Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Friday, December 27, 2013

Mandela! Mandela! Mandela! (Sehemu ya Tatu na ya Mwisho)

Kwenye makala hii ambayo imegawanywa kwenye awamu tatu, Notburga Maskini anaandika kuhusu Mzee Nelson Mandela, aliyefariki tarehe 5 Desemba na alizikwa  tarehe 15 Desemba 2013 kwenye kijiji cha Qunu nchini Afrika ya Kusini.

Mandela! Mandela! Mandela! (Sehemu ya Tatu na ya Mwisho)
Na Notburga Maskini*

Heshima katika historia ya nchi na dunia
Kilio kinachoendelea hivi sasa na heshima kubwa waliyopewa mashujaa wetu waliolala ni changamoto kubwa kwa kizazi kinachofuata. Walijitoa thamani kupigania heshima ya binadamu. Kinachoendelea sasa ni heshima kubwa kwao hata wakiwa wamelala na kama alivyowahi kusema Mzee Mandela katika nukuu zake: “Ukijiheshimu hata simba atakuogopa na kukuheshimu”. Taarifa zilizotangazwa na gazeti moja nchini kuwa Alqaida na al Shaabab hawatafanya mashambulizi katika kipindi hiki cha maombolezo ni kielelezo cha ukweli wa nukuu hiyo ya shujaa wetu, Baba wa Taifa la Afrika ya Kusini.
 
Waombolezaji wakitoa heshima zao za mwisho kwa Hayati Nelson Mandela tarehe 11 Desemba 2013, wakati mwili wake ulipohamishiwa kwenye majengo ya Union jijini Johannesburg. (Picha ya GCIS).
Hii ni heshima japo yeye hafungamani na itikadi wala vitendo vya makundi hayo bali anafungamana na upendo, msamaha na kutokulipa visasi. Naamini iwapo dunia itajifunza haraka kutoka kwa shujaa huyu pengine vitendo hivi vinaweza kuisha na wahusika kuendelea kuwa watu wa amani.

Je tuko tayari kujifunza?
Sisi tuliobaki nyuma pamoja na kuomboleza tuna maswali ya kujiuliza na kutoa majibu sasa, iwapo:
1)      Tuko tayari kurejesha na kuendeleza mfumo wa kidhalimu unaodhalilisha na kunyonya binadamu wengine hasa wafanyakazi na wakulima;
2)      kuwafanyisha kazi ngumu wafanyakazi na wakulima bila kuwalipa ujira stahiki au kuratibu bei za mazao yao kwa kisingizio cha utandawazi huku kukiwa na lengo la kushirikiana na wanyonyaji kujilimbikizia mali binafsi kupitia jasho lao;
3)      kuendeleza wizi wa mali za umma, matumizi mabaya ya madaraka dhidi ya wanyonge na kupuuza ustawi na maendeleo yao.

Ama:
1)      Tunadhamiria kujifunza kwa mashujaa wetu Mzee Mandela na Mwalimu Nyerere, kuenzi maisha yao, na kuendeleza mema yao, kwa kuwa wafanyakazi bora, watumishi waadilifu, wabunifu, na waaminifu wa wananchi wetu;
2)      Haki na nafasi za raia kumiliki rasilimali za mataifa yetu kwa usawa zinalindwa na kuwezeshwa hata kama maisha na maslahi binafsi yatatishiwa;
3)      Tutawalinda na kutetea haki za kiraia, na kuishi bila kuwatisha, kuwauwa katika kulipiza visasi au mapigano ya wenyewe kwa wenyewe,  kwa lengo la kustawisha jamii, kuondoa umaskini, na kudumisha heshima ya binadamu iliyoasisiwa na mashujaa hawa.

Kupokea mauti kwa ujasiri na fedheha za kiuongozi
Inaleta maana kuchagua kulinda na kutanguliza maslahi ya umma na Taifa, ili historia isije tuhukumu kwa kutotimiza wajibu tunaopaswa kufanya kwa jamii na nchi zetu wakati wa uhai wetu. Hali hii itatuwezesha kupokea mauti kwa ujasiri na imani kubwa. Kitendo cha fedheha kilichomkuta kiongozi mkuu wa sasa wa Afrika Kusini kuzomewa mbele ya uso wa dunia  na wananchi wake waliomchagua kidemokrasia si cha kupuuzwa hata kidogo. 

Ni muhimu kujifunza na kujitahidi kubadilika ili kuepusha shari na matokeo mengine mabaya ambayo huletwa na tabia za viongozi kuonekana wanajijali binafsi. Kuwaumbua viongozi hasa wale wasiojitambua husababisha hasira na kulipiza kisasi kwa wanaothubutu kufanya hivyo. Hali hii husababisha mitafaruku; huweza kugawa taifa na kuondoa amani. Naamini yote mazuri yaliyopiganiwa wakati wa uhai wa Mzee Mandela na Mwalimu Nyerere yamewekwa katika msingi imara ya kuwezesha kuyaendeleza. Kazi kubwa ni kwa tuliobaki nyuma kuamua na kuanzia walipoachia.

Kwaheri Mzee Nelson Rolihlalha Mandela. Mungu akupumzishe kwa amani na raha ya milele akujalie kama ulivyonuwia katika matendo na maisha yako.


*Notburga A Maskini ni Kaimu Rais wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (TUCTA).

Friday, December 20, 2013

Leo kumbukumbu ya kufariki Hayati Alex Nyirenda

Leo ni miaka mitano tangu kufariki Hayati Brigedia Alex Gwebe Nyirenda aliyefariki Dar es Salaam mwaka 2008 kwa ugonjwa wa saratani ya koo.

Usiku wa tarehe 8 Desemba mwaka 1961, muda mchache kabla ya kutimia saa 6:00 kamili usiku, siku ambapo Tanganyika ilipata uhuru wake, Brigedia Nyirenda alikuwa kileleni mwa Mlima Kilimanjaro kupandisha bendera ya taifa jipya la Tanganyika wakati bendera ya Uingereza ilipokuwa inateremshwa kwenye uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Luteni Alex Nyirenda, akiwa na bendera ya Tanganyika na Mwenge wa Uhuru kwenye kilele cha Mlima Kilimanjaro siku Tanganyika ilipopata uhuru wake, tarehe 9 Desemba 1961. (Picha ya Idara ya Habari, Maelezo
Miaka mwili kabla, tarehe 22 Oktoba 1959, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, akihutubia Baraza la Kutunga Sheria, alisema yafuatayo:

Sisi watu wa Tanganyika tunataka kuwasha mwenge na kuuweka juu ya Mlima Kilmanjaro umulike nje ya mipaka yetu na kuleta tumaini pale ambapo kulikuwa hakuna matumaini, upendo pale ambapo palikuwa na chuki, na heshima pale 

palipojaa dharau.

Miaka miwili kabla, tarehe 22 Oktoba 1959, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, akitoa hotuba kwenye Baraza la Kutunga Sheria, alisema yafuatayo: 
Huu mwenge ambao baadaye ulikuja kujulikana kama Mwenge wa Uhuru ulisimikwa juu ya Mlima Kilimanjaro na Nyirenda, ukiashiria msimamo wa muda mrefu na usiotetereka wa Tanzania kuunga mkono juhudi za ukombozi wa nchi za Kiafrika ambazo katika miaka ya mwanzo ya sitini zilibaki chini ya ukoloni na tawala za kibaguzi.

Mwaka 1958 Nyirenda alikuwa Mtanganyika wa kwanza kuhitimu kutoka Chuo cha Kijeshi cha Sandhurst cha nchini Uingereza. Aidha, kabla ya uhuru, alikuwa Mwafrika wa kwanza kuwa afisa ndani ya Kings African Rifles, jeshi la kikoloni la Uingereza ambalo baada ya uhuru ndiyo likabadilishwa na kuwa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ).

Alikuwa na uhusiano wa kiukoo na rais wa zamani wa Zambia, Dk. Kenneth Kaunda, jambo ambalo linakumbusha Waafrika kwamba wako karibu sana kuliko mipaka ya nchi zao inavyoashiria.

Wednesday, December 18, 2013

Lugha Yetu Kiswahili

Hivi karibuni, wakati nikisikiliza matangazo ya Idhaa ya Kiswahili la Shirika la Utangazaji la Uingereza (BBC) mtangazaji alisoma taarifa za majeshi ya Umoja wa Mataifa yaliyoko mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo kuanza kutumia ndege zinazosemekana kuruka bila rubani, kwa Kiingereza zikijulikana kama drones.

Ukweli ni kuwa ndege hizo zinaongozwa na marubani ambao wako ardhini kwenye vituo maalum.

Mtangazaji alitumia neno "drone" lakini akauliza iwapo lipo neno la Kiswahili lenye kutoa maana hiyo hiyo. Mimi haraka haraka niliangalia kwenye kamusi ya Kiingereza kwa Kiswahili ya Taasisi ya Uchungizi wa Kiswahili (TUKI), toleo la mwaka 2006, na nikatuma ujumbe mfupi wa maandishi BBC: "drone ni nyuki dume."

Wasikilizaji wengine nao wakatuma majibu yao, mmoja akipendekeza kuwa tafsiri sahihi iwe "ndege tiara." Hayakuwa mashindano na hakuna aliyepewa zawadi yoyote, lakini nakiri kuwa "ndege tiara" inasikika vizuri zaidi kuliko "nyuki dume."

Habari inayozungumzia shambulizi la nyuki dume dhidi ya wapiganaji itachukuliwa na maana kuwa ni nyuki ndiyo waliofanya shambulio hilo na siyo ndege inayoruka angani.

Wataalamu wa lugha ya Kiswahili mnasemaje?

Hatua kumi za mauaji ya kimbari: 7 na 8

Nimetembelea Rwanda hivi karibuni na nikiwa huko nilipata fursa ya kutembelea mojawapo ya vituo vya kumbukumbu ya mauaji ya kimbari ya mwaka 1994.

Jambo moja la msingi ambalo Watanzania tunaweza kijufunza ni kuwa maafa yaliyotokea Rwanda yanaweza kutokea pia Tanzania. Kwa mujibu wa wachunguzi wa sababu zinozogeuza binadamu mmoja kuwa adui wa binadamu mwenzake na hata kufikia hatua ya kumaliza uhai wa mwenzake ziko duniani kote.

Sababu hizi zinaanza na mchakato wenye hatua nyingi ambao hufikia mauaji kama yale yaliyotokea Rwanda. Kinachozuwia maafa kama hayo kutokea ni hatua mahususi zinazopaswa kuchukulia na jamii za kukatisha uendelezwaji wa huo mchakato.

Kwa mujibu wa Dr. Gregory Stanton wa Genocide Watch, hatua za viashiria vya kuwepo kwa mchakato na za kuzuwia maafa kama ya Rwanda ziko kumi.

Hatua ya Saba: Mipango

Hatua hii inahusisha kuunda mfumo wa kijeshi, kutoa mafunzo kwa wanamgambo, kukusanya silaha za maangamizi, na kuzitawanya kwa wauaji.

Hatua za kuepusha Mipango

Pale inapothibitishwa dalili za mipango kufanyika, basi tahadhari juu ya uwezekano wa kutokea mauaji ya kimabri utolewe. Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa litowe onyo kuwa litakuwa tayari kuchukua hatua pale tu ambapo lina uhakika kuwa litachukua hatua madhubuti za nguvu dhidi ya wahusika. Viongozi wa dunia wawaonye wale wanaokusudia kutenda maangamizi kuwa watachukuliwa hatua dhidi ya uhalifu watakaoufanya. Msaada wa kibinadamu unadaliwe. Majeshi ya kikanda yaandaliwe na kupewa uwezo wa kujiandaa na wa kifedha.
"Amri Kumi za Gitera" ni waraka uliotolewa na kiongozi wa kabila wa Wahutu kuchochea mauaji ya kabila la Watusi kabla ya mauaji ya kimbari ya Rwanda.  

Hatua ya Nane: Mateso

Katika hatua hii watu wanagawanywa kwa misingi ya ukabila na dini. wahanga wananyang'anywa mali zao. Wahanga hufukuzwa kutoka kwenye nyumba zao. Katika baadhi ya nchi wahanga walihamishwa na kuwekwa kwenye maeneo mahususi ya miji.  Katika baadhi ya nchi wahanga walikusanywa kwenye kambi za wakimbizi wa ndani.

Itaendelea na: 
  • Hatua ya Tisa: Mauaji
  • Hatua ya Kumi: Ukanushaji
Taarifa nyingine zinazohusian na hii:

Tuesday, December 17, 2013

Mandela! Mandela! Mandela! (sehemu ya pili ya awamu tatu)

Kwenye makala hii ambayo imegawanywa kwenye awamu tatu, Notburga Maskini anaandika kuhusu Mzee Nelson Mandela, aliyefariki tarehe 5 Desemba na kuzikwa leo, tarehe 15 Desemba 2013 kwenye kijiji cha Qunnu nchini Afrika ya Kusini.

Mandela! Mandela! Mandela! (Sehemu ya Pili)
Na Notburga Maskini*

Migongano ya Kitabaka
Matabaka ya mabwana na watwana yalijitokeza kutokana na unyonyaji, udhalilishaji, na ubaguzi uliofanywa na makundi dhalimu ambayo yalijitokeza na kuonekana katika mifumo ya kijamii kwa maana ya Ukomunisti na Ubepari ambapo mabwana au wenye nguvu, waliwadhalilisha wanyonge; ilitengeneza tabaka la watu wachache matajiri wa kupindukia ambao wameshikilia na kuwekeza asilimia 80 ya utajiri wa dunia katika mtaa wa tano (the 5th Avenue New York).  

Tabaka la pili ni la umma wa wakulima na wafanyakazi maskini na wanyonge katika nchi zetu na duniani ambao bidii na jasho lao haviwawezeshi kujikwamua kutokana na mirija ya dhuluma iliyopangwa na tabaka hili  la watu wachache lakini lenye nguvu kubwa kiuchumi na kiutawala. Tabaka la tatu ni tabaka la maskini wa kutupwa miongoni mwao wakiwemo wazee, wastaafu, vijana wasio na ardhi wala ajira, wanawake na watoto.

Hali hii  ya kuhuzunisha na tishio kwa amani ya nchi zetu na dunia ilionekana mapema machoni na kwenye mioyo ya viongozi hawa mashujaa Nelson Rolihlahla Mandela na Mwalimu Julius Kambarage Nyerere. Waliichukia na kufanya bidii kubwa kuchukua hatua sawia kupambana ili kuona mfumo wa haki usawa na heshima kwa binadamu unasimikwa dhidi ya mifumo ya unyonyaji, ubaguzi na udhalilishaji.

Kazi iliyobaki ya kugawa rasilimali hizi za dunia ziweze kuwafikia watu wengi na kuondoa umaskini duniani ndio njia pekee ya kumuenzi Mzee Mandela bila unafiki. Tunahitaji mashujaa kama Mzee Nelson Mandela na Mwalimu Julius Kambarage Nyerere ambao wataweka ushawishi na kupambana hasa wakati huu zinapoonekana dalili kuwa jambo hili linawezekana. Kifo cha shujaa huyu  tumeshuhudia viapo na dhamira zikiwekwa kanisani na hadharani kuashiria kuwa tayari hata kufa ili kutetea ustawi wa binadamu na amani duniani. 


State Funeral of former President Nelson Mandela, 15 Dec 2013
Picha: Maafisa wa jeshi la Afrika ya Kusini wakiwa wamebeba jeneza lenye mwili wa Marehemu Nelson Mandela kwenye mazishi ya taifa yaliyofanyika tarehe 15 Desemba 2013 kwenye kijiji cha Qunu, jimbo la Eastern Cape.

Kusaliti na kuvunja tabaka
Mzee Nelson Mandela na Mwalimu Julius Nyerere ni miongoni mwa watu waliojaaliwa na Mwenyezi Mungu kuumwa na kuchukizwa na hali mbaya ya binadamu wote. Waliona ubaya na adha inayotokana na binadamu kumdhalilisha binadamu mwingine na hatari yake kwa amani ya dunia hivyo hawakuivumilia hata kwa sekunde chache. Walipinga hali hii pamoja na uwezo waliokuwa nao kutokana elimu na nafasi zao za kuzaliwa wakiwa watoto wa machifu, ambapo wangaliweza kuungana na wadhalilishaji na kuwa wanufaikaji wa mifumo dhalimu iliyojaa uroho, uchoyo, dharau, na tamaa.

Mzee Mandela na Mwalimu Nyerere walizungumza kwa sauti kubwa na hivyo kuweka ushawishi mkubwa ndani ya jamii na nchi zao na kuanzisha vuguvugu la mapambano yaliyokusudia kuleta heshima kwa binadamu. Ni dhahiri kuwa walitumia maisha yao hapa duniani kujitoa mhanga kwa ujasiri wa kupindukia hata kuuwa matabaka yao (class suicide) kupigania usawa haki na heshima kwa binadamu. Ndiyo maana kuondoka kwao duniani Mzee Nelson Mandela aliyetanguliwa na rafiki yake mkubwa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere muongo mmoja na nusu uliopita kunaleta mshtuko na wasiwasi mkubwa kwa amani ya dunia, usawa, ubinadamu, demokrasia, na utawala bora.  Hii inatokana na ukweli kwamba binadamu wa aina hii hutokea kwa nadra sana.

Itaendelea na: Heshima katika historia ya nchi na dunia


*Notburga A Maskini ni Kaimu Rais wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (TUCTA).

Sunday, December 15, 2013

Mandela! Mandela! Mandela! (sehemu ya kwanza ya awamu tatu)

Kwenye makala hii ambayo imegawanywa kwenye awamu tatu, Notburga Maskini anaandika kuhusu Mzee Nelson Mandela, aliyefariki tarehe 5 Desemba na kuzikwa leo, tarehe 15 Desemba 2013 kwenye kijiji cha Qunnu nchini Afrika ya Kusini.

Mandela! Mandela! Mandela! (Sehemu ya Kwanza)

Na Notburga Maskini*

Hiki kimekuwa ni kilio cha dunia nzima kumwomboleza shujaa mpigania uhuru, amani, haki, utu na utawala bora duniani, mwana wa bara la Afrika mwenye asili ya Afrika ya Kusini Nelson Rolihlahla Mandela mwanaharakati, kiongozi wa chama cha ANC na Rais Mstaafu wa Afrika ya Kusini; aliyeaga dunia tarehe 5 Desemba 2013.  Mimi binafsi na kwa niaba ya wafanyakazi wa Tanzania naungana na Watanzania wenzangu, wafanyakazi wa Afrika ya Kusini na Dunia kuomboleza msiba huu mkubwa ambao ni pigo kubwa kwa tabaka la wafanyakazi duniani na vilevile ni pigo dhidi ya utawala bora, haki, amani na utu. 

South Africans mourn the
death of the late former President Nelson Mandela, 8 Dec 2013
Picha: Wanachama wa Umkhonto We Sizwe, lililokuwa jeshi la chama cha African National Congress lilioendesha mapambano ya kivita dhidi ya utawala wa kibaguzi wa Afrika ya Kusini, wakiwasili kwenye makazi ya jijini Johannesburg ya marehemu Nelson Mandela tarehe 8 Desemba 2013. (Picha ya GCIS).

Niandikapo makala hii nakumbuka mwaka 2003 nilipokuwa jijini Johannesburg kuhudhuria mkutano wa dunia kuhusu uwekezaji wa mitaji Afrika, Kusini mwa Sahara kwenye ukumbi mmojawapo katika jengo maarufu la Sandton. Wakati wa kutoka ukumbini tulikutana nae ana kwa ana mlangoni akiwa na watu wengine, nafikiri kiongozi huyu alitokea kwenye ukumbi mwingine wa mkutano katika jengo hilo. Binafsi nilifurahi sana kumuona Mzee Mandela aliyekuwa katika hali ya kawaida kabisa. Hata hivyo mimi na hata wenzangu hatukuweza kufanya chochote angalau kuweza kumsalimia kutokana na kutofahamu taratibu na mipaka ya kiitifaki.  Alikuwa ni kivutio kikubwa kwetu sote tuliokuwepo siku hiyo.

Afrika Kusini na Tanzania
Ndugu zetu wa Afrika ya Kusini kama ilivyokuwa kwetu Watanzania tarehe 14 Oktoba 1999 alipotuaga Mwasisi wa Taifa hili, mwanamapinduzi aliyeheshimika duniani, na kipenzi cha Watanzania, Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, nao wanapitia hali ngumu iliyojaa majonzi, vilio, na mashaka lakini pia wakimshukuru Mungu kwa zawadi kubwa aliyoupatia umma wa Afrika Kusini, Bara la Afrika na Dunia.

Katika kitabu chake cha dondoo Nelson Mandela By Himself, 2013 Mzee Mandela anatufariji kwa maneno yake mwenyewe kuwa: 

“kifo hakikwepeki. Wakati binadamu ameshatimiza yale aliyofikiri kuwa ni wajibu wake kwa watu wake na nchi yake, anaweza kupumzika kwa amani.  Naamini kuwa nimefanya bidii kutimiza wajibu huo na ndio maana nitalala katika umilele”  

Ni dhahiri kuwa Mzee Mandela ameondoka akiwa anaridhishwa na bidii kubwa aliyoweka katika kazi kubwa aliyoifanya ya kuondoa ubaguzi wa rangi na udhalilishwaji wa mtu mweusi katika nchi yake ya Afrika ya Kusini. Pengine Watanzania na waombolezaji tuliobaki yafaa kutafakari sasa kuhusu wajibu wetu kwa watu wetu na nchi zetu na iwapo tutaweza kuwa jasiri na kusema maneno hayo siku yetu itakapofika. 

Imani na mapenzi ya Umma dhidi ya chuki za maadui
Mzee Nelson Mandela kama alivyokuwa Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere wameteka mioyo ya walimwengu na wananchi wao kwa imani yao katika utu badala ya vitu, na kusimamia kwa vitendo bila ya kutetereka. Wanamapinduzi hawa wa Afrika waliweka mbele maslahi ya taifa na utu wa watu wao.  Walijitoa muhanga maisha yao yote kwa ajili ya nchi zao na watu wao jambo ambalo ni nadra kwa viongozi wengi tuliowashuhudia katika karne ya ishirini.

Wakati Mwalimu Julius Nyerere akiongoza mapambano ya ukombozi wa Bara la Afrika na dhidi ya udhalimu dhidi ya ubinadamu ikiwemo Afrika Kusini yenyewe, alitengeneza maadui waliotokana na kundi la wakandamizaji waliojijengea uhalali na kuamini kuwa wao ni bora kuliko binadamu wengine. Hata hivyo maadui hao kama tunavyoshuhudia leo wamejirudi na kujifunza thamani ya utu na utaifa katika kutumikia umma. 

Isingewezekana wakati ule wa mapambano ya ukombozi kuwa Afrika ya Kusini ingebadilika na kuwa kama ilivyo sasa. Kinachodhihirika hapa ni nguvu ya upendo, msamaha, na uzalendo kwa nchi na watu wake vinavyoweza kuleta mabadiliko chanya.  Hili ni somo kubwa kwa Afrika na Dunia.

Itaendelea na: Migongano ya Kitabaka

*Notburga A Maskini ni Kaimu Rais wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (TUCTA).


Friday, December 13, 2013

Afrika Kusini waomboleza kifo cha Nelson Mandela

Katika maeneo mbali mbali nchini Afrika Kusini wananchi wamejitokeza kuweka sahihi na kuweka kumbukumbu baada ya kifo cha Mzee Nelson Mandela, aliyefariki tarehe 5 Desemba 2013 baada ya kuugua kwa muda mrefu.

Kwenye picha (juu) wananchi wa Afrika Kusini waliopo Johannesburg wakiandika kwenye bango la kumbukumbu.

Mzee Mandela atazikwa tarehe 15 Desemba 2013.

Sunday, December 1, 2013

Hatua kumi za mauaji ya kimbari: 5 na 6

Nimetembelea Rwanda hivi karibuni na nikiwa huko nilipata fursa ya kutembelea mojawapo ya vituo vya kumbukumbu ya mauaji ya kimbari ya mwaka 1994.

Jambo moja la msingi ambalo Watanzania tunaweza kijufunza ni kuwa maafa yaliyotokea Rwanda yanaweza kutokea pia Tanzania. Kwa mujibu wa wachunguzi wa sababu zinozogeuza binadamu mmoja kuwa adui wa binadamu mwenzake na hata kufikia hatua ya kumaliza uhai wa mwenzake ziko duniani kote.

Sababu hizi zinaanza na mchakato wenye hatua nyingi ambao hufikia mauaji kama yale yaliyotokea Rwanda. Kinachozuwia maafa kama hayo kutokea ni hatua mahususi zinazopaswa kuchukulia na jamii za kukatisha uendelezwaji wa huo mchakato.

Kwa mujibu wa Dr. Gregory Stanton wa Genocide Watch, hatua za viashiria vya kuwepo kwa mchakato na za kuzuwia maafa kama ya Rwanda ziko kumi.

Hatua ya Tano: Uratibu

Kwa kuwa mauaji ya kimbari yanaendeshwa na makundi dhidi ya makundi mengine, yanahitaji kuratibiwa. Kwa kawaida, ni dola inayoratibu maafa haya kwa kutoa fedha na silaha kwa makundi yanayoendesha mauaji.

Mfano wa Uratibu: Rwanda

Tabaka la watu wenye uwezo ndani ya Rwanda walitoa silaha kwa kundi la Interahamwe ambalo liliendesha mauaji. Serikali na wafanyabiashara wa Kihutu walitoa mapanga 500,000 na kuandaa kambi za mafunzo za "kulinda vijiji vyao" kwa kuua Watutsi.

Hatua za kuepusha Uratibu

Kuchukulia makundi yenye muelekeo wa kuchochea mauaji kama makundi ya jinai. Chukua hatua za kufanya uanachama ndani ya makundi hayo kuwa kosa la jinai na kushinikiza viongozi wao kukamatwa.

Kunyima visa kwa viongozi wa makundi haya na kukamata mali zao zilizopo nchi za nje.

Kuweka vikwazo vya silaha dhidi ya makundi yanayoeneza chuki na dhidi ya serikali zinazounga mkono chuki kwa misingi ya dini na ukabila.
Wakati wa mauaji ya kimbari ya Rwanda ya mwaka 1994 kwenye shimo hili zilikutwa maiti za maelfu ya wahanga wa mauaji hayo.

Hatua ya Tano: Kingamizi

Katika hatua hii mambo kadhaa yanajitokea, ikiwa ni pamoja na :

  • wenye siasa kali wanakuwa na nia ya kutenganisha makundi
  • makundi yenye kuchochea chuki na kuchapisha propaganda yenye nia ya kugawa watu
  • sheria zinapitishwa kuharamisha ndoa kati ya watu na makundi yanayokusudiwa kuwa tofauti
  • wenye msimamo wa kati wananyamazishwa, kutishwa, na kuuwawa

Mifano ya Kingamizi: Ujerumani

Maandamano yaliandaliwa dhidi ya wafanyabiashara wenye asili ya Kiyahudi, na Wajerumani wenye msimamo wa kati waliopinga kitendo hiki ndiyo walikamatwa kwanza na kupeleka kwenye kambi za mauaji.

Hatua za kuepusha Kingamizi

Pinga kwa kila hali sheria na sera zinazobagua makundi au zinazonyima haki za kiraia kwa makundi. Weka walinzi wa silaha kulinda viongozi wenye msimamo wa kati, kama ambavyo imefanyika Burundi. Shinikiza kuachiliwa kwa viongozi wenye msimamo wa kati ambao wanakamatwa, na kudai na kuendesha uchunguzi kwa wale viongozi wa aina hiyo ambao wameuwawa.

Pinga kupinduliwa kwa serikali na makundi yenye siasa kali.

Itaendelea na:
  • Hatua ya Saba: Mipango
  • Hatua ya Nane: Mateso

Friday, November 29, 2013

Maajabu ya mapishi [imefanyiwa masahihisho]

Hii ni tafsiri ya makala ya lugha ya Kiingereza niliyoandika na ikachapishwa kwenye gazeti la Daily News kwenye safu yangu iliyoitwa Letter from Butiama, makala nilizoandika kati ya mwaka 2005 na 2011. Makala hiyo ilichapishwa tarehe 26 Juni 2005.
*****************************************************
Inasemekana kuwa biashara zote zinazohusu nyama ndani ya mkoa wa Mara zinadhibitiwa na Wazanaki. Utawakuta kwenye kila ngazi ya biashara hiyo kama wamiliki, kama wafanyabiashara wa kununua na kuuza ng'ombe, na muhimu zaidi, kama wamiliki wa bucha. Aidha wamepata mafanikio wakubwa kwenye biashara hiyo kwenye jiji la Mwanza.

Somo kubwa linalojitokeza katika kuchunguza masuala yanayobainisha kampuni zenye mafanikio makubwa na zile zenye mafanikio duni ni ukweli kuwa mameneja wa kampuni zenye mafanikio wamejikita kwenye shughuli za bidhaa na huduma ambazo wanazielewa vyema. Inaelekea kuwa mmoja wa wafanyabiashara wa ng'ombe niliyeonana naye anaelewa vyema ukweli huu. Alinipa somo kuhusu hali mbali mbali za nyama kutoka sehemu tofauti za mwili wa ng'ombe na kuhitimisha kuwa nyama ya ng'ombe yenye ladha bora kuliko zote ni inayopatikana sehemu ya ndani ya paja la ng'ombe. Uelewa usiyo wa kawaida kama huu pengine ndiyo chanzo cha Wazanaki kutawala biashara ya ng'ombe na nyama ndani ya mkoa wa Mara. Napata picha ya matajiri wa Kizanaki wakimiliki biashara ya nyama ya bara la Afrika kama ambavyo Wajapani wamedhibiti biashara ya magari.

Pamoja na hii hamasa ya Wazanaki juu ya ng'ombe na nyama, ukweli unabaki kuwa hisia kali ya mtu mmoja inaweza kuwa mwiko kwa mtu mwingine. Migongano mikubwa ya kitamaduni inaweza kupatikana kwenye chaguzi ambazo watu toka tamaduni mbalimbali wanafanya kuhusu chakula wanachokula na kile wasichokula. Kwa baadhi ya dini kula nyama ni mwiko. Mboga na nafaka ndiyo hutumika kama vyakula vya msingi kwa jamii hizi.

Suala la chakula lilizua taharuki kwenye ziara mojawapo ya Rais Nyerere katika miaka ya sabini kwenye nchi mojawapo ya Ulaya. Kama ilivyo desturi kwenye misafara ya viongozi wa nchi, kiongozi mwenyeji wa nchi ile aliandaa dhifa ya taifa kwa mgeni wake, na baada ya juma moja Rais Nyerere akaandaa dhifa kwa mwenyeji wake. Wakati wa dhifa ya pili, mmoja wa Watanzania waliokuwa kwenye msafara ule alimdanganya Mtanzania mwenzake kuwa miongoni mwa vyakula vilivyoandaliwa kwenye dhifa ya kwanza ilikuwa ni pamoja na vyura na kuwa yule mwenzake alikula hao vyura bila kufahamu.

Aliyetoa taarifa hiyo alikusudia yawe mazungumzo kati yao tu, lakini aliyepewa taarifa ya kula miguu ya vyura alianza kujisikia vibaya hapo hapo na akaanza kutapika wakati dhifa ikiendelea.

Nilipokuwa mwanafunzi nchini Italia mimi na rafiki yangu George kutoka Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo tulialikwa chakula cha jioni na mwenyeji wetu Mtaliani. Baada ya kutuagizia chakula alisema kuwa alikuwa ametuchagulia chakula mahususi kwa ajili yetu ambacho huandaliwa marafiki wa karibu kabisa au wageni mashuhuri. Ukweli ni kuwa alikuwa ametuagizia miguu ya vyura. Ilikuwa mara yangu ya kwanza kula miguu ya vyura na nakumbuka ladha ilikuwa kama ya samaki. Mara tulipowekewa sahani zetu mezani na mhudumu, George alishituka na alitaka kuhama kabisa ile meza tuliyokaa. Mimi na mwenyeji wetu tulipoanza kushambulia ile miguu nakumbuka George alipata shida kubwa kubaki kwenye meza moja na sisi na kuangalia kitendo ambacho ni dhahiri kilimfadhaisha sana.

Mwenyeji wetu, ambaye aliwahi kutembelea nchi kadhaa za Afrika, alishangaa sana George. Alimuuliza anawezaje kuona kinyaa kula miguu ya vyura wakati yeye ameshuhudia Waafrika wakila wale wadudu ambao hutokeza baada ya mvua kunyesha. Alikuwa anazungumzia senene. George naye alishindwa kumuelewa Giuseppe. Mtu anawezaje kulinganisha kula senene na miguu ya vyura? Alisema Giuseppe alikuwa analinganisha vitu ambavyo havipaswi kulinganishwa kabisa.

Kuacha mimi, hamna kati yao ambaye alikuwa ameshakula miguu ya vyura pamoja na senene. Kimya kimya niliwashangaa hao wawili ambao walikuwa wanabishana ubishi ambao hawakuwa na mamlaka hata kidogo ya kuuendeleza. Jambo ambalo sikuweza kulibainisha wakati ule ni chakula kipi, kati ya chura na senene, kilikuwa na ladha nzuri zaidi.

Ukweli ni kuwa yawezekana kufikia usemi kuwa ladha ya chakula ni uamuzi ambao uko kichwani mwa mtu mmoja mmoja. Nimewahi kujitwika ujasiri usiyo na mfano na nikala chakula ambacho machoni kilikuwa kinatisha kuangalia lakini nikajikuta nimeweka mdomoni chakula chenye ladha nzuri kuliko maelezo. Tofauti na mwananchi mwenzangu ambaye alikuwa kwenye ziara ya Rais Nyerere, mimi nilifahamu chakula nilichokula siku ile kwenye ule mgahawa nchini Italia, kwa hiyo jambo la kushangaza ambalo naweza kulizungumzia ni ladha nzuri tu ya miguu ya vyura.

Monday, November 25, 2013

Hatua kumi za mauaji ya kimbari: 3 na 4

Nimetembelea Rwanda hivi karibuni na nikiwa huko nilipata fursa ya kutembelea mojawapo ya vituo vya kumbukumbu ya mauaji ya kimbari ya mwaka 1994.

Jambo moja la msingi ambalo Watanzania tunaweza kijufunza ni kuwa maafa yaliyotokea Rwanda yanaweza kutokea pia Tanzania. Kwa mujibu wa wachunguzi wa sababu zinozogeuza binadamu mmoja kuwa adui wa binadamu mwenzake na hata kufikia hatua ya kumaliza uhai wa mwenzake ziko duniani kote.

Sababu hizi zinaanza na mchakato wenye hatua nyingi ambao hufikia mauaji kama yale yaliyotokea Rwanda. Kinachozuwia maafa kama hayo kutokea ni hatua mahususi zinazopaswa kuchukulia na jamii za kukatisha uendelezwaji wa huo mchakato.

Kwa mujibu wa Dr. Gregory Stanton wa Genocide Watch, hatua za viashiria vya kuwepo kwa mchakato na za kuzuwia maafa kama ya Rwanda ziko kumi.

Hatua ya Tatu: Ubaguzi

Hatua hii inaanza kutenga makundi kwa mujibu wa uainishaji wa hatua ya kwanza. Mfano mashuhuri wa ubaguzi huu ni sera za kibaguzi za Afrika ya Kusini, apartheid. Kwenye hatua hii pia ndoa kati ya mtu wa kundi moja na jingine inapigwa marufuku na wale wanaoendeleza dhana hii. Yawezekana pia hata watu wa kundi linalobaguliwa kuanza kufukuzwa kwenye kazi, kama ambavyo ilifanyika dhidi ya Wayahudi wakati wa utawala wa Hitler huko Ujerumani.

Wakati mwingine zinatolewa hoja za kutenga nafasi za kazi kwa makundi mahususi ndani ya jamii. 

Mifano: Katika kukoleza ubaguzi zinaweza kuchukuliwa hatua za kubagua watu wa kundi moja kutonunua bidhaa za watu wa kundi jingine.

Hatua za kuepuka ubaguzi: Kuweka sheria zinazozuwia ubaguzi kwa misingi ya rangi, dini, kabila, utaifa, jinsia, tabaka, au chama.

Kuwezesha watu binafsi, na siyo waendesha mashtaka wa serikali pekee, kufungua mashitaka dhidi ya watu wanaotuhumiwa kufanya ubaguzi.

Hatua ya Nne: Udhalilishaji wa Kibinadamu

Kwenye hatua hii kundi moja linajipambanua kuwa ni bora kuliko lingine na kufanya kundi linalonyanyaswa kuonekana kama siyo binadamu kamili. Udhalilishaji wa kibinadamau unaondoa kusita kwa binadamu mmoja kuchukua hatua ya kumuua binadamu mwenzake.

Mifano: Nchini Rwanda kabla ya mauaji ya kimbari, Watutsi waliitwa mende na majina mengine ya kudhalilisha.

Hatua za kuepuka udhalilishaji: Kupinga kwa nguvu zote matumizi ya maneno ya kudhalilisha binadamu mwingine, pamoja na kuzuwia watu wa aina hii visa za kusafiria kwenda nchi nyingine na kueneza chuki.

Kuchukua hatua za kisheria dhidi ya watu au makundi ya watu yanayochochea madhara dhidi ya makundi mengine.

Serikali ichukue hatua za kufungia vituo vya redio na televisheni ambavyo vinachochea uhasama baina ya makundi mbali mbali. Tanzania tumeshuhudia vituo kadhaa kufungiwa kwa muda tu na kuruhusiwa kuendelea na matangazo.

Zitolewe fursa za kuleta maridhiano kwa njia zifuatazo:
  • kuanzisha vipindi kwenye vyombo vya habari vya kitaifa vyenye maudhui yanayokusudia kupunguza au kuondoa uhasama
  • kushirikisha viongozi wa kisiasa na dini kuongea na kukemea ubaguzi na kuhubiri kustamihiliana
  • kuhimiza madhehebu na dini mbalimbali kufanya kazi pamoja dhidi ya makundi ya chuki
  • kujenga makundi yanayofanya kazi pamoja kuepusha mauaji ya kimbari  
Muongozaji wageni katika mojawapo ya vituo vya kumbukumbu ya mauaji ya kimbari ya Rwanda ya mwaka 1994 akitoa maelezo kwa wageni.
Itaendelea na:
  • Hatua ya Tano: Uratibu
  • Hatua ya Sita: Kingamizi

Wednesday, November 20, 2013

John Kitime aelezea historia yake

Zamani, kwenye miaka ya tisini, niliwahi kumiliki gazeti lliloitwa Sanaa na Michezo ambalo lilichapisha makala kuhusu maisha ya mwanamuziki John Kitime, ambaye sasa hivi yuko na Kilimanjaro Band, Wananjenje.

Wakati huo aliwasilisha maelezo yake ambayo yalitumika kuandika makala fupi iliyochapishwa kwenye gazeti hilo.

Huyu hapa tena, John Kitime, akielezea maisha yake ndani ya muziki.
"Nilianza kwanza kupiga gitaa mwaka 1968 nikiwa kwenye mwaka wangu wa kwanza wa shule ya sekondari. Tangu napata kumbukukumbu tulikuwa na gitaa nyumbani wakati wote. Baba yangu alipiga gitaa tangu alivyokuwa mdogo. Yeye ni mtaalamu wa nyimbo za asili na ana mamia ya tunzi ambazo kwa bahati mbaya hazijarekodiwa.

Mwaka 1968 nilianza masomo yangu ya sekondari na baba yangu aliniruhusu kupiga gitaa. Alikuwa ni mtu aliyesisitiza masomo kwanza.

Mwaka 1975 niliunda bendi ndogo kwetu Iringa na baadhi ya wanachama wa bendi hiyo waliendelea kimuziki na kupata umashuhuri mkubwa. Wawili kati yao, Ally Makunguru na Nicholas Mlapone, wako nje ya nchi. Makunguru yuko Mombasa, Kenya na Mlapone yuko Ujerumani.Kundi hili hili ndiyo lilikuwa chimbuko  ya bendi kubwa, Tancut Almasi Orchestra.

Mwaka 1980 niliondoka Iringa na kuelekea Dar es Salaam na nilianza kufanya kazi kama msomaji wa prufu wa gazeti la Daily News. Wakati wa ziada nilikuwa mwanamuziki wa bendi ya Osheka, bendi ambayo ilivunjika mwaka 1981. Lakini ilikuwa bendi ambayo ilikuwa na wanamuziki wazuri sana kama Martin Ubwe ambaye sasa hivi ni kiongozi wa bendi ya Mionzi ambayo iko Mbeya, na Sammy Mhina ambayo ni mpiga ngoma wa Heart Strings Band.

Mwaka 1983 nilipata fursa ya kuigiza kwenye sehemu ndogo ya filamu inayoitwa Wimbo wa Mianzi iliyotolewa kwa ushirikiano kati ya Kampuni ya Filamu Tanzania na One World Production (OUP), kampuni ya Uholanzi. Nilipewa pia mkataba wa kutunga nyimbo kwa ajili ya filamu hiyo.

Ilikuwa wakati natafuta wanamuziki wa kurekodi muziki wa filamu hiyo ndipo nilikutana na Tchimanga Assosa, mwanamuziki mashuhuri wa Congo ambaye aliwahi kupiga muziki na bendi ya Lipua Lipua na Orchestra Kamale, ambaye alikuwa anakusudia kuunda bendi na tukaunda bendi iliyoitwa Orchestra Mambo Bado. Nillikuwa na bendi hiyo kwa miaka miwili.

Baada ya hapo nikajiunga na Orchestra Makassy iliyomilikiwa na Mzee Makassy. Bendi hii wakati huo ilikuwa na mwanamuziki Fan Fan Mosesengo (aliyekuwa na Marehemu Lwambo Luanzo Makiadi} na pia Remmy Ongala, ambaye sasa amejijengea jina kubwa akiwa na Orchestra Super Matimila. Sasa hivi Fan Fan yuko London (Uingereza) akiongoza bendi yake mwenyewe, Somo Somo. Pia mwanamuziki mwingine aliyeunda Orchestra Makassy alikuwa Kinguti ambaye sasa yuko na Bicco Stars.

Baada ya hapo nikaunda bendi yangu mwenyewe, TX Seleleka. Nilipata vyombo kutoka kwa rafiki yangu Mholanzi Kick Van den Hevel ambaye baadaye tena alichukua vyombo hivyo hivyo na kuanzisha bendi ya Tatunane. TX Seleleka ilipiga muziki hoteli ya New Africa kama bendi ya hoteli kwa mwaka mmoja halafu ikavunjika baada ya Kick kuchukua vyombo vyake.

Mwaka 1986 nilirudi Iringa nikawa mwanamuziki mwanzilishi wa Tancut Almasi Orchestra bendi ambayo ilikuwa inaundwa na wanamuziki miongoni wa waliyo bora kuliko wote nchini: Kasaloo Kyanga na Kyanga Songa, mapacha wa Ki-Congo waimbaji; wapiga gitaa wawili Shaban Yohana, ambaye sasa hivi ni kiongozi wa Vijana Orchestra, na Kawelee Mutimwana, kiongozi msaidizi wa MK Group; Mafumu Bilali, mpiga saksafoni mahiri ambaye sasa yuko Japani na Zanzibar Sound;kinanda wakati huo kilipigwa na Abdul Salvador, kiongozi wa Washirika Stars, na wanamuziki wengine wengi ambao wameendelea kuwa na sifa kila walipoenda.

Mwaka 1990 nyimbo zangu mbili nilizotunga nikiwa na Tancut, Lungulye na Afrika Nakulilia, zilishinda mashindano ya Top Ten Show zikichukua nafasi ya kwanza na na pili. Nilishinda zawadi ya redio kaseti ya National ambayo nasikitika nililazimika kuiuza ili kupata pesa za kurekodi hii kaseti yangu ya sasa.

Nyimbo nane kwenye hizi ninazorekodi sasa ni uzoefu wangu kutoka kwenye hii miaka yote, bila kusahau ushawishi wa baba yangu. Hii nyimbo Ifipwepo ni utunzi wa baba yangu, nikiwa nimeupangilia kwenye muziki.

Ningekuwa na nafasi nzuri ningeweza kurekodi vizuri zaidi, na kutoa aina nyingi zaidi za muziki. Nakiri kuwa kaseti hii nimeirekodi kwa madhumuni ya kuiza kwa hadhira ya Watanzania ili niweze kurudisha pesa na kununua redio kaseti nyingine."
Taarifa nyingine zinazohusiana na hii:

Saturday, November 16, 2013

Hatua kumi za mauaji ya kimbari: 1 na 2

Nimetembelea Rwanda hivi karibuni na nikiwa huko nilipata fursa ya kutembelea mojawapo ya vituo vya kumbukumbu ya mauaji ya kimbari ya mwaka 1994.

Jambo moja la msingi ambalo Watanzania tunaweza kijufunza ni kuwa maafa yaliyotokea Rwanda yanaweza kutokea pia Tanzania. Kwa mujibu wa wachunguzi wa sababu zinozogeuza binadamu mmoja kuwa adui wa binadamu mwenzake na hata kufikia hatua ya kumaliza uhai wa mwenzake ziko duniani kote.

Sababu hizi zinaanza na mchakato wenye hatua nyingi ambao hufikia mauaji kama yale yaliyotokea Rwanda. Kinachozuwia maafa kama hayo kutokea ni hatua mahususi zinazopaswa kuchukulia na jamii za kukatisha uendelezwaji wa huo mchakato.

Kwa mujibu wa Dr. Gregory Stanton wa Genocide Watch, hatua za viashiria vya kuwepo kwa mchakato na za kuzuwia maafa kama ya Rwanda ziko kumi.

Hatua ya Kwanza: Uainishaji

Hapa inafanyika jitihada ya kuainisha makundi ndani ya jamii, "sisi na wao." Ubaguzi unaweza kuchukua njia mbalimbali kama vile dini, kabila, utaifa, na hata matabaka ya jamii.

Uainishaji unasaidia kuwagawa watu na kurahisisha kampeni za mapambano dhidi ya kundi mojawapo ndani ya jamii.

Mifano: Tanzania tumeshaanza kujipambanua kwa dini zetu kwa muda mrefu sasa, pamoja na kwa maeneo tunayotoka. Aidha, "wa bara na wa visiwani" umekuwa wimbo mashuhuri wa miaka ya hivi karibuni.

Hatua za kuepuka uainishaji: Kusisitiza utaifa zaidi kuliko makundi. Kuweka mkazo kwenye matumizi ya lugha moja inayounganisha wote, mfano Kiswahili. Kupinga kwa nguvu zote wanasiasa na vyama vya siasa vinavyoendeleza siasa za kibaguzi.

Hatua ya Pili: Uashiriaji

Hapa zinatumika alama au ishara zinazoweka mkazo wa kubainisha makundi yaliyoainishwa katika hatua ya kwanza.

Mifano: Wakristu dhidi ya Waislamu, Wazanzibari dhidi ya Watanzania bara; Itikadi nazo zinaweza kutumika kama nyenzo za kubaguana: walalahoi dhidi wa wala nchi, Wadanganyika dhidi ya Wadanganyaji, n.k.

Hata nguo zinaweza kutumika kubaguana: magwanda dhidi ya wale wa kijani na njano. Nimeshuhudia picha ya makada wa chama kimoja cha siasa wakimshambulia mwanachama wa chama tofauti kwa mawe na matofali.

Hatua za kuepuka uashiriaji: ni pamoja na kuondoa uainishaji wa kidini au kikabila kwenye vitambulisho vya aina zote. Mpaka leo hii Mtanzania yoyote anayetoa taarifa kwenye kituo cha polisi anapaswa kutaja dini na kabila lake.
Vitambulisho vya Rwanda vilitoa taarifa za kabila la mwenye kitambulisho na vilitumika kuwasaka wahanga wa mauaji ya kimbari ya mwaka 1994.
Aidha, kupinga matumizi ya maneno au majina yanayodhalilisha kundi lolote ndani ya jamii.

Itaendelea na:
  • Hatua ya Tatu: Ubaguzi
  • Hatua ya Nne: Udhalilishaji wa Binadamu
Taarifa nyingine inayohusiana na hii:

Friday, November 1, 2013

Mtwara sawa lakini Loliondo hapana?

Nimekuwa na msimamo unaofanana kidogo na sera ya serikali juu ya rasilimali za Tanzania; kwamba ni mali ya Watanzania wote, na siyo ya wale walio karibu na hiyo rasilimali. Sikubaliani na hoja kuwa wale wananchi walio karibu na rasilimali ndiyo wapewe upendeleo zaidi juu ya kufaidika na rasilimali hiyo.

Sababu yangu ya msingi ni kuwa kufanya upendeleo wa aina hiyo kutajenga ubaguzi dhidi ya Watanzania wengine. Watanzania wengine wataonekana kuwa "wanaingilia" rasilimali inayopaswa kutumika na wale wazawa wa eneo husika tu. Na ndiyo maana napata shida kuunga mkono hoja ya baadhi ya Watanzania, kama wale wananchi wa Mtwara, wanaodai rasilimali ya gesi ni yao kwanza.

Lakini hatuwezi kusema hatuelewi kwanini kuna madai kama yao. Unaweza kujenga hoja nzuri kuzungumzia kwanini wananchi wa Mtwara wanaamua kuwa gesi ya Mtwara ni yao. Ni ubovu wa sera za muda mrefu za serikali zilizopuuza umuhimu wa kuhakikisha kuwa Watanzania wanafaidika na rasilimali yao. Haya ni matokeo ya muendelezo ule wa sera zinaotoa vipengele vya upendeleo kwa wawekezaji na ulipaji wa mrahaba pekee. Mwekezaji aliweza kumiliki asilimia 100 ya mradi wa rasilimali muhimu na kuilipa serikali au kodi kidogo au kusamehewa kabisa na kiwango cha mrahaba ambacho, kimsingi, kilikuwa kidogo sana.

Wananchi waliofundishwa miaka nenda rudi kuwa yatosha kutoa misamaha ya kodi kwa wawekezaji na malipo ya mrahaba wa chini ya asilimia tano hawakuelewa hilo somo na hawataweza kulielewa hata kwa karne nzima. Matokeo yake ni kupoteza imani kabisa kwa serikali na maamuzi yoyote inayoyafanya kwenye eneo la uwekezaji. Tunachoshuhudia sasa ni wananchi "kuchukua chao mapema"; kwamba rasilimali ambazo ziko jirani nao ni lazima ziwape faida wao. Watanzania wengine wahangaike na mali zilizopo maeneo yao. 

Huu ni mwanzao wa kuparaganyika kwa nchi. Wale wasio na rasilimali watakula wapi? Watapata ajira wapi? CHADEMA wamejaribu kuelezea namna utaratibu wa kila mtu na chake (majimbo) na kidogo kilichopo kipelekwe kwenye serikali kuu lakini kwangu mimi sera hii ina walakini kuwa itaanza kupandikiza hisia kuwa Mlima Kilimanjaro una wenyewe. Hali kadhalika Serengeti, Selous, na mbuga nyingine ambazo zinaliingizia Taifa mabilioni ya shilingi kila mwaka. Vivyo hivyo kwa gesi na mafuta yanayosubiriwa kwa hamu.

Badala ya kuitaka serikali iwajibike zaidi katika kuwanufaisha wananchi wake, tunaanza kugawana kile kidogo kilicho jirani yetu. Ni sawasawa na wenyeji kugombania makombo baada ya chakula kutengewa wageni.

Kutegemea kuwa jambo litatokea (ubaguzi wa watu kutokana na maeneo yao ya asili) hakuthibitishi kuwa jambo hilo kweli litatokea. Lakini binadamu wote tunaishi kwa kufanya maamuzi kuhusu yaliyokwisha tokea zamani, ya sasa, na matarajio yetu ya yale yanayoweza kutokea. Ndiyo msingi wa mipango yote thabiti, kwa hiyo siyo rahisi kujenga hoja kupuuza hoja za aina hii.

Sasa basi tugeukie Loliondo. Wakati siungi mkono madai ya wananchi wa Mtwara naunga mkono madai ya wale wa Loliondo ambao wanapinga kusudio la serikali la kutenga kilomita za mraba 1,500 kwa wawekezaji kwa shughuli za utalii, pamoja na serikali kutaka watu hao wahame kupisha shughuli za uwekezaji. Wamasai wapatao 30,000 na ng'ombe zao wahamishwe ili kupisha shughuli za utalii.

Bado nina msimamo kuwa Tanzania ni ya wote lakini kwa wakazi wa tarafa ya Loliondo, ambao wengi wao ni wafugaji na wanaoishi maisha yanayotegemea sana ardhi wanayokalia kwa ustawi wao na wa mifugo yao, kugawa hayo maeneo kwa matumizi ya wawekezaji ni kuwanyima Watanzania hawa chanzo cha msingi kinachobeba mfumo wao wa maisha.

Hii ni sawa na kuhatarisha uhai wao. Hasara atayopata mkazi wa Loliondo atakayehamishwa haiwezi kamwe kufidiwa na kiasi chcochote cha pesa, hata kama pesa hizo zisingieishia serikalini na zikagawiwa kwa wakazi hao.

Mkazi wa Mtwara ana haki kuhoji serikali ionyeshe faida kwake (na kwa Watanzania wengine) ya sera ya muda mrefu ya uwekezaji, lakini hata kama madai ya kuweka Mtwara viwanda muhimu vya sekta ya gesi haitatimizwa, maisha ya mwana-Mtwara hayatabadilika kwa kiasi kikubwa kulinganishwa na athari na matatizo makubwa ambayo atayapata mkazi wa Loliondo ambaye maisha yake yataathrikia kutokana na kuhamishwa kwenye ardhi ambayo anaitegemea kila siku kwa maisha yake na kwa mifugo yake.

Katika mazingira haya, madai ya wananchi hawa wa Loliondo ni sahihi kabisa, kwa maoni yangu. Ya Mtwara bado yanahitaji kujengewa hoja zaidi.

Taarifa nyingine zinazohusiana na hii:
http://muhunda.blogspot.com/2010/09/john-mnyika-wa-chadema-anajibu-hoja.html
http://muhunda.blogspot.com/2010/10/amani-millanga-bado-anahoji-sera-ya.html

Sunday, October 27, 2013

Wageni toka Kagera wamtembelea Mama Maria Nyerere

Viongozi wa kikundi cha wajane na yatima kutoka mkoa wa Kagera walimtembelea Mama Maria Nyerere, kijijini Butiama hivi karibuni.
Grace Mahambuka, mwenyekiti wa kikundi cha Wajane na Yatima Kagera akitoa zawadi ya "akamwani" (kahawa ya kutafuna) kwa Mama Maria Nyerere (kushoto) Mwitongo, Butiama.
Msafara uliongozwa na mwenyekiti wao, Mama Grace Mahambuka, ambaye aliongozana na Mama Agnes Paulo Mukuta ambaye ni mdau wa maendeleo anayeunga mkono kikundi hicho. Mwingine katika msafara huo alikuwa Sittiwarth Mugasha ambaye ni yatima na msanii muimbaji wa kikundi cha Umoja wa Wanawake Wajane na Yatima Band.

Taarifa zinazohusiana na hii:
http://muhunda.blogspot.com/2011/07/wageni-wa-butiama-ujumbe-wa-veta.html
http://muhunda.blogspot.com/2011/07/wageni-wa-butiama-ujumbe-wa-veta.html
http://muhunda.blogspot.com/2010/10/kumbukumbu-ya-siku-ya-kufariki-mwalimu.html

Saturday, October 26, 2013

Madaraka Nyerere: Niliwahi kumsaidia baba pesa

Madaraka Nyerere: Niliwahi kumsaidia baba pesa

Mahojiano haya nilifanya na Stella Nyemenohi wa gazeti la Habari Leo. Yamechapishwa tena hivi karibuni wakati wa maadhimisho ya miaka 14 tangu kufariki Mwalimu Julius Kambarage Nyerere.

Bofya hapo juu kusoma mahojiano yote.

Friday, October 25, 2013

Msiofahamu vyema Kiingereza zungumzeni na andikeni kwa Kiswahili, mtafanya makosa machache zaidi

Hili nimeshalisema sana lakini naona kuna umuhimu kulirudia: tofauti na Watanzania wengi tunavyoamini, kufahamu vyema lugha ya Kiingereza siyo ishara kuwa anayeifahamu vyema lugha hiyo ni mtu aliyesoma kwa kiwango cha juu. Inasemekana kuwa John Major, waziri mkuu wa zamani wa Uingereza, alikuwa na elimu ndogo sana lakini hatuna shaka kuwa alifahamu Kiingereza vizuri sana.

Tunang’ang'ania lugha ya Kiingereza tunapoongea au kuandika kwa kuamini kuwa kwa kufanya hivyo tutaonekana ni wasomi sana. Kiingereza ni lugha kama lugha nyingine: Kichina, Kijapani, Kifaransa, na hata Kizanaki.
Ni kweli mtu anapoongea au kuandika lugha vyema inaashiria kuwa yeye ni msomi kwa maana ya kwamba yawezekana amekaa kwenye mfumo wa elimu kwa miaka mingi na bila shaka amejifunza misingi ya hiyo lugha anayoongea. Lakini ukweli unabaki kuwa hakuna uhusiano wowote wa moja kwa moja kati ya kuongea na kuandika lugha yoyote kwa ufahasaha na kiwango cha elimu cha mhusika.

Naona mara kadhaa mwenye mitandao ya jamii watu wakijaribu kujipambanua kuwa waandikaji wazuri wa lugha ya Kiingereza lakini kinachojitokeza ni kuwa hawana uwezo huo.

Unaweza kujiuliza: kwanini baadhi ya hawa wanaoamini kuwa kufahamu vyema matumizi ya lugha ya Kiingereza ni ishara ya usomi wasitumie lugha yao mama, Kiswahili, kwa sababu wengi wanaowaandikia wanafahamu lugha hiyo? Kama jamii nzima inaamini kuwa kufahamu Kiingereza ndiyo hali ya kujivunia basi ni vigumu kuona mabadiliko.

Jambo la msingi ingekuwa kwa wale wasiofahamu lugha vyema – siyo Kiingereza tu – wajifunze hizo lugha vyema ili pale wanapoongea au kuandika basi wafanye hivyo kwa ufasaha na kuweza kuwa walimu wa wengine. Ukweli ni kuwa kama hufahamu lugha ya Kiswahili vyema ni vigumu kujifunza lugha nyingine kwa ufasaha.

Lakini kuna suala moja la msingi linajitokeza: iwapo hufahamu kuwa hufahamu basi tatizo ni kubwa zaidi. Kuna mwanahabari mmoja mwandamizi aliwahi kuandika makala akisema kuwa ili mtu apate uwezo wa kufahamu kuwa hafahamu anahitaji kiwango fulani cha elimu. Kwa maana nyingine, inahitaji kuwa msomi kidogo kubaini kuwa huna uwezo na jambo fulani.

Inawezekana kuwa mfumo wetu wa elimu umekuwa duni kwa muda mrefu sana kiasi ambapo limejengeka tabaka kubwa la Watanzania ambao wako kwenye kundi hilo la kuwa watu wasiofahamu kuwa hawafahamu na basi hujikuta wakiandika na kusema vitu ambavyo siyo sahihi kwa Kiingereza wala Kiswahili.

Jambo lingine ambalo linatuangamiza kabisa ni kuwa Watanzania ni wagumu sana kusahihisha wenzao pale wanapokosea kwenye matamshi na maandishi. Mkosoaji anaonekana siyo mstaarabu au huonekana anataka kujipambanua kuwa yeye anafahamu zaidi ya wenzake. Matokeo yake ni kuwa matumizi yasiyo sahihi ya lugha yanaendelea kushamiri kwenye jamii.

Nimesikiliza mara nyingi tangazo linalosikika hivi karibuni kwenye vyombo vya habari ambapo binti anatamka namba za simu na anataja “zilo zilo” akimaanisha “ziro ziro” au “sifuri sifuri.” Hilo tangazo limepitiwa na wahusika na hawakuona kasoro yake. Matokeo yake mamilioni ya watoto wanalisikiliza na kuamini kuwa kutamka “zilo” ni sahihi. Najiuliza: hawa wahusika ndiyo wale wale waliopoteza uwezo wa kutofahamu kuwa hawafahamu, au ndiyo ule ustaarabu wetu wa kutosahihisha makosa?


Maoni yangu ni kuwa tujifunze Kiswahili vyema kwanza kabla ya kujaribu kujifunza lugha nyingine. Ni kazi ndogo zaidi kumfundisha Kiswahili mtu ambaye Kiswahili ni lugha yake mama kuliko kumfundisha Kiingereza (au lugha nyingine) mtu ambaye Kiswahili ni lugha yake mama. Na hili ni kweli hata kwa yule ambaye Kiswahili ni lugha yake mama na anayetamka “zilo zilo.”

Taarifa zinazofanana na hii:

Monday, October 7, 2013

Msafara mwingine wa Mlima Kilimanjaro wamalizika, safari hii kuchangia pesa kwa shule ya Kichalikani

Ndiyo kwanza nimemaliza kukwea Mlima Kilimanjaro katika mwaka wa 6 wa The Mwalimu Nyerere/Mt. Kilimanjaro Charity Climb kuchangisha pesa kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa shule iliyopo kwenye kijiji cha Kichalikani, wilayani Mkinga, mkoa wa Tanga.

Pamoja nami katika msafara wa Mlima Kilimanjaro alikuwa E. Gassana. Tulifika kwenye kilele cha Mlima Kilimanjaro asubuhi ya tarehe 5 Oktoba, saa 2:30 asubuhi.
Kwenye kilele cha Mlima Kilimanjaro, mita 5,895 juu ya usawa wa bahari na sehemu iliyo juu kuliko zote katika bara la Afrika, kutoka kushoto: Pius Yahoo, muongozaji wetu; E. Gassana; mwandishi wa blogu hii; na Musa Juma, muongozaji msaidizi.
Wakazi wa kijiji cha Kichalikani walianza ujenzi wa shule mwaka 2009 kwa kutumia sehemu ya ushuru uliokusanywa kwenye soko la samaki. Baada ya kuona jitihada hizi, Saidi Masimango, aliyekuwa Mkurugenzi wa Idara ya Teknolojia na Habari ya Shirika la Hifadhi ya Jamii alichangia shilingi milioni moja. Masimango alifariki mwezi Julai 2013.

Aidha, Mkuu wa Wilaya ya Rufiji, Nurdin Babu, naye alichanga mabati 33, wakati Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Mwantumu Mahiza alitoa mabati 100.

Kiasi cha shilingi milioni 7 zinahitajika kumalizia kazi za ujenzi ambazo hazijakamilika pamoja na kununua madawati.
Tafadhali changa kwa njia zifuatazo:

Jina la Akaunti: Kijiji cha Kichalikani
Benki: National Microfinance Bank
Namba ya Akaunti: 4193300163
Tawi: Mkwakwani, Tanga.

Wanaochangia wanaombwa kutuma majina kamili na viwango vilivyotolewa (kwa madhumuni ya kuchapisha orodha kamili kwenye gazeti la Jamhuri) kwa:


Hata wasiopenda majina yao yachapishwe nao wanaombwa kuwasilisha hizo taarifa kwa njia hiyo ya barua pepe (majina hayatachapishwa).

Kuchangia kwa njia ya simu tumia namba ifuatayo (pesa zitakusanywa na kuwekwa kwenye akaunti ya benki iliyotajwa juu):
+255 755 570 795

Saturday, September 14, 2013

Asikwambie mtu, Mtanzania mwenye simu siyo maskini

Baadhi ya matumizi ya simu yanaashiria kuwa Watanzania wanao uwezo mkubwa.

Nimekuwa msikilizaji wa mazungumzo ya simu ninapokuwa mitaani au safarini na katika utafiti usiyo rasmi ambao nimefanya, watu wengi wanaotumia simu hawazitumii kama nyenzo za kuongeza ufanisi katika shughuli zao, bali huzitumia kama chombo cha kupiga porojo zisizo na manufaa kwao au kwa wanaoongea nao.

Sina mamlaka kuhoji ambavyo mtu aliye huru anaamuaje kutumia salio lako kwenye simu, lakini kukosa mamlaka hayo hakufuti ukweli kuwa Watanzania wengi tunapoteza pesa zetu za mawasiliano kupiga porojo na kutuma ujumbe wa maandishi ambao hauleti maendeleo yoyote kwetu na kwa Taifa. Wanaochekelea ni wamiliki wa kampuni za simu ambao bila shaka wanatunisha mifuko yao kwa kila sekunde inayopita.

Chukua mfano huu: nimeketi ndani ya ndege iliyowasili kwenye uwanja wa ndege halafu abiria kadhaa wanawasha simu zao na kuwapigia simu watu ambao wamefika kuwapokea uwanjani wakiwaambia kuwa kuwa ndege imeshatua. Hii nimeshuhudia mara nyingi. "Vipi, umeshafika? Na sisi ndiyo tumetua."

Kwangu ingekuwa inaleta maana zaidi iwapo baada ya kutoka uwanjani na asimuone aliyempokea ndiyo apige simu kumuuliza kilichomsibu mwenyeji wake mpaka asifike uwanjani.

Siku za hivi karibuni nimeshuhudia mtu anayeongea kwenye simu karibu siku nzima. Akimaliza simu moja anapiga na kuongea na nyingine. Sijui anaongea nini kwa sababu anaongea Kizanaki (lugha ambayo siifahamu vizuri) lakini pamoja na kutofahamu lugha hiyo bado sipati picha ya suala ambalo litanifanya niongee kwa siku nzima. Hoja yangu hapa ni kuwa siyo rahisi kuongea mfululizo kwa karibu siku nzima na ukawa unapanga masuala ya kuleta maendeleo kwako au kwa jamii inayokuzunguka. Asilimia kubwa ya mazungumzo itakuwa porojo ambayo matokeo yake itakufanya kupungukiwa tu pesa ambazo ungeweza kuzitumia kwa jambo la maana zaaidi na lenye manufaa. Dakika chache kwenye simu kila siku zinafikia pesa nyingi baada ya muda mrefu.

Naweza kuwa nitatofautiana na wengi lakini ule woga wa serikali hivi karibuni kutoza shiling elfu moja kwa mwezi kwa kila mtumiaji wa simu ulikuwa woga wa kisiasa kwa sababu baadhi ya makundi ya jamii yalilivalia njuga suala hilo na kodi hiyo ya mawasiliano ilionekana kuwa ingeipunguzia serikali ushawishi kwa Watanzania. Inawezekana kuwa serikali inayo matatizo mengi 

Ukweli ni kuwa watumiaji wengi wa simu wanatumia pesa nyingi kwa mwezi kuongea na kuandika ujumbe wa maandishi usiyo na manufaa yoyote lakini ambao unawagharimu kiasi kikubwa kuliko hiyo shilingi elfu moja.

Friday, September 13, 2013

Hatari ya kuamini kila unachoambiwa

Miaka arubaini iliyopita taarifa ya kutua kwenye mwezi kwa chombo cha anga cha Marekani, Apollo 11, na kutembea kwenye mwezi kwa wanaanga wawili kutoka chombo hicho kulizua maswali mengi kutoka kwa mwanafunzi mwenzangu, Richard. Yeye hakuamini iliwezekana kwa binadamu kufika kwenye mwezi. Umri wangu ulikuwa miaka tisa na naamini Richard alikuwa na umri huo huo. Alisema, "Wanatudanganya hao!"

Mimi niliamini kuwa wale wanaanga wawili walifika kwenye mwezi. Sijui kwa sababu ipi sikuwaza kuwa ni uongo, lakini nakumbuka tu kuwa niliamini taarifa tulizosikia na kusoma bila kuhoji. Kwa umri wetu maoni yetu, ya kuamini au kutoamini, hayakutokana na ushahidi wowote tuliokuwa nao lakini ajabu ni kuwa tulikuwa na maoni tofauti.
Mwanaanga Edwin "Buzz" E. Adrin akionekana kwenye mwezi pembeni ya chombo kilichotua kwenye mwezi tarehe 20 Julai 1969. Picha ya National Space Agency (NASA).
Ukweli ni kuwa nilifikia maamuzi ambayo watu wengi hufikia katika mazingira ya aina hiyo. Tunayoambiwa tunaamini. Tatizo ya hali kama hii ni uwezekano wa kupokea taarifa za uongo kutoka mamlaka na serikali mbalimbali na kutumika kwa manufaa ya hao watoa taarifa za uongo.

Niligundua hivi karibuni kuwa wasiwasi wa taarifa zile kwa Richard za mwaka 1969 haukutokea Tanzania tu; hata baadhi ya Wamarekani hadi hii leo hawaamini kuwa Wamarekani wenzao walifika kwenye mwezi na wanasema kuwa mandhari ya mwezi ambayo tunaiona kwenye baadhi ya picha ilibuniwa na kutengenezwa hapa hapa duniani kwenye jengo moja kubwa linalohifadhi ndege kwenye uwanja mmojawapo wa ndege wa nchini Marekani.

Inawezekana kuwa tofauti ya sasa na mwaka 1969 ni kuwa watu wengi zaidi wamejenga desturi ya kutoamini taarifa za serikali na mamlaka mbalimbali. Serikali na mamlaka zimebainika mara nyingi kutoa taarifa za uongo na watu sasa wanaposikia taarifa hizo huanza kwa kutoamini hizo taarifa mpaka pale watakapopata taarifa kutoka vyanzo tofauti zinazothibitisha ukweli wa hizo taarifa za awali.

Taarifa inayofanana na hii:
http://muhunda.blogspot.com/2012/01/ingekuwa-unaishi-kwenye-sayari-ya.html

Tuesday, September 10, 2013

Enzi za Mwalimu

Baada ya kutangazwa Azimio la Arusha, mwaka 1967, baadhi ya makundi ya Watanzania kutoka maeneo mbalimbali ya Tanzania yalianza kutembea kwa mguu kutoka sehemu moja hadi nyingine ya nchi kuunga mkono Azimio la Arusha.
Picha ya Idara ya Habari Maelezo
Kwenye picha ni vijana kutoka mkoa wa Mara ambao walitembea hadi Dar es Salaam kuunga mkono sera ambayo iliweka umuhimu kwa serikali kumiliki njia kuu za uchumi na kutumia rasilimali ya Taifa kwa manufaa ya wananchi.

Ikulu, Dar es Salaam, walipokelewa na Rais Mwalimu Julius Kambarage Nyerere.

Sunday, July 28, 2013

Maendeleo (na makelele) yameingia Butiama

Butiama bado ni wilaya changa kabisa, lakini tayari mabadiliko yatokanayo na miji (na kero zake) yameanza kuonekana Butiama.

Makelele ni mojawapo ya kero za miji ambayo sehemu kama Butiama haikuwa nayo mpaka hivi karibuni. Butiama haikuwa na huduma ya basi linalosafiri moja kwa moja kwenda Mwanza na hapo awali wasafiri walilazimika kusafiri mpaka njia kuu iendayo Mwanza, sehemu iitwayo Nyamisisi, au kuanzia safari Musoma. Miaka michache iliyopita huduma ya basi la moja kwa moja kutoka Butiama hadi Mwanza ilianzishwa na kuleta kero ninazozungumzia.
Basi la kuelekea Mwanza kwenye stendi ya Butiama.
Basi hilo linapoegeshwa alfajiri kusubiri abiria ni kawaida ya madereva wake kupiga honi mfululizo kwa muda mrefu na kusababisha makelele kwenye eneo kubwa la Butiama. Butiama ni kijiji kidogo kwa hiyo mfululizo wa honi hizo za kila kukicha ni usumbufu mkubwa kwa wakazi wengi wa Butiama.

Sijaelewa mantiki ya kupiga hizo honi ingawa naamini zinakusudiwa kuwaamsha abiria wanaosafiri.Lakini ni vigumu kuelewa utaratibu wa abiria anaekusudia kwenda Mwanza kutegemea kuamshwa na honi ya basi.