Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Tuesday, October 14, 2014

Huduma kwa mteja mkoani Mara

Hili ni tukio la kweli na nimelishuhudia.

Siku moja nilikuwa abiria kutoka Nyamisisi kwenda Mwanza ndani ya basi lililoanza safari yake Tarime.

Baada ya muda kondakta alimsogelea abiria aliyekaa karibu yangu na mazungumzo yakawa hivi:

Konda: Nipe hizo hela!
Abiria: Ngapi?
Konda: Kwani hujui?!?!?!

Baada ya muda abiria akatoa nauli kamili halafu wakaendelea:

Abiria: Nifahamishe nauli sahihi kwa ustaarabu.
Konda: Kwani wewe nani? Usiniletee mambo yenu ya Kikurya!

Sehemu nyingine Tanzania watu wangekunjiana ngumi. Mkoa wa Mara ni mazungumzo ya kawaida tu kati ya mtoa huduma na mteja wake.

Saturday, October 11, 2014

Uongo wa waandishi wa habari: sikuikataa noti ya Mwalimu Nyerere

Juzi nilipewa fursa ya kutoa neno la shukurani kijijini Butiama kwenye hafla ya kuzindua onyesho la noti na sarafu kwenye Makumbusho ya Mwalimu J.K. Nyerere.

Mgeni rasmi alikuwa Naibu Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania, Juma Reli. Katika kumalizia neno la shukurani niliomba uongozi wa Benki Kuu kuangalia uwezekano wa kubadilisha picha ya Mwalimu Julius Nyerere waliyotumia kwenye noti ya shilingi elfu moja. Kwa maoni yangu ile picha haifanani kwa karibu sana na sura ya Mwalimu Nyerere. Sikuamuru wala sikuikataa noti, ila niliomba tena kwa unyenyekevu mkubwa. Lakini ukifuatilia habari zilizoandikwa juu ya ombi langu utapata picha tofauti.

ITV walifungua dimba la upotoshaji kwa kusema kuwa nilitamka kuwa picha ile inamdhalilisha Mwalimu (au familia yake?). Huu ni uongo wa mchana na siyo kweli kabisa kuwa nilitumia neno “kudhalilisha.” Nikisoma baadhi ya vichwa vya habari vya baadhi ya magazeti yaliyoandika habari hizo navyo vinapotosha.

The Citizen wameandika kuwa nimeitaka serikali kuiondoa hiyo noti. Huo nao ni uongo mwingine. Gazeti lingine limeandika kuwa familia ya Mwalimu Nyerere imeikataa noti ya shilingi elfu moja. Ni uongo juu ya uongo. Naamini orodha ni ndefu zaidi lakini sijapata fursa ya kufuatilia kwa muda mrefu.

Sikusema kuwa familia imeikataa noti. Nilichosema ni hayo niliyoandika mwanzo wa taarifa hii.

Ninayo bahati mbaya ya kutungiwa maneno ambayo sijayasema kwenye taarifa zinazonihusu. Mwanzo nilikuwa napuuzia nikiamini kuwa tatizo hili litaisha lakini kila muda unavyozidi kupita naona hali ni ile ile.

Nimekuwa nawashauri waandishi wa habari waache kutumia mtindo wa kuandika “Madaraka alisema….” na badala yake watumie maneno yangu mwenyewe na kuandika habari kwa njia ya kuninukuu. Naamini njia hii inapunguza kuweka maneno ambayo hayakutamkwa.


Naanza kufikia kuamini kuwa maneno yangu mwenyewe huwa hayauzi magazeti na inalazimika mwandishi kuweka chumvi kidogo ili magazeti mengi zaidi yatoke. Kama hii ni kweli basi hali hii inadhirihisha kuwa sifa ya weledi kwenye sekta ya habari inaanguka, na inahitaji kufanyika jitihada ya kuirekebisha.  

Saturday, October 4, 2014

Hiki ni kielelezo cha utu uzima

Leo nimetembelea kituo cha polisi kutoa taarifa ya kupotelewa vitu vyangu. Nimegundua umri umepiga hatua kubwa.

Afisa aliyechukuwa maelezo yangu aliponiuliza umri wangu nilijibu: 54.

Akauliza: miaka? Nikamjibu: ndiyo, miaka. Au naonekana nimezidisha?

Nilitamani kumwambia: Hapana. Maandazi.

Ningejibu hivyo labda saa hizi ningekuwa rumande kwa kosa la kudhalilisha Jeshi la Polisi.

Lakini nilitambua kuwa kwake yule afisa miaka 54 haikuwa kidogo.