Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Tuesday, September 30, 2014

Mila na tamaduni: Watanzania ni wakarimu (sehemu ya tano)

Hivi karibuni nimemaliza mzunguko wa kazi na mazoezi nikitumia baiskeli wa takriban kilomita 174 ndani ya mikoa ya Mwanza na Mara. Imenipa fursa ya kuthibitisha kuwa utamaduni wa ukarimu miongoni mwa Watanzania bado uko imara.

Jiunge nami kwenye sehemu ya tano na ya mwisho ya msafara huu...

Agosti 5
Ni zaidi ya kilomita 40 toka Bunda kuelekea Butiama na safari inaenda vizuri tu nikiwa nimejaa shauku ya kumaliza hili zoezi.
Hata hivyo adui mkubwa wa masafa marefu kwa baiskeli ni njaa na suala la kupata chakula cha mchana ni muhimu kabisa ili kuweza kuendesha baiskeli kwa saa zaidi ya tano kwa siku ya leo. Naenda kwa wastani wa kilomita kama 11 kwa saa. Kwa hiyo nalazimika kusimama tena Nyamisisi kukamilisha mlo wangu wa mchana kabla ya kuendeela na safari hadi Butiama. Nyamisisi ni sehemu ambayo siyo mashuhuri tu kwa matunda ila ina sifa ya kuwepo wataalamu juu ya taarifa za wanasoka na wasanii maarufu.

Napumzika sehemu ambayo nilikaa na Elvis Lelo Munis miezi kadhaa iliyopita alipopita hapa akielekea Nairobi na baadaye Moshi. Elvis ni Mtanzania ambaye alizunguka nchi zaidi ya mia moja za dunia akitumia baiskeli na alimaliza ziara yake hiyo ya maelfu ya kilomita mwezi Julai 2014. Nimekula chipsi mayai na baadaye naanza ngwe ya mwisho ya mzunguko wangu.
Mimi namalizia ziara yangu ya kilomita zaidi ya 170 lakini nahisi nahitaji mapumziko baada ya safari yangu ya kutoka Ukerewe mpaka Butiama.

Saturday, September 27, 2014

Mila na tamaduni: Watanzania ni wakarimu (sehemu ya nne)

Hivi karibuni nimemaliza mzunguko wa kazi na mazoezi nikitumia baiskeli wa takriban kilomita 174 ndani ya mikoa ya Mwanza na Mara. Imenipa fursa ya kuthibitisha kuwa utamaduni wa ukarimu miongoni mwa Watanzania bado uko imara.

Jiunge nami kwenye sehemu ya nne ya msafara huu...

Agosti 4
Sijaendesha baiskeli kwa masafa marefu kwa muda mrefu kwa hiyo leo naanza kusikia mwili unapanga njama za kuanzisha mgomo wa kutoendelea na safari. Hata hivyo hii ni njia ambayo nimeshawahi kupita kwa baiskeli kuelekea Ukerewe na muda si mrefu najikuta nimefika kwenye kiwanda cha kuchambua pamba cha Bulamba.

Inanipa matumaini kuwa safari ya kwenda Bunda imepungua kwa kiasi kikubwa. Nilipokaribia Bunda nilikimbiliwa na mtoto wa miaka sita hivi akaniomba pesa. Huwa nawakanya watoto wasiwe na tabia ya kuomba pesa kwa wapita njia ili kulinda usalama wao. Hata hivyo kwa leo ninakiuka taratibu zangu mwenyewe na kufanya naye majadiliano yafuatayo:

"Unataka pesa za nini?"
"Za kununulia pipi."

Hapo nilifungua mfuko wangu na kutoa kipande cha chokoleti kilichochanganywa na karanga. Alipofungua kifungio naamini ile taswira ya alichokiona ilimfanya asite kidogo akaniuliza:

"Hiki ni nini?"
"Kula tu ni tamu sana."

Alivyoonja alicheka ghafla akiwa na furaha isiyo na kifani halafu akaniambia: "Uwe unapita hapa kila siku!"
Alipofungua chokoleti alisita kuila.
Alinisababisha mimi pia kucheka.

Taarifa inayofuata: Naagiza chipsi mayai

sehemu ya tatu ya makala hii

Wednesday, September 24, 2014

Mila na tamaduni: Watanzania ni wakarimu (sehemu ya tatu)

Hivi karibuni nimemaliza mzunguko wa kazi na mazoezi nikitumia baiskeli wa takriban kilomita 174 ndani ya mikoa ya Mwanza na Mara. Imenipa fursa ya kuthibitisha kuwa utamaduni wa ukarimu miongoni mwa Watanzania bado uko imara.

Jiunge nami kwenye sehemu ya tatu ya msafara huu...

Agosti 3
Mapema asubuhi nilianza safari yangu ya baiskeli ya kurudi Butiama kwa kuelekea kwenye kivuko cha Rugezi na ni leo ndiyo iliyodhihirisha kwangu kuwa Watanzania bado watu wakarimu. Nilipovuka upande wa pili kwenye mji mdogo wa Kisorya, nilisimama kwa muda kwenye mgahawa kuongeza mlo wa asubuhi wa chapati mbili na chai, ingawa ilikuwa inakaribia saa tano asubuhi.

Nikiwa na uhakika kidogo wa kuendelea na safari yangu mpaka njaa itakaponilazimisha kusimama na kula chakula cha mchana, nilianza safari ya kuelekea Kibara. Hata hivyo haikuchukuwa muda nikalazimika kusimama kutafuta chakula kwenye kijiji kilicho njiani.

Pembeni yangu niliona jengo linafanana na mgahawa. Alitokeza binti mmoja na mazungumzo yakawa hivi:

"Una chakula?"
"Ndiyo"
"Chakula gani?"
"Chai na chapati"
"Mimi nimeulizia chakula, siyo chai."
"Samahani, nina chai na chapati tu."

Niliendelea kudadisi:

"Kwani wewe mchana huli chakula?"
"Nitakula.
"Unapika nini?"
"Ugali na dagaa."
"Basi ongeza na cha kwangu halafu nitakulipa."

Akakubali. Chakula kilipokuwa tayari akanikaribisha kwenye mgahawa wake, akanipa maji ninawe na yeye akanawa tukakaa pamoja kula.
Niliegesha usafiri wangu, nikapiga picha, halafu nikaingia kusubiri chakula.
Wakati nakaribia kushiba nikapata nguvu za kuongea kidogo na kumwomba radhi kuwa nimempunguzia chakula chake kwa siku hiyo. Aliniambia nisijali, na kuwa labda kuna siku na yeye atanitembelea na mimi nitamkaribisha chakula.

Nikijiandaa kuondoka nilimuuliza nimlipe kiasi gani kwa kile chakula. Alinishangaa na kuniambia: "Wewe si nilikwambia kuwa hakuna tatizo? Pesa za nini?"

Nikabaki hoi. Lakini nilifungua mfuko wa baiskeli yangu na kutoa pakiti ya biskuti nikampa na kusema ni zawadi kwa watoto wake. Alifurahi sana na kuniuliza bei ya biskuti zile. Nilimwambia shilingi elfu tatu nikapanda basikeli na kuanza safari ya kuelekea Kibara.

Vijijini wema huu bado upo. Sina hakika kama mijini hali imebakia hivi.

Taarifa ijayo: Hiki ni nini?

Sehemu ya pili ya makala hii

Saturday, September 6, 2014

Mila na tamaduni: Watanzania ni wakarimu (sehemu ya pili)

Hivi karibuni nimemaliza mzunguko wa kazi na mazoezi nikitumia baiskeli wa takriban kilomita 174 ndani ya mikoa ya Mwanza na Mara. Imenipa fursa ya kuthibitisha kuwa utamaduni wa ukarimu miongoni mwa Watanzania bado uko imara.

Jiunge nami kwenye sehemu ya pili ya msafara huu...

Agosti 2
Tulitembelea makazi ya kwanza walipofikia Wakristu wa kwanza kutua kwenye kisiwa cha Ukerewe zaidi ya miaka 100 iliyopita. Hakuna maelezo mengi sana kuhusu eneo hili ila simulizi za mauaji yaliyofanyika hapo dhidi ya baadhi ya wageni hao na mtawala wa eneo hilo wa wakati huo. Ni eneo ambalo liko kwenye kilima chenye mwinuko mkubwa unaowezesha kuona umbali mkubwa juu ya Ziwa Viktoria. Mwenyeji wangu aliniambia kuwa nyakati ambapo hakuna ukungu yawezekana kuona ndege zikipaa na kutua kwenye uwanja wa ndege wa Mwanza.
Ukerewe ni kisiwa chenye mandhari za kuvutia na visiwa vingi vinavyokizunguka. Upande wa kulia wa picha kinaonekana kisiwa cha Bwiru.
Baada ya hapo tulitembelea eneo la ufukweni wa ziwa ambapo mjasiria mali mmoja wa Nansio, makao makuu ya wilaya ya Ukerewe, anajenga hoteli itakayozingatia utunzwaji wa mazingira wa eneo hilo.

Taarifa ijayo: Watanzania ni watu wakarimu

sehemu ya kwanza ya makala hii
sehemu ya tatu ya makala hii