Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Friday, July 28, 2017

Afrika tunaibiwa sana, tena sana

Hii ni makala yangu ya tarehe 18 Julai 2017 kwenye safu yangu inayoitwa Ujumbe toka Muhunda ndani ya gazeti la Jamhuri linalochapishwa kila Jumanne.

******************************

Taarifa iliyotolewa hivi karibuni na shirika lisilo la kiserikali Global Justice Now inaeleza jinsi gani bara la Afrika linavyoibiwa rasilimali yake.

Ripoti hiyo, inayoitwa Honest Accounts 2017, inaeleza kuwa kwa mwaka 2015 mali na pesa za thamani ya Dola za Marekani bilioni 203 zimetoka Afrika kwa njia ya faida ambazo mashirika ya kimataifa yamepata kutokana na shughuli za biashara na uzalishaji barani Afrika, na kwa mianya haramu ya pesa zinazotumwa nje. Wakati huo huo ni kiasi cha Dola bilioni 161.6 tu ambazo kwa mwaka huo ziliingia barani Afrika kwa njia ya mikopo, kutuma pesa kwa watu binafsi kutoka nje ya bara la Afrika, na misaada.

Huu utafiti unatukumbusha tu kuwa bara la Afrika ni tajiri, lakini kwa bahati mbaya Waafrika tunakubali, au kwa kutokujua au kwa kudanganywa, kuwa sisi ni maskini. Hali hii inatufanya sisi na serikali zetu kuwa na mawazo ya ombaomba ambaye badala ya kutumia uwezo aliojaliwa kutafuta riziki, anazunguka mitaani kuomba watu pesa za kuendesha maisha yake.

Taarifa inaendelea kufafanua jinsi bara la Afrika linavyoibiwa na mashirika ya biashara ya kimataifa. Wakati bara la Afrika linapokea kiasi cha Dola bilioni 19 kwa njia ya misaada kutoka nje, kiasi cha Dola bilioni 68 zinahamishwa kwenda nje na mashirika haya ambayo, kwa kawaida na kwa makusudi, hayataji thamani halisi za bidhaa wanazoingiza barani Afrika na mali inayoondoshwa kwenda nje. Ni hitimisho ambalo linafanana na hitimisho lililofikiwa na taarifa ya kwanza ya makinikia. Tofauti ni kuwa taarifa hii haitolewi na wataalamu waliyotumwa na Rais John Magufuli ila na shirika lililopo Ulaya ambalo linamulika kiwango cha wizi dhidi ya Afrika.

Pamoja na shutuma hizi dhidi ya wizi unaoendelea kudhoofisha maisha ya Waafrika, ni muhimu kutofautisha aina ya wizi huu. Kwanza, upo wizi ambao lazima tukubali kuwa ni wizi halali ambao unalindwa na sera na sheria mbovu zilizopitishwa na mabunge ya nchi za Afrika kulinda mifumo inayonyima Waafrika fursa ya kufaidika na utajiri wao.

Tutakuwa tunajidanganya kama hatutakubali kuwa rushwa ni mojawapo ya vichocheo vikubwa ambavyo vilisababisha baadhi ya nchi hizi kuweka sera na sheria ambazo, kwa ujumla wake, hazilindi maslahi ya Waafrika bali zinalinda maslahi ya mashirika ya nje kufuja rasilimali za bara letu na kuwaacha wananchi wake kuwa watumwa wa mali yao wenyewe.

Hata hivyo yapo mazingira ambayo hayasukumwi na rushwa ambapo inaziweka nchi za Afrika wakati kwenye shida kubwa za kiuchumi zinazowalazimisha kuweka mazingira yasiyo na manufaa kwa wananchi wake.

Madai ya kutaka kubadilisha mifumo hii ambayo yamejitokeza sasa nchini Tanzania yamewahi kujitokeza kwenye sekta ya madini nchini Zambia. Ilipobinafsisha migodi yake ya kuchimba shaba, Serikali ya Zambia ilikuwa inakabiliwa na uzalishaji mdogo na gharama kubwa ya kugharimia uzalishaji iliyokadiriwa kufikia Dola milioni moja kwa siku.

Ilipotafuta msaada kutoka mashirika ya fedha ya nje ikaambiwa dawa ni moja tu: ubinafsishaji. Kwa usiri ule ule ambao tuna uzoefu nao hata sisi, serikali ya Zambia ilifanya majadiliano ya ubinafsishaji na wawekezaji ambao, ingawa sheria ya madini ilitaka walipe mrahaba wa asilimia 3 kwa serikali kwa mauzo ya shaba nje ya nchi, mkataba wa siri uliwaruhusu kulipa asilimia 0.6. Aidha, makampuni ya kuchimba madini yakapunguziwa kodi ya mapato kwa kiasi kikubwa kiasi kwamba wafanyakazi waliowaajiri wakawa wanalipa kodi kubwa zaidi kuliko makampuni hayo.

Huu nauita wizi halali, kwa sababu kimantiki ni wizi tu hata kama unalindwa na sheria za nchi. Pili, upo wizi ambao unakatazwa kwa mujibu wa sheria. Inakadiriwa kuwa kiasi cha Dola bilioni 29 zinafujwa barani Afrika kutokana na biashara haramu ya magogo, uvuvi, na biashara za wanyamapori na mimea. Biashara haramu ya pembe za ndovu inakadiriwa kuwa na thamani ya Dola bilioni 10.

Njia nyingine ambayo inainyima Afrika manufaa inayotokana na mali yake ni kukosekana kwa viwanda vinavyochakata malighafi zake. Tunauza pamba nje ya nchi halafu tunanunua nguo zinazotokana na pamba hiyo. Tofauti ya thamani ya malighafi na bidhaa iliyotengenezwa inabaki nje.

Tunaruhusu utaratibu wa kupeleka nje makinikia badala ya kuweka mitambo barani Afrika ya kuchakata madini, na kwa hali hiyo kukosa ongezeko la thamani ya mali inayopelekwa nje na mapato kwa serikali zetu.

Kwa kifupi ripoti iliyotolewa inatukumbusha tu kuwa sehemu kubwa ya nchi zinaozoendelea zinanufaika na utajiri wa Afrika kuliko sehemu kubwa ya Waafrika wenyewe. Zile porojo kuwa nchi tajiri zinasaidia bara la Afrika hazina ukweli wowote. Ni bara la Afrika ambalo linasaidia nchi tajiri.

Kuna hotuba nzuri sana ya Mwalimu Nyerere inayotuasa tusikubali kusikia kelele tunazopigiwa tunapoazimia kufanya jambo lenye manufaa. Kwenye hotuba anasema kuwa tunapozidi kukaribia lengo, na kelele zitazidi kuwa kubwa.


Vita vya kurudisha mikononi mwa Waafrika utajiri wao inahitaji kutumia uzoefu mkubwa na maarifa. Lakini ni vita ambayo inahitaji kuiendesha huku tukiwa tumeziba masikio kuepuka kuyumbishwa na kelele ambazo zinazidi kuongezeka ili kutuondoa kwenye safari ya kurejesha na kuimarisha hadhi na heshima ya bara la Afrika.

Friday, July 21, 2017

Mamlaka ya Mapato Tanzania yawageukia wauza spea

Nimesikia taarifa ya habari asubuhi hii kuwa Mamlaka ya Mapato Tanzania wameanza kukagua maduka ya wauza spea za magari.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo, Mamlaka inachunguza bidhaa hizo zilizopo madukani ili kupata uthibitisho wa wenye maduka kuwa wamepata hizo bidhaa kwa njia za halali.

Kwa muda mrefu inaaminika kuwa baadhi ya wenye maduka yanayouza spea za magari wananunua spea hizo kutoka kwa wezi wa magari, au wezi wanaoiba spea kutoka kwenye magari.

Hizi hatua zikiendelea kwa muda mrefu zinaweza kupunguza wizi wa spea za magari, na hata wizi wa magari.

Miaka mingi iliyopita nilipoishi Dar es Salaam niliwahi kuibiwa kioo cha mbele cha gari. Nilipotoa taarifa kituo cha polisi niliambiwa na polisi kuwa wana hakika kuwa kioo changu kitapatikana Gerezani, eneo la Dar es Salaam ambalo huuza bidhaa mbalimbali zilizotumika, nyingi ya hizo zikiwa bidhaa za wizi.

Wezi watapungua
Askari wa upelelezi wawili nilioambatana nao kuelekea Gerezani walinushauri kubaki mbali kidogo na eneo wakati wao walipoingia Gerezani na wakarudi baada ya muda na kuniambia kuwa kioo changu, ambacho kilikuwa na namba ya gari yangu, wamekiona. Hawakutaka niongozane nao kwa sababu walisema nafanana sana na polisi na tungekuwa pamoja tusingepata ukweli.

Cha ajabu ni kuwa wale polisi walinishauri ninunue kioo changu. Bila hivyo walisema sitakipata. Huo ndiyo ulikuwa utaratibu wa kupata mali ya wizi wakati huo.

Bila shaka hizi jitihada mpya za Mamlaka ya Mapato zitapunguza kasi ya wizi, na zitaleta mabadiliko chanya kwa wamiliki wa magari.

Taarifa nyingine kama hii:
https://muhunda.blogspot.com/2016/07/mada-yangu-ya-leo-mwizi-ni-mwizi-tu.html
https://muhunda.blogspot.com/2011/07/maana-sahihi-ya-neno-fisadi.html

Friday, July 14, 2017

Simulizi za Jaffar Idi Amin

Hii simulizi nilipewa na Jaffar Idi Amin, mtoto wa kiume wa aliyekuwa kiongozi wa Uganda kati ya mwaka 1971 hadi 1979, Idi Amin Dada.

Anasema kuna siku alikuwa kwenye matembezi kwenye jiji la Kampala akakuta gari aina ya Volkswagen imeegeshwa na akasimama kwa muda mrefu akiiangalia kwa sababu aliitambua kuwa ilikuwa gari ya zamani ya baba yake.

Akiwa anaiangalia akatokea mtu na kumsalimia na kumuuliza sababu za kukaa muda pale akiangalia ile gari. Mazungumzo yakawa hivi:

"Mbona unaishangaa sana hiyo gari?"
"Ilikuwa gari ya baba yangu."
"Baba yako nani?"
"Idi Amin."

Anasema alivyotamka jina la baba yake yule aliyekuwa anamhoji akashangaa sana na kusema: "Baba yako ndiyo alimuondoa baba yangu nchini!"

Aliyekuwa anaongea naye alikuwa mmoja wa watoto wa Milton Obote, Eddy Engena-Maitum. Serikali ya Rais Obote ilipinduliwa na Idi Amin, wakati huo akiwa kamanda wa jeshi la Uganda, tarehe 25 Januari 1971 wakati Obote akiwa nchini Singapore kuhudhuria mkutano wa Jumuiya ya Madola.

Idi Amin alishika madaraka mpaka mwaka 1979 baada ya Rais Nyerere kutangaza vita dhidi ya Uganda kufuatia uvamizi wa eneo la Kagera na majeshi ya Idi Amin. Baada ya kukomboa eneo lililovamiwa vita iliendelea ndani ya ardhi ya Uganda na kuhitimishwa kwa kuangushwa kwa serikali ya Amin.

Jaffar akamwambia Eddy: "Mimi nitakutambulisha kwa mtu ambaye baba yake alimuondoa baba yangu hapa Uganda." Alimaanisha mimi.

Mwalimu Nyerere akiwa na mwenyeji wake, Rais Milton Obote, wakati wa moja ya ziara zake nchini Uganda. Wa pili kutoka kulia ni Idi Amin, na kulia ni Philemon Mgaya, aliyekuwa mpambe wa Rais Nyerere.
Kabla ya siku hiyo Jaffar alipokutana na Eddy jijini Kampala, mimi na Jaffar tulikwa tumeonana kijijini Butiama katika tukio lililoandaliwa na Idhaa ya Kiswahili ya Shirika la Utangazaji la Uingereza (BBC) kuadhimisha miaka 30 ya vita vya Kagera, vita vilivomuondoa Idi Amin nchini Uganda.

***********************************
Bofya hapo chini kusoma maelezo yangu (kwa lugha ya Kiingereza) juu ya ziara ya Butiama ya Jaffar:

***********************************

Idi Amin na familia yake walikimbilia nchini Libya, na baadaye kuhamia Saudia Arabia. Milton Obote na familia yake walihamia Tanzania na wakawa majirani zetu Msasani kwa muda mrefu.

Saturday, July 1, 2017

Watoto wa mjini nimewakubali

Nimejifunza siku chache zilizopita kuwa mtoto anayeishi mjini ni tofauti sana na yule anayeishi kijijini. Wa mjini wajanja.

Nilikuwa kwenye mitaa ya Kariakoo hivi karibuni nikaamkiwa na binti mdogo aliyevaa baibui niliyemkadiria kuwa na umri usiozidi miaka saba. Aliniomba msaada wa pesa kwa ajili ya mama mlemavu aliyekuwa kwenye kiti cha walemavu upande wa pili wa barabara.

Nilitoa shilingi 5,000 nikamkabidhi na kumuuliza kama nimsaidie kuvuka barabara ya Livingstone ambayo wakati huo ilikuwa na msululu wa magari. Alinihakikishia atamudu kuvuka mwenyewe. Nikaendelea na kununua miwani kwa machinga na yeye akaondoka.

Dakika 20 baadaye nikamkuta yule mama mlemavu kwenye mtaa wa jirani nikamuuliza kama alipokea zile pesa nilizotoa.

"Pesa gani?"
"Zile elfu tano nilizompa yule binti akuletee?
"Hata sijazipata. Ngoja tumsubiri."

Wakati huo binti alikuwa kwenye duka moja akiendelea kuomba msaada kwa watu mbalimbali.

Binti alivyoniona akatabasamu kwa aibu na kukabidhi zile pesa kwa yule mama, ambaye alinijulisha kuwa ni mjukuu wake.

Nilitafakari kuwa inawezekana wanapozunguka kuomba pesa mjukuu anabaki na pesa nyingi kuliko anazokabidhi kwa bibi yake.