Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Monday, March 28, 2016

Viongozi wabaguzi ambao wanaendelea kuenziwa

Wapo viongozi wa dunia ambao wamejijengea sifa kubwa, pamoja na ukweli kuwa wanabeba kasoro kubwa za kibaguzi kwenye matamshi au maamuzi yao. Viongozi wawili ambao wanayo sifa hii ni Winston Churchill, na Mahatma Gandhi.
Sir Winston S Churchill.jpg
Winston Churchill (Picha: Wikipedia)

Churchill alikuwa kiongozi wa Uingereza ambaye aliwahi pia kuwa waziri mkuu wa nchi hiyo. Katika nyadhifa zake mbalimbali amenukuliwa akitoa matamshi na kuchukua hatua za kibaguzi dhidi ya watu mbalimbali, ikiwa ni pamoja na Waafrika, Wahindi, na Waarabu. Kwa ujumla, alikuwa mbaguzi wa rangi ha kiwango cha Hitler aliyeamini kuwa binadamu mwenye ngozi nyeupe anapaswa kutawala binadamu wengine wote. Pamoja na ukweli huu, Churchill anakumbukwa kwenye historia kama kiongozi aliyefanikiwa kuiongoza Uingereza vyema wakati wa vita vya pili vya dunia.

Gandhi naye haachwi mbali kwa matamshi yake ya kibaguzi. Akiwa anafanya kazi Afrika ya Kusini aliandika kuhusu kupinga kwake kwa wahindi kufananishwa na Waafrika, akiamini kuwa Mwafrika alikuwa na hadhi ya chini kuliko Mhindi. Gandhi ni mmoja wa wanaharakati wa India ambaye anaheshimika sana katika ulimwenguni wa mapambano dhidi ya ukoloni, haki, na usawa.

Wanataaluma wanafahamu kuwa, kwa kutumia mifumo ya habari na mawasiliano ambayo inamilikiwa na kampuni chache sana duniani, inawezekana kujenga taswira juu ya kiongozi ambayo haifanani kabisa na hali halisi. Mwizi anaweza kuonekana ni muadilifu, na mhalifu akaonekana asiye na hatia. Hali kadhalika, muadilifu na asiye kuwa na hatia akatambulishwa kuwa tofauti kabisa na hali halisi.
File:Portrait Gandhi.jpg
Mahatma Gandhi (Picha: Wikipedia)
Haipingiki kuwa historia ya kiongozi inapaswa kuakisi mazuri na mabaya yake, lakini nafikiri inapofikia suala la ubaguzi wa binadamu kwa misingi ya rangi ya ngozi, basi kinga hiyo inapotea kwa viongozi wa aina hiyo. Kiongozi asiye mbaguzi na aliyetumbukia kwenye makosa ya kiutendaji anaweza kuvumiliwa kidogo, lakini kiongozi mbaguzi hasafishiki na hapaswi kuvumiliwa hata kidogo.

Hata hivyo, uandishi wa historia unaoficha mabaya ya viongozi wa aina hii pamoja na mifumo ya habari na mawasiliano ambayo inaendelea kudhibitiwa na wamiliki wachache haitoi fursa ya kuwaanika viongozi wa aina hii pamoja na maovu yao.