Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Friday, December 28, 2012

Lugha yetu Kiswahili: Kamusi ya Kiswahili kwenye mtandao

Hivi karibuni nililazimika kutafuta maana ya Kiswahili ya neno la Kiingereza dilemma na tafsiri iliyopo kwenye Kamusi ya Kiingereza - Kiswahili iliyochapishwa na Taasisi ya Uchunguzi wa Kiswahili (TUKI) ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, tole la 2006, imetoa neno "mtanziko."

Lakini TUKI hao hao kwenye Kamusi yao ya Kiswahili - Kiingereza, toleo la 2001, hawajatoa maana ya neno hilo kwa lugha ya Kiingereza. Inawezekana kuna toleo lijalo ambalo litaweka maana ya "mtanziko" kwa lugha ya Kiingereza.
Hali kadhalika toleo la mwaka 2004 la Kamusi ya Kiswahili Sanifu iliyochapishwa na Oxford University Press nalo halina neno hilo.

Nilifanya utafiti kidogo kwenye mtandao na kugundua wavuti inayoitwa The Kamusi Project ambayo inayo kamusi ya Kiingereza - Kiswahili - Kiingereza inayoruhusu watumiaji kutafuta maana ya maneno na inaruhusu pia hata mtumiaji kuongeza maneno ambayo hayapo kwenye kamusi hiyo. Nyongeza ya maneno hupitiwa na mtaalamu na inapoonekana ni sahihi basi inaorodheshwa rasmi kwa matumizi na watumiaji wengine.

Tuesday, December 25, 2012

Mkutano wangu na Jaffar Idi Amin

Taarifa ifuatayo ni ya siku nyingi kidogo, na awali niliitoa kwenye blogu yangu ya lugha ya Kiingereza From Butiama and Beyond tarehe 15 Mei 2009. Nairudia hapa katika mfululizo wa taarifa ambazo niliwahi kuzitoa kwenye From Butiama and Beyond na ambazo naamini wasomanji wangependa kuzirudia kusoma na vilevile kutoa fursa kwa wale ambao bado hawajazisoma kuweza kutafakari niliyoyaandika wakati huo.
***************************************
Mapema mwezi Aprili mimi pamoja na Shirika la Utangazaji la Uingereza (BBC) tulikuwa wenyeji kijijini Butiama wa Jaffar Amin, mmojawapo wa watoto wa kiume wa zaidi ya watoto 50 wa kiongozi wa zamani wa Uganda Idi Amin Dada.

Nakiri kuwa kabla ya ujio wake nilijikuta kwenye mtanziko mkubwa ambao ulinifanya nisite kwa muda kuendelea kuandikia kwenye blogu yangu. Sikuwa na hakika wasomaji wangu wangechukuliaje mkutano wangu na Jaffar. Unapotamka tu 'Idi Amin' basi siku zote utaibua hisia kali, na mimi niligundua hizo hisia zilikinzana na sababu nilizoona zinaafikiana na uamuzi wangu wa kukubali wazo la BBC la kuonana na Jaffar.
Karibu Butiama: Jaffar Amin (kushoto), pamoja na mimi tukiwa Butiama ndani ya nyumba ambayo Mwalimu Nyerere alijengewa na Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) baada ya kumalizika kwa vita kati ya Uganda na Tanzania.
 Nilieleza sababu zangu kwenye makala niliyoandika kwenye safu yangu iitwayo Letter from Butiama. Kwa kifupi niliwjenga hoja kuwa matukio ya kale tuyaache yabakie ya kale na umuhimu wa matukio hayo unajitokeza pale tu ambapo tunahitaji kijufunza jambo kutokana na matukio yaliyopita ili tusirudie makosa ya zamani. Matukio yaliyopita yasitumike kama rungu la kuwapiga wale wa sasa ambao hawahusiki kabisa na matukio ya zamani.

Mkutano wetu na Jaffar ulijikita kwenye wazo la BBC la kuadhimisha, kwa kupitia vipindi kadhaa vya redio vilivyorushwa mwezi Aprili, kumbukumbu ya miaka 30 ya vita vya Kagera, vita kati ya Uganda na Tanzania vya 1979 - 1980. Solomon Mugera, mkuu wa Idara ya Kiswahili ya BBC, alieleza kuwa awali wazo lilikuwa mkutano wetu ufanyike Nairobi. Alibainisha ni Jaffar aliyependekeza kuwa mkutano uhamishiwe Butiama, badala ya Nairobi.

Kwa hiyo katikati ya mwezi Machi nlijiandaa kuonana na Jaffar jijini Nairobi lakini nikafahamu mwishoni kabisa kuwa mkutano ulihamishiwa Butiama pasipo kufahamishwa mapema hayo mabadiliko. Ninahisi kuwa BBC waliendelea na mipango ya kukutana Butiama bila kunifahamisha kwa kuhofu kuwa ningakataa wazo lao.

Nilipata shida kubwa sana kuorodhesha waalikwa. Ilikuwa rahisi kuamua nani kati ya marafiki zangu kuwaalika. Baadhi yao walinirahisishia kazi kwa kuniomba niwaalike. Orodha ngumu ilikuwa ile ya viongozi wa serikali wa mkoa. Sikuwa na hakika iwapo wangehudhuria ingawa hutembelea Butiama mara kwa mara. Niliwatumia mialiko na baadhi yao walihudhuria mkutano ule pamoja na Jaffar.

Mwisho wa yote inaelekea kuwa wale waliofuatilia matangazo ya maadhimisho yaliyorushwa na BBC pamoja na mkutano na Jaffar walibaki na maoni chanya tu kuhusu mkutano wangu na Jaffar. Mtoa maoni mmoja alipendekeza kuwa mtu aliyeibua wazo la kuwakutanisha watoto wa Idi Amin na Julius Nyerere alipaswa kupendekezwa kupokea Tuzo ya Amani ya Nobel.
Solomon Mugera wa BBC akihutubia waalikwa.
Ni matumaini yangu kuwa siku Solomon Mugera atakapoinuka akiwa amevalia vazi rasmi kupokea Tuzo ya Amani ya Nobel mjini Oslo (pamoja na kupokea hundi ya dola milioni moja) basi atakumbuka kuniorodhesha mimi pia kwenye orodha yake ya waalikwa.w

Monday, December 24, 2012

Kuzima simu ndani ya benki ni usumbufu tu

Ukiingia benki nyingi za Tanzania utakutana na tangazo linalozuwia kutumia simu ukiwa ndani ya benki na inawezekana kuambiwa kuzima simu yako ya kiganjani ukijaribu kuitumia.

Sijaelewa mantiki ya kanuni hii. Naamini kuwa wenye mabenki wana hofu kuwa mtu mwenye kusudio la kutenda uhalifu ndani ya benki anaweza kutumia simu kurahisisha uhalifu huo. Na hii inawezekana kuwa ni kweli lakini mtu aliyekusudia kufanya uhalifu atafanya hivyo katika mazingira yoyote yale.

Hapa inaleta maana kuwa jambazi asiye na simu hawezi kutenda uhalifu. Nimewahi kumueleza mfanyakazi wa benki aliyenizuwia nisiongee na simu kuwa kuna wahalifu wengi wapo nje ya nchi ambao wanaibia mabenki kwa njia ya mtandao. Wao wameambiwa nao wazime kompyuta zao? Na yule askari mwenye silaha ambaye yuko nje ya benki kazi yake nini? Kuelekeza wateja kuegesha magari tu na kutumia mashine za ATM?

Mimi imenitokea mara kadhaa simu yangu kuita nikiwa ndani ya benki lakini mara zote hujitahidi kumaliza mazungumzo haraka ili nimalize yaliyonipeleka benki kwanza halafu ndiyo, kwa wakati wangu, nimtafute huyo aliyenipigia kumalizia mazungumzo iwapo hayakuisha.

Ingeleta maana zaidi kwa wenye mabenki kusema kuwa mteja anapoingia benki amalize yaliyompeleka benki kwanza halafu ndiyo aanze kuongea na simu kwa sababu mshika mawili moja humponyoka, lakini hoja kuwa mtu siye na simu hawezi kufanya ujambazi haina uzito wowote.

Saturday, December 22, 2012

Dk. Antipas Massawe anasema Muungano umepitwa na wakati (sehemu ya pili kati ya sehemu mbili)

Katika awamu hii ya pili ya makala yake, Dk. Antipas Massawe anaendeleza na kuhitimisha hoja kuwa Muungano wa Tanganyika na Zanzibar umepitwa na wakati. Ni mawazo yake, si yangu.
*************************************
Muungano wa Tanzania umepitwa na wakati demokrasia ya vyama vingi ilipozaliwa (sehemu ya pili kati ya sehemu mbili).

Na Dk. Antipas Massawe

(inaendelea)

Kwa sehemu ya kwanza ya makala hii soma hapa:



Athari ya tatu kubwa itarajiwe kujitokeza pia pale ambapo muundo wa muungano unaojumuisha serikali mbili (ya Zanzibar na ya Muungano kati ya Zanzibar na Tanganyika) utakapokataliwa kama mfano wa kuigwa na hivyo kuwa hata kikwazo kwenye ujenzi wa Shirikisho la Afrika ya Mashariki na muungano wa  Bara la Afrika unaoshirikisha Zanzibar na Tanganyika. Muundo wa muungano kati ya Zanzibar na Tanganyika ilibidi uwe ni ule unaotarajiwa utakubalika kama mfano wa kuigwa na wengine wote kama msingi kwenye ujenzi wa Shirikisho la Afrika ya Mashariki na hatimaye muungano wa Bara la Afrika tarajiwa. 

Vinginevyo huu muungano wa Zanzibar na Tanganyika ulioundwa kwa mfumo wa serikali mbili (ya Zanzibar na ya Muungano kati ya Zanzibar na Tanganyika) utaishia kuwa kikwazo kwa ushiriki wake kamilifu na wenye manufaa makubwa ndani ya Shirikisho la Afrika ya Mashariki  na muungano wa Bara la Afrika tarajiwa.

Mfumo wa serikali moja ya Muungano ni mzuri kwani ndio wenye gharama ndogo lakini kwa Wazanzibari ambao karibu wote ni Waisilamu na Wabara ambao karibu wote ni mchanganyiko wa Waisilamu na Wakristu mfumo huu bado sio mzuri kwani utatujengea agenda za udini ndani ya demokrasia yetu ya vyama vingi na matokeo yake ni pande zote za Muungano zikijikuta kulazimishiwa serikali dhaifu na kunyimwa ile imara na kuandamwa na chuki na migogoro ya kidini kama illivyoshuhudiwa huko Zanzibar hivi karibuni. 

Mfumo huu pia sio mzuri kwani kila pande ndani ya Muungano utashindwa kubuni na kuendeleza fursa zake nyingi muhimu kwa maendeleo yake binafsi ambazo hazitaonekana muhimu katika ngazi ya Muungano. Nadhani hili ni mojawapo ya yaliyopelekea muungano wa nchi za Kisovieti kusambaratika. Ni sababu hii inaoufanya mfumo huu wa serikali moja ya Muungano kutoweza kuwa msingi mzuri wa kuigwa kwenye ujenzi wa Shirikisho la Afrika ya Mashariki na muungano wa Bara la Afrika tarajiwa.

Mifumo ya serikali mbili kwenye muungano (ya Zanzibar na ya Muungano) na mbili (ya Tanganyika na ya Muungano) sio mizuri kwa Wazanzibari ambao karibu wote ni Waisilamu na Wabara ambao karibu wote ni mchanganyiko wa Waisilamu na Wakristu kwani katika mazingira kama hayo utakuwa ukitujengea agenda za udini ndani ya demokrasia yetu ya vyama vingi na kutuletea athari zake mbaya. Mfumo huu pia sio mzuri kwani hakuna sababu zozote za msingi na zinazokubalika na pande zote mbili husika ndani ya Muungano pale ambapo upande mmoja ukiruhusiwa kuendelea kuwa na serikali yake binafsi na upande mwingine ukinyimwa fursa kama hiyo. Ni sababu hii inaoyoifanya mifumo hii ya serikali mbili za muungano kutoweza kuwa misingi mizuri ya kuigwa kwenye ujenzi wa Shirikisho la Afrika ya Mashariki na muungano wa Bara la Afrika tarajiwa.

Mfumo wa serikali tatu kwenye muungano (ya Zanzibar, ya Tanganyika na ya Muungano) sio nzuri kwani haitakuwa rahisi kujenga hoja za msingi kudhihirisha manufaa  ya kuwa na serikali ya tatu ya Muungano yenye gharama kubwa kati ya Zanzibar ambayo ni kisiwa kidogo sana ndani ya bahari ya Hindi na Tanganyika ambayo ni nchi kubwa sana ndani ya Bara la Afrika. Hata hivyo mfumo huu wa kila mhusika ndani ya Muunngano kuendelea kuwa na serikali yake ndani ya serikali ya muungano unaonekana ndio mfumo mzuri wa kuigwa kwenye ujenzi wa Shirikisho la Afrika ya Mashariki na muungano wa Bara la Afrika tarajiwa kwani kutokana na wingi wa mataifa shiriki ndani ya muungano, ajenda za udini zitakosa fursa ya kujijenga na kukua ndani yake na kila taifa shiriki na serikali yake litaendelea kuwa na fursa ya kubuni na kuendeleza zile ajenda na sera zake binafsi za maendeleo ambazo hazionekani muhimu katika ngazi ya serikali ya muungano.

Mfumo wa serikali mbili (ya Zanzibar na ya Tanganyika bila ya muungano) inaonekana ndiyo  unaofaa kuzijengea Zanzibar na Tanganyika uhusiano na ushirikiano mzuri na endelevu na uliojengeka kwenye misingi imara, urafiki na ushirikiano wa kibiashara baina ya mataifa mawili huru na jirani. Mfumo huu wa serikali mbili bila ya muungano utazipa pande zote mbili husika fursa nzuri kwa kila moja kushiriki kikamilifu kwenye mchakato mzima wa ujenzi wa Shirikisho la Afrika ya Mashariki na muungano wa Bara la Afrika tarajiwa ikizingatia maslahi yake binafsi na ya wote kwa ujumla.

Muungano wa Zanzibar na Tanganyika unaohusisha mfumo wa serikali mbili (ya Zanzibar na ya muungano kati ya Zanzibar na Tanganyika) umepitwa na wakati pale ilipozaliwa demokrasia ya vyama vingi na ni budi ujadiliwe upya kwa kina na mapana kuendana na nyakati tulizo nazo na mazingara ya demokrasia ya vyama vingi tuliyo nayo hivi sasa ili athari na faida zake ziweze kuonekana bayana na kuwawezesha Wazanzibari  na Wabara wengi kuweza kuamua ni mfumo upi wa ushirikiano unaowafaa kuendelea nao badala ya huu uliopitwa na wakati.

Makala inayohusiana na hii hapa:
Sehemu ya kwanza ya makala hii:
http://muhunda.blogspot.com/2012/12/dk-antipas-massawe-anasema-muungano.html
Makala nyingine juu ya Muungano:
http://muhunda.blogspot.com/2012/08/mada-yangu-ya-leo-muungano-una-manufaa_24.html

Friday, December 21, 2012

Dk. Antipas Massawe anasema Muungano umepitwa na wakati (sehemu ya kwanza kati ya sehemu mbili)


Katika makala hii ambayo nitaitoa hapa kwa awamu mbili, Dk. Antipas Massawe anatoa hoja kuwa Muungano wa Tanganyika na Zanzibar umepitwa na wakati. Ni mawazo yake, si yangu.
*************************************
Muungano wa Tanzania umepitwa na wakati demokrasia ya vyama vingi ilipozaliwa (Sehemu ya Kwanza kati ya sehemu mbili).

Na Dk. Antipas Massawe

Muungano wa kisiasa kati ya Tanganyika na Zanzibar ulizaliwa tarehe 26 April, 1964. Sababu kubwa iliyopelekea kuzaliwa kwake ni moyo waliokuwa nao waasisi wake (Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na Sheikh Abeid Amani Karume) wa kuunda muungano wa kisiasa baina ya nchi huru za Bara la Afrika wakianzia na shirikisho la Afrika ya Mashariki. Lengo lilikuwa kulinda na kudumisha mapinduzi ya Zanzibar ya tarehe 12 Januari, 1964 dhidi ya utawala wa wachache wa kisultani ulioondolewa madarakani na kuanzisha ujenzi wa shirikisho la Afrika ya Mashariki na muungano wa Bara la Afrika kisiasa.

Kuzaliwa kwa muungano wa Tanganyika na Zanzibar kulitokana na matakwa binafsi ya waasisi wake na wananchi wa kawaida kutoka pande mbili husika hawakushirikishwa kikamilifu katika zoezi zima la kufanya maamuzi kuhusu kuundwa kwake na haionekani mahali popote upembuzi yakinifu ulifanyika kubaini faida na athari za muungano wenyewe kwa wahusika (ukijumuisha mifumo ya serikali zake zote mbadala: moja (ya Muungano), mbili (ya Zanzibar na ya Muungano), tatu (ya Tanganyika na ya Muungano), nne (ya Zanzibar, ya Tanganyika na ya Muungano) na tano (ya Zanzibar na ya Tanganyika bila ya Muunngano). Kwa kifupi muungano wa Zanzibar na Tanganyika ulizaliwa wakati wa kipindi cha udikteta wa chama kimoja tawala ndani ya pande zote mbili husika kwenye Muungano.

Muungano wa Zanzibar na Tanganyika ni wa pekee na haujawahi kuigwa na wengine mahali popote duniani na umedumu chini ya utwala wa mfumo wa udikteta wa chama kimoja na sasa uko chini ya utawala wa demokrasia ya mfumo wa vyama vingi.

Athari  kubwa kutokana na Muungano hazikuweza kuonekana kwenye kipindi chake cha  awamu ya kwanza chini ya mfumo wa udikteta wa chama kimoja kwani kwenye kipindi hiki chama tawala ndicho kimekuwa kikiamua yote kuhusu maswala ya Muungano kitaifa na jukumu la wengine wote kutoka bara na visiwani lilikuwa ni kubariki maamuzi hayo ya chama kimoja tawala. Kwa mfano, chama kimoja tawala kikishaamua huyu ndiye atakaeyekuwa rais wa Muungano, basi jukumu la wengine wote kutoka pande mbili za Muungano limekuwa ni kupiga kura moja ya ndio kuashiria kubariki kwao chaguo la chama hicho kimoja tawala.

Kwa hiyo kutokuwepo upinzani kutoka vyama vingine vya siasa dhidi ya udikteta wa chama kimoja tawala kuhusu maswala ya Muungano na rais mteule wa chama tawala kutokuwa na ushindani wa wagombea kutoka vyama vya upinzani imekuwa ndiyo sababu ya athari kubwa tarajiwa kushindwa kujitokeza kutokana na utekelezaji wa Muungano huu baina ya Wazanzibari (ambao karibu wote ni Waisilamu) na Wabara (ambao karibu wote ni mchanganyiko wa Waisilamu na Wakristu) na fursa iliyopewa Zanzibar ya kuendelea kuwa na serkali yake ya Zanzibar wakati Tanganyika ikinyimwa fursa kama hiyo ya kuendelea kuwa na serikali yake ya Tanganyika bila sababu zozote za msingi.

Athari ya kwanza kubwa kutokana na huu Muungano wa kisiasa baina ya Wazanzibari na Wabara inatarajiwa kujitokeza kwa nguvu kwenye kipindi chake cha awamu ya pili chini ya mfumo wa demokrasia ya vyama vingi. Kwa mfano itakapojitokeza kwamba miongoni mwa wagombea wa kiti cha urais mmoja ni Mkristu na mwingine ni Mwisilamu basi itarajiwe kwamba karibu Wazanzibari wote ambao ni Waisilamu watajitokeza na kumpigia mgombea Muislamu kura ya ndio bila kuzingatia vigezo vingine vya ubora. Athari ni kwamba Muungano huu utakuwa unatujengea ubinafsi unaoambatana na agenda zenye lengo la kutujengea na kutuimarishia udini ndani ya demokrasia ya vyama vingi na matokeo yake ni Muungano kunyimwa utawala bora pale matakwa ya udini yatakapotawala chaguzi kuu za uongozi ndani ya Muungano na chuki za kidini na migogoro yake na athari zake kuanza kujitokeza  kama ilivyoshuhudiwa huko Zanzibar hivi karibuni.

Athari ya pili kubwa kutokana na huu Muungano uliowapa Wanzanzibari fursa ya kuendelea kuwa na serikali yao ya Zanzibar wakati Wabara wakinyimwa fursa kama hiyo ya kuendelea kuwa na serikali yao ya Tanganyika itarajiwe pia kujitokeza kwenye awamu yake ya pili chini ya mfumo wa demokrasia ya vyama vingi kwani sio haki Wazanzibari kufaidi kushiriki ndani ya serikali ya Tanganyika na bunge lake kupitia serikali ya Muungano na bunge lake wakati Wabara hawana fursa kama hiyo kutokana na kutoshirikishwa ndani ya serikali ya Zanzibar na bunge lake na uwezekano mkubwa wa mgongano wa maamuzi na utekelezaji wa sera za serikali ile ya Zanzibar na za ile ya Muungano.

(itaendelea...)

Ushauri wa bure kuhusu uendeshaji wa gari

Hii makala ni tafsiri ya makala yangu ya Kiingereza ambayo ilichapishwa tarehe 1 Mei 2005 kwenye makala zangu "Letter from Butiama" nilizoandika kwenye gazeti la Daily News kati ya mwaka 2005 na 20011.
*************************************************
Ikiwa habari za siasa na hususan mkutano wa wiki ijayo wa uteuzi wa mgombea urais wa Chama cha Mapinduzi kushamiri kwenye kinywa cha kila mtu mimi nageukia mada ambayo haihusiani kabisa na siasa, uendeshaji gari. Huu ni ushauri ambao unaweza kuutumia kukuwezesha kuendesha gari kwa usalama zaidi na kukuepusha na hali za kushtukiza, hasa pale unapokuwa kwenye masafa marefu.

Huu siyo ushauri wa juu juu kama ule wa kukutaka ukague maji ya rejeta kabla hujaanza safari. Ni ushauri ambao pengine hutafundishwa kwenye vyuo vya udereva. Huu ushauri unatolewa na mtu ambaye ameendesha gari kwa karibia miaka 25 akiwa na ajali moja tu ndogo.

Bado sijakutana na dereva ambaye anakiri kuwa yeye ni dereva asiye wa viwango. Kwa hiyo kanuni ya kwanza ya uendeshaji gari ni: kabla hata hujawasha gari ni muhimu kujiamini; usipojiamini hakuna mtu mwingine atakayekuamini. Jichukulie kama ni mwendeshaji bora kuliko wote duniani; kile unachopungukiwa utakipata kutokana na uzoefu. Lakini usichukulie huu ushauri kwa maana yake halisi, yaani neno kwa neno kwa sababu pamoja na kuwa unajiamini bado utahitaji mafunzo ya msingi ya udereva, pamoja na kuwepo ukweli kuwa kuna watu ambao wameweza kujifunza kuendesha gari baada ya kupata leseni zao.

Kanuni ya pili ni usitoe lifti kwa watu usiowafahamu, hasa wanaume. Kuna wanaume wengi zaidi wenye makusudio ya kutenda uhalifu kuliko wanawake wenye tabia za aina hiyo. Matokeo ya tafiti ulimwenguni yanaonyesha kuwa kuna wanaume wengi zaidi wanaokutwa na hatia za jinai zaidi ya wanawake. Kwa Uingereza kwa mwaka 1984 idadi ilikuwa 86%. Kama moyo wako unakutuma kuwasaidia wenye shida nashauri utoe lifti kwa wanawake tu, lakini kuwa mwangalifu na warembo. Mara nyingine, nyuma ya mwanamke mrembo anayeomba lifti hujificha mwanaume mwenye sura mbaya mwenye nia mbaya.

Ni maoni yangu kuwa mtu ambaye ni salama kabisa kumsaidia ni mwanamke mzee. Au bora zaidi, mwanamke mwenye watoto. Yumkini kuwa hata mwanamke mwenye kusudio la kutenda kosa la jinai atawaacha watoto wake nyumbani kabla ya kujaribu kuteka nyara gari.


Kanuni ya tatu: epuka kusimamisha gari kusaidia mtu ambaye anaonekana kama amejeruhiwa na umemkuta kalala barabarani. Mwezi Novemba mwaka jana, nikiwa safarini kutoka Mwanza kwenda Dodoma, nilikuta kizuizi barabarani usiku na mtu mmoja ambaye alikuwa amevaa kiraia alijitokeza akiwa na silaha ya kijeshi. Nilihisi kuwa na polisi kwa sababu hakuelekeza silaha dhidi yangu kudai nimpe pesa. Kabla sijaondoka alinitahadharisha kuwa kilomita 40 zilizobaki kuelekea Dodoma lilikuwa ni eneo la hatari na akaniuliza, "Unafahamu kanuni za kuendesha gari usiku?"

Nilimuuliza: "Kwa mfano?"
Akasema: "Kwa mfano, ukikuta mtu kalala barabarani utafanya nini?
Nikamwambia: "Nitamkwepa halafu nitarudi kesho asubuhi kuangalia kama bado yuko pale."
Akaniambia: "Endelea na safari. Unafahamu kanuni za uendeshaji usiku."

Kanuni ya nne: Endesha kwa kasi kubwa unayataka ukiwa mwenyewe. Unayo haki ya kusitisha maisha yako kama hiyo inakupendezesha lakini pindi unapokuwa na abiria kwenye gari yako basi onyesha staha kidogo kwa hulka ya kila mwanadamu ya kutaka kuishi milele. Nilivunja hiyo kanuni mara moja na sikujuta kufanya hivyo. Niliendesha gari toka Songea hadi Dar es Salaam nikiwa na abiria kwa mwendo wa kasi wakati wa ile safari. Tulipofika nusu ya safari tulifika tulisimama kwenye milima ya Kitonga kwa dakika chache kununua mahindi ya kuchoma njiani. Dakika 20 kabla ya kufika hapo tulikuwa tumepita mabasi mawili ya abiria ambayo yalipofika eneo lile lile (wakati sisi tulikuwa tumeshaondoka) yalivamiwa na majambazi yenye silaha ambayo yalimjeruhi kwa risasi aliyefika kwenye eneo wakati tukio la utekaji linaendelea.

Siku iliyofuata tuliposikia habari za lile tukio la ujambazi tuliafikiana kuwa jambo lililonisukuma niendeshe gari kwa kasi kubwa lilituokoa kuwepo kwenye shambulio lile la ujambazi.


Ni bora pengine kuongezea kuwa, wakati mwingine, uendeshaji wa kasi unaweza kutumika kuepukana na hali ya hatari (nakumbuka hii kanuni kutoka kwenye mafunzo yangu ya udereva miaka 25 iliyopita).

Thursday, December 20, 2012

Bondia Fadhili Majia kupambana kwenye mchujo wa kuwania ubingwa wa mkanda wa Jumuiya ya Madola


Taarifa kutoka kwa Onesmo Ngowi, Mkurugenzi wa Bodi ya Baraza la Ngumi la Jumuiya ya Madola (CBC), inaarifu kuwa bondia Fadhili Majia amepewa nafasi ya kupambana na bondia wa Ghana Isaac Quaye katika mpambano utakaoamua bondia atakayepata fursa ya kugombea mkanda wa Jumuiya ya Madola kwenye uzito wa Flyweight.

Taarifa kamili hii hapa:

Bodi ya Wakurugenzi ya Baraza la Ngumi la Jumuiya ya Madola (CBC) imepiga kura kumruhusu bondia wa Tanzania Fadhili Majia apambane na bondia Isaac Quaye wa Ghana katika mchujo (Elimination) wa kutafuta mpinzani atakayekutana na bingwa wa mkanda wa Jumuiya ya Madola katika uzito wa Flyweight Kevin Satchell wa Uingereza. Mpambano wa Fadhili Majia na Isaac Quaye utafanyika jijini Accra, Ghana tarehe 22, Februari 2013.

Rais wa Kamisheni ya Ngumi za Kulipwa Tanzania (TPBC) Onesmo Ngowi ni mmoja wa wakurugenzi wa bodi ya Baraza la Ngumi la Jumuiya ya Madola na alikuwa wa kwanza kumpigia bondia Fadhili Majia kura ili acheze na Quaye.

Hii itakuwa mara ya kwanza kwa bondia Fadhili Majia kugombea mkanda wa Jumuiya ya Madola ambayo inaziunganisha nchi zote zilizokuwa zinatawaliwa na himaya ya Uingereza.

Wakati huo huo Bodi ya Wakurugenzi ya Baraza la Ngumi la Jumuiya ya Madola imepitisha azimio la kuruhusu ubingwa wa baraza hilo katika bara la Afrika. Ubingwa huo utakuwa unajulikana kama “CBC Africa Zone” na tayari wapo mabondia kadhaa wa nchi za Afrika ya Magharibi ambao wameshandaa mapambano mwakani.

Napenda kuwahamasisha mapromota wa Kitanzania kuchangamkia fursa hizi adimu na kuandaa mapambano ya ubingwa wa "CBC Africa Zone" kwa manufaa ya mabondia wetu.

TPBC imejiandaa kuwatafutia mabondia wa Kitanzania mapambano mengi ya nje ili waweze kujijenga kimchezo na pia kuweza kupata kipato kizuri.

Imetumwa na mimi:

Onesmo Ngowi
Rais, Kamisheni ya Ngumi za Kulipwa Nchini (TPBC)
Mkurugenzi wa Bodi ya Baraza la Ngumi la Jumuiya ya Madola (CBC)

Bondia Fadhili Majia kupambana kwenye mchujo wa kuwania ubingwa wa mkanda wa Jumuiya ya Madola


Taarifa kutoka kwa Onesmo Ngowi, Mkurugenzi wa Bodi ya Baraza la Ngumi la Jumuiya ya Madola (CBC), inaarifu kuwa bondia Fadhili Majia amepewa nafasi ya kupambana na bondia wa Ghana Isaac Quaye katika mpambano utakaoamua bondia atakayepata fursa ya kugombea mkanda wa Jumuiya ya Madola kwenye uzito wa Flyweight.

Taarifa kamili hii hapa:

Bodi ya Wakurugenzi ya Baraza la Ngumi la Jumuiya ya Madola (CBC) imepiga kura kumruhusu bondia wa Tanzania Fadhili Majia apambane na bondia Isaac Quaye wa Ghana katika mchujo (Elimination) wa kutafuta mpinzani atakayekutana na bingwa wa mkanda wa Jumuiya ya Madola katika uzito wa Flyweight Kevin Satchell wa Uingereza. Mpambano wa Fadhili Majia na Isaac Quaye utafanyika jijini Accra, Ghana tarehe 22, Februari 2013.

Rais wa Kamisheni ya Ngumi za Kulipwa Tanzania (TPBC) Onesmo Ngowi ni mmoja wa wakurugenzi wa bodi ya Baraza la Ngumi la Jumuiya ya Madola na alikuwa wa kwanza kumpigia bondia Fadhili Majia kura ili acheze na Quaye.

Hii itakuwa mara ya kwanza kwa bondia Fadhili Majia kugombea mkanda wa Jumuiya ya Madola ambayo inaziunganisha nchi zote zilizokuwa zinatawaliwa na himaya ya Uingereza.

Wakati huo huo Bodi ya Wakurugenzi ya Baraza la Ngumi la Jumuiya ya Madola imepitisha azimio la kuruhusu ubingwa wa baraza hilo katika bara la Afrika. Ubingwa huo utakuwa unajulikana kama “CBC Africa Zone” na tayari wapo mabondia kadhaa wa nchi za Afrika ya Magharibi ambao wameshandaa mapambano mwakani.

Napenda kuwahamasisha mapromota wa Kitanzania kuchangamkia fursa hizi adimu na kuandaa mapambano ya ubingwa wa "CBC Africa Zone" kwa manufaa ya mabondia wetu.

TPBC imejiandaa kuwatafutia mabondia wa Kitanzania mapambano mengi ya nje ili waweze kujijenga kimchezo na pia kuweza kupata kipato kizuri.

Imetumwa na mimi:

Onesmo Ngowi
Rais, Kamisheni ya Ngumi za Kulipwa Nchini (TPBC)
Mkurugenzi wa Bodi ya Baraza la Ngumi la Jumuiya ya Madola (CBC)

Naibu Waziri atembelea Butiama, achangia utalii wa utamaduni

Naibu Waziri wa Viwanda na Bisahara, Mhe. Gregory Teu, ametembelea Butiama hivi karibuni na kutoa Shs.160,000/- kuchangia shughuli za utalii wa utamaduni zinazoratibiwa na Butiama Cultural Tourism Enterprise (BCTE).
Kutoka kushoto kwenda kulia: Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Gregory Teu, msaidizi wake ambaye jina lake haliweza kupatikana mara moja, na mimi, wakati nilipokuwa natoa maelezo ndani ya Maktaba ya Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere iliyopo kwenye nyumba ya Mwalimu Nyerere aliyojengewa na Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), eneo la Mwitongo, Butiama.
Katika ziara yake fupi aliyofanya akiwa safarini kutoka Tarime kuelekea Mwanza, Mhe. Teu alizuru eneo la Mwitongo ambalo lenye makazi ya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, kaburi la Mwalimu Nyerere, maktaba ya Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere, na vivutio vingine vilivyopo Mwitongo.

Friday, December 14, 2012

Francis Cheka avuliwa ubingwa wa mabara wa IBF

Kwa mujibu wa taarifa ya Rais wa  International Boxing Federation (IBF), bondia Francis Cheka ambaye alitwaa unbingwa wa mabara wa IBF wa uzito wa middleweight tarehe 28 Aprili 2012 baada ya kumshinda bondia Mada Maugo, amevuliwa ubingwa huo baada ya kushiriki kwenye pambano ambalo halikupata idhini ya IBF.

Pambano lililomvua ubingwa Cheka ni aliloshiriki dhidi ya Karama Nyilawila tarehe 29 Septemba 2012.
Francis Cheka alipotwaa ubingwa wa mabara wa IBF, tarehe 28 Aprili 2012.
Taarifa fupi ya Lindsay Tucker, ambaye ni mwenyekiti wa ubingwa wa IBF/USBA imeeleza kuwa kutokana na kanuni 5.H iwapo bingwa anashiriki katika pambano ambalo halijaidhinishwa na IBF katika uzito wake, basi ubingwa wake utatangazwa kuwa wazi pasipo kuzingatia iwapo bingwa huyo ameshinda au ameshindwa hilo pambano.

Wednesday, December 5, 2012

Mtanzania Mariagoreth Ndangio afariki Uingereza, mwili wasafirishwa nyumbani kwa mazishi

Jana, tarehe 4 Desemba 2012, muda wa saa tano Watanzania waishio Luton Uingereza, ndugu na marafiki kwa ujumla walijumuika katika kanisa la Kikatoliki la Holy Ghost Westbourne, Luton, Uingereza, katika ibada ya kumuaga MariaGoreth Ndangio tayari kwa safari ya mazishi kuelekea nyumbani Tanzania.
Marehemu Mariagoreth Ndangio
Katika ibada hiyo mama mzazi wa marehemu aliwashukuru watu wote waliojitoa kwa kila hali wakati wa kumuuguza mwanae mpaka mauti ilipomkuta. Pia kaka wa marehemu alisoma historia fupi ya marehemu na kueleza upendo na ushirikiano aliokuwa nao na watu wote.

Mwili wa marehemu unatarajiwa umesafirishwa leo Jumatano kuelekea Tanzania kwa ajili ya mazishi.

Mwenyekiti wa Jumuiya ya Watanzania Luton ( Luton Tanzanian Community ) Bw. John Mbwete kwa niaba ya familia ya marehemu na Jumuiya ametoa shukurani kubwa kwa watu wote waliojitoa kwa hali na mali, Ubalozi wa Tanzania nchini Uingereza na Tanzania Association kwa ushirikiano waliotoa katika kufanikisha safari ya mwisho ya Mariagoreth kuelekea Tanzania.

Bwana ametoa na Bwana ametwaa, sifa na utukufu kwa Mwenyezi Mungu.
Shukrani.
*******************************
Taarifa imetolewa na:
Abraham Sangiwa
Katibu – Luton Tanzanian Community ( TLC )

Saturday, November 24, 2012

Jimmy ChangChuu, msanii toka Bagamoyo atembelea Butiama

Jimmy ChangChuu, ni msanii anayeishi na kufanya kazi Bagamoyo. Baadhi ya kazi anazofanya ni pamoja na kuchonga vinyago, kufinyanga, kuandaa michoro ya grafiti (michoro ya ukutani) na ni mwanamitindo.

Aidha hushiriki kwenye matangazo ya televisheni na anafahamisha kuwa ameshiriki kwenye kipindi televisheni cha cha Dume Challenge. Hivi karibuni alitembelea Butiama na yafuatayo ni maoni yake kuhusu Butiama.
***************************************************

"Naishi hizi sehemu mbili, Dar es Salaam na Bagamoyo, kwa sababu Bagamoyo ni sehemu yangu ambayo napata msukumo, ni sehemu iliyotulia. Mizunguko ya Dar es Salaam kidogo inakuwa inanishinda lakini ninapohitajika Dar es Salaam nakuwepo na familia.

Hii ni mara yangu ya kwanza kufika Butiama. Mara ya kwanza nilipokuja tu ile mandhari ilinifanya nijisikie kama niko na amani, nilipata amani kwenye moyo. Mazingira yametulia, yaani hakuna kitu ambacho kinaweza kikajiingiza wakati unafikiria kufanya kitu fulani au wakati uanataka kufanya kitu. Kwa hiyo ni sehemu ambayo imetulia ambayo inaweza kukupa msukumo.

Ni ngumu sana kupata msukumo kwenye sehemu ambapo kuna vitu vinapita ambavyo vinakuvuruga lakini hapa unaona hali asili ya mazingira, unaona ndege, yaani vitu ambavyo vinakufanya unaona kuwa kuna Muumba ambaye ametengeneza hivi vitu. Ni vitu ambavyo vinavutia kweli.

Kitu ambacho kinaweza kufanya niwaambie watu waje Butiama ni mazingira na hali ya utulivu halafu nikiangalia chimbuko la kabila la Wazanaki kuna vitu ambavyo nilikuwa nikiviangalia ambavyo vina nguvu kubwa ambavyo ukiviangalia kwa juu juu huwezi kuviona, lakini kuna vitu ambavyo vipo ambavyo vimemfanya Mwalimu Nyerere akawa ana nguvu kwenye maamuzi yake, vitu ambavyo vinaendana na tamaduni yetu ya Kitanzania na ambavyo Mwalimu aliviweka kwenye siasa yake na kwenye mila na hakutoka nje ya mila yake kusikiliza mila za kigeni. Alisimama yeye pale aliposimama kutoka kwenye chimbuko la tamaduni yake.

Kwa hiyo unakuta sasa hata katika utawala wake hakutoka nje sana kwa sababu hata nikiangalia nilivyokwenda makumbusho [Makumbusho ya Mwalimu J.K. Nyerere] kule kuna vitu ambavyo nimesoma na Nyerere mwenyewe alikuwa anakwambia elimu ya wakoloni ilikuwa inawaandaa wao kuwatumikia wakoloni siyo kuwaandaa kuweza kujiendeleza wao wenyewe.

Kitu kizuri kama watu wanataka kuwa kwenye siasa na kuwa viongozi wazuri wanapaswa kujifunza kutoka kwa Nyerere na aliyoyafanya. Tangu akiwa shuleni alianza kuwa kiongozi na alichaguliwa na watu. Watu waliona Mwalimu alikuwa na kitu fulani wakamchagua. Siyo kwamba yeye alipendekeza 'mimi nataka kuwa kwenye nafasi hii.' Watu walimuona kuwa ana kitu ambacho anaweza kuchangia kwa wengine na pia alikuwa na uwezo wa kushawishi wengine."

Monday, November 12, 2012

Sijiuzulu ng'o! Hata mkija na winchi ya bandari

Jenerali David Petraeus wa Marekani amejiuzulu hivi karibuni kwa sababu ya mahusiano na mwanadada ambaye jina lake haliko kwenye cheti cha ndoa cha Jenerali huyo. Kwa Kiswahili anaitwa nyumba ndogo; kwa Kizanaki anajulikana kama kitungo.

Haya yangetokea Tanzania hamna mtu yoyote angeachia ngazi, na suala hili linaibua mitazamo tofauti kati ya utumishi wa umma hapa Tanzania na utumishi wa umma katika nchi nyingine.

Ukweli ni kuwa hata katika mijadala niliyoisikia kwenye vyombo vya habari vya nje kuna wale ambao wanaona kuwa Jenerali Petraeus hakustahili kung'atuka kwa sababu haya ni mambo ambayo yanatokea kwa watumishi wa ngazi za juu kwenye nchi mbalimbali duniani. Mtakumbuka kuwa Rais mstaafu Bill Clinton naye alikutwa na masuala yanayofanana na haya, na aliwekwa kiti moto kwa muda mrefu lakini hakujitoa kwenye uongozi. Tuhuma kubwa dhidi yake ilikuwa kusema uongo baada ya kula kiapo.

Kwa mantiki hiyo, inaelekea wadhifa wa Jenerali Petraeus kama Mkurugenzi wa shirika la ujasusi la Marekani, Central Intelligence Agency, ni nyeti zaidi katika nafasi ya uongozi wa nchini Marekani kuliko hata ule wa Rais wa Marekani, na inasemekana kuwa mkuu wa kazi wa Jenerali Petraeus ndiye aliyemshauri kuachia ngazi na yeye akafuata ushauri huo.

Nimetafakari suala hili iwapo aliyehusishwa na mahusiano haya angekuwa Mkuu wa Usalama wa nchi tofauti na Marekani na iwapo mkuu huyo angekuwa ni Mzanaki.

Soma mahojiano haya ya kubuni:

Mwandishi: Ndugu Madaraka, ninayo taarifa kuwa unahusishwa na tuhuma kuwa una uhusiano wa nje ya ndoa na [jina limehifadhiwa na gazeti] na...

Madaraka: Ndugu? Nani ndugu yako? Bwana mdogo, mimi ni mheshimiwa, tena mheshimiwa sana na ukitaka nijibu maswali yako nataka unipe heshima yangu. Na inaandikwa "m-h-e-" kabla ya jina...

Mwandishi: Samahani, mheshimiwa, nilikuwa nauliza....

Mhe. Madaraka: Swali nimelisikia. Bwana mdogo, nyie wasomi wa siku hizi mnafahamu sana mila na tamaduni za Ulaya na Marekani, lakini cha ajabu mnashindwa kudumisha na kuheshimu mila na tamaduni zenu wenyewe. Na ndiyo maana siku zote mtaendelea kutawaliwa kimawazo. Na ukishatawaliwa kimawazo utapangiwa mpaka maneno ya kuongea na mkeo nyumbani.

Sasa ngoja nikupe somo la bure kuhusu mila na tamaduni za kabila langu. Huyo mama ambaye wewe unashindwa kutaja jina lake, jina lake halisi ni [jina tumelihifadhi] na wala siyo siri kuwa ni mke wangu...

Mwandishi: Atakuwaje mke wako wakati tunafahamu mke wako ni......

Mhe. Madaraka: Mura! Enye ndakuburra ni mkane, bhono ni wazo? [Kijana! Mimi nakwambia ni mke wangu, sasa ni wako?] Bwana mdogo, ukitaka nikujibu usiniingilie ninapokujibu. Ukitaka kunipangia idadi ya kina mama zangu kwa sababu ulisomea Marekani, nashauri umuulize haya maswali Petraeus. Hapa siyo Marekani. Wao wana mila zao na mimi najaribu kukueleza mila zangu, kama utanisikiliza. Hutaki, kafanye kazi Marekani kwa sababu mimi hapa hatutaelewana.

Huyo nyie mnayemwita nyumba ndogo kijijini kwangu ana heshima yake, na wala hafichwi. Tunamuita kitungo, kama umeshawahi kusikia. Na kama ulifikiri utanitoa upepo kwa kunipa hofu kuwa umekalia siri ambayo utaifichua na kuniaibisha utakuwa unapoteza muda. Kwa taarifa yako ndugu zangu wote wanamfahamu, pamoja na mke wangu. Na hii ni pamoja na mamlaka iliyoniteua.

Haya, una lingine?

Mwandishi: Sawa mheshimiwa. Sasa pamoja na kwamba hizo ndiyo mila za Kizanaki, lakini wewe ni mtumishi wa Serikali na unashika wadhifa unaohusiana na usalama na maslahi ya Taifa. Utakuwa unafahamu kuwa nchi hii haiendeshwi kwa taratibu za kabila la Kizanaki. Inafuata kanuni, taratibu, na sheria. Huoni kama kwa kuwa na mahusiano haya yasiyo rasmi unaweza kuwa unahatarisha kuvujisha siri za nchi na kuwa unastahili kujiuzulu.

Mhe. Madaraka: Hivi wewe una akili timamu? Huyo aliyeniteuwa hana akili? Mimi mwenyewe sina akili? Kwamba nitaleweshwa na mahusiano yangu binafsi halafu nianze kuzianika siri za Serikali? Mbona hamkuwa na wasiwasi kuwa nitatoa siri kwa mke wangu, iweje leo nizitoe kwa huyu bi mdogo? Kama tatizo ni mahusiano na kina mama basi hizi kazi wawe wanafanya mapadri, watu ambao hawafungi ndoa. Lakini ni jambo ambalo pia mtalipinga, mtasema hatuwezi kuchanganya dini na Serikali maana hamksoi cha kusema nyie.

Unafahamu ile winchi ya badnari inayobeba kontena la futi 40? Nakwambia hata mkiileta ile kujaribu kuniondoa hapa, sitang'oka

Uchaguzi nafasi 10 za wajumbe wa NEC - CCM Tanzania Bara, Wassira aongoza

Matokeo ya chaguzi za nafasi 10 za wajumbe wa NEC Tanzania Bara wa Chama cha Mapinduzi zinazoendela Dodoma yametoka. Matokeo haya hapa:

1.  Stephen Wassira                  - 2,135
2.  January Makamba               - 2,093
3.  Mwigulu Nchemba             - 1,967
4.  Martine Shigela                  - 1,824
5.  William Lukuvi                  - 1,805
6.  Bernard Membe                 - 1,455
7.  Mathayo David Mathayo   - 1,414
8.  Jackson Msome                  - 1,207
9.  Wilson Mukama                 - 1,174
10. Fenela Mukangara            -     984

Saturday, November 10, 2012

Konyagi watoa ala za muziki kwa Msondo Ngoma

Kampuni inayotengeneza kinywaji Konyagi imetoa zawadi ya ala za muziki kwa bendi kongwe ya muziki wa dansi nchini, Msondo Ngoma.
Msondo Ngoma jukwaani.
Akikabidhi hizo ala, Mkurugenzi Mkuu wa Tanzania Distilleries Limited ambao ndiyo watangenezaji wa Konyagi, alisema vifaa hivyo vimetolewa kwa ajili ya kuenzi utamaduni wa Mtanzania na kuiwezesha Msondo Ngoma kuwa imara katika kutoa burudani kwa Watanzania.

Alisema, "Msondo ni bendi kongwe tangu kuanzishwa kwake mwaka 1964. Imesimama imara katika kutoa burudani ya uhakika kwa Watanzania na kutumia nyimbo zake katika kuelimisha, na kufunza jamii ya Watanzania walio wengi."

Alisema kwa kuwapatia vyombo hivyo, Msondo Ngoma itakuwa moto wa kuotea mbali katika kutoa burudani ya uhakika, hali itakofanya bendi nyingine kuwa wasindikizaji katika tasnia ya muziki wa dansi nchini.

Mkurugenzi wa bendi hiyo, Maalim Gurumo, alisema kwa sasa wana deni kubwa kwa Watanzania na kampuni ya Konyagi katika kutoa burudani ya uhakika baada ya kupatiwa vifaa hivyo.
Mkurugenzi wa Tanzania Distilleries Limited David Mgwasa, wa pili kutoka kulia, akikabidhi ala kwa wanamuziki wa Msondo Ngoma.
"Tunaamini baada ya leo kupata vifaa hivi tutatoa burudani ya uhakika sanjari na kukijenga vyema kikosi chetu kwa lengo la kukiimarisha," alisema Gurumo.

Kiongozi wa bendi, Saidi Mabela, alitoa shukurani kwa kampuni ya Konyagi kwa kuwapatia vyombo na aliahidi kuendelea kutoa burudani safi kwa Watanzania na Afrka kwa ujumla.
Habari kamili ziko hapa.

Tuesday, November 6, 2012

Mlima Kilimanjaro unapendeza zaidi tokea Tanzania au Kenya?

Kuna mdau hapa anauliza swali: Mlima unaonekana vizuri tokea Tanzania au Kenya? Huyu mdau anahisi kuna hujuma inafanywa na jirani zetu kuvutia wageni wengi zaidi waende Kenya na ndiyo maana hoja hii inaibuliwa.

Hili swali halipaswi hata kuulizwa. Mlima Kilimanjaro unavyoonekana kutokea Kenya ni tofauti kidogo na unavyoonekana upande wa Tanzania. Kama kuna mtu kapendezewa na taswira ya mlima tokea Kenya huwezi kumlazimisha afurahie taswira ya mlima huo kutoka upande wa Tanzania.

Lakini huu utaratibu wa kulalamikia jirani zetu wa Kenya kunufaika na Mlima Kilimanjaro wakati sisi wenyewe tumekaa na kuongea tu pia hauna manufaa yoyote kwa maendeleo yetu.

Ninavyoamini mimi, mgeni yoyote aliyetoka nje ambaye amekuja kukwea mlima huu maarufu hajali kama uko Kenya, Tanzania, au kwenye sayari ya Zuhura. Mgeni anavutiwa na mlima wenyewe na siyo mipaka ya nchi.

Mimi nimeshakwea Mlima Kilimanjaro mara kadhaa na ukweli ni kuwa ni Watanzania wachache sana wanakwenda huko kulinganisha na wageni wa nje. Kwa kweli kule mlimani Mtanzania ndiyo mgeni na wageni ndiyo wenyeji kwa sababu idadi yao ni kubwa sana. Hivi karibuni nimekutana na Wakenya kibao kwenye njia ya Marangu wakielekea kileleni.

Mimi ningefurahi sana kuona hawa wenye uchungu na mlima huu kusemwa uko Kenya basi wawe wanajitokeza mara moja moja nao kukwea huu mlima. Hiyo itawawezesha kuzungumzia mlima wao kwa kujiamini badala ya kuuliza maswali tu na kulalamika.
Mlima Kilimanjaro unavyoonekana kutoka upande wa Tanzania.
Kitu ambacho watajifunza ni kuwa mandhari nzuri kuliko zote za mlima huu ziko huko huko mlimani. Lakini haya ni maoni yangu tu.

Sunday, November 4, 2012

Lugha yetu Kiswahili

Jana kwenye redio nimesikia marudio ya majadiliano kutoka kwenye vikao vya Bunge la Muungano vinavyoendelea sasa hivi. Alisikika mbunge mmoja, akiwa anatetea hoja kuwa lugha ya Kiswahili itumike kwenye uendeshaji wa shughuli za mahakama, akisema yafuatayo (siyo nukuu halisi kwa maana ya neno kwa neno lakini ni sahihi kwa maana ya nukuu yenyewe):

"...mienendo yote ya shughuli za mahakama iendeshwe kwa lugha ya Kiswahili tu, na kusiwe na option ya Kiswahili au Kiingereza, iwe ni Kiswahili tu."

Anayesisitiza matumizi ya Kiswahili pekee kwenye shughuli za mahakama za Tanzania anajenga hoja yake kwa kutumia neno la Kiingereza.

Ni kazi kweli kweli.

Kwenye kamusi neno option lina maana kadhaa, ikiwa ni pamoja na: uchaguzi, na hiari.

Thursday, November 1, 2012

Mada ya yangu ya leo: aliyeikashifu Kurani aadhibiwe

Kwa hali ya kawaida, mtoto aliyedhalilisha kitabu kitukufu cha dini ya Kiislamu angeweza kuadhibiwa kwa kuchapwa bakora na mzazi wake au kupewa adhabu nyingine nzito ambayo watoto wote wanaokosea hupewa.

Lakini tukio liliotokea siyo la kawaida, kama ambavyo tumeshuhudia madhara yaliyofuata na vurugu zilizotokana na kitendo kile. Makanisa yalivamiwa na mali nyingi kuporwa na kuharibiwa. Uporaji wa mali haufanani hata kidogo na Uislamu kwa hiyo ni dhahiri kuwa katika kundi la watuhumiwa wa matukio haya ambalo linasemekana kuwa ni la waumini wa dini ya Kiislamu walishiriki pia watu ambao hawakusukumwa na hasira ya kudhalilishwa kwa Kurani na dini ya Kiislamu bali ni watu waliyoona fursa ya kuharibu na kupora mali.

Tanzania inayo sheria inayosimamia watuhumiwa ambao wako chini ya umri wa miaka 18. Ni dhahiri hakuna ubishi kuwa huyo mtoto alifanya kosa hilo. Jambo moja ambalo linaweza kuepusha manung'uniko ya dhati ya waumini wa dini ya Kiislamu kulalamikia kile kitendo ni kufikisha suala la yule mtoto mahakamani bila uchelewesho. Kufanya hivyo kutaondoa kabisa kisingizio cha wale ambao wanatafuta fursa ya kufanya fujo kwa kisingizio cha kutetea hadhi na heshima ya dini ya Kiislamu.

Nina hakika yule mtoto tayari anajutia kitendo chake, lakini suala la kutafuta suluhu baina ya waumini wa dini mbalimbali, na suala la kulinda amani nchini linahitaji hatua za kisheria zichukuliwe haraka dhidi yake.

Wednesday, October 31, 2012

Mada yangu ya leo: Jinsi elimu duni inavyohatarisha amani

Nimewahi kuuliza waandishi wa habari wawili, mmoja toka Kenya na mwingine Mtanzania, swali moja: raia wanaamini yuko kiongozi ambaye si mwizi? Mkenya alisema Wakenya wote wanaamini kuwa viongozi wao siyo waaminifu. Mtanzania naye alisema Watanzania wengi zaidi nao wanaamini kuwa viongozi wetu siyo waaminifu.

Madhumuni ya msingi ya kutoa elimu ni kumwezesha mwanafunzi kusoma, kuhesabu, na kuandika. Madhumuni mengine ya muhimu ni kumwezesha mwanafunzi kuwa mdadisi, mchambuzi, mwenye uwezo wa kufikiri, na hata mwenye uwezo ya kupinga kwa hoja yale ambayo anafundishwa. Pengine hili la pili lingeweza kuwa muhimu kuliko lile la kwanza kama isingekuwa haiwezekani kupata uwezo huu wa pili bila kuwa na uwezo wa kusoma, kuhesabu, na kuandika.

Hali duni ya elimu iliyopo sasa inatoa nafasi ndogo sana kwa wanafunzi kuvuka ngazi ya kwanza na kuingia ngazi ya pili. Tunao wanafunzi wa sekondari wasiokuwa na uwezo wa kusoma na kuandika. Tunao wahitimu wa elimu ya juu ambao hawana uwezo wa kuridhisha kulinganisha na wenzao waliosoma miaka ya sitini na ya sabini.
Maisha ya baadaye ya hawa watoto yatakosa amani iwapo mfumo wa elimu hautaboreshwa.
Leo hii wanaopta elimu nzuri ni asilimia ndogo sana ya mamilioni ya Watanzania ambao wanapata elimu hafifu. Kwa sababu hii kila mwaka ongeko la Watanzania wenye uwezo wa kuchambua, kutafakari, kudadisi, na kupinga kwa hoja masuala mbabali mbali wanazidi kupunguka na tena kwa kasi kubwa.

Siasa ya vyama vingi imefanikiwa kifuchua maovu mengi ya siasa za chama kimoja, lakini pia vyama vingi vimejenga pia imani kwa mwananchi wa kawaida kuwa kila mtu ni mwizi. Juzi juzi nimetoka kupanda Mlima Kilimanjaro na wanafunzi wa Shule ya Sekondari ya Wasichana ya Loreto na nilimsikia mmoja wao akisema kuwa "kila mtu ni mwizi."

Hatuwezi kuacha kulaumu mienendo ya baadhi ya viongozi wetu ambayo inawafanya raia waamini kuwa viongozi wa umma waaminifu hawapo tena.

Elimu hafifu inapunguza uwezo wa raia wa kuchambua masuala mbali mbali, lakini siasa ya vyama vingi imefanya kazi nzuri ya kumfanya raia ashuku kila kitu na kila mtu. Kwa taratibu za kisheria za mfumo wa sheria unaojulikana kama civil law ni wajibu wa yule anayetuhumiwa kuthibitisha kuwa siyo mwizi, au hafanyi janja janja ya aina fulani anapokuwa kiongozi au mtumishi wa umma.

Hatari ya hali hii ni kuwa hata pale jambo linapokuwa halina mizengwe ni vigumu kwa raia kuamini hivyo. Raia wanapokuwa hawana tena imani na viongozi na mfumo wa utawala, misingi ya amani itaanza kupata nyufa. Na matukio ya miaka ya hivi karibuni yanaashiria kuwa miaka ijayo haitakuwa na amani ambayo Watanzania wamekuwa nayo kwa muda mrefu.

Sunday, October 28, 2012

Kwaya ya Mt. Cecilia ya mjini Singida yatembelea Butiama

Leo jioni wanakwaya wa Kwaya ya Mt. Cecilia ya Kanisa Katoliki mjini Singida wametembelea Butiama na kuzuru kaburi la Mwalimu Julius Kambarage Nyerere.


Wanakwaya hao ambao wako kwenye ziara ya Mkoa wa Mara walipita Butiama wakitokea Musoma na wakiwa njiani kwenda Isenye.

Friday, October 26, 2012

Wazanaki na vitungo

Mzee wa Kizanaki anapokaribia nyumbani kwake baada ya giza kuingia huanza kuimba kwa sauti ya juu wimbo unaojulikana kama kibanziko. Kwa desturi ni wimbo unaoimbwa na mzee ambaye amekunywa pombe kidogo, na madhumuni ya wimbo huu ni kuwafahamisha watu wote watakaomsikia kuwa mzee mwenye nyumba anarudi nyumbani. Mwanaume yoyote ambaye anaweza kuwa nyumbani kwa huyu mzee na ambaye hawezi kutoa maelezo ya kuridhisha kwanini yuko pale atafahamu kuwa ni wakati wa kuondoka haraka. Kila mzee wa Kizanaki ana kibanziko chake.

Mzee wa Kizanaki na heshima zake hawezi kumvizia mkewe kwa madhumuni ya kumfumania. Ni tabia ambayo haikubaliki.

Mzee Ginga Kihanga, mwenye umri wa miaka 93 alinisimulia kuwa wazee hupendelea kuwatisha waviziaji badala ya kujiingiza kwenye makabiliano ambayo yanaweza kusababisha majeraha makubwa au hata kifo.
Hata hivyo haina maana kuwa zama zile watu hawakufumaniwa. Enzi za ukoloni wale walioshikwa kwenye fumanizi walidhalilishwa hadharani kwa kuvuliwa nguo, kuchapwa bakora, na kutozwa faini ya ng'ombe wawili. Tofauti ilikuwa mtemi anapokuwa ndiyo mlalamikaji; yeye aliruhusiwa kupanga faini aliyoona inastahili.

Kibanziko kina madhumuni mengine ya ziada. Mzee Ginga alisema, kwa kawaida, tendo lile haramu lilifanyika kwenye vichaka, mbali na nyumba ya wenye ndoa. Ilikuwa ni fedheha kubwa kwa mwanaume Mzanaki anapofumania nyumbani kwake. Kwa hiyo, kwa namna nyingine, uimbaji wa kibanziko ilikuwa ni njia ya kuzuwia hiyo aibu na kumsababisha huyo 'mwizi' aondoke na kuepusha aibu ndani ya jamii.
Yawezekana kuwa desturi hii ya kuwapa upenyo hawa 'wezi' inatokana na tamaduni ile ya kupanga ndoa. Mzee huyo huyo ambaye jana aliimba kibanziko alipokaribia nyumbani kwake yawezekana alikuwa amepitia kwenye kilabu cha pombe na kufanya makubaliano na mzee mwenzake kuwaoza watoto wao.
Aliporudi nyumbani alimwambia mwanae wa kiume kuwa umewadia wakati wa kufunga ndoa na kuwa ameshamtafutia mchumba anayefaa ambaye anatoka kwenye familia ya wachapakazi hodari ambao hawana historia ya magonjwa ya kurithi, na kuwa siyo wachawi.
Lakini kabla ya kupangiwa hizi ndoa na wazee yawezekana kuwa hao wanandoa watarajiwa walikuwa tayari wana mahusiano na watu tofauti. Na yawezekana kwa kutambua uwezekano huo kuwa mtu anapolazimishwa ndoa ambayo hakuitaka anaweza akawa na mahusiano mengine ya pembeni, basi jamii ya Kizanaki ikaja na kibanziko kama njia ya kuruhusu yale ambayo yalifungwa na ndoa za kupangawa na wazee.
Kuna msemo wa Kizanaki unaoashiria kukubali hali hii unaosema, wiguru na wiyasi, ukimaanisha kuna yule wa juu na yule wa chini; kuna mume, na kuna mviziaji - kune mume (au mke), na kuna kitungo.

Kwa kawaida kitungo ndiyo alikuwa mchumba ambaye angeolewa iwapo kijana angeruhusiwa kuchagua, lakini hakuweza kumuoa huyo kwa sababu ya ndoa ya kupangwa na baba mzazi. Na kwa sababu ndoa aliyopanga mzazi haikuwa na majadiliano kilichotokea ni kuwaunganisha watu wawili ambao walikuwa hawana upendo baina yao.

Matokeo yake ni kuwa walikuwa na mahusiano kama maadui badala ya wanandoa. Mwanaume alimuamrisha mwanamke ndani ya nyumba na mwanamke, kwa hulka, alikuwa mkaidi. Ahueni ilitafutwa kwa kitungo.

Na lugha ya kitungo ilikuwa tamu, ya kubembeleza. Walitumia majina ya wapendanao kama 'Nyababiri', Nyabasasaba' au 'Nyabanane' majina yenye kumaanisha 'wa pili', 'wa saba', 'wa nane' na majina ambayo siyo rahisi kutumika baina ya wanandoa.
  
Kama ilivyo kwa mila na desturi nyingi, kibanziko nacho kinapotea na nyakati. Leo hii vijana wanarudi majumbani mwao bila taarifa. Yawezekana pia kuwa hawana uwezo wa kuimba kama wazee wa Kizanaki.

Thursday, October 25, 2012

Msanii Kingkapita ametoa nyimbo mpya

Msanii wa Hip Hop, Kingkapita, ametoa kibao kipya chenye jina: Shikamoo pesa.



Taarifa aliyoisambaza mwenyewe inaeleza:
"Nilimshirikisha Tash, mzee wa chapia mulemule kutoka Arachuga. Nyimbo imerekodiwa katika studio za Rocanna Basemennt chini ya producer Jimmy Jizze na master kumaliziwa Home Town Record chini ya master Traveller."

Sikiliza kibao hicho hapa: http://www.hulkshare.com/7u4tpclsbwu8

Tuesday, October 23, 2012

Huduma ya bure kufasiri Kiswahili kwa Kiingereza*

*Vigezo na viwango kuzingatiwa: kutokana na kuwa na majukumu mengine naweza kupokea kazi kidogo tu kwa siku.

Nimechunguza kiwango cha watu wengi kumudu uandishi wa lugha ya Kiingereza - na hata lugha yetu ya Kiswahili - na, kwa maoni yangu, picha inayojitokeza ni kuwa kiwango hakiridhishi. Hapa nazungumzia Watanzania wa kada mbali mbali, kuanzia wasomi na wale ambao hawakupata fursa ya kupata elimu ya juu.

Kwa bahati mbaya imejengeka tabia inayohusisha uongo kuwa mtu anayeongea au kuandika kwa lugha ya Kiingereza ndiyo anadhihirisha kuwa ana elimu nzuri. Kwa sababu hii, watu wengi ambao wangeweza kufanya mawasiliano kwa lugha ya Kiswahili hung'ang'ana kuongea au kuandika kwa Kiingereza pasipo kuwepo uwezo mzuri wa kufanya hivyo. Kama ambavyo kutofahamu Kichina haihusiani na kutokuwa na elimu, vivyo hivyo kutofahamu Kiingereza hakuashirii kutokuwa na elimu.

Hata hivyo kuna ukweli kuwa yapo mazingira yanayolazimu mtu kuandika au kuwasilisha mada kwa lugha ya Kiingereza. Hapa naamini naweza kusaidia kutokana na uwezo wangu wa zaidi ya miaka 20 wa uandishi kwa lugha za Kiingereza na Kiswahili na uandishi kwa ujumla.

Najitolea kufasiri maandishi kutoka lugha ya Kiswahili kwenda kwenye lugha ya Kiingereza iwapo maandishi hayo hayatazidi kurasa moja ya ukubwa wa A-4. Lakini nikiri kuwa nikiona dalili kuwa kazi ni kubwa nitatoza ada kuanzia kurasa ya pili na kuendelea.

Mimi si mtaalamu wa lugha kwa hiyo siwezi kutoa tafsiri rasmi, ila nina uzoefu wa kutosha wa uandishi katika lugha za Kiswahili na Kiingereza kiasi cha kuweza kutoa tafsiri zinazokidhi viwango vya kuridhisha vya uandishi.

Nitumie maandishi yako kwa barua pepe na nitakurudishia tafsiri siku inayofuata:

kiswahilikwakiingereza@gmail.com

Monday, October 1, 2012

Mwanafunzi wa kidato cha nne afika kilele cha Mlima Kilimanjaro

Mwanafunzi Placidia Prudence wa Shule ya Sekondari ya Wasichana Loreto ya jijini Mwanza ambaye alikuwa kwenye msafara wa kukwea Mlima Kilimanjaro amefanikiwa kufika kilele cha mlima huo tarehe 28 Septemba 2012.

Nami nilikuwa kwenye msafara huo ambao ulishirikisha wanafunzi wengine 15 toka shule hiyo pamoja na walimu watatu. Katika wote tulioshiriki ni yeye peke yake alifanikiwa kufika kileleni ambako alifika akiongozana na muongozaji Entold Mpunga.
Placidia Prudence akiwa kwenye kambi ya Horombo baada ya kufika kwenye kilele cha Mlima Kilimanjaro. Kushoto, juu, unaonekana Mlima Kilimanjaro.
Mwanafunzi Nusra Alkarim, mwalimu wa michezo Isack Katambi, na mimi tulifanikiwa kufika Gillman's Point, mita 5,685 juu ya usawa wa bahari na kiasi cha mwendo wa kama saa moja na nusu toka kilele cha Uhuru alikofika Placidia. Kilele cha Mlima Kilimanjaro kina urefu wa mita 5,895 juu ya usawa wa bahari.

Msafara huo ulipangwa kwa madhumuni ya kuchangisha pesa za mradi wa kuboresha na kufikisha maji safi na salama kwenye shule ya Loreto.

Placidia ana umri wa miaka 20 na ameniarifu anakusudia kuwa mhandisi.

Sunday, September 23, 2012

Pambano la ndondi Oktoba 14 kumuenzi Mwalimu Nyerere

Mabingwa wa uzito wa kati (kilo 72.5) wa Uganda na Tanzania wanaotambuliwa na Tanzania Professional Boxing Organization (TPBO) watapambana tarehe 14 Oktoba mwaka huu Friends Corner Bar, Manzese, Dar es Salaam katika pambano lilioandaliwa kumuenzi Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, aliyefariki zaidi ya miaka 12 iliyopita.

Pambano hilo litawapambanisha bingwa wa Tanzania Thomas Mashali, juu, na bingwa wa Uganda, Med Sebyala, chini.


Mchezo huo utakuwa wa kuwania ubingwa wa Afrika Mashariki.

Bondia Sebyala ameshawahi kupambana na kushindwa kwa pointi na bondia Francis Cheka, bingwa wa mabara wa Afrika anayetambuliwa na International Boxing Federation (IBF). Aidha, ameshawahi kupambana na Rashidi Matumla na ingawa mapambano yote alishindwa kwa pointi, alitoa upinzani mkali kwa mabondia hao Watanzania.

Bondia Mashali anayo sifa ya kutoa vichapo vikali kwa wapinzani wake na kuwapumzisha kwa knock-out za mapema.

Taarifa kutoka TPBO zinaeleza kuwa kwa kumuenzi Mwalimu Nyerere na kuthamini juhudi zake za kuendeleza michezo TPBO itaandaa mapambano ya ngumi kwenye kila maadhimisho ya kifo chake tarehe 14 Oktoba.

Friday, September 21, 2012

Twist mpaka chini: harusi za Tanzania zinafanana sana

Sijui ni hisia zangu tu, lakini nahisi kama mtiririko wa ratiba za harusi ninazohudhuria siku hizi zinafanana sana.

Kwenye harusi nilizohudhuria hivi karibuni nimeshuhudia kuna wakati wa kuita kamati iliyoandaa harusi na kila mwanakamati hujitambulisha. Salama ipo kama wanakamati bado hawajachangamka kwa vinywaji vinavyoondoa aibu mbele ya kadamnasi. Lakini kama wanakamati wameshachagamka mambo huwa hayatabiriki.
Mara wanapomaliza kujitambulisha na kueleza mambo waliyofanya kufanikisha harusi, basi muongozaji wa sherehe anaagiza DJ aweke twist ya uhakika.

Na mara zote nimeshuhudia kuwa wimbo unaopigwa ni ule ule. Uchezaji nao ni ule ule, haujabadilika tangu miaka ya hamsini ingawa silalamikii uchezaji nao ubadilike.

Monday, September 17, 2012

Msondo Ngoma bado wanatamba

Wapiga gitaa wa bendi ya Msondo Ngoma Abdul Ridhiwani, kushoto, na Zahoro Bangwe, kulia,
wakiburudisha mashabiki wao hivi karibuni wakati bendi hiyo ilipotumbuiza kwenye ukumbi wa Max Bar, Ilala Bungoni, Dar es Salaam.

Msondo Ngoma ni moja ya bendi kongwe za muziki wa dansi za Tanzania. Zamani ilikuwa inaitwa NUTA Jazz.

Picha na habari zimetolewa na Rajabu Mhamila.

Sunday, September 16, 2012

Mada yangu ya leo: polisi na waandamanaji

Kuna mambo mawili muhimu yanajitokeza baada ya kuuwawa kwa mwandishi wa habari wa Channel Ten wa Iringa, Daudi Mwangosi, tarehe 2 Septemba 2012. Kwanza, Jeshi la Polisi, ambalo mmoja wa askari wake ameshafikishwa mahakamani kwa tuhuma za kuhusika na mauaji hayo, linahitaji kutoa mafunzo maalum ya namna polisi waliyopo kwenye eneo la maandamano wanavyopaswa kusimamia suala la amani katika maandamano.

Siyo kila tukio la mkusanyiko wa watu linahatarisha mali au maisha ya raia, kwa hiyo ni dhahiri pia kuwa siyo lazima kila mara kutumia nguvu zisizokuwa za lazima dhidi ya raia. Polisi wanafunzi wanapaswa kupewa elimu inayojenga taswira kuwa anaepinga serikali iliyoko madarakani siyo lazima pia awe ni adui wa Taifa au anaetishia usalama wa Taifa.

Picha inayojitokeza baada ya baadhi ya matukio ambapo polisi wameua raia ni kama vile kazi kuu ya polisi ni kuhakikisha kuwa upinzani halali wa kisiasa unaminywa kiasi cha kutosha na kuondoa kabisa uwezekano wa serikali iliyopo madarakani kuondolewa madarakani kwa njia za kidemokrasia.

Polisi wapate mafunzo kuwaelimisha kuwa kazi yao siyo kulinda maslahi ya kisiasa ya serikali iliyopo madarakani, na wafunzwe kukubali uwezekano kuwa chama chochote kilichopo upande wa upinzani kinaweza hatimaye kushinda uchaguzi na kuongoza serikali.

Jambo la pili na ambalo ni muhimu sana ni kuwa sasa waandishi wa habari wapate mafunzo ya namna ya kukusanya habari kwenye maeneo yenye usalama mdogo ili kupunguza tishio kwa usalama na maisha yao. Polisi anafanya kazi kwa amri, na kuna mazingira mengi ya kisheria yanayomruhusu polisi kutumia silaha kwa jinsi ambavyo anaona ni sawa kutokana na mazingira yanayomkabili. Polisi anayefukuzwa na kundi la waandamanaji ambao anaamini wanakusudia kumuua hatasita kutumia silaha yake dhidi ya kundi hilo. Huu ni mfano tu; haya sidhani kama ni mazingira yaliyotokea kwenye tukio lilisobabisha kifo cha Daudi Mwangosi.

Jambo la msingi ni kuwa, hata pale ambapo tunajua tunayo haki, si busara hata kidogo kubishana na mtu ambaye ameshika silaha na anaamini kuwa anatekeleza amri halali aliyopewa na mkubwa wake. Na hili haliwezi kubadilika mpaka itolewe elimu ambayo itambadilisha polisi Mtanzania ili atumie mbinu tofauti kukabiliana na waandamanaji.

Friday, September 14, 2012

Biashara ya vyuma chakavu na ufisidi (ni ufisidi, siyo ufisadi)

Miaka kadhaa iliyopita, mafundi toka Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) walijenga mnara mdogo wa kumbukumbu kijijini Butiama, sehemu ambapo ilianguka ndege ya kivita aina ya Mig, mara baada ya kuanza vita vya Kagera mwaka 1978.

Ujenzi huo uliambatana na njia ya kupita kwa miguu iliyojengewa mabomba ya chuma kuanzia barabara kuu mpaka sehemu ilipoanguka ndege, umbali wa kama mita 100 hivi.


Manara wa kumbukumbu ilipoanguka ndege ya JWTZ, eneo la Mwitongo, Butiama. Vyuma vyote vilivyo pembeni vimenyofolewa na wachuuzi wa vyuma chakavu.
Haikupita muda mrefu, wachuuzi wa biashara ya vyuma chakavu walikata mabomba yote na kuyapeleka kwa wanunuzi wa vyuma chakavu. Mnunuzi mmoja mkku wa vyuma chakavu yuko Mwanza.

Ni hawa hawa unaweza kuwasikia wakipigia makelele kuwepo kwa ufisidi (ni ufisidi, siyo ufisadi) nchini, wakinyoosha vidole kwa baadhi ya viongozi wetu, wakati hata wao wanayoyafanya hayapishani sana na yale wanayoyakemea.

Thursday, September 13, 2012

Mada yangu ya leo: kufahamu Kiingereza siyo kuwa msomi

Mada yangu leo si ndefu sana, lakini naamini ni muhimu.

Nianze na tukio moja la zamani. Niliwahi kufahamiana na raia mmoja wa Uingereza ambaye aliishi na kufanya kazi Dar es Salaam kwenye miaka ya tisini, akiwa mwajiriwa wa kampuni moja ya ulinzi. Huyu alikuwa mtu mmoja mcheshi, na mchangamfu kwa wengi aliyefahamiana nao ingawa kwa aliyewaongoza kazini alikuwa mkali sana.

Kuna Mtanzania mwenzangu ambaye naye alikuwa akifahamiana naye na alimheshimu sana, siyo tu kama binadamu mwenzake lakini naamini kwa wadhifa wake muhimu wa kuongoza kampuni yenye wafanyakazi wengi wenye jukumu la kulinda mali na makazi ya wateja wa hiyo kampuni.

Miaka kadhaa ilipita na yule Mtanzania mwenzangu siku moja aliniambia: "Unafahamu? Kumbe yule jamaa amesoma mpaka darasa la nne tu!"

Mtanzania mwenzangu, ambaye alikuwa na shahada ya chuo kikuu, hakuamini kuwa mtu aliyemdhania ni msomi mwenzake kumbe alikuwa amesoma mapaka darasa le nne tu, pamoja na kupewa jukumu la kuongoza kampuni moja mashuhuri ya Tanzania.

Tatizo nililoliona mimi lilikuwa la lugha. Kwa kipimo cha Mtanzania mwenzangu yule Mwingereza alikuwa anazungumza Kiingereza safi kabisa kuliko ambacho yeye alikuwa anamudu kuongea na kwa mantiki aliyofikia ingekuwa ni dhahiri kuwa yule jamaa alikuwa ni msomi. Kwa sababu tu anaongea Kiingereza kizuri kuliko cha kwake.

Nilimuuliza: "Sasa utamdharau kwa sababu ya ya elimu yake, wakati wote huo ukimwona ni mtu wa maana sana?"

Haya yalitokea zaidi ya miaka 20 iliyopita lakini tatizo la kumpa mtu uzito mkubwa zaidi kwa sababu anaongea Kiingereza vizuri bado lipo mpaka leo.

Jeneral Ulimwengu achangia majadiliano ya katiba mpya

Kwa idhini ya Jenerali Ulimwengu, natoa sehemu ya mada ailiyotoa kwenye kongamano la kujadili katiba mpya lililofanyika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, tarehe 15 Januari 2012.

************************************************
Ninavyoangalia jamii ya Tanzania ilivyo sasa hivi, pamoja na mambo yote mema tuliyonayo, tumejaliwa watu wenye kuheshimiana, wenye kupendana,  kwa kiwango kikubwa. Tunaanza kuchukiana chukiana, lakini kwa sababu ya mipangilio mibaya na kujitawala vibaya. Lakini kimsingi, watu wetu ni watu wema. Watawala wao ndiyo waovu.
 
Matokeo yake ni kuwa tumejenga jamii ya watu katika kiwango ambacho kinatisha cha watu wa aina zifuatazo:-
-          Watu wasioaminika
-          Matapeli
-          Wababaishaji
-          Na wapuuzi
Sisi, pamoja na watawala wetu.
 
Watu warushaji katika mahusiano ya kibiashara kiasi kwamba hatuaminiki katika nchi jirani. Mara mafuta yamechakachuliwa; mara ukiuza pamba wameweka mawe. Ali mradi, tumekuwa sisi ni waNigeria wa eneo hili la Afrika.
 
Watu tunaoonea wanyonge. Kuwaibia masikini. Kuwapora wahanga wa ajali, na kuwaua albino kwa imani za kijinga. Washirikina tunaoamini ujinga wakati uthibitisho wa teknolojia tunao mikononi. Kwamba tunaweza ku-Google, search engine ya Google, kutafuta mchawi mahiri yuko wapi.
 
Ujuha wa kiasi hicho. Na wengine sasa wanakwenda bungeni. Watu na jamii fasta fasta. Wenye tamaa ya kupata utajiri wa haraka bila kufanya kazi. Tumekubali wito wa:
-          Kuwa mjanja!
-          Chizika!
-          Pandisha mzuka!
-          Full kujirusha!

 Ambayo yote yametujaza upuuzi wa kibambucha.

Jamii isiyopenda kujifunza. Tumevifanya vitabu ni kama wakwe zetu, tunaogopa kuvifunua wakati tunaona jinsi majirani zetu, kwa mfano, Kenya, vijana wanavyohangaika kujisomea. Ukienda Nairobi, nenda Saritz Centre, uende bookshop ile angalia jinsi wanavyosoma halafu mnaogopa Wakenya watachukuwa nafasi zetu; Wakenya watachukuwa ardhi yetu.

Bora waje Wakenya kuliko kuwa na wajinga wakaharibu nchi hii. 

Watu wakutoa majibu mepesi mepesi kwa maswali mazito. Kwa sababu hatupendi kusumbua akili zetu. Wapiga kura wanaouza kura zao kwa bakuli la kunde, na kisha kulalamika wasipopata uongozi wa kuwafanyia kazi. Watu wasiojua misingi ya haki. Wanaochoma moto mwizi wa kuku, lakini mwizi wanamchagua kumpeleka bungeni.

Kumi, kwa ufupi, watu na jamii iliyopotea.

Jamii hii haiwezi kuandika katiba. Mpaka i-address masuala haya. Mimi naamini kabisa tukienda kuandika katiba sasa hivi, nakubaliana na Issa [Prof. Issa Shivji], kwamba kama hiyo Tume ya Rais itakuwa na watu wanawakilisha makundi mbalimbali, itaanza kuzungumza na hali yenyewe tuliyo nayo ndiyo hii, yaani fanya unavyotaka, hutapata chochote cha maana kwa sababu humu ndani kutakuwa na wezi, wazandiki, matapeli, wababaishaji, wala rushwa. Kila mtu anajaribu kuweka nafasi yake mbele. Na maslahi yake mbele.

Sasa tufanye nini? Yuko Mzee Ibrahim Kaduma hapa. Natumai kuwa kitabu chake kilichozinduliwa juzi kitakuwa hapa. Ili kupambana na haya niliyoyasema, ambayo ni magonjwa makubwa, ni majanga makubwa, na ndiyo yanatawala, hebu turudi kwenye misingi.

Moja: Binadamu wote ni ndugu zangu na Afrika ni moja.
Nitatumikia nchi yangu na watu wake wote.
Nitajitolea nafsi yangu kuondoa umasikini, ujinga, maradhi, na dhuluma.
Ongeza na rushwa.
Nne: Rushwa ni adui wa haki sitapokea wala kutoa rushwa.
Cheo ni dhamana, sitatumia cheo changu wala cheo cha mtu mwingine kwa faida yangu.
Hebu niambie ni watu gani ndani ya Serikali wanaweza kusimama hadharani wakasema maneno haya?
(Hadhira: hawapo!)
Sasa tuwafanye wayaseme haya. Katika uandikaji...katika mchakato mzima wa kujadili katiba mpya, tufike mahala tuwalazimishe watu waliomo katika utawala, wasimame mbele yetu waseme hivi: Cheo ni dhamana. Sitatumia cheo changu wala cha mtu mwingine kwa manufaa yangu. Waseme! Halafu tuwapime.
Nitajielimisha kwa kadri ya uwezo wangu na kutumia elimu yangu kwa faida ya Nchi.
Nyie wasomi hapa chuoni mnasema hiyo? Au? Nasikia wanafunzi wengi sana mnasoma accountancy. Accountancy ni somo zuri lakini sasa sijui mnataka kwenda kufanya kazi wapi?
Nitashirikiana na wenzangu wote kujenga nchi yetu.
Nitasema kweli daima. Fitna kwangu mwiko.
Nitakuwa raia mwema wa Tanzania, Afrika, na Dunia nzima.

Tuyatafakari hayo. Tuwe na muafaka wa kitaifa. Tuwe na maridhiano, tuwe na makubaliano. Tuwe na national charter,  kutokana na hilo sasa ndiyo twende na michakato mingine aliyosema Shivji [Prof. Issa Shivji] ya kujenga misingi ya maelewano nchini na kuandika katiba mpya itakayotuongoza kwa miaka hamsini au mia ijayo. Nawashukuruni sana.