Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Monday, September 21, 2015

Ushauri kwa wanaopiga kura kwa mara ya kwanza

Nimepiga kura kwa mara ya kwanza mwaka 1985. Ningeweza kupiga kura mwaka 1980 lakini sikuwa nchini wakati huo, nilikuwa masomoni. Naamini kuna vijana wengi ambao watakuwa wanapiga kura kwa mara ya kwanza mwaka huu na naomba nitoe ushauri mdogo kwao.
Nikiwa na Mwalimu wangu, Godian Muikza (kushoto) ambaye ni diwani anayemaliza muda wake wa Kata ya Ikondo, Wilaya ya Muleba Kusini.

Kwanza lipo suala muhimu la kuchambua ahadi. Kwenye uchaguzi mkuu wa mwaka 1985 nilimpa kura ya urais Alhaji Ali Hassan Mwinyi na ya ubunge nilimpa Kapteni Ukiwaona Ditopile Ramadhani Mwinshehe Mzuzuri. Siku zile sikuwahi kuhudhuria mkutano wowote wa kampeni za uchaguzi kwa hiyo kura yangu ya ubunge sikupiga kutumia kigezo kikubwa zaidi ya kufurahishwa na jina la mgombea. Sikumbuki hata alikuwa anagombea nafasi ile dhidi ya nani, lakini nakumbuka ilikuwa wanawania nafasi ya ubunge wa jimbo la Ilala. Mgombea urais, Mzee Mwinyi, alikuwa ana fursa ya kusikika zaidi ya wagombea ubunge kwenye vyombo vya habari kwa hiyo yeye tulimsikia zaidi ya wagombea ubunge.

Hata mwaka huu naamini kuna wapiga kura wengi watajitokeza wa aina yangu, kama nilivyokuwa mimi mwaka 1985 na kupiga kura kwa kufurahishwa na jina la mtu tu bila hata kuchambua kwa makini sera anazowakilisha mgombea huyo. Mwaka 1985 hatukuwa na vyama vingi, lakini sasa vipo. Kwa hiyo, hakuna sababu ya msingi ya mpiga kura yoyote kuacha kuweka sera za vyama kwenye mizania na kuamua chama kipi kitapata kura yake. Hatuna uhakika kuwa yanayoahidiwa yatatekelezwa, lakini bado ni muhimu kuchambua sera tofauti. Akishinda mtu wako na asipotekeleza ilani yake angalau unayo sehemu ya kuanzia kumhoji. Kama ulimchagua kwa mkumbo tu hutakuwa na kigezo cha kuamua kuwa hajatimiza ahadi zake.
Wapiga kura wa Butiama wakipiga kura kwenye uchaguzi mkuu wa mwaka 2010


Pili, nazungumzia wale ambao wana uhakika mkubwa wa matokeo ya ushindi kwa wanaowaunga mkono, ikiwa ni vyama vya siasa au mgombea mmoja mmoja. Kusikiliza na kuamini na kauli kama “ushindi ni lazima” ni mwanzo wa kukaribisha vurugu. Kama kiongozi anatumia kauli hiyo kuhamasisha tu wafuasi wake ili waweke juhudi kubwa kwenye kampeni inaweza kuwa haina madhara. Lakini kauli hiyo inaweza kufasiriwa kuwa “tumeshashinda hata kabla ya kupiga kura na mtu yoyote atakayesema kuwa hatujashinda ni muongo na ametuibia kura.” Hapo tunakaribisha vurugu.

Mwaka 2010 niliteuliwa wakala wa mgombea ubunge na nilijifunza kitu kimoja cha msingi. Kama wakala wa mgombea yuko makini, siyo rahisi kuibiwa kura. Sikulala siku hiyo mpaka matokeo yalipothibitishwa na msimamizi wa uchaguzi alfajiri ya siku iliyofuata. Wanaoibiwa kura ni wale ambao wameweka mawakala ambao siyo waaminifu au ambao hawakuwa makini. Mtu akitaka kuibiwa, ataibiwa.
Kulia ni Mhe. Vincent Nyeerere, Mbunge wa Musoma Vijijini kupita Chama cha Maendeleo na Demokrasia (CHADEMA) anayemaliza kipindi chake cha ubunge aliyeniteua kusimamia kura zake kwenye uchaguzi mkuu wa mwaka 2010. Kushoto ni aliyekuwa Mkuu wa Wilaya ya Musoma, Kapteni Godfrey Ngatuni.
Tangu kuanzishwa mfumo wa vyama vingi tumesikia shutuma kuwa Chama cha Mapinduzi (CCM) ndiyo wataalamu wa kuiba kura. Kama hizo shutuma ni za kweli, sioni sababu yoyote ya kutoana roho kwa sababu sasa hivi Mhe. Edward Lowassa amehamia upande wa pili. Yeye amekulia na kujifunza siasa ndani ya CCM na, kwa vyovyote vile, atakuwa amehama na uelewa uliobobea wa mbinu zinazotumika kuiba kura na atakuwa anafahamu mbinu za kutumika kuzuwia wizi huo. Mwizi hawezi kumuibia mwizi.
Mwanachama wa Chama cha wananchi (CUF) akielekea kwenye mkutano wa kampeni jijini Mwanza mwaka 2010.

Kwa sababu hii sioni kabisa busara ya mtu yoyote kutamka kuwa kaibiwa kura kama yeye mwenyewe hataki kuibiwa kura. Labda atumie kauli hiyo kama kisingizio cha kupinga matokeo. Tunao wajibu wa kujenga mazingira yenye kulinda amani, lakini tunao pia uwezo wa kuweka mazingira yanayobomoa amani.

Uchaguzi huu umeibua ushindani mkubwa kati ya CCM na vyama vinavyowakilishwa na UKAWA. Kwa bahati mbaya, ushindani unaonyesha dalili za uhasama na muelekeo kuwa kipindi hiki cha kampeni kitaibua matukio ya kuvunjika kwa amani. Lakini amani itavunjika tu iwapo wapiga kura tutakubali ivunjike. Na amani inapovunjika hutasikia hata siku moja kuwa Mhe. John Magufuli au Mhe. Edward Lowassa kavunjika mguu kwa sababu ya vurugu za kisiasa.


Bado sijaona sababu ya msingi ya kuvunjika kwa amani kutokana na uchaguzi. Usikubali kuwa chanzo cha kuvunjika kwa amani.

Thursday, September 10, 2015

Mada yangu ya leo: Hii siyo siasa

Tuawasikia baadhi ya viongozi waandamizi wa Chama cha Mapinduzi (CCM) wakimtaka mgombea urais wa UKAWA akubali wakutane kwenye mdahalo ili waeleze maovu yake. Yeye anasema kama wana ushahidi kuhusu maovu yake waende mahakamani. Hii siyo siasa.

Nionavyo mimi, siasa ingekuwa hivi:

1. Kama una tuhuma dhidi ya mgombea urais husubiri awe rais kwanza. Unasema yale unayoyafahamu. Akisha kuwa rais halafu utafanya nini? Utaomba mdahalo?

2. Mpiga kura ana haki ya kufahamu taarifa zote muhimu juu ya wagombea kabla hajafikia uamuzi wa kumchagua yule ambaye anaona anafaa. Kuamua kuwa taarifa hizo ni kama mali adimu haina tofauti na kujifanya mtaalamu wa bishara (au taaluma nyingine) ambaye ametumia muda mwingi kupata elimu na uzoefu kwenye taaluma yake halafu anaamua, kwa haki kabisa, kuwa taarifa hizo hazitoki mpaka kwa masharti yanayomnufaisha yeye, au kwa pesa au kwa njia nyingine atakayoamua. Ni wajibu wa kiongozi yoyote makini kumpa mpiga kura taarifa sahihi, hasa wakati wa uchaguzi.

3. Mpaka sasa, tumemsikia mtuhumiwa akisema kuwa hana tuhuma yoyote na, kwa mantiki hiyo, anaposema nendeni mahakamani ni sawa kabisa. Wale wenye taarifa hizo wakaziibue mahakamani. Watuhumiwa wachache sana hukubali kosa nje ya mahakama.

Kwa hayo machache, sisemi kuwa tuhuma ni za uongo.

Ninachoona ni kundi moja ambalo limekosa ujasiri wa kutamka wanalotaka kutamka na badala yake kuwafanya wapiga kura kubaki wanabishana wenyewe kwa wenyewe na ujinga wao* (kama ujinga huo upo kweli) bila kuwapa taarifa ambazo zinaweza kuwasaidia kufanya chaguo sahihi.

Kama huo ujasiri unakosekana, basi ni bora kunyamaza tu. Kuwafanya wapiga kura kuwa wajinga mara ya pili ni hatari kisiasa.

Huo ndiyo ujumbe wango leo hii.

*Wale ambao mtakimbilia kwenye Tume ya Mawasiliano kunilalamikia kuhusu kutumia neno "ujinga" ni kwamba siyo tusi, ni hali ya kutofahamu tu.