Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Saturday, December 31, 2011

Maoni ya Amani Millanga kuhusu mafuriko ya Dar: sehemu ya pili kati ya nne

Maoni ya Amani Millanga kuhusu mafuriko ya Dar: sehemu ya pili kati ya nne

Kuhamisha bila viwanja na fidia ni dhuluma
Serikali imetoa mwezi mmoja kwa waathirika kuwa wamehama. Jambo hili si sawa kwa sababu: kwanza, nyumba ya kuishi haijengwi ndani ya mwezi mmoja kutokana na waathirika kutokuwa na pesa za kununulia vifaa vya ujenzi katika hali ya mfuko wa bei na ughali wa maisha ulioko nchini. Pili, tukumbuke kwamba waathirika tunaowaongelea hapa ni kina mama lishe, wafagia barabara, walinzi korokoroni, wachimba mitaro, machinga na watu wenye hali duni. Kipato chao ni kidogo mno hata hawawezi kupata milo mitatu kwa siku. Ni watu wasio na akiba benki. Ni watu ambao hawawezi kupata mikopo benki kwani benki haimkopeshi maskini hata siku moja. Na hata kama wanayo akiba benki lakini ni ndogo sana, haiwezi kujenga nyumba ndani ya mwezi mmoja ukizingatia ughali wa vifaa vya ujenzi.

Iweje leo tuwaambie waondoke wakajenge nyumba ili hali tunajua fika kwamba hawana uwezo wa kujenga nyumba? Tatu, ipo hoja kwamba waathirika waliwahi kupewa viwanja wakati Mzee Makamba akiwa mkuu wa mkoa wa Dar es Salaam nao wakaviuza. Hawakuhama. Na sasa tunawalaumu kwa kuacha kuhama wakati ule. Lakini tusisahau kwamba waathirika hawa wameishi katika maeneo haya kwa miaka mingi sana. Hawakuhamia jana wala juzi. Wana historia ya vizazi na vizazi. Mtu kazaliwa pale, kakulia pale, kaoa au kuolewa pale na sasa ana wajukuu tunamwambia ahame eti aepuke mafuriko (ambayo hayatokei kila mwaka) bila kulipwa fidia. Hivi hoja hii itakuingia akilini hata kama ni wewe? Kama ni mimi sihami ng'o.

Waathirika walipaswa kulipwa fidia ya nyumba zao ili kupitia hapo wapate nguvu ya kifedha ya kuwawezesha kwenda kujenga huko waendako. Naamini hakuna mwathirika hata mmoja aliyewahi kulipwa fidia enzi za Makamba akiwa mkuu wa mkoa ili ahame.  Sasa kama hawakulipwa fidia kwa nini leo  tunawalaumu? Uko wapi utu katika suala hili? Iko wapi sheria inayolinda haki na utu wa waathirika hawa?

Nafahamu kabisa kuwa serikali au jiji litatumia mabavu kuwahamisha waathirika kwani limewahi kufanya hivi mara nyingi tu na kuwahamisha watu. Niseme wazi kabisa, kwamba, kitendo cha kuzibomoa nyumba za waathirika bila fidia inayolingana na thamani ya eneo hilo lililoko katika jiji, na bila kuwapa viwanja, kitakuwa ni kitendo cha dhuluma. Na pia kuwapa viwanja tu, au kuwalipa fidia tu, ni dhuluma vilevile. Tutakuwa tumefanya uonevu. Tutakuwa tumekiuka haki za binadamu. Tutakuwa tumeudhalilisha utu wa waathirika. Baya zaidi tutakuwa tumewafanya waathirika kuwa maskini zaidi na zaidi.

Tukumbuke kuwa wakati wanajenga serikali ilikuwepo. Mbona haikuwazuia? Bomoabomoa ikifanyika bila kuwatendea haki itakuwa ni udhalimu. Katika hali sasa upo uwezekano wa kutolewa hoja kwamba serikali haiwezi kuwalipa fidia waathirika wanaoishi mabondeni. Swali hapa ni kama ni halali kuilipa Dowans zaidi ya shilingi bilioni 94, iweje haramu kuwalipa waathirika?

Kimsingi huenda pesa watakayolipwa waathirika isifikie hata robo ya malipo ya Dowans. Kivipi? Wako waathirika takriban 5,000. Ukiwa na wastani wa watu watano kwa familia moja ina maana una familia 1,000 za waathirika ambazo ni kaya au nyumba 1,000. Tuseme tunawalipa shilingi milioni 20 kila familia. Unapata jibu kwamba ni shilingi milioni 20 zidisha kwa familia 1,000 ambazo ni jumla ya shilingi bilioni 20.

Pesa hizi zitabaki nchini hazitakwenda nje kama Dowans. Pesa hizi zitaondoa umaskini kwa waathirika kinyume na zile za Dowans zitakazoongeza umaskini kwa kila mtanzania. Shilingi bilioni 94 ukizigawa kwa watu milioni 43 tulionao sasa utapata kila mmoja wetu analipa shilingi 2,186.05. Asilimia 50 ya Watanzania kwa mujibu wa takwimu zetu ni maskini wanaoishi chini ya dola moja kwa siku. Dola moja ni sawa na shilingi 1,583.50 leo hii tunawataka kila mmoja alipe dola 1.38 sawa na shilingi 2,186.05 kwa Dowans. Kama mlo wa Mtanzania maskini ni shilingi 1,000 kwa siku basi hii ina maana kwamba maskini wasile siku mbili ili tukawalipe Dowans. Ajabu sana hii.

Itaendelea.

Tuesday, December 27, 2011

Maoni ya Amani Millanga kuhusu mafuriko ya Dar: sehemu kwa kwanza kati ya nne

Waathirika wa mafuriko wahame: sehemy ya kwanza kati ya nne
Na Amani Millanga

Ndugu zangu Watanzania, naungana nanyi kutoa mkono wa pole kwa waathirika wote wa mafuriko. Poleni sana kwa kupoteza ndugu, jamaa, na marafiki waliofariki katika mafuriko haya. Pia poleni sana kwa kupoteza mali zenu na vitu vyenu vyote kama nyaraka za umiliki wa nyumba zenu, vtambulisho na hata picha za familia n.k. ambavyo ni sehemu ya historia ya maisha yenu. Poleni sana na inshaallah Mungu atawasaidia. Anauona unyonge wenu. Auona umaskini wenu. Anauona udhalili wenu. Na kubwa zaidi Mungu muumba anauthamini sana utu wenu enyi waja wake mlioathirika na mafuriko. Naamuomba Mola Karima aziweke roho za marehemu pema peponi, inshallah. Nazipongeza jitihada zilizofanywa na watu binafsi, mwashirika binafsi pamoja na serikali za kutoa msaada wa kila hali na mali katika kuwafariji waathirika. Inshallah Mungu atakulipeni kwa sadaka zenu.

Wahame Mara Ngapi?
Haya si mafuriko ya kwanza kwa jiji la Dar es Salaam lakini n mafuriko ya kwaanza kufanya uharibifu mkubwa kama tulivyoshuhudia. Mafuriko yamefika hadi Ikulu, ofisi za UN na UNDP. Athari za mafuriko haya zimesababisha kuwepo kwa hoja nyingi kuhusiana na waathirika. Hoja inayotawala sana kwa baadhi ya watu na vyombo vya habari ni ile inayosema "waathirika wahame". Hoja hii haina mantiki wala mashiko yoyote. Hivi kweli hatuoni kwamba tayari waathirika wamekwishahamishwa na mafuriko? Hawako tena majumbani mwao. wanalala nje. Hivi tunataka wahame mara ngapi ili hali mvua imeishawahamisha? Kwa kweli hoja hii ya "wahame" tumeitoa katika wakati usiofaa kabisa. Huu si wakati wa kuwalaumu na kuwatia hofu ya kuwahamisha waathirika. Huu ni wakato wa maombolezo, huruma na huduma. Waathirika wanawalilia watoto zao, ndugu zao na jamaa zao waliofariki. wanalilia mali zao na historia yao. Kusema "wahame" si uungwana na si utu. Tukumbuke kwamba waathirika hawakuomba mafuriko. Lakini nitaitumia hoja hii ya "wahame" katika makala haya kutoa mchango wangu wa nini kifanyike katika wakati huu mgumu kwa taifa ambalo limesherehekea miaka 50 ya uhuru wake hivi karibuni.

Hoja za msingi kwa wakati huu: ni namna gani waathirika wanapata chakula na maji safi na salama; ni namna gani waathirika wanapata vyoo na bafu; ni namna gani waathirika wanalala; na ni namna gani waathirika wanapata nguo za kujisitiri; na tumejipanga vipi kuwakinga waathririka na magonjwa ya kuambukiza ya kipindupindu, malaria, kuhara, minyoo, n.k. Haya ndiyo mambo muhimu ya kufanywa kwanza. Ingawa baadhi yanafanyika basi tuongeze juhudi zaidi ya kutoa huduma zaidi. Pili, ni suala la wapi wanahamia waathirika hawa baada ya Mchikichini. Suala hili linaibua maswali mengi, lakini baadhi yake ni: Je, wahamishiwe wapi? Je, tumeishayatenga au kuyapima maeneo hayo ya kuwahamishia waathirika? Je, tutawalipa fidia za nyumba na ardhi yao? Je, fidia hiyo itachukua muda gani kumfikia muathirika? Je, wwanza kuhamishwa huko kwenye maeneo mapya lini? Maswali ni mengi yanayohusu huduma za afya, elimu na jamii huko wanakohamishiwa maana watu takribani 5,000 si wachache.

Itaendelea.

Monday, December 26, 2011

Matumla na Maneno nguvu sawa

Mabondia Rashidi 'Snake Man' Matumla, na Oswald 'Mtambo wa Gongo' Maneno wametoka sare katika pambano lao la jana lisilo la ibingwa kwa kugawana pointi 99 kwa 99.
Rashidi Matumla, kushoto, anakwepa ngumi ya Maneno Oswald katika pambano la jana.
Rashidi Matumla akiamka baada ya kuteleza kwenye pambano la jana.
Pambano lilifanyika jana katika Ukumbi wa Heineken, Mtoni Kijichi, Dar es Salaam. Kwa matokeo haya Matumla ameshinda mapambano mawili kati yao na kutoka sare pambano moja, wakati Maneno ameshinda pambano moja na kutoka sare moja.

Bila shaka tutasikia mpambano mwingine kati ya hawa mabondia wawili.

Picha na baadhi ya taarifa kwa hisani ya www.superdboxingcoach.blogspot.com

Saturday, December 24, 2011

Mabondia Rashidi Matumla na Oswald Maneno wapima uzito tayari kwa pambano lao kesho

Mratibu wa pambano za ngumi za kulipwa Shabani Adios "Mwayamwaya', katikati, akishuhudia mabondia Maneno Oswald "Mtambo wa Gongo", kushoto, na Rashidi 'Snake Man' Matumla kulia, wakitunishiana misuli mara baada ya kupima uzito leo kabla ya pambano lao lisilo la ubingwa litakalofanyika Dar es Salaam siku ya Noeli kwenye ukumbi wa Heineken, Mtoni Kijichi.
Picha na habari kwa hisani ya www.superdboxingcoach.blogspot.com

Thursday, October 27, 2011

Waziri Mary Nagu azindua ofisi ya kituo cha uekezaji Mbeya


Taarifa zifuatazo zimetolewa na blogu ya Mbeya Yetu:

Waziri Mary Nagu amezindu ofisi ya kanda ya Kituo cha Uwekezaji mjini Mbeya juma liliopita.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Uwezeshaji na Uwekezaji), Dk. Mary Nagu akikata utepe kuzindua ofisi ya kituo cha uwekezaji (TCI) nyanda za juu kusini mjini Mbeya.
Akizindua ofisi hiyo mwishoni mwa wiki jijini Mbeya, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Uwezeshaji na Uwekezaji), Dk. Mary Nagu alisema ofisi hiyo ni muhimu katika kusaidia wajasiriamali na wawekezaji wa mikoa ya Ruvuma, Iringa Rukwa na Mbeya kuitumia kwa ajili ya kuanzisha miradi mbalimbali ya uwekezaji.

Ufunguzi huo pia ulihudhuriwa na Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Kituo cha Uwekezaji, Balozi Elly Mtango, Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC), Raymond  Mbilinyi, Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Abbas Kandoro.

Monday, October 10, 2011

Mbwana Matumla ajiandaa kwa pambano dhidi ya Francis Miyeyusho

Mabondia Mbwana Matumla (kushoto) na Mussa Sunga (kulia) wakipigana wakati wa mazoezi ya kambi ya Ilala Dar es salaam hivi karibuni. Kulia ni kocha Mohamedi Chipota. 
Matumla anajiandaa na mpambano wake wa ubingwa dhidi ya Francis Miyeyusho litakalofanyika mwishoni mwa mwezi huu.(Picha na habari kwa hisani ya www.superdboxingcoach.blogspot.com)

Siku ya Nyerere, 14 Oktoba, kuadhimishwa Washington D.C.


Taarifa hii imetolewa na Mubelwa T. Bandio:
Maadhimisho ya nne ya kuenzi maisha na kazi za Mwl Julius K. Nyerere yatafanyika Oktoba 15, 2011 hapa Washington DC
Mmoja wa waasisi wa Julius Nyerere Commemoration Bwn Rick Tingling anaelezea maandalizi ya siku hiyo katika video hapa chini:

NYOTE MNAKARIBISHWA

Itafanyika 
Howard University Basement Auditorium
725, 2225 Georgia Ave, NW, Washington, DC 20059
FROM 3PM-6PM

MAELEKEZO KUELEKEA Howard University Hospital Basement Auditorium:

  1. Ingilia mlango wa mbele wa Hospitali unaotazamana na Georgia Avenue.
  2. Pita kwenye dawati la maelezo kwa utambulisho
  3. Endelea mbele mpaka kwenye "lift" zilizo kama yadi 50 toka dawati la mapokezi.
  4. Chukua "lift" / elevator kuelekea sakafu ya chini (basement).
  5. Elekea upande wa kulia ukifuata alama zinazoelekeza ulipo ukumbi.
AMBATANISHO: MAELEZO KUHUSU MAADHIMISHO HAYO.
NOTE: Mabadiliko pekee niliyojulishwa ni kuwa Balozi Mwanaidi Maajar hataweza kuhudhuria kwa kuwa atakuwa nje ya mji.

Tuesday, September 20, 2011

Mada yangu ya leo: Kumekucha


Wakati majadiliano ya madai ya katiba mpya yanaanza niliwahi kuandika makala kwenye safu yangu ya Letter from Butiama, iliyopo kwenye gazeti la Serikali, Daily News, nikitabiri kuwa yatatokea makundi tusiyoyatarajia katika mchakato huu wa kudai haki ndani ya katiba mpya.

Baadhi ya makundi hayo yameanza kuibuka, gazeti la Majira linaripoti. Toleo lake la Septemba 16, 2011 linanmnukuu mwakilishi wa kundi la mashoga akidai nao watambuliwe ndani ya katiba mpya ili kulinda haki zao kama raia. Alinukuliwa akisema kuwa hubaguliwa wanapoomba kazi na kwa kukosa ajira wanaendelea na tabia ambazo hazikubaliki ndani ya jamii.

Hoja yangu, ambayo niliitoa kwenye makala yangu ya Kiingereza kwenye gazeti la Daily News ni kuwa suala zima la mabadiliko ya kikatiba linajikita kwenye kumpa fursa kila raia kufurahia uraia wake bila bugudha toka kwa mtu, taasisi, au kundi lingine lolote la raia. Katiba pia inaainisha wajibu wa raia katika masuala mbalimbali.

Lakini tatizo ni kuwa kwenye nchi nyingi huwa hakuna makubaliano ya mipaka ya haki hizi, na wakati nchi nyingine zinaainisha haki kwa makundi fulani ya raia wake, nchi nyingine zinaweza kuweka marufuku kwa haki hizo hizo kwa makundi ya aina hiyo.

Mfano niliotoa kwenye makala yangu ni kuwa baadhi ya nchi zimepitisha sheria zinazoruhusu ndoa za jinsia moja wakati suala hilo ni ukiukwaji wa sheria kwenye nchi nyingi duniani. Rais Robert Mugabe, ambaye ni mpinzani mkubwa wa sera hizi akihutubia nchini Zimbabwe alisema kuwa sheria hizi zinataka kuruhusu "bibi yangu (nyanya) mzazi kuona na bibi yako."

Kwetu sisi migongano hiyo sasa imefika. Raia shoga anadai haki za kikatiba. Kwa misingi ya wale wanaotufundisha kuwa kila raia anapaswa kuwa na haki chini ya katiba ya nchi ni dhahiri kuwa raia huyu anapaswa kupewa haki zake ndani ya mabadiliko mapya ya katiba.

Iko hoja itakayotolewa na waumini wa dini kadhaa, kuwa suala la ushoga ni kinyume na mafundisho ya dini. Lakini misingi ya kikatiba na haki kwa raia inakinzana na maadili kama haya ya kidini. Kwa mitazamo hiyo hiyo ya haki kwa kila raia, raia wote – wenye dini na wasiyo nayo – wanapaswa kupata haki ile ile ya msingi chini ya katiba.

Kwa mantiki hiyo, yoyote anayepinga ushoga kwa misingi ya dini anaweza kujibiwa kuwa suala la dini haliwezi kuwa kigezo kwa raia ambaye hana dini na anayedai haki zake chini ya katiba.

Maadili, mila na desturi, na tamaduni vimekuwa vigezo vinavyoongoza jamii zetu tangu enzi za mababu na bado zinaongoza jamii katika sehemu nyingi za Tanzania ambapo vigezo hivi vinatumika. Lakini maingiliano na wageni yameleta na yanazidi kuleta vigezo vipya ambavyo vitaleta mkanganyiko mkubwa ndani ya jamii kwa ujumla, na hususani ndani ya huu mjadala wa katiba mpya.

Ni dhahiri kuwa kuna mengi yatapingwa kuhusu hivi vigezo vipya na kuna uwezekano mkubwa kuwa Watanzania wengi hawatakubali kuingizwa kwa haki za mashoga kwenye katiba. Lakini litakapokataliwa ina maana kuwa tutakuwa tumeamua kuchagua 'yanayotufaa' na 'yasiyotufaa'. Na uamuzi kuwa hili linafaa na hili halifai unakinzana na azma ya kumpa kila raia uhuru wa kuwa kile anachotaka kuwa. Kwa maana nyingine, kuna mipaka ya kitamaduni inayoshinikiiza kuwa siyo kila uhuru utakubalika ndani ya jamii ya Kitanzania.

Siyo kazi rahisi kuongoza Serikali katika nyakati hizi za sasa. Zamani ilikuwa rahisi kusema hili halifai, na hili linafaa. Siku hizi kila mtu ana haki. Siku hizi tunaambiwa hata watoto ambao bado wanajikojolea kitandani wanapaswa kupewa uhuru wa kuamua wanayoyataka wao.

Ni mkanganyiko usio mdogo. Ndio maana nasema, kumekucha.

Saturday, September 17, 2011

Mwanaharakati Brian Haw wa Uingereza amefariki

Nilivyotembelea Uingereza mwaka 2006 nilipata fursa ya kumtembelea mwanaharakati Brian Haw, aliyeweka hema mbele ya viwanja vya bunge la Uingereza kwa muda unaokaribia miaka kumi akiishi hapo na kutumia kipaza sauti chake kuendeleza kampeni yake dhidi ya vita vya Irak.
Brian Haw, kushoto, mimi, na mke wake Kay, kulia.
Taarifa ambazo nimechelewa kuzipata zinaeleza kuwa alifariki jijini Berlin, Ujerumani, tarehe 18 Juni, 2011 kutokana na ugonjwa wa saratani ya mapafu.

Nilipomtembelea alinieleza kuhusu kusudio lake la kumfikisha aliyekuwa waziri mkuu wa Uingereza Tony Blair kwenye mahakama ya makosa ya kivita kwa kuiingiza Uingereza kwenye vita vya Irak.

Jim Becket, Jaffar Amin, na Andrea Wobmann watarajia kupanda Mlima Kilimanjaro wiki ijayo


Niko njiani kuelekea Moshi kwa ajili ya maandalizi ya kupanda Mlima Kilimanjaro chini ya The Mwalimu Nyerere/Mt. Kilimanjaro Charity Climb

Nilikusudia kusafiri moja kwa moja hadi Moshi kupitia njia ya Serengeti lakini kwa bahati mbaya sikufanikiwa. Hivi sasa niko Mwanza na natarajia kufika Moshi kesho kupitia Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA).

Kutokana na maandalizi hafifu ya uchangishaji wa pesa za hisani ambao nafanya kila mwaka ninapokwea Mlima Kilimanjaro, yawezekana kuwa azma ya kuchangisha pesa za hisani haitafana sana mwaka huu. Katika siku chache zijazo na kabla ya kuanza msafara nitafanya uamuzi iwapo itawezekana kufanikisha kuchangisha pesa za hisani au iwapo nitalazimika kuahirisha uchangishaji huu mpaka msafara ujao wa kukwea Mlima Kilimanaro.

Suala lingine katika msafara wa mwaka huu ni kuwa muongozaji mashuhuri wa filamu toka nchini Marekani, Jim Becket, anakusudia kupiga picha za filamu wakati wa msafara huu. Jaffar Amin naye anatarajia kuungana nami katika msafara huu kutokana na makubaliano yetu wakati wa msafara wa mwaka jana kuwa tutaendeleza jitihada za kuchangisha pesa za hisani.

Kwa kuwa Jaffar atakuwa nasi, Jim anakusudia kujumuisha ndani ya filamu yake historia ya mahusiano kati ya Tanzania na Uganda na jinsi gani haya mahusiano yamebadilika, akijikita juu ya malengo ambayo mimi na Jaffar tunayo katika masuala ya hisani.

Mwanadada Andrea Wobmann ambaye amewahi kufanya kazi ya kujitolea jijini Mwanza naye pia anajiunga nasi kuukwea Mlima Kilimanjaro

Wednesday, September 14, 2011

Wageni wa Butiama: Kelvin Bernard


Muda si mrefu uliyopita, Kelvin Bernard, wa pili toka kulia kwenye picha hii hapa chini,
pamoja na wanafunzi wenzake Benedicto David, Raphael Nenebwa, and Kelvin Ryoba toka Mwanza walitembelea Butiama kwa ajili ya kukamilisha somo lao kuhusu Mwalimu Nyerere.

Walifanya utafiti wao kwenye Makumbusho ya Mwalimu Nyerere, kwenye maktaba ya Mwalimu Nyerere, na kwenye makazi ya Mwalimu Nyerere yaliyopo Mwitongo, Butiama.

Sunday, September 11, 2011

Mashambulizi ya Septemba 11: Marekani imeelewa somo?


Leo ni miaka kumi tangu kutokea mashambulizi ya Septemba 11 2011 yaliyofanyika katika miji ya Washington na New York nchini Marekani na kusababisha vifo vya zaidi ya watu 3,000.

Katika maadhimisho hayo vyombo kadhaa vya habari na taarifa nyingi zilizopo kwenye mtandao zimejikita kwenye kuwauliza walioshuhudia mashambulizi hayo kukumbuka hali ilivyokuwa kwao siku ya shambulio.

Lakini ni sehemu ndogo ya vyombo hivyo vya habari vinavyohoji kwanini shambulio lilitokea, na iwapo sababu ambazo zilisababisha shambulio hilo bado zipo, na ni hatua gani zimechukuliwa kuepuka kutokea tena shambulio kama hilo ambalo lilihusishwa na Osama Bin Laden, ambaye aliuwawa hivi karibuni.

Kama ni kweli kuwa shamubilizi hilo liliongozwa na Osama na wafuasi wake, kuna maswali ya kuuliza. Tofauti za kiitikadi na kidini zinazosemekana zilisukuma mashambulizi hayo bado zipo? Kama zipo, jitihada gani zimefanyika na Serikali ya Marekani na washirika kuziondoa? Kuna uwezekano wa kufikia muafaka utakaoweza kufuta hizo tofauti, na kuzifanya pande zote mbili kusitisha mapambano kati yao?

Afisa mwandamizi wa shirika la ujasusi la Uingereza MI5 alinukuliwa hivi karibuni akisema kuwa uwezekano wa kupambana na kuwashinda wafuasi wa makundi ya Kiislamu kama lile linaolomuunga mkono Osama ni ndogo sana, na nchi za Magharibi sasa zinaangalia uwezekano wa kukubali yaishe, yaani kukaa meza moja na upande wa pili kutafuta suluhisho lisilohusisha matumizi ya nguvu.

Mwandishi mmoja wa Marekani akihojiwa hivi karibuni alisema anaona kama bado Marekani haijajifunza kutokana na mashambulizi ya Septemba 11, 2001. Anaeleza kuwa badala ya kuwa ingefanyika jitihada kubwa ya kujaribu kuelewa tamaduni na desturi za watu wengine duniani, inaonekana kama vile Wamarekani bado wanajiona kuwa wanachoona sawa wao ndiyo sawa kwa binadamu wengine wote na wanaonekana hawajali sana yanayotokea sehemu nyingine ya dunia.

Thursday, September 8, 2011

Mimea ya Mlima Kilimanjaro


Mlima Kilimanjaro una mimea ambayo haipatikani sehemu nyingine yoyote duniani. Mmea huu unaitwa Giant Groundsel (jina la kisayansi ni Senecio 
keniodendron) na hustawi kwenye maeneo ambayo kwa kawaida yana ukungu mwingi. Kwenye picha ya hapo juu ni eneo lililopo karibu na kambi ya Barranco iliyopo mita 3,900 juu ya usawa wa bahari.

Tuesday, September 6, 2011

Matunda ya Nyamisisi

Ukifika Nyamisisi, eneo liliopo karibu ya Butiama, kwenye barabara kuu ya Mwanza - Musoma, utakuta harakati hizi za wafanyabiashara wanaouza matunda kwa abiria wa mabasi na gari ndogo zinazosimama eneo hilo.
Matunda mengi yanatokea Tarime na kuletwa Nyamisisi na wafanyabiashara.

Lugha yetu Kiswahili


Taswira ya lugha ya Kiswahili na ya wale wanaotumia lugha hiyo ni masuala ambayo yanaleta mitazamo na maana mbalimbali.

Nina rafiki yangu toka Kagera alinisimulia kuwa kwa baadhi ya Wahaya katika nyakati ambazo wenye uwezo wa kuongea Kiswahili fasaha walikuwa wachache, hasa kwenye maeneo ya vijijini, mtu yoyote aliyeongea lugha Kiswahili vizuri alionekana ni mtu mmoja mjanja mjanja ambaye hakuwa mtu wa kuaminika kwa urahisi.

Nakumbuka simulizi nyingine pia toka Uganda zinazoeleza kuwa kwa sababu lugha ya Kiswahili ilikuwa inatumika na wanajeshi (na inaendelea kutumika mpaka sasa) basi lugha hiyo imehusishwa katika historia ya Uganda na nyakati ambapo jeshi lilionekana kama kinara wa ukandamizaji na ukiukwaji wa haki za binadamu.

Katika matumizi fasaha ya lugha ya Kiswahili, mtu anayeitwa Mswahili, pamoja na kuwa na maana nyingine, ni mtu mwenye maneno mengi, na mjanja.

Friday, July 22, 2011

Maana sahihi ya neno 'fisadi'

Leo hii wakati nikisikiliza kipindi cha Kipima Joto cha ITV kinachoongozwa na Rainfred Masako, nimemsikia Profesa Tigiti Sengo akitoa ufafanuzi kuhusu matumizi sahihi ya neno 'fisadi'. Alisema:
Fisidi ndiyo mwizi; fisadi ni malaya na mlevi.
Huyu ni gwiji wa lugha ya Kiswahili. Natabiri kuwa miaka 20 tangu leo hii, Watanzania wataendelea kutumia neno ‘fisadi’ kama ambavyo linavyotumika sasa hivi kwa makosa. Au inawezekana mafisidi hawatakuwepo wakati huo.

Tuesday, July 19, 2011

Takwimu: Viwango vya mfumuko wa bei kwa baadhi ya nchi Ulimwenguni


Kwa wachumi, kipimo kimojawapo cha hali ya uchumi ni kasi ya ongezeko la bei za bidhaa na huduma. Kwa ujumla, kasi kubwa ya ongezeko haileti manufaa kwa uchumi na kazi mojawapo muhimu ya Serikali yoyote ni kudhibiti ongezeko la bei kwa kupitia sera zake. Aidha, ongezeko la bei linapunguza uwezo wa wafanyakazi kumudu gharama za maisha na linaweza kuwa chachu ya migomo ya wafanyakazi na ukosefu wa amani kwenye nchi.

Sifa mojawapo ya Serikali ya Awamu ya Tatu ya Tanzania ya Rais Benjamin Mkapa ilikuwa mafanikio yake ya kudhibiti kasi ya mfumuko wa bei.

Zipo nchi kadhaa duniani ambazo takwimu zake zinaonyesha kuanguka kwa mfumuko wa bei. Maana yake, ni kuwa bei za bidhaa na huduma zinapungua badala ya kupanda. Hizi, kwa mujibu wa wavuti ya Wikipedia ni pamoja na Seychelles, Ireland, na Gabon.

Orodha kamili ya Wikipedia inapatikana hapa. Baadhi ya nchi zilizopo kwenye orodha hiyo na kasi ya ongezeko la mfumuko wa bei ni kama ifuatavyo:

Nafasi Duniani
Nchi
Kasi ya Mfumuko wa Bei (%)
1
Seychelles
-2.2
2
Ireland
-1.6
3
Gabon
-1.3
7
Japan
-0.7
24
Ujerumani
1.1
27
Senegal
1.2
34
Burkina Faso
1.4
34
Marekani
1.4
40
Canada
1.6
50
Cameroon
1.9
55
Umoja wa Falme za Imarati
2.2
84
Libya
3.0
92
Uingereza
3.3
121
Kenya
4.2
130
Afrika ya Kusini
4.5
140
China
5
142
Zimbabwe
5.03
166
Rwanda
6.4
179
Tanzania
7.2*

*Hizi ni takwimu za 2010

Friday, July 15, 2011

Wageni wa Butiama: Dk. Thomas Molony


Mtafiti mwandamizi wa Kituo cha Masomo ya Afrika kilichopo Chuo Kikuu cha Edinburgh, Dk. Thomas Molony, yuko kijijini Butiama mwezi huu wa Julai akiandika kitabu juu ya muasisi wa Tanzania, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere (1922 – 1999).
Dk. Thomas Molony
Kitabu hicho kitahusu sehemu ya maisha ya Mwalimu kati ya mwaka 1922 alipozaliwa hadi mwaka 1952, baada tu ya kuhitimu masomo yake kwenye Chuo Kikuu cha Edinburgh na kabla hajajitupa kwenye harakati za kudai uhuru toka kwa Waingereza. 

Kwa kujiandaa na uandishi wa kitabu hiki, Dk. Molony amefanya utafiti nchini Uingereza na Tanzania na ni mara yake ya pili kutembelea Butiama. Anatarajia kitabu chake kitachapishwa kabla ya mwisho wa mwaka, kuwahi maadhimisho ya miaka 50 ya uhuru tarehe 9 Desemba.