Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Saturday, December 13, 2014

Mwisho wa kampeni Butiama za uchaguzi wa serikali za mitaa

Viongozi na wagombea wa Chama cha Mapinduzi wa kijijini Butiama wakiomba kura mbele ya wakazi wa Butiama siku moja kabla ya uchaguzi wa serikali za mitaa utakaofanyika nchini kote kesho tarehe 14 Desemba 2014.
Mkutano huu (picha ya juu) ulifanyika eneo la stendi, Butiama. Wapinzani wao wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) walifanya mkutano wa mwisho wa kampeni kwenye kitongoji cha Mtuzu, Butiama.

Friday, December 12, 2014

Mabondia na unga (sehemu ya tatu ya awamu tatu)

Promota wa ndondi za kulipwa, Ibrahim Kamwe, anaeleza kwa nini baadhi ya mabondia wanajiingiza kwenye biashara ya madawa ya kulevya.
Ibrahim Kamwe
Ukiangalia umbumbumbu na maskini tulionao mabondia, hapo wajanja wenye pesa zao, wafanyabiashara, na baadhi ya viongozi wanatumia udhaifu tulionao mabondia kutuhadaa kwa kutupatia safari za nje za kimichezo au matembezi ya kwenda kufanya mazoezi ughaibuni na hatimaye kutubebesha mihadarati (madawa ya kulevya) bila kujua kwa kutuwekea katika mizigo tunayosafiri nayo. Wakati mwingine kuna baadhi ya wafanya biashara hao wenye pesa zao hukuweka wazi wakati unaenda pigana umbebee mzigo wake na atakulipa pesa nyingi. Hapo ndipo tunapobanwa ukiangalia nyumbani tunalalia telemka tukaze, tunashindia tembele mlo mmoja, msosi wa kengele tena kwa masimango, mfukoni huna kitu na wala huna kazi itakayokupatia pesa ya kula kwa wakati huo. Hapo sijaingiza mambo ya kodi, na demu wangu namlinda vipi.

Hii njaa na umaskini tulio nao mabondia ndiyo inawapa nguvu vigogo kututumia kwa kutubebesha madawa ya kulevya kusafirisha nje wakijua wazi hatuwezi kataa kutokana na dhiki tuliyo nayo. Tutakubali tu kwani hakuna apendae kulala njaa, kulala pachafu, au kuvaa midabwada.

“Siwezi acha dili la pesa kama hili wakati jina langu kubwa kila kona linatajwa mitaani na vyombo vya habari lakini mimi binafsi nauli ya daladala sina. Siku ya tatu leo nakula mlo mmoja kwa siku, watoto hawapo katika hali nzuri, mazoezi yenyewe sifanyi kwa raha nafikiria nitapata wapi mshiko. Leo unaniletea ishu ya pesa niikatae si nitakuwa kichaa?”


“Wadau wenzangu wa ngumi ,wapambe wao, na walio karibu na sisi mabondia wana nguo za bei kubwa wanapendeza, wana magari. Ukiangalia mimi bondia ndiye mtendaji wao mkuu nipo ovyo sina kitu mfukoni wala tumboni, madeni kibao yaani majanga matupu.”

Ushauri wangu kwa serikali au taasisi zinazohusika na wanaolichukia jambo hili kiukweli - maana wengine hujifanya kulichukia mdomoni pembeni ndiyo watendaji wakuu wa kuwatumia wanamichezo au wasanii kwa faida zao - mabondia au wanamichezo tuboreshewe maeneo yetu ya michezo ikiwemo katika vilabu vyetu na maeneo ya mazoezi, na vifaa viongezwe. Ikiwezekana kodi ya vifaa vya michezo ipunguzwe ili viwe vingi nchini mabondia wasibabaike na vya kuazima au kuangalia katika TV vifaa vya wenzetu.


Serikali iwajali mabondia, isaidie kudhamini semina za walimu wa ngumi ili wawaongoze vyema vijana wao. Magym ya makusudi yajengwe na maeneo ya wazi wasigawane wenye pesa na viongozi kwa faida zao. Wajenge sehemu za michezo ya ndani, na kama pia itatumika njia ya kutoa madarasa matupu katika mashule yetu kwa ajili ya kutuachia sehemu ya mazoezi ya jioni itasaidia sana kukuza mchezo na walimu wenye taaluma kufundisha vizuri kuliko mabondia kufundishana vichochoroni na kutokuwa na nidhamu ya mchezo wala maisha.

Sunday, December 7, 2014

Mabondia na unga (sehemu ya pili ya awamu tatu)

Promota wa ndondi za kulipwa, Ibrahim Kamwe, anaeleza kwa nini baadhi ya mabondia wanajiingiza kwenye biashara ya madawa ya kulevya.
Siku za hivi karibuni kuna vimaendeleo kidogo kwa baadhi ya mabondia; tunafanya mazoezi katika vilabu vya pombe kwa kuwalipa kodi ya mazoezi wenye baa. Naweza kusema Tanzania hakuna sehemu rasmi za kufanyia mazoezi ya ndani zilizotengwa na serikali kwa ajili ya raia wake wapenda michezo na kama zipo ni chache na ziko katika makambi ya jeshi kwa masharti magumu kwa raia wa kawaida. 

Siku za nyuma wakazi wa mjini kama vile Kisutu, Gerezani na Kariakoo walikuwa wanafanya mazoezi pale Arnatoglou. Siku hizi huwezi kusikia kuna mwanamichezo katokea Gerezani au Kariakoo. Iliyobaki kwao ni kuuza na kutumia madawa ya kulevya na kukimbizana na wafanyabiashara wa maeneo hayo. Naweza kuilaumu serikali kwa kutoendeleza michezo bali ilishiriki kuuwa kabisa michezo maeneo hayo na mengineyo zaidi.

Kwa sisi tulioanza kukua kimichezo pambano la ngumi likiandaliwa huwa tunalipwa kuanzia shilingi 5,000/- mpaka 20,000/- kwa mapambano haya madogomadogo na iwapo kutakuwa na pambano kubwa na kupata bahati ya kucheza unaweza kulipwa shilingi 40,000/- mpaka 100,000/-. Mapambano makubwa yanaweza kuwa moja, mawili, au matatu kwa mwaka; hayazidi hapo. Haya mapambano madogo tunaweza pata mawili mpaka sita kwa mwaka.

Msiwaone mabondia wakicheza mkadhani wana kipato kikubwa. La hasha! Ni wale tu wachache waliobahatika kupata wadhamini au waratibu wenye uwezo wa kipesa ndiyo kidogo hutoka.

Kwa sisi wengine ukiangalia elimu ya kusoma hatuna, kazi hakuna, na mchezo wa ngumi tunaupenda na pengine tuna vipaji na kufanya vizuri katika mapambano yetu. Hivyo mchezo ndiyo huwa kama ajira yetu kwa sababu tunapata chochote kidogo kupitia mchezo huo kuliko kuiba au kukimbizana na mapolisi katika kamari na kuishia jela.

Kwetu sisi mabondia huona ni jambo la kifahari na hufurahi mno pale tu tunapopata pambano la nje ya nchi na hufurahia kupanda ndege na vile vimisosimisosi tunavyopata tukiwa mahotelini ugenini. Tukihadithiana mambo ya safari uswahilini kwetu tunahisi tunakosa mambo mengi ya raha.

Hapo ndipo mawakala wa ngumi hutupata na mabondia huwa wanadiriki kukubali kwenda kucheza popote tukijua tutapanda ndege, tunakula raha bila kujali  na wala kuhoji tuendako tutalipwa kiasi gani cha pambano nitakalocheza wala kujua usalama wangu.


(itaendelea na sehemu ya tatu)