yafuatayo ni masuala matano ya Mwitongo ambayo pengine huyafahamu.

1. Ajali ya ndege
Mwaka 1978, baada ya majeshi ya Idi Amin Dada kiongozi wa kijeshi wa Uganda kuvamia eneo la mkoa wa Kagera, Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) lilianza kampeni ya kuondoa majeshi ya Idi Amin kwenye ardhi ya Tanzania.

Katika harakati za kujiandaa na vita hivyo, kikosi cha anga cha JWTZ kilihamisha baadhi ya ndege zake za kivita kutoka kituo cha Ngerengere na kuzipeleka kwenye uwanja wa ndege wa Mwanza.

Kwa sababu ya kasi ya hizo ndege, marubani wawili waliorusha hizo ndege walipitiliza Mwanza na kulazimika kuzunguka kuelekea upande wa kaskazini mashariki ili warudi tena kutua Mwanza. Uamuzi huo ukasababisha waruke juu ya anga ya mji wa Musoma.

Askari wa kikosi cha mizinga kilichokuwa kinalinda eneo la Musoma, kwa kukosa taarifa juu ya ndege hizo na kudhania kuwa ni ndege za adui, walizishambulia. Moja ya ndege hizo ilianguka Musoma, na nyingine iliangukia Mwitongo, kwenye msitu wa Muhunda.

Eneo la Mwitongo ilipoanguka ndege ya pili umejengwa mnara wa kumbukumbu.
Mnara wa kumbukumbu ya ajali ya ndege kwenye msitu wa Muhunda.
2. Msitu wa Muhunda
Msitu wa Muhunda ni sehemu ya eneo la Mwitongo. Ni msitu ambao, kwa mujibu wa mila na desturi za kabila la Wazanaki wa eneo la Butiama, ndiyo makazi ya mzimu wao, Muhunda. Msitu una ukubwa wa ekari 5.

Ni marufuku kukata miti iliyopo ndani ya msitu huo. Inaruhusiwa kukusanya kuni za matawi yaliyoanguka chini tu. Wazee wa kimila hufanya mitambiko ndani ya msitu huo.

Inaaminika kuwa mzimu huo hujibadilisha kuwa mojawapo ya viumbe vifuatavyo: nyani mkubwa, chui, mbuzi mkubwa, au nyoka mkubwa.

3. Mamba Mweusi (Black Mamba)
Mwinuko wa Mwitongo upo ndani ya eneo lililozungukwa na vichaka misitu, na majabali makubwa.

Ni eneo ambalo lina viumbe wadogo wadogo, pamoja na nyoka wa aina mbalimbali. Mojawapo wa nyoka hawa ni mamba mweusi.
Picha ya Mamba Mweusi. Jina lake la kisayansi ni Dendroaspis polylepis. Picha inatumika kwa idhini ya Creative Commons License. Taarifa kamili zipo hapa: http://creativecommons.org/licenses/by-sa/3.0/deed.en
Huyu ni moingoni mwa nyoka wenye sumu kali kabisa duniani, na inasemekana kuwa nyoka pekee ambaye hushambulia binadamu kwa makusudi, tofauti na aina nyingine ya nyoka ambao hushambulia tu wanapotishiwa usalama wao.

4. Ziwa Viktoria
Mwitongo ni eneo la mwinuko wa mita 1,405 juu ya usawa wa bahari. Kwa sababu ya mwinuko huo mtu anayesimama Mwitongo anaweza kuona kingo za Ziwa Viktoria zilizopo umbali wa kilomita 40 magharibi mwa Butiama.
Ziwa Viktoria.

5. Nelson Mandela
Rais wa kwanza wa Afrika Kusini, Nelson Mandela, alitembelea Mwitongo mwezi Novemba 1999. Alifika Mwitongo kuhani kifo cha Mwalimu Nyerere aliyefariki tarehe 14 Oktoba 1999.

Mzee Mandela aliandaliwa chumba maalum cha kulala wakati wa ziara yake. Kitanda maalum kiliwekwa kwenye chumba hicho. Hata hivyo, ratiba yake haikuruhusu kulala, na akaondoka siku hiyo hiyo kurudi Afrika Kusini. Kitanda kile hakijaondolewa kwenye chumba kile hadi hii leo.