Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Friday, December 27, 2013

Mandela! Mandela! Mandela! (Sehemu ya Tatu na ya Mwisho)

Kwenye makala hii ambayo imegawanywa kwenye awamu tatu, Notburga Maskini anaandika kuhusu Mzee Nelson Mandela, aliyefariki tarehe 5 Desemba na alizikwa  tarehe 15 Desemba 2013 kwenye kijiji cha Qunu nchini Afrika ya Kusini.

Mandela! Mandela! Mandela! (Sehemu ya Tatu na ya Mwisho)
Na Notburga Maskini*

Heshima katika historia ya nchi na dunia
Kilio kinachoendelea hivi sasa na heshima kubwa waliyopewa mashujaa wetu waliolala ni changamoto kubwa kwa kizazi kinachofuata. Walijitoa thamani kupigania heshima ya binadamu. Kinachoendelea sasa ni heshima kubwa kwao hata wakiwa wamelala na kama alivyowahi kusema Mzee Mandela katika nukuu zake: “Ukijiheshimu hata simba atakuogopa na kukuheshimu”. Taarifa zilizotangazwa na gazeti moja nchini kuwa Alqaida na al Shaabab hawatafanya mashambulizi katika kipindi hiki cha maombolezo ni kielelezo cha ukweli wa nukuu hiyo ya shujaa wetu, Baba wa Taifa la Afrika ya Kusini.
 
Waombolezaji wakitoa heshima zao za mwisho kwa Hayati Nelson Mandela tarehe 11 Desemba 2013, wakati mwili wake ulipohamishiwa kwenye majengo ya Union jijini Johannesburg. (Picha ya GCIS).
Hii ni heshima japo yeye hafungamani na itikadi wala vitendo vya makundi hayo bali anafungamana na upendo, msamaha na kutokulipa visasi. Naamini iwapo dunia itajifunza haraka kutoka kwa shujaa huyu pengine vitendo hivi vinaweza kuisha na wahusika kuendelea kuwa watu wa amani.

Je tuko tayari kujifunza?
Sisi tuliobaki nyuma pamoja na kuomboleza tuna maswali ya kujiuliza na kutoa majibu sasa, iwapo:
1)      Tuko tayari kurejesha na kuendeleza mfumo wa kidhalimu unaodhalilisha na kunyonya binadamu wengine hasa wafanyakazi na wakulima;
2)      kuwafanyisha kazi ngumu wafanyakazi na wakulima bila kuwalipa ujira stahiki au kuratibu bei za mazao yao kwa kisingizio cha utandawazi huku kukiwa na lengo la kushirikiana na wanyonyaji kujilimbikizia mali binafsi kupitia jasho lao;
3)      kuendeleza wizi wa mali za umma, matumizi mabaya ya madaraka dhidi ya wanyonge na kupuuza ustawi na maendeleo yao.

Ama:
1)      Tunadhamiria kujifunza kwa mashujaa wetu Mzee Mandela na Mwalimu Nyerere, kuenzi maisha yao, na kuendeleza mema yao, kwa kuwa wafanyakazi bora, watumishi waadilifu, wabunifu, na waaminifu wa wananchi wetu;
2)      Haki na nafasi za raia kumiliki rasilimali za mataifa yetu kwa usawa zinalindwa na kuwezeshwa hata kama maisha na maslahi binafsi yatatishiwa;
3)      Tutawalinda na kutetea haki za kiraia, na kuishi bila kuwatisha, kuwauwa katika kulipiza visasi au mapigano ya wenyewe kwa wenyewe,  kwa lengo la kustawisha jamii, kuondoa umaskini, na kudumisha heshima ya binadamu iliyoasisiwa na mashujaa hawa.

Kupokea mauti kwa ujasiri na fedheha za kiuongozi
Inaleta maana kuchagua kulinda na kutanguliza maslahi ya umma na Taifa, ili historia isije tuhukumu kwa kutotimiza wajibu tunaopaswa kufanya kwa jamii na nchi zetu wakati wa uhai wetu. Hali hii itatuwezesha kupokea mauti kwa ujasiri na imani kubwa. Kitendo cha fedheha kilichomkuta kiongozi mkuu wa sasa wa Afrika Kusini kuzomewa mbele ya uso wa dunia  na wananchi wake waliomchagua kidemokrasia si cha kupuuzwa hata kidogo. 

Ni muhimu kujifunza na kujitahidi kubadilika ili kuepusha shari na matokeo mengine mabaya ambayo huletwa na tabia za viongozi kuonekana wanajijali binafsi. Kuwaumbua viongozi hasa wale wasiojitambua husababisha hasira na kulipiza kisasi kwa wanaothubutu kufanya hivyo. Hali hii husababisha mitafaruku; huweza kugawa taifa na kuondoa amani. Naamini yote mazuri yaliyopiganiwa wakati wa uhai wa Mzee Mandela na Mwalimu Nyerere yamewekwa katika msingi imara ya kuwezesha kuyaendeleza. Kazi kubwa ni kwa tuliobaki nyuma kuamua na kuanzia walipoachia.

Kwaheri Mzee Nelson Rolihlalha Mandela. Mungu akupumzishe kwa amani na raha ya milele akujalie kama ulivyonuwia katika matendo na maisha yako.


*Notburga A Maskini ni Kaimu Rais wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (TUCTA).

Friday, December 20, 2013

Leo kumbukumbu ya kufariki Hayati Alex Nyirenda

Leo ni miaka mitano tangu kufariki Hayati Brigedia Alex Gwebe Nyirenda aliyefariki Dar es Salaam mwaka 2008 kwa ugonjwa wa saratani ya koo.

Usiku wa tarehe 8 Desemba mwaka 1961, muda mchache kabla ya kutimia saa 6:00 kamili usiku, siku ambapo Tanganyika ilipata uhuru wake, Brigedia Nyirenda alikuwa kileleni mwa Mlima Kilimanjaro kupandisha bendera ya taifa jipya la Tanganyika wakati bendera ya Uingereza ilipokuwa inateremshwa kwenye uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Luteni Alex Nyirenda, akiwa na bendera ya Tanganyika na Mwenge wa Uhuru kwenye kilele cha Mlima Kilimanjaro siku Tanganyika ilipopata uhuru wake, tarehe 9 Desemba 1961. (Picha ya Idara ya Habari, Maelezo
Miaka mwili kabla, tarehe 22 Oktoba 1959, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, akihutubia Baraza la Kutunga Sheria, alisema yafuatayo:

Sisi watu wa Tanganyika tunataka kuwasha mwenge na kuuweka juu ya Mlima Kilmanjaro umulike nje ya mipaka yetu na kuleta tumaini pale ambapo kulikuwa hakuna matumaini, upendo pale ambapo palikuwa na chuki, na heshima pale 

palipojaa dharau.

Miaka miwili kabla, tarehe 22 Oktoba 1959, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, akitoa hotuba kwenye Baraza la Kutunga Sheria, alisema yafuatayo: 
Huu mwenge ambao baadaye ulikuja kujulikana kama Mwenge wa Uhuru ulisimikwa juu ya Mlima Kilimanjaro na Nyirenda, ukiashiria msimamo wa muda mrefu na usiotetereka wa Tanzania kuunga mkono juhudi za ukombozi wa nchi za Kiafrika ambazo katika miaka ya mwanzo ya sitini zilibaki chini ya ukoloni na tawala za kibaguzi.

Mwaka 1958 Nyirenda alikuwa Mtanganyika wa kwanza kuhitimu kutoka Chuo cha Kijeshi cha Sandhurst cha nchini Uingereza. Aidha, kabla ya uhuru, alikuwa Mwafrika wa kwanza kuwa afisa ndani ya Kings African Rifles, jeshi la kikoloni la Uingereza ambalo baada ya uhuru ndiyo likabadilishwa na kuwa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ).

Alikuwa na uhusiano wa kiukoo na rais wa zamani wa Zambia, Dk. Kenneth Kaunda, jambo ambalo linakumbusha Waafrika kwamba wako karibu sana kuliko mipaka ya nchi zao inavyoashiria.

Wednesday, December 18, 2013

Lugha Yetu Kiswahili

Hivi karibuni, wakati nikisikiliza matangazo ya Idhaa ya Kiswahili la Shirika la Utangazaji la Uingereza (BBC) mtangazaji alisoma taarifa za majeshi ya Umoja wa Mataifa yaliyoko mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo kuanza kutumia ndege zinazosemekana kuruka bila rubani, kwa Kiingereza zikijulikana kama drones.

Ukweli ni kuwa ndege hizo zinaongozwa na marubani ambao wako ardhini kwenye vituo maalum.

Mtangazaji alitumia neno "drone" lakini akauliza iwapo lipo neno la Kiswahili lenye kutoa maana hiyo hiyo. Mimi haraka haraka niliangalia kwenye kamusi ya Kiingereza kwa Kiswahili ya Taasisi ya Uchungizi wa Kiswahili (TUKI), toleo la mwaka 2006, na nikatuma ujumbe mfupi wa maandishi BBC: "drone ni nyuki dume."

Wasikilizaji wengine nao wakatuma majibu yao, mmoja akipendekeza kuwa tafsiri sahihi iwe "ndege tiara." Hayakuwa mashindano na hakuna aliyepewa zawadi yoyote, lakini nakiri kuwa "ndege tiara" inasikika vizuri zaidi kuliko "nyuki dume."

Habari inayozungumzia shambulizi la nyuki dume dhidi ya wapiganaji itachukuliwa na maana kuwa ni nyuki ndiyo waliofanya shambulio hilo na siyo ndege inayoruka angani.

Wataalamu wa lugha ya Kiswahili mnasemaje?

Hatua kumi za mauaji ya kimbari: 7 na 8

Nimetembelea Rwanda hivi karibuni na nikiwa huko nilipata fursa ya kutembelea mojawapo ya vituo vya kumbukumbu ya mauaji ya kimbari ya mwaka 1994.

Jambo moja la msingi ambalo Watanzania tunaweza kijufunza ni kuwa maafa yaliyotokea Rwanda yanaweza kutokea pia Tanzania. Kwa mujibu wa wachunguzi wa sababu zinozogeuza binadamu mmoja kuwa adui wa binadamu mwenzake na hata kufikia hatua ya kumaliza uhai wa mwenzake ziko duniani kote.

Sababu hizi zinaanza na mchakato wenye hatua nyingi ambao hufikia mauaji kama yale yaliyotokea Rwanda. Kinachozuwia maafa kama hayo kutokea ni hatua mahususi zinazopaswa kuchukulia na jamii za kukatisha uendelezwaji wa huo mchakato.

Kwa mujibu wa Dr. Gregory Stanton wa Genocide Watch, hatua za viashiria vya kuwepo kwa mchakato na za kuzuwia maafa kama ya Rwanda ziko kumi.

Hatua ya Saba: Mipango

Hatua hii inahusisha kuunda mfumo wa kijeshi, kutoa mafunzo kwa wanamgambo, kukusanya silaha za maangamizi, na kuzitawanya kwa wauaji.

Hatua za kuepusha Mipango

Pale inapothibitishwa dalili za mipango kufanyika, basi tahadhari juu ya uwezekano wa kutokea mauaji ya kimabri utolewe. Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa litowe onyo kuwa litakuwa tayari kuchukua hatua pale tu ambapo lina uhakika kuwa litachukua hatua madhubuti za nguvu dhidi ya wahusika. Viongozi wa dunia wawaonye wale wanaokusudia kutenda maangamizi kuwa watachukuliwa hatua dhidi ya uhalifu watakaoufanya. Msaada wa kibinadamu unadaliwe. Majeshi ya kikanda yaandaliwe na kupewa uwezo wa kujiandaa na wa kifedha.
"Amri Kumi za Gitera" ni waraka uliotolewa na kiongozi wa kabila wa Wahutu kuchochea mauaji ya kabila la Watusi kabla ya mauaji ya kimbari ya Rwanda.  

Hatua ya Nane: Mateso

Katika hatua hii watu wanagawanywa kwa misingi ya ukabila na dini. wahanga wananyang'anywa mali zao. Wahanga hufukuzwa kutoka kwenye nyumba zao. Katika baadhi ya nchi wahanga walihamishwa na kuwekwa kwenye maeneo mahususi ya miji.  Katika baadhi ya nchi wahanga walikusanywa kwenye kambi za wakimbizi wa ndani.

Itaendelea na: 
  • Hatua ya Tisa: Mauaji
  • Hatua ya Kumi: Ukanushaji
Taarifa nyingine zinazohusian na hii:

Tuesday, December 17, 2013

Mandela! Mandela! Mandela! (sehemu ya pili ya awamu tatu)

Kwenye makala hii ambayo imegawanywa kwenye awamu tatu, Notburga Maskini anaandika kuhusu Mzee Nelson Mandela, aliyefariki tarehe 5 Desemba na kuzikwa leo, tarehe 15 Desemba 2013 kwenye kijiji cha Qunnu nchini Afrika ya Kusini.

Mandela! Mandela! Mandela! (Sehemu ya Pili)
Na Notburga Maskini*

Migongano ya Kitabaka
Matabaka ya mabwana na watwana yalijitokeza kutokana na unyonyaji, udhalilishaji, na ubaguzi uliofanywa na makundi dhalimu ambayo yalijitokeza na kuonekana katika mifumo ya kijamii kwa maana ya Ukomunisti na Ubepari ambapo mabwana au wenye nguvu, waliwadhalilisha wanyonge; ilitengeneza tabaka la watu wachache matajiri wa kupindukia ambao wameshikilia na kuwekeza asilimia 80 ya utajiri wa dunia katika mtaa wa tano (the 5th Avenue New York).  

Tabaka la pili ni la umma wa wakulima na wafanyakazi maskini na wanyonge katika nchi zetu na duniani ambao bidii na jasho lao haviwawezeshi kujikwamua kutokana na mirija ya dhuluma iliyopangwa na tabaka hili  la watu wachache lakini lenye nguvu kubwa kiuchumi na kiutawala. Tabaka la tatu ni tabaka la maskini wa kutupwa miongoni mwao wakiwemo wazee, wastaafu, vijana wasio na ardhi wala ajira, wanawake na watoto.

Hali hii  ya kuhuzunisha na tishio kwa amani ya nchi zetu na dunia ilionekana mapema machoni na kwenye mioyo ya viongozi hawa mashujaa Nelson Rolihlahla Mandela na Mwalimu Julius Kambarage Nyerere. Waliichukia na kufanya bidii kubwa kuchukua hatua sawia kupambana ili kuona mfumo wa haki usawa na heshima kwa binadamu unasimikwa dhidi ya mifumo ya unyonyaji, ubaguzi na udhalilishaji.

Kazi iliyobaki ya kugawa rasilimali hizi za dunia ziweze kuwafikia watu wengi na kuondoa umaskini duniani ndio njia pekee ya kumuenzi Mzee Mandela bila unafiki. Tunahitaji mashujaa kama Mzee Nelson Mandela na Mwalimu Julius Kambarage Nyerere ambao wataweka ushawishi na kupambana hasa wakati huu zinapoonekana dalili kuwa jambo hili linawezekana. Kifo cha shujaa huyu  tumeshuhudia viapo na dhamira zikiwekwa kanisani na hadharani kuashiria kuwa tayari hata kufa ili kutetea ustawi wa binadamu na amani duniani. 


State Funeral of former President Nelson Mandela, 15 Dec 2013
Picha: Maafisa wa jeshi la Afrika ya Kusini wakiwa wamebeba jeneza lenye mwili wa Marehemu Nelson Mandela kwenye mazishi ya taifa yaliyofanyika tarehe 15 Desemba 2013 kwenye kijiji cha Qunu, jimbo la Eastern Cape.

Kusaliti na kuvunja tabaka
Mzee Nelson Mandela na Mwalimu Julius Nyerere ni miongoni mwa watu waliojaaliwa na Mwenyezi Mungu kuumwa na kuchukizwa na hali mbaya ya binadamu wote. Waliona ubaya na adha inayotokana na binadamu kumdhalilisha binadamu mwingine na hatari yake kwa amani ya dunia hivyo hawakuivumilia hata kwa sekunde chache. Walipinga hali hii pamoja na uwezo waliokuwa nao kutokana elimu na nafasi zao za kuzaliwa wakiwa watoto wa machifu, ambapo wangaliweza kuungana na wadhalilishaji na kuwa wanufaikaji wa mifumo dhalimu iliyojaa uroho, uchoyo, dharau, na tamaa.

Mzee Mandela na Mwalimu Nyerere walizungumza kwa sauti kubwa na hivyo kuweka ushawishi mkubwa ndani ya jamii na nchi zao na kuanzisha vuguvugu la mapambano yaliyokusudia kuleta heshima kwa binadamu. Ni dhahiri kuwa walitumia maisha yao hapa duniani kujitoa mhanga kwa ujasiri wa kupindukia hata kuuwa matabaka yao (class suicide) kupigania usawa haki na heshima kwa binadamu. Ndiyo maana kuondoka kwao duniani Mzee Nelson Mandela aliyetanguliwa na rafiki yake mkubwa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere muongo mmoja na nusu uliopita kunaleta mshtuko na wasiwasi mkubwa kwa amani ya dunia, usawa, ubinadamu, demokrasia, na utawala bora.  Hii inatokana na ukweli kwamba binadamu wa aina hii hutokea kwa nadra sana.

Itaendelea na: Heshima katika historia ya nchi na dunia


*Notburga A Maskini ni Kaimu Rais wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (TUCTA).

Sunday, December 15, 2013

Mandela! Mandela! Mandela! (sehemu ya kwanza ya awamu tatu)

Kwenye makala hii ambayo imegawanywa kwenye awamu tatu, Notburga Maskini anaandika kuhusu Mzee Nelson Mandela, aliyefariki tarehe 5 Desemba na kuzikwa leo, tarehe 15 Desemba 2013 kwenye kijiji cha Qunnu nchini Afrika ya Kusini.

Mandela! Mandela! Mandela! (Sehemu ya Kwanza)

Na Notburga Maskini*

Hiki kimekuwa ni kilio cha dunia nzima kumwomboleza shujaa mpigania uhuru, amani, haki, utu na utawala bora duniani, mwana wa bara la Afrika mwenye asili ya Afrika ya Kusini Nelson Rolihlahla Mandela mwanaharakati, kiongozi wa chama cha ANC na Rais Mstaafu wa Afrika ya Kusini; aliyeaga dunia tarehe 5 Desemba 2013.  Mimi binafsi na kwa niaba ya wafanyakazi wa Tanzania naungana na Watanzania wenzangu, wafanyakazi wa Afrika ya Kusini na Dunia kuomboleza msiba huu mkubwa ambao ni pigo kubwa kwa tabaka la wafanyakazi duniani na vilevile ni pigo dhidi ya utawala bora, haki, amani na utu. 

South Africans mourn the
death of the late former President Nelson Mandela, 8 Dec 2013
Picha: Wanachama wa Umkhonto We Sizwe, lililokuwa jeshi la chama cha African National Congress lilioendesha mapambano ya kivita dhidi ya utawala wa kibaguzi wa Afrika ya Kusini, wakiwasili kwenye makazi ya jijini Johannesburg ya marehemu Nelson Mandela tarehe 8 Desemba 2013. (Picha ya GCIS).

Niandikapo makala hii nakumbuka mwaka 2003 nilipokuwa jijini Johannesburg kuhudhuria mkutano wa dunia kuhusu uwekezaji wa mitaji Afrika, Kusini mwa Sahara kwenye ukumbi mmojawapo katika jengo maarufu la Sandton. Wakati wa kutoka ukumbini tulikutana nae ana kwa ana mlangoni akiwa na watu wengine, nafikiri kiongozi huyu alitokea kwenye ukumbi mwingine wa mkutano katika jengo hilo. Binafsi nilifurahi sana kumuona Mzee Mandela aliyekuwa katika hali ya kawaida kabisa. Hata hivyo mimi na hata wenzangu hatukuweza kufanya chochote angalau kuweza kumsalimia kutokana na kutofahamu taratibu na mipaka ya kiitifaki.  Alikuwa ni kivutio kikubwa kwetu sote tuliokuwepo siku hiyo.

Afrika Kusini na Tanzania
Ndugu zetu wa Afrika ya Kusini kama ilivyokuwa kwetu Watanzania tarehe 14 Oktoba 1999 alipotuaga Mwasisi wa Taifa hili, mwanamapinduzi aliyeheshimika duniani, na kipenzi cha Watanzania, Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, nao wanapitia hali ngumu iliyojaa majonzi, vilio, na mashaka lakini pia wakimshukuru Mungu kwa zawadi kubwa aliyoupatia umma wa Afrika Kusini, Bara la Afrika na Dunia.

Katika kitabu chake cha dondoo Nelson Mandela By Himself, 2013 Mzee Mandela anatufariji kwa maneno yake mwenyewe kuwa: 

“kifo hakikwepeki. Wakati binadamu ameshatimiza yale aliyofikiri kuwa ni wajibu wake kwa watu wake na nchi yake, anaweza kupumzika kwa amani.  Naamini kuwa nimefanya bidii kutimiza wajibu huo na ndio maana nitalala katika umilele”  

Ni dhahiri kuwa Mzee Mandela ameondoka akiwa anaridhishwa na bidii kubwa aliyoweka katika kazi kubwa aliyoifanya ya kuondoa ubaguzi wa rangi na udhalilishwaji wa mtu mweusi katika nchi yake ya Afrika ya Kusini. Pengine Watanzania na waombolezaji tuliobaki yafaa kutafakari sasa kuhusu wajibu wetu kwa watu wetu na nchi zetu na iwapo tutaweza kuwa jasiri na kusema maneno hayo siku yetu itakapofika. 

Imani na mapenzi ya Umma dhidi ya chuki za maadui
Mzee Nelson Mandela kama alivyokuwa Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere wameteka mioyo ya walimwengu na wananchi wao kwa imani yao katika utu badala ya vitu, na kusimamia kwa vitendo bila ya kutetereka. Wanamapinduzi hawa wa Afrika waliweka mbele maslahi ya taifa na utu wa watu wao.  Walijitoa muhanga maisha yao yote kwa ajili ya nchi zao na watu wao jambo ambalo ni nadra kwa viongozi wengi tuliowashuhudia katika karne ya ishirini.

Wakati Mwalimu Julius Nyerere akiongoza mapambano ya ukombozi wa Bara la Afrika na dhidi ya udhalimu dhidi ya ubinadamu ikiwemo Afrika Kusini yenyewe, alitengeneza maadui waliotokana na kundi la wakandamizaji waliojijengea uhalali na kuamini kuwa wao ni bora kuliko binadamu wengine. Hata hivyo maadui hao kama tunavyoshuhudia leo wamejirudi na kujifunza thamani ya utu na utaifa katika kutumikia umma. 

Isingewezekana wakati ule wa mapambano ya ukombozi kuwa Afrika ya Kusini ingebadilika na kuwa kama ilivyo sasa. Kinachodhihirika hapa ni nguvu ya upendo, msamaha, na uzalendo kwa nchi na watu wake vinavyoweza kuleta mabadiliko chanya.  Hili ni somo kubwa kwa Afrika na Dunia.

Itaendelea na: Migongano ya Kitabaka

*Notburga A Maskini ni Kaimu Rais wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (TUCTA).


Friday, December 13, 2013

Afrika Kusini waomboleza kifo cha Nelson Mandela

Katika maeneo mbali mbali nchini Afrika Kusini wananchi wamejitokeza kuweka sahihi na kuweka kumbukumbu baada ya kifo cha Mzee Nelson Mandela, aliyefariki tarehe 5 Desemba 2013 baada ya kuugua kwa muda mrefu.

Kwenye picha (juu) wananchi wa Afrika Kusini waliopo Johannesburg wakiandika kwenye bango la kumbukumbu.

Mzee Mandela atazikwa tarehe 15 Desemba 2013.

Sunday, December 1, 2013

Hatua kumi za mauaji ya kimbari: 5 na 6

Nimetembelea Rwanda hivi karibuni na nikiwa huko nilipata fursa ya kutembelea mojawapo ya vituo vya kumbukumbu ya mauaji ya kimbari ya mwaka 1994.

Jambo moja la msingi ambalo Watanzania tunaweza kijufunza ni kuwa maafa yaliyotokea Rwanda yanaweza kutokea pia Tanzania. Kwa mujibu wa wachunguzi wa sababu zinozogeuza binadamu mmoja kuwa adui wa binadamu mwenzake na hata kufikia hatua ya kumaliza uhai wa mwenzake ziko duniani kote.

Sababu hizi zinaanza na mchakato wenye hatua nyingi ambao hufikia mauaji kama yale yaliyotokea Rwanda. Kinachozuwia maafa kama hayo kutokea ni hatua mahususi zinazopaswa kuchukulia na jamii za kukatisha uendelezwaji wa huo mchakato.

Kwa mujibu wa Dr. Gregory Stanton wa Genocide Watch, hatua za viashiria vya kuwepo kwa mchakato na za kuzuwia maafa kama ya Rwanda ziko kumi.

Hatua ya Tano: Uratibu

Kwa kuwa mauaji ya kimbari yanaendeshwa na makundi dhidi ya makundi mengine, yanahitaji kuratibiwa. Kwa kawaida, ni dola inayoratibu maafa haya kwa kutoa fedha na silaha kwa makundi yanayoendesha mauaji.

Mfano wa Uratibu: Rwanda

Tabaka la watu wenye uwezo ndani ya Rwanda walitoa silaha kwa kundi la Interahamwe ambalo liliendesha mauaji. Serikali na wafanyabiashara wa Kihutu walitoa mapanga 500,000 na kuandaa kambi za mafunzo za "kulinda vijiji vyao" kwa kuua Watutsi.

Hatua za kuepusha Uratibu

Kuchukulia makundi yenye muelekeo wa kuchochea mauaji kama makundi ya jinai. Chukua hatua za kufanya uanachama ndani ya makundi hayo kuwa kosa la jinai na kushinikiza viongozi wao kukamatwa.

Kunyima visa kwa viongozi wa makundi haya na kukamata mali zao zilizopo nchi za nje.

Kuweka vikwazo vya silaha dhidi ya makundi yanayoeneza chuki na dhidi ya serikali zinazounga mkono chuki kwa misingi ya dini na ukabila.
Wakati wa mauaji ya kimbari ya Rwanda ya mwaka 1994 kwenye shimo hili zilikutwa maiti za maelfu ya wahanga wa mauaji hayo.

Hatua ya Tano: Kingamizi

Katika hatua hii mambo kadhaa yanajitokea, ikiwa ni pamoja na :

  • wenye siasa kali wanakuwa na nia ya kutenganisha makundi
  • makundi yenye kuchochea chuki na kuchapisha propaganda yenye nia ya kugawa watu
  • sheria zinapitishwa kuharamisha ndoa kati ya watu na makundi yanayokusudiwa kuwa tofauti
  • wenye msimamo wa kati wananyamazishwa, kutishwa, na kuuwawa

Mifano ya Kingamizi: Ujerumani

Maandamano yaliandaliwa dhidi ya wafanyabiashara wenye asili ya Kiyahudi, na Wajerumani wenye msimamo wa kati waliopinga kitendo hiki ndiyo walikamatwa kwanza na kupeleka kwenye kambi za mauaji.

Hatua za kuepusha Kingamizi

Pinga kwa kila hali sheria na sera zinazobagua makundi au zinazonyima haki za kiraia kwa makundi. Weka walinzi wa silaha kulinda viongozi wenye msimamo wa kati, kama ambavyo imefanyika Burundi. Shinikiza kuachiliwa kwa viongozi wenye msimamo wa kati ambao wanakamatwa, na kudai na kuendesha uchunguzi kwa wale viongozi wa aina hiyo ambao wameuwawa.

Pinga kupinduliwa kwa serikali na makundi yenye siasa kali.

Itaendelea na:
  • Hatua ya Saba: Mipango
  • Hatua ya Nane: Mateso