Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Friday, March 30, 2018

Jinsi ya kutamka kwa usahihi

Kuna wengi tunapata shida kubwa ya kutamka kwa usahihi maneno na majina - hasa yale ya lugha za kigeni. Au kurudia kuiga jinsi wageni wanavyotamka kwa makosa maneno ya Kiswahili, au majina yetu ya asili.

Siku hizi siyo lazima kujifunza lugha ili kuweza kutamka vyema majina na maneno yanayotokana na lugha za kigeni.

Unaweza kutumia Google Search ukaandika neno unalotaka kujifunza kutamka likitanguliwa na neno la Kiingereza define. Katika ukurasa utakaojitokeza taarifa ya kwanza kabisa itaorodhesha tafsiri ya neno kwa lugha ya Kiingereza ikifuatiwa na alama hii hapa chini.

Image result for audio symbol

Ukibofya kwenye alama hiyo utasikia matamshi sahihi ya neno husika.

Matamshi ya majina yanapatikana kwa wingi zaidi kupitia mtandao wa YouTube kwa kutumia search na kutanguliza "how to pronounce" kabla ya neno jina husika. Mfano: how to pronounce Ngorongoro.

Nimesikia mara nyingi watangazaji wa redio na runinga za Tanzania wakishindwa kutamka majina ya Kiafrika ambayo wasio Waafrika wanayatamka vizuri. Mfano mzuri ni [Rais Emerson] Mnangagwa wa Zimbabwe.

Friday, March 23, 2018

Ukitaka kula usiende jikoni

Nina desturi ya kununua mahindi ya kuchoma yanayouzwa mitaani. Nilichoshuhudia miezi kadhaa iliyopita kimenipunguzia hamu ya kula tena mahindi hayo.

Nilisogelea mchoma mahindi na kuchagua mhindi uliyokuwa tayari juu ya jiko la mkaa. Baadaye kidogo, mmoja wa mahindi aliyokuwa akichoma ulianguka chini na kuseleleka mbali na alipokaa.

Alimtuma mwanae kuuokota chini na akaurudisha jikoni kuendelea kuuchoma baada ya kuufuta mchanga. Haukuwa ule mhindi niliyouchagua mimi ila nilitambua kuwa muda si mrefu atafika mteja kama mimi na kulishwa mhindi huo na, bila shaka, kuambukizwa minyoo.

Lakini haikuwa hatari ya kupata minyoo tu. Mchoma mahindi alikuwa na kikohozi. Na kila alipokohoa aliziba mdomo akitumia mkono wake wa kulia, ikiwa ni tabia ile ambayo baadhi wamefundishwa ili kuwakinga wengine kuathirika na athari za maambukizo yanayoweza kusambazwa na anayekohoa.

Tatizo ni kuwa ni mkono huo huo aliutumia kugeuzia mahindi aliyokuwa anachomea wateja, pamoja na langu. Mkono ulikuwa unatoka mdomoni na kushika mhindi.

Aliponiambia mhindi wangu umeiva, badala ya kuanza kula pale pale kama ilivyokuwa desturi yangu, nikamuomba aufunge vizuri nikaondoka nao lakini sikuula na ndiyo ikawa mwisho wa kununua mahindi ya njiani.

Labda kwa sababu nimeanza kulima mahindi nitakuwa nachoma mahindi ninayovuna shambani kwangu.

Nimewahi kusikia msemo kuwa ukitaka kula chakula cha mgahawa usiingie jikoni. Utakayoyaona huko yatakatisha njaa yako.

Friday, March 9, 2018

Muswada wa Sheria ya Makosa ya Mtandao 2015 una hitilafu kubwa


Hii ni moja ya makala zangu zinazochapishwa kwenye safu yangu iitwayo Ujumbe Kutoka Muhunda ndani ya gazeti la Jamhuri. Ilichapishwa tarehe 14 Aprili 2015.
*************************************
Nilipata fursa ya kushuhudia kwenye runinga majadiliano ya muswada wa Sheria ya Makosa ya Mtandao 2015. Kwa mtazamo wangu sheria ikianza kutumika kutakuwa na ongezeko kubwa la watumiaji wa mawasiliano, hasa ya simu, kubebeshwa makosa, kulipa faini, na kutumikia vifungo gerezani.

Kusudio la itakayokuwa Sheria ya Makosa ya Mtandao 2015, kwa mujibu wa muswada uliowasilishwa bungeni na serikali, ni: “...kutunga sheria ambayo itaainisha makosa yanayohusiana na matumizi ya mfumo wa kompyuta na Teknolojia ya Habari na Mawasiliano, kuweka utaratibu wa upelelezi, ukusanyaji na matumizi ya ushahidi wa kielektroniki.”

Ni kweli kuwa vipo vipengele ndani ya muswada vinavyoainisha makosa ambayo yanastahili adhabu. Mfano, wahalifu wengi leo wanatumia mtandao kuiba pesa kutoka kwenye akaunti za benki, pamoja na kutumia majina ya watu wasiyokuwa na hatia kufanya uhalifu huo ili kuficha utambulisho halisi wa wahalifu hao. Aidha, kutoa taarifa zinazolinda ulinzi na usalama wa taifa bila shaka kunastahili adhabu kali.

Hakuna ubishi pia kuwa kushirikisha watoto kwenye vitendo vya ngono na kutumia picha au taarifa hizo kwenye mitandao ya kompyuta na simu ni makosa ambayo hayapaswi kuvumiliwa. Wanaoshiriki vitendo vya aina hii wanastahili kuhamishiwa gerezani na kubaki huko maisha yao yote.

Aidha, nimewahi kuandika kwenye safu hii kuwa wanaotumia mtandao wa habari na mawasiliano kusambaza uongo hawatumii vyema wajibu wao kama wanajamii. Hawa, kwa maoni yangu, wanastahili adhabu iliyoainishwa kwenye kifungu cha 16 cha muswada wa sheria hii.

Lakini pamoja na yale ambayo wengi tutakubaliana ni makosa dhahiri, kuna makosa yaliyoainishwa kwenye muswada ambavyo yatawakumba wasiokusudiwa. Kifungu 7(2)(b), ambacho kinabainisha kuwa anayepokea data kompyuta ambayo haijaidhinishwa atakuwa ametenda kosa mwa mujibu wa sheria hii, kinampa mwanya mtu yoyote mwenye nia mbaya uwezo wa kutuma data hizo kwa mtu mwingine bila anayepokea taarifa hizo kuziomba, na hizo taarifa zilizopokelewa zitakuwa ushahidi wa kumtia hatiani anayekutwa nazo. Pamoja na kuwa muswada unatambua kuwa ni kosa kwa mtu kutuma taarifa kwa mwingine bila ya ridhaa ya anayezipokea, teknolojia iliyopo inaruhusu kutotambuliwa kwa aliyezituma. Sheria hii inaacha mwanya kwa watu kukutwa na hatia na kulipa faini au kutumikia vifungo kutokana na vitendo vya makusudi vya watu wengine.

Sheria hii itasababisha umiliki wa simu kuwa sawa na ule wa silaha. Inakuwaje pale mtu anapoiba simu yangu na kutuma ujumbe ambao maudhui yake, kwa mujibu wa sheria hii, ni kosa la jinai? Mtu anaweza kujibu kuwa ni wajibu wangu kuhakikisha naichunga simu yangu, kama ambavyo mmiliki wa silaha anavyowajibika kuchunga silaha yake isitumike kwenye matukio ya uhalifu. Tayari wanadamu hatuaminiani kwa mengi, na hali hii itatuongezea sababu nyingine ya kutoaminiana.

Katika muswada huu ipo dhamira ya kuzuwia uhalifu, lakini yawezekana pia kuna kusudio la kudhibiti harakati za kijamii na za kisiasa. Kipengele 20(1) kinachoelekeza kwamba ni hatia kutuma ujumbe bila ya ridhaa ya anayeupokea una sura mbili. Kwanza upo ujumbe tunaopokea kila siku wa kampuni za simu ambazo zinaleta usumbufu mkubwa kwa baadhi ya wateja kutokana na kuwa siyo kila anayezipokea anazihitaji. Naafiki kuzuwia taarifa za aina hii. Mtumiaji wa simu anapaswa kupewa uwezo wa kuchaguwa iwapo anataka kupokea taarifa za kibiashara kupitia kwenye kampuni za simu.

Lakini kuna sura ya pili inayoibuliwa. Zipo taarifa za kijamii na kisiasa ambazo pia tunapokea. Siku kadhaa zilizopita nimepokea ujumbe wa mgombea mtarajiwa wa jimbo mojawapo la ubunge ambaye anajiandaa kugombea ubunge, akiomba kuungwa mkono kwenye harakati zake. Sheria ikipitishwa huyu naye anapaswa kwenda na maji, kwa kunitumia ujumbe bila ridhaa yangu. Hapa naona kuna kasoro kidogo.

Ni kweli kuwa naye ni msumbufu kwa watumiaji wa mtandao wa simu, lakini kuna umuhimu wa kulinda haki ya raia kupokea taarifa zenye madhumuni ya kupanua ufahamu wao na uwezo wao wa kushiriki kwenye michakato inayojenga demokrasia. Kwa mtazamo wangu, hizi taarifa ni muhimu kuliko taarifa za kila siku ambazo tunapokea kutoka kwenye kampuni za simu.

Kampeni za uchaguzi zikipamba moto huyu mgombea angeweza kutumia simu yake kutuma taarifa kuwaelimisha wapiga kura wake kuhusu masuala muhimu ya harakati zake lakini sheria inatishia kudhibiti fursa hiyo, na itawanyima wapiga kura wake fursa ya kupata taarifa hizo kwa urahisi. Baya zaidi, sheria inawapa fursa wapinzani wake kulalamika kupokea bila ridhaa yao ujumbe wake na hivyo kuhatarisha yeye kukutwa hatiani. Ni kipengele kinachodhibiti uhuru wa kupata habari.

Mpaka leo hii ninayo nafasi ya kupokea ujumbe wa harakati mbalimbali za kijamii na kisiasa kutoka kila pembe ya Tanzania, lakini ikishapitishwa sheria hii nitategema taarifa za vyombo vya habari pekee. Siamini kama demokrasia inalindwa kwa kutegemea taarifa za waandishi wa habari tu. Wakati mwingine tatizo la baadhi ya vyombo vya habari ni kuelemea na kuwa na misimamo ambayo inaunga mkono upande mmoja dhidi ya mwingine. Siyo vibaya kuwa na misimamo ya aina hiyo, lakini ni muhimu pia kuwepo fursa kwa wapokea taarifa kuunganishwa moja kwa moja na watoa taarifa bila kuwekewa chujio wala chumvi. Anayeamini kuathirika na taarifa za uongo kwa njia hii bado anabaki na fursa ya kutumia sheria kupata haki dhidi ya mtoa taarifa.

Hii itakuwa sheria inayodhibiti maovu kadhaa katika matumizi ya kompyuta na teknolojia ya habari na mawasiliano, lakini ni sheria ambayo pia itatishia uhuru wa kupokea habari na kubadilishana mawazo.

Taarifa nyingine kama hii:

Friday, March 2, 2018

Hii ndiyo mila ya Kizananki ya kurudisha mahari

Miaka ya hivi karibuni baada ya kufariki mmoja wa shangazi zangu, nilipigiwa simu na baba yangu mdogo kunipa taarifa ya msiba na kunitaka nifike kwenye msiba.

Nilichelewa kidogo kufika kwenye msiba na aliendelea kunipigia simu mara kwa mara kunihimiza nifike mapema kwenye msiba. Alisema: "huu ni msiba wenu, njoo haraka!"

Sikuelewa maana ya ule kuwa "msiba wetu" mpaka baadaye.

Katika mila ambayo ilifuatwa miongoni mwa Wazanaki, mume anaweza kurudishiwa mahari na ndugu wa mke ili kuhalalisha wanandoa wawili kuachana na mke kurudi kwa ndugu zake.

Hili hutokea kwa sababu za kutoelewana kwa wanandoa, na hasa kama ndugu wa mke wanaamini kuwa dada yao anateswa au kudhalilishwa na mume wake.

Nilichojifunza kwenye msiba ni kuwa Mwalimu Nyerere alirudisha mahari kwa mume wa shangazi yangu na shangazi akarudi kuishi miongoni mwa ndugu zake.

Kwa desturi ya enzi hizo mke anayerudi nyumbani anatunzwa na ndugu zake. Kwa huyo shangazi, Mwalimu Nyerere alimjengea nyumba na aliendelea kuishi kwenye kijiji cha Butiama mpaka alipofariki.

Kwa mila hii mahitaji yake yote makubwa pamoja na ya watoto wake yatatimizwa  na ndugu zake. Aidha, inapotokea binti zake kuolewa basi mahari yao inachukuliwa na hao waliomrudisha nyumbani. Kwa mantiki hiyo, hata unapotokea msiba gharama za msiba zinabebwa na waliomtoa kwa mume wake.

Na ndiyo hapo nikaelewa kauli ya baba yangu mdogo: "huu ni msiba wenu!" Mwalimu Nyerere ana warithi wake ambao wanapaswa kurithi pia majukumu yake.

Lakini mila na desturi zinabadilika. Wakati wa msiba uliibuka ubishi mkali kati ya wazee juu ya mila hiyo. Baadhi yao waliona kuwa haipaswi kufuatwa kwa sasa.