Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Wednesday, November 11, 2015

Adha za Mwenge wa Uhuru

Sina tatizo na madhumuni ya mbio za Mwenge wa Uhuru, lakini ninaona kasoro kubwa katika baadhi ya vipengele vya mchakato wa mbio hizo unavyoendeshwa.

Mwenge unapohamishwa kutoka sehemu moja kwenda nyingine, barabara zote huwa au hazipitiki au zinapitika kwa shida. Barabara zinafungwa mpaka Mwenge upite. Wale wenye shida za dharura wanakuwa hawawezi kutumia usafiri wa barabara kufuatilia shida zao.

Hata mgonjwa mahututi ambaye anapelekwa hospitali au kwenye kituo cha afya anaweza kujikuta ndani ya gari akisubiri Mwenge upite kwanza, ndipo gari alilopanda (kama siyo la kubeba wagonjwa) liweze kuruhusiwa na kuendelea na safari yake.

Gari zikiwa zimesimamishwa eneo la Kisesa, Mwanza, zikisubiri msafara wa Mwenge wa Uhuru upite.
Na isingekuwa vibaya sana iwapo watu wangelazimika kusubiri kwa muda kidogo tu kupisha Mwenge upite. Tatizo ni kuwa wakati mwingine watu husubirishwa kwa muda mrefu sana ili msafara wa Mwenge upite, hata pale ambapo msafara huo unaelekea njia tofauti. Ili mradi tu unapishana nao, basi utalazimika kusimama.

Mwenge wa Taifa ni nembo ya Taifa na nadhani maana ya kusimamishwa watu njiani ni kutoa heshima kwa hiyo nembo ya Taifa. Sijui kama hii ndiyo mantiki ya hatua hizi, lakini inawezekana pia kuwa watu husimamishwa kwa sababu ya kipengele kimoja ambacho nadhani kipo kwenye Sheria ya Usalama Barabarani ambacho kinatamka kuwa msafara rasmi ni lazima upishwe.

Nadhani msafara wa Mwenge unapewa hadhi ya msafara rasmi, kama msafara wa rais au viongozi wengine wa ngazi ya juu. Hatari iliyopo ni kuwa msafara wa Mwenge unaweza kumsubirisha mgonjwa mahututi na asiwahi kupata huduma ya matibabu ambayo inaweza kuokoa maisha yake.

Tuesday, November 10, 2015

Mwalimu Nyerere na nguzo ya uwajibikaji kwa wote katika uongozi

Kwenye kijitabu chake, Ujamaa ni Imani 1: Moyo kabla ya silaha, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere anasema:

Alinijia Mzanaki mmoja mwaka 1961, mara tu baada ya kupata uhuru. Anataka kazi; anasema, "Mzanaki ndiye Rais, basi sisi Wazanaki tutainuka." Nikamwambia, "Nenda, uko utaratibu wa kupata kazi." Akaniambia, "Na mimi vilevile niende huko?" Nikamwambia, "Kwa nini usiende huko?" Akasema, lazima nije kwako; sasa Mwalimu wewe umekwisha pata, ndugu zako wengine vile vile wapate. Sasa tusipoanza sisi Wazanaki waanze nani? Na wakubwa ndio wa kula, na wakati wa kula umefika; basi tule!"
            (Uk. wa 40)

Yameharibika mengi kwenye nchi hii kwa sababu viongozi wengi wanaamini kuwa uongozi ni sehemu ya kujineemisha wao na familia zao. Na kwa wale ambao hawana ndugu au marafiki kwenye sehemu muhimu za uongozi, uwezekano wa kupata ajira au haupo kabisa au ni finyu sana.
Mwalimu Nyerere

Kurudisha mfumo ambao unatoa fursa sawa kwa wote inawezekana kabisa.

Sunday, November 8, 2015

Yanayotokea niliyatabiri

Kwenye makala yangu ya tarehe 14 April 2015 kwenye gazeti la Jamhuri nilitoa maoni yangu juu ya Sheria ya Makosa ya Mtandao 2015 na kutahadharisha kuwa ni sheria ambayo itawafikisha wengi mahakamani, na hata gerezani.

Na tayari kuna kesi zimeshafikishwa mahakamani dhidi ya watu wanaotuhumiwa kukiuka sheria hii.

Nilitoa hoja kuwa, pamoja na kuwa sheria hii inakusudia kudhibiti uhalifu unaotokea kwa matumizi ya mifumo ya mtandao wa habari na mawasiliano, ni sheria ambayo ina hitilafu kubwa zenye kuhatarisha uhuru wa kusambaza na kutoa maoni mbalimbali ndani ya jamii.

Hakuna raia ambaye analazimishwa kupenda sheria mbalimbali ambazo anaona zina kasoro au hitilafu. Lakini zinabaki kuwa ni sheria na yoyote ambaye hataki, kwa makusudi, kusimama kizimbani kujibu mashtaka ya kukiuka hizo sheria anapaswa kuwa mwangalifu asifike huko.

Njia muafaka ya kuepuka kuishia kubaya ni kuweka mikakati ya pamoja ya kupinga hizi sheria zenye kasoro kwa taratibu zilizopo, za kisheria.

Hoja ya kuwa unawezaje kupinga sheria zenye hitilafu kwa kutegemea serikali ambayo ilipitisha sheria hizi ni hoja yenye nguvu. Kwa mara ya kwanza katika historia ya Tanzania chama tawala kimeshinda uchaguzi kwa asilimia ndogo kuliko kwenye chaguzi zote zilizopita. Mimi naamini kuwa ushindi huo mwembamba unaweza kuleta mabadiliko hata kwa serikali ya Chama cha Mapinduzi (CCM) kuwa tofauti na serikali zake zilizopita, ikawa ni serikali ambayo inasikiliza maoni ya Watanzania na kuanza kupitia upya zile sheria ambazo zinalalamikiwa na watu.

Wasiposikiliza wajiandae kuongeza mahakimu, na kujenga magereza kwa wingi.