Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Sunday, November 8, 2015

Yanayotokea niliyatabiri

Kwenye makala yangu ya tarehe 14 April 2015 kwenye gazeti la Jamhuri nilitoa maoni yangu juu ya Sheria ya Makosa ya Mtandao 2015 na kutahadharisha kuwa ni sheria ambayo itawafikisha wengi mahakamani, na hata gerezani.

Na tayari kuna kesi zimeshafikishwa mahakamani dhidi ya watu wanaotuhumiwa kukiuka sheria hii.

Nilitoa hoja kuwa, pamoja na kuwa sheria hii inakusudia kudhibiti uhalifu unaotokea kwa matumizi ya mifumo ya mtandao wa habari na mawasiliano, ni sheria ambayo ina hitilafu kubwa zenye kuhatarisha uhuru wa kusambaza na kutoa maoni mbalimbali ndani ya jamii.

Hakuna raia ambaye analazimishwa kupenda sheria mbalimbali ambazo anaona zina kasoro au hitilafu. Lakini zinabaki kuwa ni sheria na yoyote ambaye hataki, kwa makusudi, kusimama kizimbani kujibu mashtaka ya kukiuka hizo sheria anapaswa kuwa mwangalifu asifike huko.

Njia muafaka ya kuepuka kuishia kubaya ni kuweka mikakati ya pamoja ya kupinga hizi sheria zenye kasoro kwa taratibu zilizopo, za kisheria.

Hoja ya kuwa unawezaje kupinga sheria zenye hitilafu kwa kutegemea serikali ambayo ilipitisha sheria hizi ni hoja yenye nguvu. Kwa mara ya kwanza katika historia ya Tanzania chama tawala kimeshinda uchaguzi kwa asilimia ndogo kuliko kwenye chaguzi zote zilizopita. Mimi naamini kuwa ushindi huo mwembamba unaweza kuleta mabadiliko hata kwa serikali ya Chama cha Mapinduzi (CCM) kuwa tofauti na serikali zake zilizopita, ikawa ni serikali ambayo inasikiliza maoni ya Watanzania na kuanza kupitia upya zile sheria ambazo zinalalamikiwa na watu.

Wasiposikiliza wajiandae kuongeza mahakimu, na kujenga magereza kwa wingi.

No comments: