Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Wednesday, November 11, 2015

Adha za Mwenge wa Uhuru

Sina tatizo na madhumuni ya mbio za Mwenge wa Uhuru, lakini ninaona kasoro kubwa katika baadhi ya vipengele vya mchakato wa mbio hizo unavyoendeshwa.

Mwenge unapohamishwa kutoka sehemu moja kwenda nyingine, barabara zote huwa au hazipitiki au zinapitika kwa shida. Barabara zinafungwa mpaka Mwenge upite. Wale wenye shida za dharura wanakuwa hawawezi kutumia usafiri wa barabara kufuatilia shida zao.

Hata mgonjwa mahututi ambaye anapelekwa hospitali au kwenye kituo cha afya anaweza kujikuta ndani ya gari akisubiri Mwenge upite kwanza, ndipo gari alilopanda (kama siyo la kubeba wagonjwa) liweze kuruhusiwa na kuendelea na safari yake.

Gari zikiwa zimesimamishwa eneo la Kisesa, Mwanza, zikisubiri msafara wa Mwenge wa Uhuru upite.
Na isingekuwa vibaya sana iwapo watu wangelazimika kusubiri kwa muda kidogo tu kupisha Mwenge upite. Tatizo ni kuwa wakati mwingine watu husubirishwa kwa muda mrefu sana ili msafara wa Mwenge upite, hata pale ambapo msafara huo unaelekea njia tofauti. Ili mradi tu unapishana nao, basi utalazimika kusimama.

Mwenge wa Taifa ni nembo ya Taifa na nadhani maana ya kusimamishwa watu njiani ni kutoa heshima kwa hiyo nembo ya Taifa. Sijui kama hii ndiyo mantiki ya hatua hizi, lakini inawezekana pia kuwa watu husimamishwa kwa sababu ya kipengele kimoja ambacho nadhani kipo kwenye Sheria ya Usalama Barabarani ambacho kinatamka kuwa msafara rasmi ni lazima upishwe.

Nadhani msafara wa Mwenge unapewa hadhi ya msafara rasmi, kama msafara wa rais au viongozi wengine wa ngazi ya juu. Hatari iliyopo ni kuwa msafara wa Mwenge unaweza kumsubirisha mgonjwa mahututi na asiwahi kupata huduma ya matibabu ambayo inaweza kuokoa maisha yake.

No comments: