Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Tuesday, August 28, 2012

Hatimaye, watu wa sensa hawa hapa

Jumapili, tarehe 26 Agosti, nilikaa nyumbani siku nzima nikisubiri kuhesabiwa kwenye Sensa ya Taifa lakini sikuona mtu hata mmoja kuja kuniuliza swali. Hatimaye leo maafisa wa sensa ya Taifa wamefika kunihoji maswali yao 62, ambayo kila mshiriki anapaswa kuyajibu.

Wengi wetu hatukukumbuka kuwa ni zoezi la juma zima.
Mimi, kushoto, nikijibu maswali ya Sensa ya Taifa leo asubuhi. 
Ndani ya muda wa dakika kumi zoezi lilimalizika na wakaondoka.

Pamoja na kwamba wengine tulikuwa na shauku kubwa ya kukamilisha kazi hii kuna Watanznia wenzetu ambao kabla ya zoezi hili kuanza wamekuwa wakiendesha kampeni ya wazi kuhimiza Waislamu wasishiriki kwenye sensa kwa sababu maswali yale 62 hayaulizi dini ya anayehesabiwa.

Nimejaribu kuuliza hili swali lakini mpaka leo sijasikia jibu lake: tunataka kujua kuna Watanzania wangapi wa dini mbalimbali ili tutumie hizo takwimu kufanya nini? Mwenye jibu naomba anifahamishe.

Sunday, August 26, 2012

Wageni wa Butiama: Agustino Lyatonga Mrema

Butiama inatembelewa na wageni wengi, baadhi yao mashuhuri, lakini wengi ambao siyo mashuhuri. Wengi wa wageni mashuhuri waliowahi kutembelea Butiama walifika hapo kwa sababu ya kumtembelea Mwalimu Julius Kambarage Nyerere.
Mmojawapo wa hao wageni ni Mhe. Agustino Mrema ambaye amewahi kufika Butiama mara kadhaa. Katika picha hii anaonekana akisalimiana na Mwalimu Nyerere mwaka 1997 wakati wa msiba wa Bibi Mugaya wa Nyang'ombe, mama mzazi wa Mwalimu Nyerere.

Friday, August 24, 2012

Mada yangu ya leo: Muungano una manufaa

Pamoja na kuwepo malalamiko mengi juu ya muungano uliounganisha Unguja na Tanganyika na kutoa Tanzania, tushukuru kuwepo kwa muungano huu kwa kutuepusha na majanga mengi.

Na wanaopaswa kushukuru zaidi ni Watanzania wa upande ulioitwa Tanganyika kabla ya tarehe 26 Aprili 1964, siku ulipozaliwa Muungano.

Bila Muungano kusingekuwepo Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ). Bila shaka ingekuwepo JWTZ lakini labda ingekuwa ni Jeshi la Wananchi wa Tanganyika.

Leo hii, makamanda wa Jeshi la Wananchi wa Tanganyika wangekuwa wakikuna vichwa kutafakari namna ya kupambana na nchi mbili: Malawi na Zanzibar. Yote hii kutokana na kutokuafikiana kwa pande mbili za Muungano kuhusu mgawanyo wa mapato yatakayotokana na mafuta yanayokisiwa kuwepo ndani ya mipaka ya Tanzania kwenye eneo la Bahari ya Hindi, na pia kutokana na madai ya Malawi kuwa eneo lote la Ziwa Nyasa ni mali ya Malawi, ikiwa ni suala linaloibuliwa na kuwepo kwa uwezekano kuwa kuna shehena kubwa ya mafuta chini ya Ziwa Nyasa. Tanzania haitambui madai hayo ya Malawi na kubainisha kuwa mpaka kati yao upo katikati ya Ziwa Nyasa.

Kwa bahati nzuri Amiri Jeshi Mkuu wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania, Rais Jakaya Kikwete, ametamka hivi karibuni kuwa mgogoro kati ya Malawi na Tanzania juu ya mpaka wa Ziwa Nyasa hautahusisha vita na kuwa utamalizwa kwa njia za kidiplomasia.

Lakini hapa tusisahau kuwa hata majeshi ya Idi Amin yalipovamia maeneo ya Tanzania mwaka 1978 Serikali ya Tanzania ilifanya jitihada kubwa za kutatua ule mgogoro kwa njia za kidiplomasia. Zile jitihada hazikufaulu kumaliza mgogoro na matokeo yake Tanzania na Uganda zikaingia kwenye vita ambayo ilileta madhara makubwa kwa pande zote mbili.

Hasara ya Uganda: gari la kijeshi lililoteketezwa na majeshi ya Tanzania ndani ya eneo la Tanzania kwenye mji mdogo wa Mutukula.
Na kwa uhakika kwa sababu ya Muungano, mgogoro kati ya Tanzania Visiwani na Tanzania Bara hautahusisha vita. Bila hivyo zingepigwa mpaka mmoja aelewe hoja ya mwenzake. Anaesema Muungano hauna faida yoyote atafakari tena.