Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Tuesday, July 29, 2014

Mwisho wa Tanzania siyo Kibaha

Kuna watumishi wengi katika sekta ya umma na ya binafsi ambao kwao Tanzania ni Dar es Salaam. Sisi tunaoishi bara hatuna tofauti na kuwa wakazi wa Kandahar nchini Afghanistan.

Nitatoa mifano. Jana nilitaka kukamilisha usajili wangu wa shahada mojawapo ya chuo kikuu kimojawapo cha Tanzania. Waliopitia zoezi hili wanafahamu kuwa maombi yote yanafanyika kwenye mtandao. Ukikwama wakati wa kujaza maombi zimetolewa namba za simu ambazo unaweza kupiga kupewa maelekezo. Nilikwama mapema kwa sababu nina stashahada ya nje ya nchi ambayo mchakato wa maombi hauitambui. Nilipiga simu hizo kwa muda mrefu lakini au hazipokelewi au haziko hewani.

Bahati nzuri nilipata namba nyingine ya Kamisheni ya Vyuo Vikuu (TCU) ambayo nilipiga na kuunganishwa na mama mmoja. Nilimueleza tatizo langu. Akaniambia kuwa TCU bado haijakamilisha tathmini ya shahada za nje na kwa hiyo nilipaswa kupeleka shahada yangu “ofisini” ili ihakikiwe.

Nilimwambia kuwa mimi niko Musoma. Akanijibu: “Sasa mimi nifanyeje?” Ilikuwa ni kama vile ananieleza: “Nani kakutuma kuishi bara?”

Sifahamu kama watu wanaopanga taratibu mbovu kama hizi wanatambua kuwa safari kutoka baadhi ya sehemu za Tanzania ni zaidi ya kilomita 1,000 hadi Dar es Salaam na inagharimu pesa. Hawa wanatoa majibu kama vile Watanzania wote milioni 45 wanaishi Dar. Naamini kuna makumi ya maelfu ya waombaji wa kusoma kwenye vyuo vikuu ambao hawako Dar. Kwanini inashindikana kuwepo mwakilishi wa Kanda ili mimi niliye Butiama nisilazimike, mathalani, kusafiri hadi Dar kuhakiki cheti changfu? Ingetosha kusafiri hadi Mwanza tu, ingawa wakati mwingine hata Mwanza pia naona ni mbali ambako ingewezekana kupanga muda maalumu wa kuonana na huyu mhakiki na gharama yake kujunuishwa kwenye gharama ya maombi. Ongezeko la gharama hii haitazidi gharama za kusafiri kwenda Dar.

Ukweli ni jukumu la serikali kuhakikisha kuwa raia wake wote wanapata huduma kwa haki na usawa ule ule. Ningekuwa na muda (na pesa) ningefungua kesi mahakamani kudai kukiukwa kwa haki zangu za msingi kama raia ambaye anastahili kupata huduma ile ile ya umma kama raia anayeishi Dar es Salaam.

Mfano mwingine, na hapa nasisitiza kwa nini nimesema kuwa hata Mwanza ni mbali, unahusu kampuni za simu. Kuna aina nyingi za matatizo ambayo yanaweza kumalizwa kwenye simu, lakini baadhi ya watoa huduma za kampuni za simu watakwambia unapaswa kwenda kwenye ofisi zao ili kutatua shida fulani.

Nagombana mara kadhaa na watoa huduma wa kampuni ya simu ya Voda. Watoa huduma wa Voda wanayo sentensi wanayopenda sana kutumia kumaliza tatizo: “Nenda Voda Shop.” Mimi kwenda Voda shop iliyo karibu ni kilomita 80 (kwenda na kurudi). Mimi nilifikiri maana ya kuwa na simu ni kupunguza ulazima wa kufunga safari zisizo za lazima, na kuongeza ufanisi katika kazi. Ukiniambia niende Voda Shop napoteza siku nzima ya kazi bila sababu ya msingi.

Halafu siku ukitoa takwimu kuwa una wateja milioni 10 na mimi pia utanihesbau katika usawa ule ule na mteja wa Dar es Salaam wakati mimi nalazimika kulipia gharama za ziada ili kutumia huduma yako?

Nasema haya siyo kwa kukosoa tu bila sababu ila kwa kutoa hoja kuwa kuna baadhi ya taratibu zinapaswa kupitiwa upya ili kutoa huduma sawa kwa mteja wa Butiama kama ambavyo anafaidika mteja wa Dar. Kuna ukweli kuwa foleni za Dar zinaweza kusababisha hata mkazi wa Dar kuona kuwa safari ya kwenda Voda Shop badi ni kero kwake. Kama hii ni kweli, basi hata yeye ana haki ya kulalamika.

Teknolojia ina manufaa ni na ingerahisisha sana shughuli za utawala na biashara nchini lakini bado ziko hitilafu nyingi za kurekebisha. La msingi ni kuwa Tanzania ni nchi kubwa na inahitaji mtazamo huo mpana kupanga mipango ya kuhudumia raia na wateja.

Saturday, July 26, 2014

Mada yangu ya leo: siyo kila aliye chumbani amelala usingizi

Siyo kweli kuwa kila aliye chumbani amelala usingizi. Nitafafanua.

Ninapokuwa kijijini Butiama sehemu kubwa ya kazi yangu inahusu kutangaza kijiji hiki kama kivutio cha utalii wa kihistoria na kiutamaduni. Nafanya kazi hiyo kwa taarifa ninazoweka mtandaoni na kwa mawasiliano ya moja kwa moja (kwa simu na barua pepe) na wale wanaopanga safari za kutembelea Butiama.Vitendea kazi vyangu ni kompyuta ambayo ninayo chumbani kwangu, na simu. Chumba changu ni ofisi yangu. Mimi nikisema naenda ofisini inanichukua chini ya dakika moja kufika kazini, kwa sababu ni safari ya kutoka kitandani kwangu mpaka kwenye meza yenye kompyuta.

Nafahamu wataalamu wanasema zipo athari za kuweka ofisi nyumbani lakini hiyo siyo mada yangu ya leo. Ninachosisitiza sasa ni kuwa mabadiliko ya teknolojia yamerahisisha kuhama na ofisi sehemu yoyote tunayotaka. Kompyuta na simu zimepunguza ulazima wa aina fulani za wafanyakazi kuwepo ndani ya jengo mahususi ili kutekeleza majukumu yao.
Ofisini kwangu.
Kwa bahati mbaya mabadiliko haya ya teknolojia hayako wazi kwa kila mtu. Kwa wengi kazi halisi ni inayofanyika katika sehemu mahususi, mathalani shambani, kiwandani, au ofisini, na kwa kijijini inaonekana kuwa ni kazi iwapo tu inamtoa mtu jasho.

Ukijifungia chumbani (kwangu ni ofisini) kuanzia asubuhi mpaka jioni unadhaniwa kuwa umelala usingizi. Kuna siku nilisikia mgeni anaambiwa kuwa nimelala na nikalazimika kutoka ndani kumkaribisha chumbani aliyetamka maneno hayo na kumuonyesha kuwa chumbani kwangu ni ofisini kwangu.

Kama nilvyosema siyo kila aliyekuwa chumbani amelala usingizi.

Wednesday, July 16, 2014

Tujisahihishe

Watanzania tuna sifa ya kuwa waoga sana kuwasahihisha wenzetu wanapokosea. Naomba kuwa tofauti kwa leo. Na ni kwa nia nzuri tu.

Kombe la Dunia la FIFA limeisha hivi karibuni na nilisikia (kwenye redio na runinga) na kuona kwenye maandishi, haswa kwenye mitandao ya jamii, matumizi yasiyo sahihi ya majina ya baadhi ya timu zilizoshiriki kwenye mashindano hayo.

"Ujerumani" iliandikwa "Ujeruman." Na kwa Kiingereza badala ya kuandika "Germany", baadhi ya watu waliandika "German." Tatizo hili la matumizi ya lugha lisichukuliwe kuwa ni kwa lugha au majina ya kigeni pekee. Jana nikiwa kwenye ndege nilisikia mfanyakazi wa ndani ya ndege akitutangazia abiria kuwa "tumetua kwenye uwanja wa ndege wa kimataifa wa Julius Nyerele." Huyo ni Mtanzania anashindwa kutamka "Nyerere." Na haikuwa mara yangu ya kwanza kusikia "Nyerere" kuitwa Nyerele." Kama ungeondoa muktadha ungefikiri alikuwa anazungumzia nyenyere.

Lakini jambo la kushangaza zaidi ni kuwa baada ya kutamka hivyo alianza kuongea kwa Kiingereza kutoa taarifa hiyo hiyo kwa abiria tuliokuwa ndani ya ndege, lakini alipoongea kwa Kiingereza alitamka "Nyerere" kwa usahihi.
Nilipanda ndege ya shiriki hili. Safari ilikuwa nzuri, lakini lugha ilikuwa na walakini.
Hii mifano inaashiria matatizo mawili. Kwa mfano wa kwanza ni kutojuwa matumizi sahihi ya majina au lugha ("Germany" ni nchi; "German" ni Mjerumani) au kutojali kuwa makini tunatamkaje majina au maneno (huyo huyo aliyetamka "Nyerele" anatamka "Nyerere" baada ya sekunde chache).

Nawasilisha hoja.

Sunday, July 13, 2014

Wakati mwingine picha zinadanganya

Hii (chini) ni picha ya eneo la Dar es Salaam, katika makutano ya barabara ya Bibi Titi na Mtaa wa Zanaki, ambalo kwa miaka mingi nimekuwa napita kwa mguu na ni eneo ambalo limebadilika sana katika kipindi hicho cha karibia miaka 30. 

Kushoto mwa picha hii (hapaonekani) kuna jengo kubwa lenye ofisi na maduka kwenye ghorofa za chini na nyumba za kuishi kwenye ghorofa za juu. Ni sehemu ambayo zamani waliishi Watanzania wa jamii ya Kiasia . Jengo lililojengwa hapo lilibadilisha kabisa taswira ya eneo hilo na liliongeza idadi ya majengo mapya ambayo yanachipuka Dar es Salaam kila kukicha. Majengo mengi ya zamani na ya kihistoria yanaendelea kubomolewa.


Lakini pamoja na mabadiliko makubwa yanayoendelea kutokea kwenye baadhi ya maeneo ya Dar es Salaam ninahisi kuwa picha hii haiakisi ukweli wa hali ilivyo katika eneo hilo. Ukweli ni kuwa picha hii inapamba zaidi hali halisi.

Nimeshapita kwenye eneo hili mara mia kadhaa lakini sijaona hali hiyo nzuri ambayo naiona kwenye picha hii. Kwa hakika teknolojia ya kamera imefanikiwa kupamba ukweli kwa sifa bandia.

Saturday, July 12, 2014

Wageni wa Butiama: Urmila Jhaveri

Ni Watanzania wachache wa kizazi kipya wanatambua mchango wa baadhi ya Watanzania wenye asili ya Kiasia kwenye harakati za kudai uhuru wa Tanganyika. Mmoja wa wanaharakati hawa ni Urmila Jhaveri ambaye hivi karibuni alitembelea Butiama.
Mama Urmila Jhaveri akiwa Butiama kwenye Makumbusho ya Mwalimu J.K. Nyerere. 
Mama Jhaveri, mwenye umri wa miaka 83 na ambaye alizaliwa kwenye kisiwa cha Pemba, ni mjane wa Kantilal Jhaveri aliyekuwa miongoni mwa wanasheria watatu wa upande wa utetezi kwenye kesi ya kashfa ya jinai ya mwaka 1958 iliyomkabili Mwalimu Julius Kambarage Nyerere wakati wa harakati za kudai uhuru iliyofunguliwa dhidi yake na serikali ya kikoloni ya Uingereza. Kantilal Jhaveri alifariki nchini India Januari 2014.

Wakati wa kudai uhuru wakati mume wake akiwa mmoja wa viongozi wa chama cha Waasia, Indian Association, kilichoshirikiana na kuunga mkono sera za Tanganyika African National Union (TANU), Urmila alishiriki kwenye harakati hizo akiwa mwanachama wa kitengo cha wanawake cha TANU ambacho kilijulikana kama TANU Women's Section.

Hivi karibuni amechapisha kitabu juu ya maisha yake kiitwacho Dancing with Destiny ambacho atakizindua tarehe 19 Julai  2014 jijini Dar es Salaam.

Itakuwa fursa nzuri kwa wote kukumbuka mchango muhimu wa makundi mbali mbali ya Watanzania kwenye harakati za kudai uhuru.